Advertisements

Saturday, July 1, 2017

JESHI LA MAGEREZA KUTOA ELIMU YA NAMNA YA KUANZISHA KILIMO CHA KISASA KWA KUTUMIA MAENEO YENYE UFINYU WA NAFASI

  Na Christina Mwangosi, MOHA

Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza nchini Dk. Juma Malewa amesema Jeshi la Magereza nchini litatoa elimu ya namna kila Mtanzania hata aishie kwenye nyumba za ghorofa ama maeneo yenye nafasi ndogo ya kuanzisha kilimo cha mbogamboga, anavyoweza kutumia eneo dogo kuendeshea shughuli za kilimo cha mbogamboga wakati huu Maonyesho ya SabaSaba yanayoendelea katika Viwanja vya SabaSaba jijini Dar es salaam.
Kamishna Jenerali Dk. Malewa amesema kuwa pamoja na kuandaa Shamba Darasa kwa ajili ya kutoa elimu ya shughuli mbalimbali za kilimo, Jeshi la Magereza  limeandaa bidhaa mbalimbali ambazo zitaonyeshwa wakati wote wa Maonyesho pamoja na kuuzwa wakati wote wa Maonyesho hayo.

Dk. Malewa amesema miongoni mwa bidhaa hizo ambazo ziko kwenye Banda la Magereza ni samani  mbalimbali kwa ajili ya matumizi ya ofisi na nyumbani ikiwemo makabati ya vyombo na nguo,  meza na viti,  madawati kwa ajili ya shule za  msingi na sekondari, vitanda, sofa, ‘dressing table’  pamoja na viatu vya ngozi vya kike na kiume.

Amesema Jeshi la Magereza pia litauza pia majiko sanifu  yanayotumia kuni kidogo, mashuka, foronya, vikoi pamoja na sabuni zenye ubora kwa ajili ya kufua nguo ambazo zinatengenezwa katika Kiwanda cha Sabuni kilichopo Mkoa wa Mbeya.
Amesema Jeshi la Magereza katika kipindi hiki cha Maonyesho litatoa elimu ya shughuli za kilimo cha kisasa bure na kwa wale wananchi ambao maeneo yao yanafikika Wataalamu wa Magereza wanaweza kuwatembelea wananchi kwenye maeneo yao na kuwafundisha namna ya kuanzisha kilimo hicho kinachojulikana kama ‘kilimo cha jikoni’. 



No comments: