Advertisements

Saturday, July 9, 2016

SHEREHE ZA KUFUNGA MAFUNZO YA AWALI YA UASKARI MAGEREZA ZAFANA CHUO CHA MAGEREZA, KIWIRA MKOANI MBEYA

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira(katikati) katika Jukwaa akipokea Salaam kutoka kwa Gwaride la Wahitimu wa Mafunzo ya Awali ya Uaskari Magereza(hawapo pichani) katika hafla ya kufunga Mafunzo hayo leo Julai 9, 2016 Chuo cha Magereza, Kiwira Mbeya. Kushoto ni Kamishna Jenerali wa Magereza, CGP- John Casmir Minja.
Mgeni rasmi ambaye ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira akikagua Gwaride la Wahitimu wa Mafunzo ya Awali ya Uaskari Magereza, Kozi Na. 28 ya Mwaka 2016.
Wahitimu wa Mafunzo ya Awali ya Uaskari Magereza, Kozi Na. 28 ya Mwaka 2016 wakila kiapo cha Utii kwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama inavyoonekana katika picha wakiwa wakakamavu.
Mgeni rasmi akimkabidhi cheti cha sifa mmoja wa Askari Wahitimu ambaye amefanya vizuri zaidi katika nyanja ya Nidhamu katika kipindi chote cha Mafunzo hayo.
Gadi Maalum ya Gwaride la kunyakua iliyoundwa na Wahitimu wa Mafunzo ya Awali ya Uaskari Magereza wakitoa heshima mbele ya Jukwaa la Mgeni rasmi ambaye ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi(hayupo pichani).
Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Magereza wakifuatilia kwa karibu Maonesho mbalimbali katika Uwanja wa Gwaride kwenye hafla ya kufunga Mafunzo hayo.
Wakufunzi kutoka Kikosi Maalum cha Kutuliza Ghasia Magerezani(KMKGM) wakionesha onesho la kijasiri kama inavyoonekana katika picha.
Kamishna Jenerali wa Magereza, CGP - John Casmir Minja akitoa maelezo mafupi kabla ya kumkaribisha Mgeni rasmi kutoa hotuba yake ya kufunga rasmi kwa Mafunzo ya Awali ya Uaskari Magereza katika Chuo cha Magereza, Kiwira Mbeya.
Kamishna Jenerali wa Magereza, CGP - John Casmir Minja(wa pili kulia)akiwa ameongozana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi(wa pili kulia) mara baada ya sherehe za kufunga Mafunzo ya Awali ya Uaskari Magereza, Chuo cha Magereza, Kiwira Mbeya(wa kwanza kulia) ni Mkuu wa Chuo cha Magereza - Kiwira, SACP. Stanford Ntirundura(Picha zote na Lucas Mboje wa Jeshi la Magereza).

Na; Lucas Mboje, Rungwe

JUMLA ya Wahitimu 1364 wa Mafunzo ya Awali ya Uaskari Magereza wamehitimu kuwa Askari kamili wa Jeshi hilo ambapo kati yao wanaume ni 977 na wanawake 377, Mafunzo hayo yamefungwa rasmi Julai 9, 2016 katika Chuo cha Magereza Kiwira, Wilayani Rungwe Mkoani Mbeya.

Akizungumza katika sherehe za kufunga Mafunzo hayo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira amesema Askari wote wa Jeshi la Magereza nchini wanatakiwa kufanya kazi kwa kuzingatia Misingi ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kila wakati wanapotekeleza majukumu yao ya kazi.

Aidha, Meja Jenerali Rwegasira amewataka Askari wahitimu wakazingatie elimu waliyopewa wakati wa mafunzo ili kuwezesha kuongezeka kwa ufanisi katika majukumu ya Jeshi la Magereza.

Sambamba na hilo, amewaasa kudumisha nidhamu mahala pa kazi kwani nidhamu ndiyo msingi wa kufanikisha utendaji kazi mahala pa kazi hususani katika Taasisi za Kijeshi.

"Hivyo ili kudumisha utendaji wenu wa kazi, mnapaswa kuzingatia nidhamu katika utekelezaji wenu wa majukumu yenu kulingana na maelekezo mtakayokuwa mnapewa". Alisisitiza Meja Jenerali Rwegasira.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja amesema kuwa changamoto nyingi ambazo kwa kiasi fulani zimeathili utekelezaji wa majukumu ya Jeshi hilo ni pamoja na ufinyu wa bajeti, makazi duni ya maafisa na askari, uhaba wa vitendea kazi na uchakavu wa vyombo vya usafiri.

Kamishna Jenerali Minja ameongeza kuwa tayari Jeshi hilo limechukua hatua mbalimbali za kufanya maboresho kwa lengo la kufanya Jeshi la Magereza kuwa la kisasa katika kutekeleza majukumu yake kisayansi na kwa ufanisi unaotarajiwa.

No comments: