Advertisements

Friday, July 28, 2017

WASICHANA WAISHUKURU TGGA KUFANIKISHA ZIARA YA MAFUNZO NJE YA NCHI

 Wasichana wanachama wa Tanzania Girl Guides wakiwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, wakitokea kwenye ziara ya programu ya miezi sita ya mafunzo ya kubadilisha uzoefu katika masuala ya utamaduni, uongozi na maadili. Kutoka kushoto ni Ummy Mwabondo alikwenda Zambia, Edna Chembele (Zimbabwe), Elizabeth Betha (Madagascar) na Farida Mjoge aliyekuwa Uganda. PICHA, HABARI NA RICHARD MWAIKENDA;KAMANDA WA MATUKIO BLOG

WASICHANA wanne wanachama wa Chama cha Tanzania Girl Guides (TGGA) wamerejea nchini kutoka kwenye programu ya mafunzo ya miezi sita katika nchi mbalimbali za Afrika.

Wasichana hao waliokuwa kwenye mafunzo ya kubadilishana uzoefu katika mambo ya utamaduni, uongozi na maadili katika nchi za Zambia, Zimbabwe, Madagascar na Uganda wameipongeza TGGA kwa kufanikisha ziara hiyo yenye mafanikio makubwa katika maisha yao.

Walipowasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam jana kwa ndege ya Kenya Airways, walilakiwa na Katibu Mkuu wa TGGA, Grace Shaba, ndugu jamaa na marafiki huku wengine wakivishwa mashada na kupatiwa zawadi mbalimbali. Wasichana waliokwenda kwenye mafunzo hayo ni; Ummy Mwabondo, Elizabeth Betha, Edna Chembele na Farida Mjoge ambao kila mmoja anaeleza jinsi alivyonufaika na ziara hiyo.

Elizabeth Betha ambaye programu yake aliifanyia Madagascar, anaeleza kuwa Wananchi wa Kisiwa hicho utamaduni wao ni tofauti kabisa na wa Tanzania na  maeneo mengine ya Afrika, ambapo mara nyingi hutumia lugha yao ya asili na  kifaransa kama Lugha yao ya Taifa, ni wakarimu sana na wana upendo.

Anasema kuwa licha ya kuwafundisha mambo mengi ya Tanzania ikiwemo utamaduni, mapishi ya vyakula mbalimbali, lugha ya kiswahili na vivutio mbalimbali vya kitalii pia wakiwa huko walipanda  miti, kufundishana kwa uwazi masuala ya hedhi salama, kuzuia ukatili wa kijinsia pamoja na kuwapa stamina ya kujiamini na kujithamini.


Edna Chembele, ambaye alikwenda  Zimbabwe, anasema akiwa huko alijifunza kuhusu uendeshaji wa Guides, kuishi maisha ya kawaida mashuleni na mitaani, mambo ya kimila na kiutamaduni, msichana kujiamini na kujithamini.  Pia walitembelea maeneo mbalimbali maarufu nchini humo. kuwaeleza wasichana kwamba nao wana  uwezo kufanya kazi zinazofanywa na wanaume.

Farida Njope yeye alipelekwa Uganda ambako anaelezea kuwa alijifunza mambo mengi kuhusu  Utamaduni, mavazi, mapishi ya aina mbalimbali za vyakula kama vile matoke chakula kinachotokana na ndizi zilizopondwa pondwa.

Naye aliwafundisha Girl Guides wa huko, kujiamini na kujielewa kwa kuthamini usichana wao katika jamii, pia aliona tofauti ya matumizi ya Lugha ambapo Tanzania lugha ya Taifa ni Kiswahili na Uganda Lugha yao ya Taifa ni Kiingereza ambayo alidai inawasaidia sana kujieleza kirahisi katika mambo mbalimbali yakiwemo ya kimataifa.

Alishauri Serikali ya Tanzania kubadilisha mitaala Kiingereza kitiliwe mkazo kwa kuwa somo la lazima kuanzia shule za awali hadi chuo kikuu akidai lugha hiyo ni muhimu sana kwa mawasiliano kimataifa.

"Naishukuru sana TGGA kunipepeleka Uganda nimejifunza mengi. imenijenga kiakili na kuishi na watu wa aina mbalimbali nikiwa  mbali na wazazi wangu jambo ambalo sitolisahau kati maisha yangu."Alisema kwa msisitizo.

Naye Ummy Mwabondo ambaye programu ya kubadilisha uzoefu alifanyia Zambia, anasema alijifunza mambo mengi ikiwemo  

Jinsi ya kushirikiana na watu na kuongea nao hivyo kuimarisha uwezo wake wa kuzungumza jambo ambalo awali hakuwa nalo, alishiriki pia kupanda miti katika mikoa mbalimbali ya nchi hiyo.

Anasema alipata wasaa wa kuwafundisha wasichana kuwa wakakamavu na kujiamini kutenda mambo mbalimbali katika jamii ikiwemo kupinga ukandamizaji, unyanyasaji dhidi ya watoto wa kike pamoja na kutoa elimu ya hedhi salama kwa wasichana kwa kuwafanya wasiogope kuwa kwenye hali hiyo kwani jambo hilo ni la maumbile ya kibailojia.
 Girl Guides wakiwasili na mizigo yao
 Katibu Mkuu wa TGGA, Grace Shaba  (kushoto) akiwalaki Girl Guides Uwanja wa Ndege Dar es Salaam
 Ni furaha iliyoje
 Grace Shaba akiwa na Girl Guides wanaoonesha moja ya alama za TGGA
 Elizabeth na Farida wakilakiwa na ndugu zao uwanja wa ndege
 Edna Chembele akilia kwa furaha alipowaona ndugu zake waliofika kumpokea Uwanja wa Ndege Dar es Salaam
 Ummy akivishwa shada la maua na dadake
 Farida akikubatiana kwa furaha na dadake Grace Mjoge aliyefika kumlaki
 Farida Mjoge (wa pili kuli) akikata keki kwa furaha aliyoletewa na ndugu zake kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa
 Farida Mjoge akilishwa keki na dadake Grace
 Katibu Mkuu, Grace Shaba akiwa na Girl Guides hao
 Shaba akiwa na Girl Guide pamoja na ndugu waliofika kuwalaki
Farida Mjoge akimlisha keki Katibu Mkuu wa TGGA, Grace Shaba.

No comments: