Advertisements

Monday, December 11, 2017

Babu wa Loliondo asema wengi watafuata kikombe




By Filbert Rweyemamu, Mwananchi efilbert@mwananchi.co.tz

Ngorongoro. Mchungaji Ambilikile Mwasapile maarufu Babu wa Loliondo aliyehudumia maelfu ya watu ndani na nje ya nchi kwa dawa aliyoitoa kwa kipimo cha kikombe amedai ameoteshwa kuwa umati utarudi kijijini Samunge kupata dawa.

Amesema ana uhakika wa jambo hilo kwa kuwa hata mwaka 2011 kabla ya maelfu ya watu kufika nyumbani kwake alioteshwa, hivyo amejiandaa kuweka miundombinu bora zaidi na hasa ujenzi wa vibanda atakavyovitumia kutoa huduma.

Mchungaji Mwasapile alisema hayo jana Jumapili Desemba 10,2017 mbele ya ujumbe wa Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tamisemi, Joseph Kakunda aliyekuwa mkoani Arusha kukagua miradi ya maendeleo, ikiwemo ya kuwawezesha wananchi kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Miongoni mwa waliofika kupata ‘kikombe’ kwa gharama ya Sh500 mwaka 2011 walikuwemo wafanyabiashara maarufu, wanasiasa na viongozi waandamizi serikalini.

Akizungumzia dawa yake anayodai inatibu maradhi mengi amesema kwa sasa anaitoa kwa watu wachache wanaofika kijijini hapo.

Miongoni mwao amesema ni watalii wanaofika kutembelea vivutio vya kitalii vilivyopo katika Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

"Huwa nawauliza watalii namna walivyoifahamu dawa yangu wanasema habari za ‘kikombe cha Babu’ imeenea katika nchi zao za Ulaya na Amerika," amesema Mwasapile.

Naibu Waziri wa Tamisemi, Kakunda akiwa na ujumbe wake baada ya kupata kikombe alimshukuru Mchungaji Mwasapile kwa alivyolifanya Taifa kujulikana na kusababisha maendeleo ya kijamii katika Kijiji cha Samunge.

Ametoa mfano wa barabara ya kutoka wilayani Longido na Kigongoni wilayani Monduli ambazo zimeboreshwa kutokana na idadi kubwa ya watu waliokuwa wakifika kupata huduma ya dawa.

Amesema hata huduma ya mitandao ya mawasiliano ya simu ilifika eneo hilo kwa haraka kutoka na watu wengi waliohitaji kuwasiliana na ndugu zao.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro, Raphael Siumbu amesema Mwasapile amechangia shughuli za maendeleo kutokana na idadi kubwa ya waliokwenda kijijini hapo na kusababisha mzunguko wa fedha kuwa mkubwa.

Amesema watu wengi kijijini Samunge wamepanda miti inayotumika kutengenezea dawa hivyo kuchangia utunzaji wa mazingira na huduma za kijamii kuongezeka.

No comments: