Advertisements

Wednesday, December 13, 2017

WAZIRI KALEMANI AKAGUA MIRADI YA UMEME REA III KONGWA NA KONDOA

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (aliyeshika kipaza sauti) akiwasalimu wananchi wa Kijiji cha Pembamoto, Wilaya ya Kongwa, mkoani Dodoma, alipofanya ziara kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III)
Spika wa Bunge ambaye pia ni Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai (kushoto), akimpokea Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kulia) alipowasili jimboni kwake Kongwa kukagua Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III).

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kushoto), akifafanua jambo kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bilinith Mahenge (kulia), alipofika ofisini kwake hivi karibuni, kabla ya kutembelea Wilaya za Kongwa na Kondoa kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III). Kushoto kwa Waziri ni Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli, Mhandisi Innocent Luoga. Wengine ni watendaji kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Wakala wa Nishati Vijijini (REA) pamoja na wakandarasi wanaotekeleza Mradi husika katika Wilaya hizo.

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kushoto) akimkabidhi Spika wa Bunge ambaye pia ni Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai, kifaa kinachotumika kuunganisha umeme katika nyumba pasipo kutandaza nyaya, kijulikanacho kama UMETA. Waziri alitoa kifaa hicho kama zawadi kwa baadhi ya wazee katika Kijiji cha Makole, Wilaya ya Kongwa, wakati wa ziara yake kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini (REA III) pamoja na kuzungumza na wananchi.
Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani (kulia), akifafanua jambo kwa Spika wa Bunge ambaye pia ni Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai (kushoto), alipokuwa katika ziara ya kazi jimboni humo kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III). Wengine pichani ni viongozi mbalimbali wa Serikali pamoja na wataalam kutoka wizarani, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Diwani wa Kata ya Nhumbi, Wilaya ya Kongwa, Sina Mude akizungumza wakati wa ziara ya Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III).
Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) Wilaya ya Kongwa, Seif Shabani (kulia), akiorodhesha jina la mmojawapo wa wazee waliopatiwa zawadi ya kifaa cha Umeme Tayari (UMETA) na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani wakati wa ziara yake kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III)

Sehemu ya umati wa wananchi katika Vijiji vya Makole, Pembamoto na Bereko wilayani Kongwa na Kondoa, wakimsikiliza Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (hayupo pichani) wakati wa ziara yake kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III).
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (aliyeshika kipaza sauti), akiwatambulisha wakandarasi wanaotekeleza Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III) katika Wilaya ya Kongwa, wakati wa ziara yake kukagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi huo. 
Mkuu wa Wilaya ya Kondoa, Sezaria Makota (kulia) akiwa pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo wakimpokea Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (wa pili kutoka kulia) alipowasili wilayani humo kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III). Kulia kwa Waziri ni Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli, Mhandisi Innocent Luoga.
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (aliyeshika kipaza sauti), akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Bereko, Wilaya ya Kondoa wakati wa ziara yake kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III).
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango ambaye pia ni Mbunge wa Kondoa, Ashatu Kijaji, akizungumza wakati wa ziara ya Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati – mbele) wilayani humo kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III)
Kazi ya kuunganisha umeme katika Kijiji cha Bereko, Wilaya ya Kondoa ikiwa katika hatua za mwisho, kama mafundi hawa walivyokutwa na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani, wakati wa ziara yake kukagua utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III).

Na Veronica Simba – Dodoma
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amekagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III) katika Wilaya za Kongwa na Kondoa mkoani Dodoma.

Katika ziara hiyo ya siku moja iliyofanyika Jumatatu Desemba 11, 2017, Waziri Kalemani aliwasisitiza viongozi wa Halmashauri ambako Mradi wa REA III unapita, kuhakikisha wanatenga fedha kwa ajili ya kuunganisha umeme hususan katika Taasisi mbalimbali za umma.

“Siyo vema Taasisi muhimu za umma zikaendelea kukosa umeme kwa kutokuwa na fedha hivyo kuwatesa wananchi. Hakikisheni mnatenga fedha kwa shughuli hiyo muhimu.”

Aidha, alibainisha kuwa, maeneo yanayopewa kipaumbele katika Mradi wa REA III ni Taasisi zote za umma ili kuhakikisha zinatoa huduma bora kwa wananchi.

Pia, aliwataka wakandarasi wanaotekeleza Mradi huo katika maeneo mbalimbali nchini, kukutana na viongozi wa maeneo husika wakiwemo wabunge ili wapewe mwongozo wa sehemu muhimu za kipaumbele zinazotakiwa kuunganishiwa umeme.

Kwa upande wake, Spika wa Bunge ambaye pia ni Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai, akizungumza wakati wa ziara ya Waziri jimboni kwake, aliwaasa watendaji katika Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuongeza uwajibikaji kwa wateja wao ili kuboresha utoaji huduma ya umeme kwa wananchi.

“Bado zipo changamoto kadhaa katika utoaji wa huduma ya umeme kwa wananchi. Tanesco ongezeni uwajibikaji ili wananchi wanufaishwe na huduma hiyo muhimu kama Serikali ilivyodhamiria.”

Naye Naibu Waziri wa Fedha na Mipango ambaye pia ni Mbunge wa Kondoa, Dkt. Ashatu Kijaji, alitoa pongezi na shukrani kwa Serikali kupitia Wizara ya Nishati kwa kupanga kuviunganishia umeme vijiji 24 vya Wilaya hiyo, kupitia REA III.

“Kwa niaba ya wananchi wa Kondoa, natoa pongezi za dhati kwa Serikali na kuiomba iendeleze jitihada hizi za kuwaletea wananchi wake maendeleo kupitia upatikanaji wa nishati muhimu ya umeme,” alisema.

Katika ziara hiyo, Waziri Kalemani alifuatana na viongozi na wataalam mbalimbali kutoka wizarani, Tanesco na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), akiwemo Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli, Mhandisi Innocent Luoga.

No comments: