Advertisements

Tuesday, September 10, 2013

KANALI ALIYETOROKA JESHINI AIPASUA KICHWA JWTZ

LUTENI Kanali Coelestine Seromba aneyedaiwa kutoroka ndani ya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), bado hajulikani alipo hadi hivi sasa. Msemaji wa JWTZ, Meja Erick Komba ameliambia gazeti hili jana kuwa kazi ya kumtafuta Luteni Kanali Seromba inaendelea kimyakimya na kusisitiza kuwa suala hilo halihitaji kutangazia umma wamefikia hatua gani. 
Komba alisema wanajeshi kadhaa walikimbia katika jeshi hilo lakini hawajatangazwa na wao kama jeshi hawaoni sababu ya kufanya hivyo kwani wana utaratibu wao. “Huyo Luteni Kanali Coelestine Seromba anayedaiwa kukimbia ni mwanajeshi mtoro kama wanajeshi wengine watoro na pindi atapopatikana atatiwa hatiani kama kanuni za jeshi zinavyosema,” alisema Meja Komba.

Akijibu swali aliloulizwa na mwandishi wa habari hizi kuhusu kuchelewa kukamatwa kwa Luteni Kanali Seromba, Meja Komba alisema hatua za kumfuatilia si lazima zitangazwe na pia mahali lilipofikia jeshi hilo katika kumtafuta ni siri yao.

Meja Komba alisisitiza kuwa Luteni Kanali Seromba hakuondoka na nyaraka yoyote ya jeshi hilo wala vifaa vyovyote kama inavyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari. 

Komba aliwasihi waandishi wa habari kuzingatia maadili ya uandishi kwa kuandika habari za kweli na zenye tija kwa pande zote ili kutojenga chuki baina ya jeshi na taasisi zingine. 

Alitolea mfano kuwa miaka ya hivi karibuni ambapo baadhi ya wanasiasa walitamka wazi kuwa jeshi hilo linakula bure hivyo hakuna umuhimu wa kutengewa bajeti kubwa huku wakisahau jukumu la jeshi hilo ni kulinda amani ya nchi na mipaka yake ili wananchi waishi kwa usalama.

Meja Komba alitoa mfano wa vurugu zilizotokea bungeni hivi karibuni kuwa kama Polisi wangeshindwa kudhibiti vurugu hizo hatua ya mwisho ilikuwa jeshi kuingilia kati, lakini watu wanadai wanajeshi wanakula bure. “Kikubwa ninachoweza kueleza hapa ni kalamu za waandishi kutumika vizuri ili kutoweka chuki kati ya taasisi zingine likiwemo jeshi letu nje ya nchi,” alisema Meja Komba huku akigusia namna msuguano kati ya viongozi wa Tanzania na Rwanda ulivyoripotiwa.

“Mengi yaliyoripotiwa ni kama nchi hii na Rwanda zinaingia vitani na uhasama huo kuhamia kwa wananchi na kujenga chuki na baadaye kuchukiana na hata kuweza kugombana wenyewe kwa wenyewe,” alisema.

Pia aliwakumbusha wananchi kuendeleza amani iliyopo kwani vita vina gharama kubwa na endapo nchi ipo vitani hata Bunge linaweza kusitishwa kutokana na fedha nyingi kupelekwa katika mapigano. 

Chanzo kimoja kutoka ndani jeshi hilo kimesema kutoroka kwa Luteni Kanali Seromba aneyedaiwa kukimbilia Rwanda hakuwezi kuleta tishio lolote ndani ya jeshi hilo.

Pia taarifa zilizopatikana ndani ya jeshi hilo zinadai kuwa kitengo alichokuwa Luteni Kanali Seromba ni kitengo cha kawaida na kwamba mafunzo yake hutolewa kimataifa na kila nchi ina mtu kama huyo.

Source: Jambo leo|Na Peter Ambilikile

No comments: