Advertisements

Thursday, April 6, 2017

PROF. MBARAWA ARIDHISHWA NA KASI YA UJENZI BARABARA DODOMA-BABATI

 Mkuu wa Mkoa wa Manyara Dkt. Joel Bendera (kushoto), akizungumza na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia), mara baada ya kumkaribisha kuanza ziara ya ukaguzi wa barabara katika Mkoa huo leo.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia), akifuatilia taarifa ya ujenzi wa mradi wa barabara ya Mela-Bonga KM 88.8 inayojengwa kwa kiwango cha lami, wakati alipokagua barabara hiyo mkoani Manyara, leo, Kushoto ni Mhandisi Mshauri wa mradi huo Eng. Kini Kuyonza.
 Muonekano wa sehemu ya barabara ya Mela-Bonga KM 88.8 inayojengwa kwa kiwango cha lami na kuunganisha mikoa ya Dodoma na Manyara. Barabara hiyo inayojengwa na  Mkandarasi M/S China Railyway Seventh Group, imebaki KM 18 kukamilika.
 Mhandisi Mshauri wa ujenzi wa barabara ya Mela-Bonga KM88.8, Eng. Kini Kuyonza, akimuonesha Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia), tabaka la juu la kokoto kabla barabara hiyo kuwekwa lami, mkoani Manyara, leo.
 Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Manyara Eng. Bashiru Rwesingisa, akifafanua jambo kwa waandishi wa habari kuhusu ujenzi wa mradi wa barabara ya Mela-Bonga KM 88.8  inayojengwa kwa kiwango cha lami. Barabara hiyo inaunganisha mikoa ya Manyara na Dodoma ambayo ni sehemu ya barabara kuu ya Afrika Great North Road, inayoanzia Capetown (Afrika kusini) hadi Cairo (Misri).
 Muonekano wa Daraja la Kelema lenye urefu wa mita 220, linaounganisha Wilaya ya Chemba na Kondoa katika barabara kuu ya Dodoma-Babati likiwa katika hatua za mwisho za ujenzi.
Muonekano wa barabara ya Mayamaya-Mela KM 99.35 ambayo ujenzi wake kwa kiwango cha lami upo katika hatua za mwisho kukamilika. Barabara hiyo inaunganisha mikoa ya Manyara na Dodoma ambayo ni sehemu ya barabara kuu ya Afrika Great North Road, inayoanzia Capetown (Afrika kusini) hadi Cairo (Misri).


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa barabara ya Dodoma-Babati yenye urefu wa kilometa 188.15 ambayo inajengwa kwa kiwango cha lami na kusisitiza kuwa ujenzi huo utakamilika mwezi Oktoba mwaka huu.
Akizungumza mkoani Manyara mara baada ya kukagua barabara hiyo, Waziri Prof. Mbarawa amewataka Makandarasi M/S China Railyway Seventh Group anayejenga barabara ya Mela-Bonga KM88.8 na M/S China Henan International Cooperation Group anayejenga barabara ya Mayamaya-Mela Km 99.35 kuzingatia viwango vya ubora katika ujenzi wao kama ilivyo kwenye mkataba, ili idumu kwa muda mrefu na kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
"Barabara hii ni kiungo muhimu kwa mikoa ya Arusha, Manyara, Dodoma, Iringa na nchi za Ukanda wa Afrika, hivyo naamini kukamilika kwake kutaibua fursa nyingi za uchumi na kuchochea maendeleo ya wananchi", amesema Profesa Mbarawa.
Aidha, Waziri Mbarawa amewataka wananchi wa mkoa wa Manyara na Dodoma kutumia fursa ya kukamilika kwa barabara hiyo kujiendeleza kiuchumi na kuilinda ili iweze kudumu kwa muda mrefu kwani ujenzi wake una gharama kubwa.
Kwa upande wake Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Manyara, Eng. Bashiru Rwesingisa na Kaimu Meneja wa TANROADS mkoa wa Dodoma, Eng. Salome Kabunda wamemhakikishia Waziri Mbarawa kuwa watawasimamia Makandarasi hao ili kuhakikisha wanafanya kazi kwa ubora na kumalizika Oktoba mwaka huu kama ilivyopangwa.
Barabara ya Dodoma - Babati (km 188.15) inayojengwa kwa kiwango cha lami ni kiungo muhimu kwa uchumi wa Tanzania, kwani inaunganisha nchi za bara la Afrika kutokea Capetown (Afrika kusini) hadi Cairo (Misri).


Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

No comments: