ANGALIA LIVE NEWS

Friday, June 5, 2026



Na Mvuda Jaffer,WAF:Dar-es-Salaam


Wizara ya Afya imezitaka Mikoa na Halmashauri nchini kuimarisha huduma za chanjo kwa kubuni mbinu mpya za kuwafikia watoto ambao hawajapata chanjo kabisa (zero-dose) au ambao hawajakamilisha ratiba za chanjo, ili kuongeza kinga dhidi ya magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.

Maelekezo hayo yametolewa na Mkurugenzi wa Huduma za Tiba, Dkt. Hamad Nyembea, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif  Shekalaghe, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Tathmini ya Utekelezaji wa Huduma za Chanjo nchini unaofanyika jijini Dar es Salaam.

Dkt.Nyembea amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa huduma za chanjo kwa zaidi ya miaka mitano mfululizo ambapo walengwa zaidi ya asilimia 80 wameendelea kufikiwa, bado kuna makundi ya watoto katika jamii za wafugaji, wavuvi, maeneo ya migodini pamoja na baadhi ya maeneo ya mijini ambayo hayajafikiwi kikamilifu na huduma hizo.





“Serikali imeandaa Mpango Mkakati wa Taifa wa Chanjo wa mwaka 2026–2030 unaolenga kuhakikisha huduma za chanjo zinawafikia walengwa wote na kujenga jamii yenye kinga dhidi ya magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.”amesema Dkt.Nyembea

Aidha, Dkt.Nyembea ameeleza kuwa bado kuna changamoto ya ufuatiliaji wa magonjwa yanayozuilika kwa chanjo ikiwemo Surua na Polio, hali inayosababisha kushindwa kuwabaini mapema wahisiwa wa magonjwa hayo na kuchukua hatua stahiki za kinga na udhibiti.

“Wizara ya Afya imezitaka Halmashauri na vituo vya kutolea huduma za afya kutumia kikamilifu fursa ya usafirishaji wa sampuli kupitia Shirika la Posta pamoja na kutenga rasilimali kwa ajili ya uibuaji wa wahisiwa, uchukuaji wa sampuli na usafirishaji wake ili kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa hayo.”amesema Dkt. Nyembea

Pia Dkt.Nyembea amesisitiza umuhimu wa kuimarisha huduma za mkoba na huduma tembezi katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa huduma za afya, akieleza kuwa huduma hizo ni nyenzo muhimu ya kuwafikia walengwa ambao hawawezi kufika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.

Sambamba na hilo, Dkt.Nyembea amewaelekeza Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri kuhakikisha huduma za chanjo zinatolewa kila siku katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa mujibu wa miongozo ya Taifa, pamoja na kusimamia matumizi sahihi ya chanjo kwa kuzingatia utaratibu wa kutumia kwanza chanjo zinazokaribia kuisha muda wake.

“Mafanikio ya huduma za chanjo yatategemea zaidi uwezo wa wataalamu wa afya, viongozi wa jamii na wadau mbalimbali kushirikiana katika kuwafikia walengwa mahali walipo na kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa huduma za chanjo kutokana na changamoto za umbali, taarifa au mazingira ya makazi.”amesema Dkt.Nyembea















Thursday, June 4, 2026

DCC BELEKO ARIDHISHWA NA MWITIKIO WA WANANCHI KATIKA BANDA LA TFS WIKI YA MAZINGIRA



Na Mwandishi Wetu, Dodoma

NAIBU Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) anayesimamia Masoko na Matumizi ya Rasilimali za Misitu, DCC Salehe S. Beleko, ameridhishwa na mwitikio mkubwa wa wananchi wanaotembelea banda la TFS katika Maonesho ya Wiki ya Mazingira yanayoendelea jijini Dodoma, akisema hali hiyo inaonesha kuongezeka kwa uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.

Beleko aliyasema hayo Juni 3, 2026, alipotembelea banda la TFS katika Viwanja vya Ukumbi wa Jakaya Kikwete, ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali za utoaji elimu kwa wananchi pamoja na maonesho ya bidhaa na huduma zinazotolewa na wakala huo.

Alisema maonesho hayo ni jukwaa muhimu kwa TFS kuonesha mchango wake katika uhifadhi wa mazingira, kukuza uchumi wa kijani na kuhamasisha wananchi kushiriki katika matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.

Katika ziara hiyo, Beleko alitembelea maeneo mbalimbali ya banda hilo na kujionea elimu inayotolewa kuhusu uhifadhi wa misitu, uzalishaji wa miche ya miti, ufugaji nyuki na fursa za uwekezaji zinazotokana na sekta ya misitu.

Pia alikagua mazao na bidhaa mbalimbali zinazotokana na misitu, zikiwemo asali, nta na bidhaa zilizoongezwa thamani, ambazo zimeendelea kuvutia wageni na wadau wanaotembelea maonesho hayo.

Akizungumza na watumishi wa TFS wanaoshiriki maonesho hayo, Beleko aliwapongeza kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kutoa elimu kwa wananchi na kutangaza fursa zilizopo katika sekta ya misitu na nyuki, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kutumia maonesho hayo kufikisha ujumbe wa uhifadhi wa mazingira kwa umma.

Maonesho ya Wiki ya Mazingira yalianza Juni 1 na yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 5, 2026, yakihusisha taasisi mbalimbali za umma na binafsi zinazoshiriki kuhamasisha uhifadhi wa mazingira na matumizi endelevu ya maliasili.









BALOZI SAIDI YAKUBU AKUTANA NA UJUMBE WA TANZANIA KUTOKA COSOTA, NCHINI UFARANSA



Paris, Ufaransa

Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika UNESCO, Mhe. Saidi Othman Yakubu amekutana na ujumbe wa Tanzania kutoka COSOTA ulioshiriki mkutano wa CISAC Regional Committee for Africa (CAF), Paris.

Mhe Balozi Saidi Yakubu amebainisha kuwa: "Tumebadilishana mawazo kuhusu mustakabali wa hakimiliki, matumizi ya Akili Unde (AI), ukusanyaji wa mirabaha na fursa za uchumi wa ubunifu barani Afrika.

Nimefurahishwa kuona wataalamu wetu wakifanya tafiti za Shahada ya Uzamivu (PhD) katika maeneo muhimu ya hakimiliki na usimamizi wa mapato ya wasanii. Tanzania itaendelea kuunga mkono juhudi za kulinda ubunifu na kuhakikisha wasanii wetu wananufaika ipasavyo na kazi zao." Amesema Mhe. Balozi Saidi Yakubu.








Wednesday, June 3, 2026

HOSPITALI YA RUFAA YA KANDA YA MBEYA (MZRH) NA MAMLAKA YA BANDARI TANZANIA (TPA) ZAINGIA MAKUBALIANO YA KUWAPATIA WAFANYAKAZI TPA HUDUMA ZA MATIBABU YA DARAJA LA JUU


Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya (MZRH) na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) zimesaini rasmi makubaliano ya kutoa huduma za matibabu ya kibobezi na daraja la juu (VIP) kwa wafanyakazi wa mamlaka hiyo, huku hospitali ikitangaza mapinduzi makubwa ya kimatibabu yaliyolenga kuifanya kuwa kituo kikuu cha tiba utalii kwa nchi za SADC.

Hatua hiyo imefikiwa leo, Juni 3, 2026, baada ya pande zote mbili kuridhia na kusaini Hati ya Makubaliano (MoU) pamoja na Mkataba wa Kiwango cha Huduma (SLA). Nyaraka hizo zimesainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa MZRH, Dkt. Godlove  Mbwanji, na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Bw. Plasduce Mkeli Mbosa mara baada ya kuwasilishwa na Mashaka Karume, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TPA.

Akizungumza katika hafla hiyo, iliyofanyika mapema leo katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya Dkt. Godlove Mbwanji ameelezea kuwa ushirikiano huo ni sehemu ya mikakati ya hospitali hiyo kusogeza huduma za afya maeneo ya kazi, sambamba na kuonyesha maboresho makubwa ya kibingwa yaliyofanyika katika kuanzishwa kwa upasuaji wa moyo na kukaribia kukamilika kwa maabara ya kisasa ya uchunguzi wa mishipa ya damu (Cathlab), Kuimarika kwa huduma za upasuaji wa ubongo, moyo na mishipa ya fahamu pamoja  huduma za kibingwa za kubadilisha na kupandikiza nyonga na magoti.



Kwa upande wake, mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Ndg. Mashaka Karume, amebainisha kuwa mkataba huo unaenda kuleta mageuzi makubwa kiutendaji kwa kuondoa vikwazo vya kiafya vinavyowakabili wafanyakazi wa mamlaka hiyo, hasa wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini. 

Karume amezitaja faida kuu tatu watakazozipata watumishi kuwa ni pamoja huduma za VIP zitapunguza kwa kiasi kikubwa muda ambao watumishi walikuwa wanautumia kusubiri matibabu, Watumishi wa TPA waliopo Kanda ya Nyanda za Juu Kusini hawatakuwa na haja ya kusafiri umbali mrefu kwenda Dar es Salaam kufuata matibabu ya kibobezi, kwani huduma hizo sasa zinapatikana hapa Mbeya, pia wataalamu wa MZRH watakuwa wakifika maeneo ya kazi ya TPA kutoa elimu ya afya, mtindo bora wa maisha, na kufanya uchunguzi wa mapema wa magonjwa kama shinikizo la damu na sukari.

"Mkataba huu ni ukombozi mkubwa kwetu. Tunamshukuru Dkt. Mbwanji na uongozi mzima wa MZRH kwa mapinduzi haya ya huduma za kibingwa hapa mkoani Mbeya. Sasa wafanyakazi wetu watatibiwa kwa haraka, kwa viwango vya VIP, na watarudi majukumu yao wakiwa na afya imara ili kuendeleza uchumi wa nchi," amesema Karume.







TANAPA, WADAU WA UTALII WASUKA MIKAKATI KABAMBE KUELEKEA MSIMU MPYA WA UTALII



Na. Calvin Katera - Babati.


Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) imekutana na wadau wa utalii na uhifadhi ili kusuka mikakati itakayochagiza ongezeko la watalii na kuridhika kwa wageni watakaotembelea Hifadhi ya Taifa Tarangire. Mikakati hiyo imefanyika leo Juni 03, 2026 katika kikao cha pamoja kilichofanyika katika hifadhi hiyo inayosifika kwa tembo wengi na wakubwa nchini Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. 

Kikao hicho ni hatua ya maandalizi kuelekea msimu mpya wa utalii (High season) unaoanza mwezi Juni hadi mwishoni mwa mwezi Januari kila mwaka. 

Katika kikao hicho Mkuu wa Kanda ya Kaskazini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Dkt. Beatrice Kessy alieleza kuwa wadau na wawekezaji kwa kushirikiana na hifadhi wanapaswa kutoa huduma bora zitakazoongeza hamasa na kuridhika kwa wageni ili waende kuisemea vizuri hifadhi na Taifa kwa ujumla. Kama inavyojulikana katika soko la utalii mgeni anaporidhika kwa huduma na mapokezi mazuri anaporudi nchini kwake huwa ni balozi mzuri kwa yale mema aliyofanyiwa. 

Sambamba na hilo Kamanda Kessy aliongeza; “Hifadhi ya Taifa Tarangire imeboresha miundo mbinu ya barabara na malazi. Aidha, ikolojia imeendelea kuimarishwa ili wanyamapori wapate malisho ya kutosha na wanyama waonekane kwa urahisi, kwani malisho yanapokuwa mengi wanyamapori hawatembei umbali mrefu hivyo kuwawezesha watalii kuona wanyama wote waliowakusudia katika safari yao.

Kwa upande wake, Bw. Loseku Dorop kutoka Kampuni ya Conserve Safari alieleza kuwa wadau wa utalii wawekeze nguvu katika matumizi ya nishati safi, vitambulisho kwa watoa huduma wa makampuni ya kitalii na usafi wa mazingira kwa kuepuka kurusha taka, kwani taka huathiri mazingira na wanyamapori.

Kwa upande wake Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Tarangire Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Dkt. Tutindaga George alieleza kuwa licha ya hifadhi hiyo kushika nafasi ya tatu kwa mapato na wingi wa watalii, mikakati yao ni kuwa ya pili au ya kwanza kuzipiku Hifadhi za Taifa Serengeti na Kilimanjaro.

Kikao hicho mbali na kuweka mikakati kuelekea msimu mpya wa utalii pia ni utaratibu wa hifadhi hiyo kukumbushana kanuni na taratibu mbalimbali za uhifadhi na kuwahamasisha wadau hao kuendesha utalii endelelevu kwa maslahi yao binafsi na maslahi ya Taifa kwa ujumla.








Tuesday, June 2, 2026

KUJIANDAA NA MSIMU WA UTALII: WATUMISHI WANOLEWA USIMAMIZI WA MAPATO ,HUDUMA BORA NA USIMAMIZI WA SHUGHULI ZA UTALII KATIKA HIFADHI ZA TAIFA



Mafunzo ya usimamizi wa mapato na utoaji huduma bora  yanafanyika kuanzia  tarehe 1/6/2026 hadi 4/6/2026 katika Hifadhi ya Taifa Tarangire .

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa kwa ushirikiano wa Kitengo cha Maendeleo ya Biashara TANAPA,Kanda ya Kaskazini na Hifadhi ya Taifa Tarangire yamejumuisha washiriki kutoka Hifadhi tano (5)ambazo ni Tarangire,Ziwa Manyara ,Arusha , Mkomazi na Kilimanjaro. 

Akifungua Mafunzo hayo Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Tarangire ,Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Dr Tutindaga George alisema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuimarisha uwezo wa watumishi katika kusimamia ukusanyaji wa mapato , kutoa huduma bora na kusimamia shughuli za utalii hasa tunapoelekea msimu mkubwa wa utalii. 

Kupitia mafunzo hayo washiriki wamejifunza mbinu mbalimbali za uthibiti wa mapato pamoja na kufanya ukaguzi katika hoteli na kambi za kitalii pamoja na kujifunza usimamizi wa shughuli za utalii ndani ya Hifadhi. 

Hatua hizi zinaendelea kuimarisha uwajibikaji , ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ,huduma bora na uhifadhi endelevu wa rasilimali za utalii nchini.

Mafunzo haya yataendelea kwa Hifadhi zingine zilizopo Magharibi, Mashariki na Kusini mwa nchi ili kuweza kujipanga na kuweka mikakati thabiti katika utoaji wa huduma za utalii.