Advertisements

Saturday, May 25, 2019

NEMC yawatoa hofu watumiaji wa viwanja vya ndege

 Mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Manchare Heche (aliyenyanyua mikono) akisisitiza jambo wakati akiongea na wadau wanaotoa huduma mbalimbali kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), juu ya katazo la mifuko ya plastiki iliyopigwa marufuku kuendelea kutumika nchini ifikapo Juni Mosi mwaka huu. Wapili kulia ni Mkurugezi wa JNIA, Paul Rwegasha na wa kwanza kushoto ni mkuu wa kitengo cha Mazingira cha TAA, Maxmilian Mahangila.
 Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha (aliyesimama) akielezea mikakati iliyowekwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), ya namna ya kutekeleza  agizo la serikali la katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki kwa watumiaji wa viwanja vya ndege nchini. Wapili kushoto ni Mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Manchare Heche.
 Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Hali ya Hewa kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Joachim Philipo akitoa ushauri kwenye mkutano wa wadau wanaotoa huduma mbalimbali JNIA ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), na kuhusisha Wataalam kutoka Baraza ka Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), ambao walitoa maelezo mbalimbali juu ya katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki litakaloanza rasmi Juni Mosi, 2019 kwa mujibu wa sheria.
 Mmoja wa wadau wanaotoa huduma kwenye Jengo la Kwanza la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNI-TBI), Uyeka Rumbyambya akiongea katika mkutano ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) leo kwenye Ukumbi wa Watu Mashuhuri (VIP), na kuwashirikisha Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), katazo hilo la matumizi ya mifuko ya plastiki litakaloanza rasmi Juni Mosi, 2019.
 Mrakibu Msaidizi wa Uhamiaji, Anna Mushi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), leo akizungumza katika mkutano wa wadau wanaotoa huduma mbalimbali JNIA katika mkutano ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), na kuwahusisha Wataalam kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kutokana na katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki ifikapo Juni Mosi, 2019.
Mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Manchare Heche akiwaonesha wadau wanaotoa huduma mbalimbali kwenye Kiwanja cha Ncdege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) moja ya mifuko ya plastiki iliyopigwa marufuku kuendelea kutumika nchini ifikapo Juni Mosi, 2019 katika mkutano uliofanyika leo kwenye ukumbi wa Watu Mashuhuri (VIP).  

BARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), leo limewaondolea hofu wadau wanaoendesha huduma mbalimbali kwenye Viwanja vya ndege, katika mkutano ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), uliofanyika kwenye Ukumbi wa Watu Mashuhuri (VIP), kuhususiana na katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki ambalo litaanza rasmi Juni Mosi, 2019.

Mwanasheria wa NEMC, Manchare Heche amesema kwa upande wa viwanja vya ndege ipo mifuko, ambayo itaendelea kutumika kwa mujibu wa Kanuni namba tisa (9) ya sheria ya kuzuia matumizi ya mifuko ya plastiki ya mwaka 2019, lakini baada ya kutumika inatakiwa ihifadhiwe sehemu maalum na kupekekwa mahali itakapoteketezwa.

“Kweli katazo linahusu Watanzania wote na wageni na hapa Airport wapo wanaotumia nikiwa na maana ya wafanyakazi na wateja wakiwemo abiria, lakini katika sheria ukiangalia kanuni ya tisa 9 ipo mifuko ya vifungashio ambayo haijazuiwa ni kama ile ya kuhifadhi vyakula, dawa, kilimo na inayohifadhia takataka, mfano korosho au keki wanazopewa abiria kwenye ndege mfuko wake upo katika kipengele cha chakula, hivyo itaendelea kutumika lakini baada ya matumizi tu itahuifadhiwa sehemu iliyoelekezwa tayari kwa kwenda kuteketezwa,” alisisitiza Heche.

Alisema kwa upande wa plastiki zinazofungia mizigo ya abiria wanaosafiri kutoka ndani na nje ya nchi kwa usafiri wa ndege itatakiwa kuondolewa abiria anapofika nchini, na zitakusanywa na kuhifadhiwa maeneo maalum kabla ya kupelekwa eneo lililotengwa kwa ajili ya kuziteketeza.

Hatahivyo, kutokana na matumizi makubwa ya mifuko ya plastiki nchini imesababisha uharibifu mkubwa wa mazingira ikiwemo ya kuziba kwenye mifereji ya maji, kuua wanyama, na kuharibu ardhi, Heche amesema kufuatia katazo hilo serikali imefuta leseni za viwanda vinavyotengeneza mifuko ya plastiki na pia haijawapa tena leseni wale wote leseni zao zilizomaliza muda, ili kuhakikisha sheria na kanuni ya kuzuia matumizi ya mifuko ya plastiki namba 394 ya mwaka 2019.  

Heche ametoa angalizo kwa wale wote wanaohusika na ukamataji wa watumiaji wa mifuko hiyo, kutotumia nguvu ili kuepusha mikwaruzano na kutoelewana. 
Hatahivyo, amewataka wadau hao kuhakikisha wanadai vitambulisho kwa wale wote watakaofika kwenye maeneo yao ya kazi kudai wanakagua endapo wanaendelea kuuza au kutumia mifuko ya plastiki.

Kwa upande wa Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha amesema tayari kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), wameshatoa taarifa inayokwenda kwenye vituo vyote vya Kimataifa, ambapo kuna shirika la ndege linaloleta abiria Tanzania, ikitaarifu juu ya katazo la mifuko ya plastiki.

“Hii taarifa inajulikana kitaalam kama ‘timatic pre-information’ ambayo inatumwa kwenye centre zote duniani, ambapo kuna shirika la ndege ambalo linaleta abiria Tanzania itakuwa rahisi wao kupata taarifa ya katazo hilo na kuwafanya wasibebe mifuko hiyo,” amesema Rwegasha.

Pia amewataka wadau wote wanaofanya shughuli mbalimbali kwenye viwanja vya ndege kutoa ushirikiano mkubwa kuwaeleza abiria juu ya katazo hilo, na kuwaelekeza watumie mifuko mbadala, ambayo itakuwa ikipatikana kwenye maduka yaliyopo kwenye majengo ya Kwanza na Pili ya JNIA.
Kwa mujibu wa NEMC imesema watumiaji wa kawaida endapo watakamatwa na mifuko hiyo watatozwa faini ya Tshs. 30,000, kifungo cha siku saba, au vyote kwa pamoja;  wakati kwa muuzaji anapigwa faini ya Tshs 100,000 haizidi Tshs 500,000, kifungo cha miezi mitatu; na watengenezaji watapigwa faini ya kuanzia Tshs milioni 20 na haitazidi bilioni moja na kifungo cha miaka miwili. 

No comments: