Advertisements

Monday, January 22, 2018

MWALIMU AFUNGUKA MADAI KUWA SI MKAZI WA KINONDONI

Mgombea ubunge wa Kinondoni kupitia Chadema, Salum Mwalimu amwajibu baadhi ya watu wanaodai kuwa yeye si mkazi wa wilaya ya Kinondoni, hivyo hana sifa za kuwa mbunge wa jimbo hilo.
Akizungumza leo Januari 22, 2018 katika mahojiano na kituo cha tevisheni cha Azam, Mwalimu ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema- Zanzibar amesema ni mkazi wa wilaya hiyo na anajua matatizo ya wananchi wake.
“Nilianza maisha Kinondoni baada ya kumaliza chuo. Nimeishi kwa miaka 14 na niko Kinondoni kwa miaka zaidi ya 30. Kwa nini Kinondoni? Si kwamba fursa zimejitosheleza lakini ninaifahamu na ninayajua matatizo ya Kinondoni kuhusu barabara, afya na elimu.”
Amesema alipomaliza Chuo Kikuu mwaka 2008 aliishi mtaa wa Togo kisha akahamia Hananasif, kufafanua kwamba madai kwamba si mkazi wa Kinondoni hazina ukweli wowote.
Kuhusu suala la kugombea ubunge akiwa na wadhifa Chadema amesema, “Ninachotafuta ni uwakilishi wa wananchi, kwa sasa ni mwakilishi ndani ya chama. Hata CCM kuna wenye vyeo viwili. Tunatafuta mwakilishi madhubuti ndani ya Bunge na katika chama chetu hakuna changamoto ya kofia moja au mbili.”
“Kama ni kofia mbili au moja mbona kuna mawaziri ambao ni wabunge, ili uwe mbunge ni lazima uwe raia wa Tanzania, lakini mbona Rais John Magufuli ni mwenyekiti wa CCM, mbona Rais wa Zanzibar ni makamu mwenyekiti wa CCM, kwa hiyo hilo la vyeo halitupi shida.”
Amesema yeye kiuhalisia ni mzaliwa wa Kikwajuni Zanzibar huku akigusia kwa kifupi kwamba anaungwa mkono na CUF.

Chanzo: Mwananchi

No comments: