Advertisements

Monday, September 19, 2016

Tume ya Mipango yakamilisha Mafunzo ya Usimamizi wa Uwekezaji wa Umma Mikoa ya Singida, Manyara na Dodoma

Kaimu Katibu Mtendaji kutoka Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri (katikati) akitoa hotuba ya kufunga mafunzo ya Usimamizi na Utayarishaji wa Miradi ya Uwekezaji katika Sekta ya Umma kanda ya kati iliyojumuisha mikoa ya Dodoma, Singida na Manyara katika ukumbi wa VETA mjini Dodoma. Kulia ni mkufunzi wa mafunzo hayo, dkt. John Mduma kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kushoto ni Kaimu Naibu Katibu Mtendaji, Klasta ya Uchumi Jumla,Tume ya Mipango, dkt. Lorah Madete.
Washiriki wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo kutoka kwa Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume Ya Mipango Bibi Florence Mwanri.
Washiriki kundi la kwanza wakijadili maswali waliyopewa na wakufunzi kabla ya kuhitimishwa kwa mafunzo hayo Septemba 16, 2016.
Washiriki kundi la pili wakifanya maswali waliyopewa na wakufunzi mara baada ya kuhitimisha somo.
Washiriki kundi la tatu wakifanya maswali kutoka kwa wakufunzi katika ukumbi wa VETA mjini Dodoma.
Washiriki wanaounda kundi la nne wakijadili maswali juu ya utayarishaji na uchaguzi wa Miradi ya uwekezaji.

Na Adili Mhina, Dodoma.

Tume ya Mipango imehitimisha mafunzo ya Usimamizi na Utayarishaji wa Miradi ya Uwekezaji katika sekta ya Umma yaliyowahusisha maofisa mipango wa Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri kutoka Mikoa ya Singida, Manyara na Dodoma yaliyofanyika tarehe 12-16 Septemba, 2016 katika ukumbi wa VETA mjini Dodoma.

Akifunga mafunzo hayo Kaimu Katibu Mtendaji kutoka Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri aliwasihi washiriki kutumia ujuzi waliyoupata katika kuandaa, kutekeleza miradi ya Umma kwa njia za kisasa ili kuongeza ufanisi wa miradi na kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Alisema kuwa Tume ya Mipango imefanikiwa kutekeleza wajibu wake wa kuwajengea uwezo maafisa hao katika hatua zote muhimu zinazopaswa kuzingatiwa katika kufanya maandalizi, kutekeleza, kusimamia, kufuatilia na kufanya tahmini ya miradi ya maendeleo.

“Ni matumaini yangu kuwa hizi siku tano hazijapotea, mmepata elimu ya kutosha kutoka kwa wataalamu wetu katika masuala yote muhimu yanayohusu miradi ya Umma. Jukumu mlilonalo kwa sasa ni kuhakikisha mnatumia mbinu mlizofundishwa katika kutekeleza miradi ya serikali kwa usahihi ili tufikie malengo ya mpango wa pili wa maendeleo wa miaka mitano,” Alisema.

Nao washiriki wa mafunzo hayo walieleza kuwa wamepata elimu muhimu ambayo itarahisisha utendaji katika kusimamia miradi na kutoa ushauri wa kitaalamu katika ngazi mbalimbali za maamuzi.

Walieleza kuwa mafunzo hayo yamewasisitiza kutumia vigezo muhimu wakati wa kufanya uchambuzi wa kiuchumi na kifedha ili kufikia uamuzi wa kutambua miradi ipi ina manufaa na inaweza kupata mikopo katika soko la mitaji.

“vigezo kama mzunguko wa mradi (project cycle) ikiwa ni pamoja na andiko la awali (concept note), mchanganuo wa faida na hasara (cost-benefit analysis) vigezo vya kuchanganua mradi kama vile uwezo wa uzalishaji (internal rate of return) na thamani halisi ya uwekezaji (Net Present Value) vimetolewa ufafanuzi mzuri na vimeeleweka na tumevielewa” Alisema mmoja wa wakufunzi aliyejulikana kwa jina la Jemsi.

Tume ya mipango inaendelea na zoezi lake la kutoa mafunzo kwa walengwa wakuu ambao ni wataalam wa Sera na Mipango ambapo kuanzia Septemba 19 wataalamu wa mafunzo hayo watakuwa Mkoani mbeya kwa ajili ya zoezi hilo.

MWISHO

No comments: