Advertisements

Thursday, August 3, 2017

KINACHOSABABISHA WATOTO KUZALIWA WAMEUNGANA HIKO HAPA

By Herieth Makwetta, Mwananchi hmakweta@mwananchi.co.tz

Kutotibu ugonjwa wa malaria wakati wa ujauzito, matumizi ya vyakula na vinywaji visivyo salama hasa vyenye gesi na tindikali, ni chanzo cha kuzaa watoto wenye maumbile tofauti ikiwamo pacha walioungana.

Vitu hivyo vimetajwa kuwa sababu ambazo huvuruga mfumo wa utengenezwaji wa viungo kipindi ambacho mtoto huanza kukua tumboni.

Hayo yalielezwa jana na daktari bingwa wa upasuaji wa watoto kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Zaituni Bokhari alipokuwa akitoa majibu ya vipimo vya pacha wa kike waliozaliwa hivi karibuni mkoani Morogoro wakiwa wameungana.

Watoto hao walizaliwa katika Hospitali ya Misheni ya Berega, Julai 21.

Dk Bokhari alisema hakuna sababu maalumu mpaka sasa, lakini kuna vitu ambavyo husababisha kujifungua mtoto ambaye si wa kawaida.

“Mama akiwa mjamzito anatakiwa kuhudhuria kliniki mapema kwani kuna maelekezo kuhusu anapaswa ale nini ambacho kitamjenga mtoto, kama vyakula vyenye calcium, protini, atapewa dawa ambazo zitakaza misuli ya mtoto, folic acid zinasaidia kumjenga mtoto akiwa bado tumboni,” alisema na kuongeza kuwa kuna dawa ambazo huzuia maambukizi ya watoto wakiwa tumboni kwani wapo wanaozaliwa wakiwa na malaria.

“Pia, kujifungua katika umri mkubwa, kula vyakula visivyo salama, vinywaji visivyo salama vyenye gesi na tindikali, vyote vinaweza kusababisha kupata shida, lakini wakati mwingine ni matatizo ya kurithi,” alisema Dk Bokhari.

Namna pacha walivyoungana

Akitoa majibu ya vipimo kuhusu pacha hao, Dk Bokhari alisema watoto hao wameungana sehemu ya kifua na tumbo na vipimo vya CT Scan vinaonyesha kuwa kuna baadhi ya viungo vimeshikana.

“Tulipenda pia kujua je, mishipa ya damu wanashirikiana? Imetusaidia kujua kwamba kila mmoja ana mfumo wake, mbali na vipimo vya X Ray, tukaangalia full blood picture bahati nzuri ikaonyesha upande wa damu hakuna shida, wingi wa damu ni mzuri wana damu zaidi ya 12 kwa wao siyo mbaya,” alisema Dk Bokhari.

Hata hivyo, alisema majibu ya CT Scan ya tumbo na kifua yalionyesha kuna baadhi ya viungo wanashirikiana ikiwamo ini na katika moyo kuna chemba nyingi za milango wanazoshirikiana, pia majibu yaliyotokana na kipimo cha ECO yameonyesha kuna muungano katika moyo.

ECO ni kipimo ambacho kinaangalia hali ya moyo kama uko sawa au una tatizo lolote.

“Kutokana na jinsi walivyokaa kuona moyo ilikuwa ngumu kwenye kipimo cha ECO. Wakashauri tufanye kipimo cha ST Scan ya moyo pekee na hivyo kipimo kwa sasa bado hakijafanywa,” alisema.

Kuhusu afya za watoto hao alisema wanaendelea kuangaliwa kwa ukaribu wodini walipo na wanapewa maziwa ya mama kupitia mpira.

Kutenganishwa miezi sita ijayo

Kuhusu kutenganishwa, Dk Bokhari alisema kutokana na majibu hayo kazi hiyo inaweza kufanywa baada ya miezi sita ijayo.

Alisema kwa sasa wanachokifanya ni kuhakikisha wanakuwa na afya njema kwa kumpa mama Rebecca Mwendi lishe zote zinazotakiwa ili aweze kutoa maziwa bora kwa watoto wake.

“Kwa sasa mama yupo na watoto anakaa katika chumba cha ndani kilichopo ICU, amepumzishwa huko karibu na watoto wake anakula vizuri na maziwa yanatoka vizuri na watoto wanakula vizuri, japokuwa aliathirika kisaikolojia lakini kwa sasa yupo vizuri baada ya tiba aliyopewa na wataalamu wa saikolojia,” alisema.

Alisema awali, watoto hao waliozaliwa na uzito wa kilo 4.270 walikutwa na maambukizi kwenye kitovu na mmoja alikuwa hapumui vizuri na kwamba walipofika walianzishiwa dawa ya antibiotic ya mishipa kwa ajili ya kusafisha kitovu chao kila siku. Alisema mwingine alikuwa ameumia paja wakati wa kuzaliwa na baada ya kipimo cha X Ray wataalamu wa Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) walimtibu.

Upasuaji utakuwaje?

Kuhusu mipango ya upasuaji hapo baadaye, Dk Bokhari alisema kutakuwa na wataalamu wa upasuaji wa watoto kutoka vitengo mbalimbali kutokana na namna walivyoungana na kwamba kazi hiyo itachukua saa nyingi hivyo lazima kila kitu kiwekwe sawa hasa itakapofika kutenganisha ini na moyo, wataalamu zaidi wataongezeka.

“Ni upasuaji ambao tutashirikiana na wataalamu wengi wa aina mbalimbali, madaktari bingwa wa upasuaji wa watoto katika kifua na moyo lakini pia wakati wa kuwatenganisha kuna ngozi inayofunika viungo vya ndani iko ndogo lazima itafutwe, hivyo madaktari bingwa wa upasuaji wa kurekebisha maumbile lazima wawepo,” alisema.

No comments: