Advertisements

Monday, October 16, 2017

PROF. MBARAWA AMCHARUKIA MKANDARASI WA SIA

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, (kushoto) , akikagua ujenzi wa jengo la abiria linalojengwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe (SIA), Waziri huyo alifanya ziara ya ukaguzi na kuangalia maendeleo yaliyofikiwa ya ujenzi huo hadi sasa. Kulia ni Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Mbeya Eng. Paul Lyakurwa.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, ametoa miezi mitatu kwa mkandarasi GM Construction anayejenga jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe (SIA), kukamilisha ujenzi huo.


Amesema Serikali hairidhishwi na kasi ya ujenzi wa jengo hilo ambalo limetumia miaka minne badala ya miwili iliyokubalika katika mkataba wa awali hivyo kumtaka mkandarasi huyo kuhakikisha analikabidhi jengo hilo ifikapo Januari 30 mwakani.


“Kushindwa kukamilisha jengo hili ifikapo mwezi Januari mwakani itakuwa ndio tiketi yako ya mwisho ya kutopewa kazi kwasababu Serikali hii inafanya kazi kwa kuzingatia ubora na muda”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.


Prof. Mbarawa amemuagiza Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Mbeya Eng. Paul Lyakurwa kusimamia kikamilifu ujenzi huo ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati na kwa ubora uliokusudiwa.




“Ujenzi wa miundombinu ya viwanja vya ndege kwa sasa unasimamiwa na TANROADS na uendeshaji wake unasimamiwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA), ikiwa ni mkakati wa Serikali wa kuongeza kasi ya ujenzi wa viwanja vya ndege na ubora wa huduma zinazotolewa katika viwanja hivyo”, amesisitiza Prof. Mbarawa.

Katika hatua nyingine Prof. Mbarawa, amekagua upanuzi wa barabara katika mji wa Tunduma unaolenga kupunguza msongamano wa magari katika eneo hilo na kuwahakikishia wananchi kuwa ujenzi wake utakamilika mwishoni mwa mwezi ujao.

Amewataka wakazi wa Tunduma kuilinda miundominu ya barabara hizo kwa kuzingatia matumizi sahihi ili kuleta usalama kwa wananchi.

Naye Meneja wa TANROADS, mkoa wa Songwe Eng. Yohane Kasaini, amemuhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kwamba barabara za michepuko zitaongezwa katika eneo la Tunduma ili kurahisisha shughuli za kibiashara na uzalishaji katika mji huo.


Prof. Mbarawa yupo katika ziara ya kukagua miundombinu katika mikoa ya Mbeya, Songwe na Rukwa.
Mhandisi Mshauri anayesimamia ujenzi wa jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe (SIA), Eng. Nyamhanga Wanda, akitoa maelezo ya mradi kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo, mkoani Mbeya.
Mkandarasi anayejenga jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe (SIA), Kannan Thiyagamoorthy, akifafanua jambo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo, mkoani Mbeya.
Muonekano wa Jengo la abiria linalojengwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe (SIA). Jengo hilo limetakiwa kukamilishwa mwishoni mwa mwezi Januari, 2018.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kushoto), akizungumza na wananchi wa Tunduma wakati akikagua upanuzi wa njia nne ya barabara ya Tunduma-Sumbawanga KM 1.45, mkoani Mbeya.
Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Songwe Eng. Yohane Kasaini (katikati), akitoa maelezo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia), wakati wa ukaguzi wa upanuzi wa njia nne ya barabara ya Tunduma-Sumbawanga KM 1.45, mkoani Mbeya.
Muonekano wa sehemu ya barabara ya Tunduma-Sumbawanga KM 1.45 inayojengwa kwa njia nne, mkoani Mbeya ili kupunguza msongamano wa magari jijini hapo.

No comments: