Advertisements

Wednesday, December 13, 2017

DC MUFINDI: MKATABA WA HUDUMA KWA MTEJA UTASAIDIA KUTOKOMEZA RUSHWA KWENYE OFISI ZA UMMA NCHINI.

 Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Mh. Jamhuri William, akiwahutubia wanafunzi wa chuo cha Rungemba pomoja na wananchi wakati maadhimisho ya siku ya Maadili na haki za Binadamu, iliyoadhimishwa kiwilaya katika chuo cha maendeleo ya jamii Rungemba kilichopo Mjini Mafinga Wilayani Mufindi.
 Sehemu ya Wanachuo wa Chuo cha Rungemba pamoja na Wananchi wakisikiliza hotuba ya mgeni wa heshima wakati wa kufungwa kwa maadhimisho ya siku ya Maadili na haki za Binadamu, iliyoadhimishwa kiwilaya katika chuo cha maendeleo ya jamii Rungemba kilichopo Mjini Mafinga Wilayani Mufindi.
Mkuu Takukuru Wilaya ya Mufindi Bw. Orest Mushi, akiwasilisha mada wakati wa maadhimisho ya siku ya Maadili na haki za Binadamu, iliyoadhimishwa kiwilaya katika chuo cha maendeleo ya jamii Rungemba kilichopo Mjini Mafinga Wilayani Mufindi.


Na Afisa Habari Mufindi
Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Mh. Jamhuri William amesema, endapo Ofisi za Umma  hazitodhibiti ipasavyo  mifumo na urasimu uliowekwa kwenye Ofisi za Serikali, masuala hayo yanaweza kuwa kichocheo kikubwa cha kuendelea kukua kwa tatizo la rushwa katika ofisi hizo.

Mkuu huyo wa Wilaya ametoa kauli hiyo wakati akifunga maadhimisho ya siku ya Maadili na haki za Binadamu, iliyoadhimishwa kiwilaya katika chuo cha maendeleo ya jamii Rungemba kilichopo Mjini Mafinga Wilayani Mufindi.

Mh. Jamhuri amesema, urasimu uliyowekwa kwa nia njema ya kuthibiti utendaji kazi ukitumiwa vibaya, unaweza kuwa chanzo cha rushwa, hivyo akatoa rai kwa taasisi zote za umma kuhakikisha zinazingatia suala la kuwa na mkataba wa huduma kwa wateja na kusisitiza kuwa, hiyo ni moja kati ya njia kuu za kuondoa suala la rushwa katika Ofisi za umma.

Awali Mkuu wa taasisi ya kuzui na kupambana na rushwa Wilayani Mufindi bw. Orest Mushi, ametanabaisha kuwa tafiti  za hivi karibuni zinazoonesha kupungua kwa rushwa nchini, zinatokana na utashi wa kisiasa uliopo, chini ya Rais John Pombe Magufuli, huku akibainisha malengo ya maadhimisho hayo, kuwa ni pamoja na  kuiwezesha Serikali kufuatilia na kufahamu hali ya rushwa nchini, kubainisha madhara ya rushwa na kutambua umuhimu wa kuendelea kupambana nayo, kutambua changamoto za mapambano dhidi ya rushwa, kuweka mikakati ya kupambana na rushwa, sanajari na kuisaidia nchi  kutathimini ushiriki wake  dhidi ya mapamabano ya rushwa kimataifa.

Mwaka 2005 serikali iliamua kwamba maadhimisho haya yawe yanafanyika disemba 10 ambapo, nchi yetu huungana na mataifa mengine duniani kuiadhimisha kama siku ya maadili na haki za binadamu. Kaulimbiu ya mwaka huu ni wajibika piga vita rushwa, zingatia maadili na haki za binadamu, kuelekea uchumi wa kati.

No comments: