Advertisements

Thursday, June 15, 2017

Save the Children yaadhimisha siku ya Mtoto wa Afrika jijini Dar

Meneja wa Mradi wa Elimu ya Afya ya Uzazi na Haki kwa vijana na watoto, Bi. Ellen Otaru akitoa elimu katika tukio hilo la siku ya Mtoto wa Afrika 2017, ambapo maadhimisho hayo yamefanyika mapema leo Juni 15, Manispaa ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam. Kushoto kwake ni Mratibu wa Ulinzi kwa Watoto wa Save The Children, Bi. Haika Harrison. 
Baadhi ya watoto waliokuwa kwenye shughuli hiyo ya siku ya Mtoto wa Afrika iliyofanyika Manispaa ya Kinondoni leo Juni 15.2017.
 
Mratibu wa Ulinzi kwa Watoto wa Save The Children, Bi. Haika Harrison akiwaimbisha watoto nyimbo mbalimbali
Watoto hao wakitoa burudani
 
Afisa wa Save the Children kutoka Sweden- Award Manager, SCS, Bwana. Olle Kvist akizungumza na watoto hao wakati wa tukio hilo
Afisa mipango wa Save the Children, Mzee John Komba 'JK' Kijana akizungumza jambo katika tukio hilo
Baadhi ya walimu wakifuatilia tukio hilo

Shirika la Save the Children nchini limeadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika kwa kukutana na Watoto mbalimbali wa shule za Msingi na Sekondari za Manispaa ya Kinondoni Mkoa wa Dar es Salaam. Katika maadhimisho hayo Walimu na Maafisa wa Ustawi na Maendeleo ya Jamii walishiriki na kuchangia mijadala iliyoibuliwa na watoto wenyewe kuhusu malengo ya usawa na haki ya jinsia ifukapo mwaka 2030. 
Katika tukio hilo baadhi ya shughuli walizofanya watoto ni pamoja na kuibua mijadala ya Haki na Wajibu wa Mtoto, Unyanyasaji na changamoto za kurepoti kesi za unyanyasaji. Watoto walipata majibu jinsi ya kuripoti kesi za ukatili na unyanyasaji katika kituo cha dawati la jinsia kwenye kituo cha Polisi karibu nao. 
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Bi. Halili Katani wakati wa kufungua mjadala wa Siku ya Mtoto wa Afrika, alieleza kuwa, Watoto wana haki na wajibu wa kusaidiwa pamoja na kulindwa kama wajibu wa Serikali na Jamii yote. Alitoa wito na rai kwa wazazi na walezi kuhakikisha kuwa, haki za watoto zinatimizwa na kulindwa na kuwafikia watoto zikiwemo za elimu, ulinzi na malezi bora.
 Aidha, aliwataka watoto hao wakawe mabalozi wazuri wa kutoa elimu kwa wenzao kwa kuwapa elimu waliopata katika siku ya Mtoto wa Afrika. Bi Halili aliwataka watoto Manispaa ya Kinondoni na maeneo mengine kuhakikisha wanaripoti matendo ya kikatili pindi watakapofanyiwa huko mitaani ama na walezi wao kwa kutoa taarifa kwa watu wanaowaamini ikiwemo Walimu, Maafisa wa Ustawi wa jamii na madawati ya Jinsia katika ngazi mbalimbali ikiwemo kwenye Kata, Vituo vya Polisi na sehemu zingine. Naye Meneja wa Mradi wa Elimu ya Afya ya Uzazi na Haki kwa vijana na watoto, Bi. Ellen Otaru amesema kuwa, watoto wenyewe wamebaini kutokuwa na usawa katika malezi yao huku wakilalamika kuwa wamekosa upendo kutoka kwa wazazi / walezi kutokana na aina ya maisha ya baadhi ya familia. 
“Shughuli hii ni maalum kwa watoto wa Manispaa ya Kinondoni ambapo watoto wenyewe pamoja na walimu wao wameweza kuelezea hali halisi wanayopambana nayo huko majumbani na mashuleni hivyo changamoto hizo zimepokelewa na walimu wenyewe pamoja na maafisa Maendeleo ya Jamii hatua zaidi ya utekelezaji zimewekwa bayana hapa.” Alieleza Bi. Ellen. Aidha, amewasihi wazazi kuwa na desturi ya kufuatilia watoto wao hasa mienendo ya maisha na makuzi yao kwani watoto wamekuwa na maisha mabaya katika makuzi yao. 
Shughuli zingine kwenye tukio hilo ni pamoja na watoto hao kuonyesha igizo maalum, mijadala ya wazi ya wao kwa wao pamoja na kuamsha mijadala ya kujifunza kutoka kwa maafisa wengine waliokwemo . Kwa mwaka huu Siku ya Mtoto wa Afrika Kitaifa inatarajia kufanyika hapo kesho Juni 16.2017, Mkoani Dodoma huku ikiwa na kauli mbiu “Imarisha Ulinzi na Fursa Sawa kwa Watoto”.
 Katika maadhimisho hayo, Jumla ya shule 10 za Manispaa hiyo ya Kinondoni ziliweza kushiriki huku baadhi ya shule hizo ni pamoja na : Mbezi Ndumbwi, Salasala, Mikocheni A, Ushindi, Mikocheni B Sekondari, Nakasangwe, Changanyikeni, Makongo Juu na nyinginezo. Tazama hapa tukio hilo.

No comments: