Monday, August 13, 2012

Jela miaka 30 kwa kubaka mke wa rafiki yake

Mkazi kijiji cha Mekomariro, wilayani Bunda, Nkanga Daudi, amehukumiwa na mahakama ya wilaya hiyo kutumikia kifungo cha miaka 30 jela, baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka mke wa rafiki yake.

Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Masoud Mohamed, mshitakiwa alitenda kitendo hicho Julai 26 mwaka 2009, majira ya saa 8:00 mchana, nyumbani kwa mlalamikaji.

Alidai kuwa, siku ya tukio mshitakiwa alikwenda nyumbani kwa rafiki yake na kumkuta mwanamke huyo akiwa ndani, na kutoa panga alilokuwa nalo na kumlazimisha kufanyanaye mapenzi kwa nguvu.

Alidai baada ya tendo hilo mshitakiwa alikimbia, lakini mwanamke huyo alipiga yowe la kuomba msaada na ndipo wananchi ambao baadhi yao walitoa ushahidi mahakamani hapo, walifika na kushuhudia akitimua mbio.

Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Mwandamizi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Bunda, Joackim Tiganga, alisema ameridhika pasipo shaka juu ya ushahidi uliotolewa na kutoa adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela na mshitakiwa atakapomaliza kutumikia kifungo hocho amlipe fidia ya Sh. 800,000 mlalamikaji.

CHANZO: NIPASHE

No comments: