Advertisements

Monday, November 29, 2021

Huawei Yatoa Vifaa Vya Maabara Ya TEHAMA Kwa Chuo Kikuu Cha Dodoma

 


Kampuni ya Huawei Technologies Tanzania imetoa msaada wa maabara ya TEHAMA kwa Chuo Kikuu cha Dodoma ikiwa na nia ya kuibua mawazo ya kibunifu na kuboresha sekta ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano nchini.

 

Maabara hiyo ina miundomsingi ya kisasa na ambayo inaweza kuwasaidia wanafunzi kupata ujuzi halisi wa vitendo unaohitajika katika mapinduzi ya nne ya viwanda. Kwa zaidi ya miaka miwili, Huawei imekuwa ikishirikiana na UDOM katika masuala ya TEHAMA hasa katika kujenga uwezo na usimamizi wa maarifa ikiwa ni sehemu ya mchango wa kampuni hiyo katika maendeleo ya taifa.

 

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa maabara hiyo inayojulikana kama Huawei ICT Lab katika Chuo Kikuu cha Dodoma, Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia, Mhandisi. Kundo Andrea, aliipongeza Huawei kwa maabara ya hiyo akisema kuwa ni hatua kubwa kuelekea mabadiliko ya kidijitali nchini.

 

Alisema kwa kuwekeza kwenye TEHAMA, kwa wabia hao wawili imekua ni chachu ya ukuaji wa uchumi wa nchi kwani kuwekeza katika sekta hiyo ni muhimu kwa kuzingatia dira ya maendeleo ya 2025.

 

‘’Pongezi kubwa kwa Huawei kwa kufanikisha mpango huu muhimu. Tangu kuanzishwa kwake nchini Tanzania miaka 13 iliyopita, Huawei imekuwa na mchango mkubwa katika kutoa mafunzo na kulea wanafunzi wa ndani wa TEHAMA kupitia programu yake maarufu ya Huawei ICT Academy iliyoanzishwa mwaka 2018. Wizara itaendelea kushirikiana na Huawei kuongeza uelewa wa TEHAMA, kuweka miundombinu ya TEHAMA, na kutoa maudhui na ujuzi kwa wanafunzi kote nchini''. Alisema Eng. Kundo.

 

Mbali na maabara ya TEHAMA ya UDOM-Huawei, Naibu Waziri alizindua maabara za ukarabati na matengenezo ya simu za mikononi. Alisema UDOM ni mfano wa wazi wa taasisi zilizowekeza kwa dhati katika TEHAMA.

 

Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Huawei Bw. Tom Tao alisema kampuni yake imedhamiria kuwekeza katika kizazi kipya kwa kuwapa ujuzi muhimu unaoweza kusaidia nchi kupata maendeleo kupitia teknolojia ya kidijitali.

 

"Kipaumbele chetu ni kukuza vipaji vya vijana hasa katika tasnia ya ICT ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi na kizazi cha vijana kimeonekana kuwa rasilimali yenye ushawishi kwa nchi," alisema Bw. Tao.

 

Akizungumzia faida za Maabara hiyo iliyotolewa na Kampuni ya Huawei Technologies, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk.Leonard Akwilapo amewataka walengwa wa Maabara hiyo kuitumia ipasavyo kwa maendeleo ya nchi.

 

‘’Sote tunafahamu lengo la nchi la kufikia uchumi wa kidijitali, katika kufikia lengo hilo nchi inahitaji Wataalamu wenye ujuzi wa TEHAMA. Maabara iliyotolewa na Huawei itatusaidia kupata ujuzi wa vitendo unaohitajika katika mapinduzi ya nne ya viwanda. Nawahimiza wote mtumie fursa hii ipasavyo kwa manufaa ya nchi. Naipongeza Huawei kwa mpango huo na kuwakaribisha wadau wengine kufanya hivyo’’ alisema Dk Akwilapo.

 

Kwa upande wake, Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Profesa Leonard Mselle, aliishukuru Kampuni ya Huawei Technologies kwa kuwa mstari wa mbele siku zote katika kuchangia kuwajengea uwezo vijana wa Kitanzania.

 

Alisema UDOM inaiona Huawei kama mshirika wa kimkakati ambaye anasaidia Chuo Kikuu katika kuendeleza dira yake.

 

"Tunapanga kuweka mtambo wa kwanza kabisa wa kuunganisha vifaa vya kielektroniki kwa teknolojia ya juu zaidi, katika juhudi za kukamilisha ajenda ya nchi ya uanzishaji wa viwanda." Alisema Prof Mselle ambaye alionyesha imani kuwa katika siku za usoni chuo kikuu kitakuwa na mtambo huo.

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia, Eng. Kundo Andrea (kushoto) akizindua maabara ya TEHAMA kwa Chuo Kikuu cha Dodoma iliyotolewa kwa msaada wa Kampuni ya Huawei wakati wa hafla fupi iliyofanyika Jijini humo jana. Wanaotazama ni Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Profesa Leonard Mselle (kulia), Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Huawei Bw. Tom Tao (wa pili kulia)

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia, Eng. Kundo Andrea (katikati -walioketi) akiwa katika picha ya pamoja na Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Profesa Leonard Mselle (Kulia walioketi), Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Huawei Bw. Tom Tao (kushoto - walioketi) na wanafunzi wa chuo hicho wakati wa hafla ya uzinduzi wa maabara ya TEHAMA kwa Chuo Kikuu cha Dodoma iliyotolewa kwa msaada wa Kampuni ya Huawei iliyofanyika Jijini hapa jana.

No comments: