▪️Rais Ouattara asisitiza uongezaji thamani wa mazao
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameshiriki ufunguzi wa Mkutano wa siku mbili wa Maafisa Watendaji Wakuu barani Afrika ulioanza leo Mei 12, 2025, katika ukumbi wa hoteli ya Sofitel jijini Abidjan, Ivory Coast.
Mheshimiwa Majaliwa amemwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mkutano huo ambao umefunguliwa na Rais wa Ivory Coast, Alassane Ouattara na kuwakutanisha Maafisa Watendaji Wakuu zaidi ya 3000, wawekezaji na Wakuu wa Nchi na Serikali.
Akizungumza na washiriki wa jukwaa hilo, Rais Ouattara amesema kuwa mkutano huo utawawezesha washiriki kujadili changamoto zinazolikabili bara la Afrika na kutoa majawabu ya changamoto hizo katika maeneo ya uchumi, fedha, mazingira na biashara.
Ameongeza kuwa ili bara la Afrika liweze kuendelea kuimarisha uchumi wake, viongozi wanapaswa kuendelea kuweka na kutekeleza mikakati ya kuongezea thamani mazao yanayozalishwa.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu ameshiriki Mjadala wa Marais ulioendeshwa na Mwandishi wa Kujitegemea wa CNN, Larry Madowo na kuwashirikisha Marais wa Afrika Kusini, Rwanda, Mauritania na Makamu wa Rais wa Ivory Coast.