Kama si Mungu, tusingekutana tena leo katika kona yetu ya kuelekezana mambo haya na yale juu ya kufanya maisha yetu kwa upande wa uhusiano yawe mazuri yenye kuvutia. Hatuna budi kumshukuru yeye, maana imempendeza kabisa sisi kukutana leo na kupeana elimu hii muhimu. Karibuni sana marafiki!
Leo nahitimisha mada iliyoanza wiki iliyopita, kama inavyosomeka hapo juu. Nilianza na kisa cha msomaji wetu, ambaye alieleza jinsi anavyosumbuliwa na mwanaume ‘kicheche’ambaye hajatulia kabisa. Wiki jana niliandika vipengele vitatu, kwa faida ya ambao hatukuwa nao ni pamoja na kuangalia kama mwenzi huyo anaweza kubadilika, umri wake kama unalingana na makosa yake na kama ni mwenzi sahihi.
Sasa tunaendelea pale tulipoishia...
NANI KAKWAMBIA UNA NUKSI?
Moyo unatudanganya sana rafiki zangu, lakini kumekuwa na mawazo mengine ya kitumwa yanayotawala hisia zetu bila kujua. Eti mtu anafikiria kwamba, kukaa bila kuolewa ni nuksi! Unajua kinachotokea? Anakubali kuwa na mwanaume yeyote hata kama ana matatizo, ili awe ameondoa nuksi.
“Rafiki zangu wote niliomaliza nao shule wameshaolewa, wadogo zangu nao wameolewa, nimebaki mimi tu, siwezi kumuacha huyu mwanaume hata kama ana matatizo. Nitaendelea kuvumilia ili niondoe hii nuksi,” haya ni baadhi ya mawazo ‘mgando’ yaliyomo katika vichwa vya wanawake wengi.
Jipe moyo dada yangu, huna nuksi. Tulia, pima mambo, kisha panga maisha yako ya baadaye, kama wewe huku ukimwachia Mungu kazi ya kukutafutia mume sahihi. Unadhani kwa nguvu zako utaweza?
UNADHANI HUVUTII?
Hili ni tope lingine lililopo vichwani mwa wanawake wengi, hawajiamini. Wanadhani wao si wazuri au hawavutii, kwahiyo wanapokuwa na mwanaume, wanahisi kama wamebahatika tu, hivyo hawataki kuachia bahati hiyo! Huko ni kujidaganya.
Wapo wanaoshinda kwenye vioo wakijitazama na kuhakikisha kama kweli ni wazuri, kwa bahati mbaya vioo huwapa majibu tofauti kidogo...kwamba si wazuri kiiivyo! Halafu kuna hizi filamu na video za wasanii wa Kizazi Kipya, basi kutwa nzima mwanamke anashinda akijifananisha na msanii fulani kwenye sinema.
Akiona aina ya wanawake wanaosalitiwa kwenye ndoa za kwenye hadithi za sinema au nyimbo za wasanii husika, hujifananisha nao! Si kweli. Wewe ni mwanamke mzuri, ambaye unapendeza kwa mwanaume wako atakayekupenda. Si rahisi kupendwa na kila mtu. Unaweza kuambiwa na mpenzi wako anakupenda, lakini mtu mwingine akashangaa, kwanini mwenzi wako anakupenda!
Kila mtu ana mzuri wake jamani. Hata hivyo, ili uwe mzuri ni lazima kwanza uanze kwa kujikubali wewe mwenyewe. Kwamba wewe ni bora, unavutia na umeumbwa kipekee. Unajua ukianza kuwaza hivyo, hata tembea yako itakuwa ya kike na kujiamini, utavaa vizuri na kujipamba sawasawa. Utavutia zaidi ya unavyofikiria.
Kubwa zaidi, hata afya yako itakuwa njema, maana mawazo yako si ‘mtindi’ tena!
KUOLEWA SI KILA KITU!
Kitu kibaya kingine kinachofikiriwa na baadhi ya wanawake ni kwamba kuolewa ni kila kitu! Mwanamke akishaolewa anakuwa amemaliza kila kitu. Hili si wazo baya sana, maana heshima ya mwanamke ni kuolewa. Lakini vipi kama utaolewa na mwanaume ambaye si sahihi, akutese, akutukane, akupige, akusimange na kukufanyia kila aina ya vitu vibaya? Si utakuwa mwanzo wa kuharibu maisha yako?
Heshima ya ndoa ni kuishi kwa amani na furaha, hapo utakuwa umekamilisha kipengele hicho sawia. Kama kijisehemu hicho hapo juu kinavyosema, ni bora kuandaa maisha yako mwenyewe, uwe na uhakika na kesho yako, ukiweka malengo na kuyatimiza taratibu, ili uwe mwanamke bora. Kuwa mwanamke bora ni mwanzo wa kuelekea kuwa MKE BORA.
UMIA MARA MOJA UFURAHI MILELE
Inawezekana kichwani mwako kuna mambo mengi, likiwemo la mapenzi ya dhati kwa mwanaume wako, lakini tayari amepoteza sifa za kuwa mume sahihi, uendelee kuwa naye? Hata kama unampenda sana, moyo unakusisitizia hivyo, lakini tayari taa nyekundu inawaka mbele yako.
Fanya maamuzi, bora uumie mara moja halafu ufurahi milele, maana kukubali machozi ya mara moja na kuachana na mtu ambaye ni kikwazo kwako, kutafungua mlango wa aliye bora kuingia. Utaonekana vipi kama hutoki nje? Tafakari!
ANZA UPYA
Tua mzigo, halafu anza kwa upya. Yupo mwanamuziki mmoja amewahi kuimba; Kuanza upya si ujinga! Ni kweli kabisa, hakuna uwendawazimu wowote katika kuanza upya hasa unapogundua kwamba kuna makosa uliyoyafanya. Inamaanika kwamba anayekubali kukosea na kutaka kuanza upya, huwa bora zaidi katika hicho anachorudia, maana tayari anakuwa ameshajua kosa lake lilikuwa wapi!
UPO HAPO?
Naamini umesoma vipengele vyote kwa makini, umeelewa na una kitu cha kufanya. Ni bora kama utakuwa upo upande wangu, ingawa pia si lazima, kulingana na uamuzi wako binafsi.
Ikiwa upo upande wangu, nina hakika utakuwa umefungua ukurasa mpya wa maisha yako ya uhusiano ukiwa na furaha na nguvu mpya. Usikubali kuteswa na mapenzi!
Mada imeisha.
Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Mambo ya Mapenzi ambaye anaandikia magazeti ya Global Publishers, unaweza kuwasiliana naye kwa simu 0712 170745 au waraka pepe HYPERLINK “mailto:joeshaluwa@yahoo.com” joeshaluwa@yahoo.com kwa maoni na ushauri zaidi.