Advertisements

Tuesday, July 10, 2018

OLENASHA- IFIKAPO 2019 VIJIJI 35 VITAPATA UMEME WA REA NGORONGORO

Naibu waziri wa Elimu ambaye pia ni mbunge wa Ngorongoro akizungumza na wananchi.

Na Vero Ignatus, Ngorongoro.
Naibu Waziri wa Elimu sayansi na Teknolojia ambaye pia ni mbunge wa Ngorongoro Mhe. Wiliam Olenasha amesema hadi kufikia mwaka 2019 vijiji 35 vitakuwa vimepata umeme wa REA awamu ya tatu na baadae wataendelea na maeneo mengine.

Ameyasema hayo tarehe 8 August 2018 katika kijiji cha Sakala alipofanya mkutano wa hadhara wa wananchi na kusema kuwa kila nyumba lazima itawaka umeme kinachotakiwa ni wananchi kuwa tayari kuupokea umeme huo.

Olenasha amesema tayari nguzo za umeme zinaendelea kupita katika maeneo mbalimbali lengo ni kuhakikisha ngorongoro inabadilika kuanzia miundombinu iliyopo mpaka mazingira yenyewe ya maisha ya watu na kuwa ngorongoro mpya.

“Wote ni mashahidi hili hatuzungumzi tena siyo hadithi nguzo tayari zinasambaa katika vijiji tunategemea ifikapo mwaka 2019 vijiji 35 vitakua vinawaka umeme”Alisema Olenasha.

Wakati wanaendelea kusubiria kupata wa umeme Olenasha amewataka wananchi kuendelea kujenga nyumba zenye ubora zaidi ili mazingira yabadilike kwa kuwa Ngorongoro iliyokuwa inajulikana mwanzo kwa migogoro sasa inajulikana kwa maendeleo chanya.


Wakitoa maoni yao baadhi ya wananchi wamesema kuwa kuwepo kwa umeme utawarahisishia wao kufanyashughuli za maendeleo ikiwemo kukuza kipato kwa wafanyabiashara ambao wanategemea umeme tofauti na ilivyo hivi sasa wanapata changamoto ya huduma ya matumizi ya vitu vinavyohitaji umeme.


Katika ziara Mbunge huyo ya kuwatembelea wananchi , wadau wa maendeleo pamoja na wananchi wamempongeza kwa kuendelea kutekeleza ahadi zake alizoahidi kipindi alipoomba kura ya kuchaguliwa kuliongoza jimbo hilo.

Jimbo la Ngorongoro lina kata 28 Olenasha amezitembelea zote na kuzungumza na wananchi hii ikiwa ni mara yake ya nne kufanya hivyo .

No comments: