Advertisements

Saturday, July 29, 2017

WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA AZINDUA MELI MBILI WILAYANI KYELA

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikata utepe kuzindua meli mbili  zilizonunuliwa na serikali ili  zihudumie wananchi katika ziwa Nyasa . Uzinduzi huo ulifanyika kwenye bandari ya Kiwira wilayani Kyela Julai 29, 2017.   Meli hizo zimejengwa na Kampuni ya Kizalendo ya Songoro Marine Transport Limited. Wapili kushoto kwake ni Naibu Spika wa Bunge, Dkt. Tulia Ackson Mwansasu na Kulia kwa Waziri Mkuu ni Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla. (PIcha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama chumba cha kulala cha mabaharia wa moja kati ya meli mbili alizozizindua kwenye bandari ya Kiwira  wilayani Kyela Julai 29, 2017. Meli hizo zimenunuliwa na serikali na zimejengwa na Kampuni ya Kizalendo ya Songoro Marine Transport Limited ili ziwahudumie wananchi katika ziwa Nyasa. 
 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akipata maelezo katika chumba cha mitambo ya  moja ya meli mbili alizozizindua katika bandari ya Kiwira wilayani Kyela Julai 29, 2017. Meli hizo zimenunuliwa na serikali na kujengwa na kampuni ya kizalendo ya Songoro Marine Transport Limited  ili ziwahudumie wananchi katika ziwa Nyasa.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa katika chumba cha nahodha wa moja kati ya meli mbili zilizonunuliwa na serikali ili zihudumie wananchi katika ziwa Nyasa, baada ya kuzindua meli hizo kwenye bandari ya Kiwira wilayani Kyela Julai 29, 2017.Kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa ndani ya moja kati ya meli mbili alizozizindua kwenye badari ya Kiwira wilayani Kyela Julai 29, 2017. Meli hizo zimenunuliwa na serikali ili ziwahudumie wananchi katika ziwa Nyasa na zimejengwa na Kampuni ya Kizalendo ya Songoro Marine Transport Limited. 
Moja kati ya meli mbili zilizonunuliwa na serikali na kujengwa na Kampuni ya Songoro Marine Transport Limited ikiondoka kwenye gati la bandari Kiwira wialyani Kyela baada ya kuzinduliwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Julai 29, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

*Ameonya zisitumike kuvushia wahamiaji haramu na dawa za kulevya


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezindua meli mbili za mizigo za Mv Njombe na Mv Ruvuma zitakazotumika katika kusafirishia mizigo kwenye ziwa Nyasa na kuonya kwamba zisitumike kama eneo la kuvushia wahamiaji haramu na dawa za kulevya.

Amesema kukamilika kwa ujenzi wa meli hizo zilizogharimu sh. bilioni 11.253 ni utekelezaji wa ahadi ya Rais Dkt. John Magufuli alizozitoa katika ilani ya uchaguzi ya CCM ya  mwaka 2015-2020 kwa lengo la kutatua changamoto ya usafiri wa abiria na mizigo katika ziwa Nyasa.

Amesema ni jambo la faraja na la kujivunia kwa Serikali na wananchi kwa pamoja kushuhudia meli zilizotengenezwa na Mtanzania, zikiwa zimekamilika tayari kwa kuanza kazi ya kuwahudumia wananchi, ambapo awali suala hilo lilikuwa likifanywa na raia wa kigeni.

Waziri Mkuu amezindua meli hizo zilizojengwa na kampuni ya Kitanzania ya M/S Songoro  Marine Transport leo (Jumamosi, Julai 29, 2017) katika bandari ya Kiwira wilayani Kyela akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Mbeya.

Amesisitiza kwamba meli hizo zitumike katika kukuza uchumi wa wananchi kwa kusafirisha mizigo na biashara halali kati ya nchi za Tanzania na Malawi na zisitumike kama eneo la kuingiza wahamiaji haramu pamoja na dawa za kulevya nchini.

Waziri Mkuu amewataka wananchi wa maeneo hayo kuwa walinzi na kuhakikisha meli hizo zifanya shughuli halali za kiuchumi ambazo zitawaletea tija wao na Taifa kwa ujumla na kamwe wasikubali zikatumika kama kichaka cha uhalifu.

“Changamoto ya usafiri wa mizigo katika ziwa Nyasa itakuwa historia kwani meli hizi zitarahisisha usafiri na kupanua wigo wa biashara kati ya Tanzania nan chi za Malawi na Msumbiji, hivyo tunamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa kutoa ahadi hii ambayo leo utekelezaji wake umekamilika.”

Awali,Naibu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) anayeshughulikia Miundombinu, Mhandisi Karim Mataka alisema ujenzi wa meli hizo ulianza Juni 2015 zina uwezo wa kubeba tani 1,000 za mizigo kwa kila moja.

Mhandisi huyo alisema mbali na kukamilika kwa mradi huo pia TPA imeingia mkataba na kampuni ya M/S Songoro Marine Transport Ltd kwa ajili ya ujenzi wa meli ya abiria yenye uwezo wa kubeba abiria 200 na tani 300 za mizigo. Mradi huo ambao upo katika hatua za mwisho kamilika utagharimu sh. bilioni 9.12.

No comments: