Advertisements

Sunday, January 17, 2021

TUMEAMUA KUANZISHA MFUKO WA UMWAGILIJIA KATIKA KILA SKIMU – NAIBU WAZIRI BASHE

Naibu Waziri Kilimo Hussein Bashe akiongea na Wakulima wa Skimu ya Mwamalili katika Hamashauri ya wilaya ya Shinyanga Vijijini alipofika kuitembea na kukagua shughuli za skimu hiyo ambayo ina ukubwa wa hekari 5,000 ambayo imesimama kwa sasa
Naibu Waziri Kilimo Hussein Bashe akimsikiliza Mkulima kutoka katika Kijiji cha Seseko ambaye alimuomba Naibu Waziri kuona namna ambavyo yeye na Wanakijiji wenzake wanavyoweza kunufaika na uwepo wa Skimu ya Mwamalili baada ya ukarabati; Ombi ambalo lilikubaliwa.
Sehemu ya miundombinu ya skimu ya umwagiliaji ya Mwamalili ambayo imesimama kwa sasa katika Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Vijijini.
Sehemu ya miundombinu ya skimu ya umwagiliaji ya Mwamalili ambayo imesima kwa sasa katika Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Vijijini.
Naibu Waziri Kilimo Hussein Bashe akiwa kwenye kikao cha majumuisho pamoja naye kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Bi. Yasintha Mboneko ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mjini na Kaimu Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga Bwana Joachim Otalu wengine ni Mwakilishi wa Mrajis Mkuu wa Vyama vya Ushirika nchini Bwana Charles Malunde na Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Bwana Daud Kaali.

Naibu Waziri Wizara ya Kilimo Hussein Bashe amesema Wizara ya Kilimo kuanzia mwaka huu wa fedha wa 2020/2021 imeamua kuanzisha mfuko wa maendeleo ya umwagiliaji katika kila skimu ya nchini lengo likiwa ni kutumia fedha hizo kwa ajili ya kugharamia ukarabati wa skimu hizo pamoja na mambo yote yanayohusu maendeleo ya skimu za umwagiliaji zilizopo katika Halmashauri za Miji na Wilaya kote nchi.

Waziri Bashe amesema Mfuko wa Umwagiliaji kwa kila skimu utagharamiwa na Wakulima wenyewe walio katika ushirika wa skimu husika na kuongeza kuwa Wakulima hawatachangishwa fedha kwa ajili ya uanzishwaji wake bali utaanzishwa kwa kutumia mchango wa mazao ya wakulima.

Waziri Bashe ameongeza kuwa kila Mkulima atachangia kiasi cha mazao mfano gunia moja au mawili ya mpunga na si fedha ambapo; Mavuno hayo yatauzwa na fedha zitakazopatikana, zitawekwa benki katika akaunti ya maendeleo ya skimu hiyo ili baadae fedha hizo zitatumika katika kugharamia shughuli ndogo ndogo kama za ukarabati wa miundombinu ya skimu hiyo au kuendeleza eneo la umwagiliaji.

“Mfuko wa Umwagiliaji wa Skimu ni mfuko binafsi wa Wakulima na utasimamiwa na Wakulima wenyewe kwa kuratibiwa na Wakulima wa skimu husika”.

“Kuna skimu kadhaa zimekufa kutokana mambo kadhaa moja wapo ni kushindwa kugharamia gharama za ukarabati wa skimu kwa wakati. Wakulima wanakodishwa maeneo, wanayalima na wanapata fedha lakini linapokuja suala la kukarabati; Wakulima wanasubiri Serikali ifanya kazi hiyo. Hapana; Tumeamua kuzifufua skimu za namna hii ikiwemo skimu ya Mwamalili katika Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Vijijini ili Wakulima na wao wawe sehemu ya uwekezaji”. Amekaririwa Naibu Waziri Bashe.

Naibu Waziri Bashe ameyasema hayo mapema leo tarehe 15 Januari, 2021 wakati akikamilisha ziara yake katika mkoa wa Tabora na Shinyanga ambapo alipata nafasi ya kutembelea skimu za umwagiliaji maji mashambani katika mkoa wa Tabora na Shinyanga.

Skimu alizotembelea ni pamoja na Inala (Manispaa ya Mji wa Tabora) skimu ya Mwamalili na Nyida (Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Vijijini – Shinyanga).

Aidha Waziri Bashe ameshindwa kuzitembelea skimu ya Idudumo na Lusu (Halmshauri ya Mji wa Nzega – Tabora) kutokana na kukatika kwa huduma ya barabara kutokana na mvua kukata mawasiliano ya barabara katika maeneo kadhaa ya Halmashauri ya Nzega Mji.

Wakati huo huo Waziri Bashe amemwagiza Mtendaji Mkuu wa Tume ya Umwagiliaji nchini Bwana David Kaali kwa kushirikiana na Waandisi wa Umwagiliaji katika Ofisi za Mikoa ya Tabora na Shinyanga kuanza mara moja kufanya tathmini ya skimu zote za mkoa wa Shinyanga na Tabora hususan katika ukubwa na urefu wa mifereji, ukubwa wa maeneo ndani ya skimu hizo pamoja na kufanya tathmini ya gharama za ukarabati kwa kila skimu ili ukarabati uanze kwa kutumia fedha za ndani ili zianze kwa mtindo wa “Force Account”.

Aidha Waziri Bashe amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mazao ya Kilimo nchini (TARI) Dkt. Geofrey Mkamilo kutuma Wataalam kwa ajili ya kufanya tathmini ya afya ya udongo ili kuona mazao gani yatafaa kulimwa kwenye skimu hizo katika mkoa wa Tabora na Shinyanga na si kulima mpunga tu kama ilivyozoeleka na wakati huohuo taarifa hizo zisaidie kushauri kuhusu aina sahihi ya mbolea inayohitajika

No comments: