Advertisements

Wednesday, August 2, 2017

SERIKALI, WENYE ULEMAVU, KUSHIRIKIANA MAANDALIZI RIPOTI YA UTEKELEZAJI WA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU NCHINI

 Picha ya Pamoja ya washiriki wa kikao kazi cha maandalizi ya ripoti ya awali ya kitaifa kuhusu haki za watu wenye ulemavu
(Waliokaa wa pili kushoto ni Bi Sarah Mwaipopo,Mkurugenzi Ofisi ya AG, wa tatu ni Bwana Erick Shitindi- Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu na wa nne ni Bwana Coomaravel Pyaneandee-Makamu Mwenyekiti Kamati ya Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya walemavu na wa nne kutoka kulia ni Bi. Josephine Lyenge-Kamishna wa Masuala ya Walemavu Nchini.
Baadhi ya washiriki wa kikao kazi -Kutoka kushoto ni Mwakilishi kutoka Mamlaka ya Udhhibiti wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, Mjumbe kutoka Ofisi ya Mwansheria Mkuu Zanzibar, Mwakilishi wa Under the Same Sun na mjumbe kutoka Chama cha watu wenye Ualbino Tanzania.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kushirikiana na watu wenye ulemavu na wadau mbalimbali katika usimamizi wa haki za watu wenye ulemavu ikiwemo kuratibu maandalizi ya  ripoti  za utekelezaji wa haki za watu wenye ulemavu nchini.
Wadau wa haki za watu wenye ulemavu nchini wanakutana Mkoani Morogoro katika kikao kazi mahsusi kinachofanyika kuanzia tarehe 31 Julai hadi 2 Agosti, kwa lengo la kuandaa rasimu ya awali ya ripoti ya kwanza ya kitaifa kuhusu utekelezaji wa haki za watu wenye ulemavu, ikiwa ni hatua stahiki katika Utekelezaji wa Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watu wenye Ulemavu.

Akifungua kikao kazi hicho, Ndugu Erick Shitindi, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Vijana,Kazi Ajira na Watu wenye ulemavu) ameeleza kua kuandaliwa kwa taarifa hiyo kutaifanya Tanzania kutekeleza Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watu wenye Ulemavu, ambao unazitaka nchi zilizoridhia mkataba huo kuwasilisha ripoti  ya kitaifa ndani ya miaka miwili tangu kusainiwa kwa Mkataba, jambo ambalo kama nchi haijawahi kulifanya.
“Maandalizi ya ripoti hii yamekuja wakati muafaka na  yataifanya Tanzania kuingia katika historia ya kutekeleza Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watu wenye Ulemavu, ikiwa ni pamoja na ukweli kuwa kama nchi tulishaanza kuchukua hatua mbalimbali zenye lengo la kuwalinda watu wenye ulemavu kwa kutunga Sheria ya watu wenye ulemavu nchini” alisema Katibu Mkuu Shitindi.
Aidha, Bwana Shitindi ametumia fursa hiyo kuipongeza Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora,Mashirika yasiyo ya Serikali  pamoja na Asasi za Kiraia kwa kazi kubwa na jitihada wanazofanya kushirikiana na Serikali katika kutekeleza haki za watu wenye ulemavu.
Kwa upande wake Bi. Sarah Mwaipopo, Mkurugenzi anayeshughulikia masuala ya Katiba na Haki za Binadamu, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameeleza kua Serikali inao wajibu Kikatiba na kisheria  kuratibu maandalizi ya ripoti na kufanya tathmini na kutolea taarifa masuala  mbalimbali ya utekelezaji wa haki za binadamu nchini kama ilivyoainishwa katika Sheria ya Utekelezaji wa  Majukumu ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali[Section 14 of the Attorney General (Discharge of Duties) Act,2005].
Akizungumza katika kikao hicho, Bwana Coomaaravel Pyaneandee, ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Haki za watu wenye ulemavu ya Umoja wa Mataifa ameeleza kuwa changamoto mbalimbali  zinzathiri  usimamizi na utekelezaji  wa haki za watu wenye ulemavu  ambazo ni pamoja na ukosefu wa takwimu sahihi za idadi ya watu wenye ulemavu; kuendelea kuwepo unyanyapaa katika jamii na ngazi ya familia; kukosekana mfumo mzuri wa elimu jumuishi; asasi za kiraia kushindwa kutumia nafasi yake kufanya kazi ipasavyo na Serikali kuendelea kutokuwepo uelewa kuhusu watu wenye ulemavu na mahitaji yao mahsusi.
Katika kutatua changamoto hizo, Serikali inaendelea kuchukua hatua kutekeleza jukumu lake la msingi la kuhamasisha na kulinda haki za watu wenye ulemavu ikiwemo kuridhia Mkataba wa Haki za Watu wenye ulemavu 2009, [the Convention on the Rights of Persons with Disabilities (ICRPD)]; kutunga Sheria ya Watu wenye Ulemavu ya Zanzibar 2006, (the Persons with Disabilities [Rights and Priviledges]Act 2006);  na  kutunga Sheria ya Watu wenye Ulemavu 2010  Tanzania Bara,  (the Persons with Disabilities Act, 2010) na uanzishaji wa Baraza la Watu wenye Ulemavu mwaka 2015.
Hatua nyingine ni  pamoja na kuhakikisha kuwa,  watu wenye ulemavu wanajumuishwa katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2025;  utambuziwa watu wenye ulemavu uliofanyika mwaka 2012 kupitia Sensa ya Watu na Makazi;  utungwaji wa Sera Mpya ya Elimu ya 2014 ambayo inahakikisha kuwa watoto wote wenye ulemavu wanapatiwa elimu na kufanya mapitio katika sekta ya afya yanayowaondolea gharama za matibabuu wazee na watu wenye ulemavu pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria wahusika wote walioshiki katika uvunjifu wa haki za watu wenye ulemavu.
Kikao kazi hicho kimeandaliwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ufadhili wa Umoja wa Mataifa na kinashirikisha wadau Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Zanzibar;Chama cha watu wenye Ualbino Tanzania; Shirikisho la Watu wenye Ulemavu Tanzania; Tume ya Uchaguzi Tanzania Bara na Zanzibar; Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora; Chama cha Walemavu wenye mtindio wa Ubongo na Chama cha Wazazi wenye watoto wenye vichwa vikubwa na mgongo wazi.
Wengine ni  Wizara ya Habari, Sanaa,Utamaduni na Michezo; Jeshi la Polisi Tanzania; Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii; Wizara ya Afya Zanzibar; Chama cha Watu walioumia Uti wa mgongo Tanzania; Under the Same Sun; Wizara inayoshughulikia masuala ya uwezeshaji wazee,watoto na watu wenye ulemavu Zanzibar; Chama cha Wasiiona

No comments: