ANGALIA LIVE NEWS

Thursday, July 9, 2026

TFS KUIMARISHA UREJESHAJI WA MISITU ILIYOHARIBIWA



Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeanza kutekeleza ahadi ya kurejesha ardhi ya misitu iliyoharibiwa kwa kiwango kikubwa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha ardhi inaendelea kuwa hai na yenye uwezo wa kuhimili mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Akizungumza katika kikao kazi cha kujadili Mradi wa Urejeshaji endelevu wa Mazingira na Uhifadhi wa Bayonuai, Naibu Katibu Mkuu Muungano kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdallah Mitawa, amesisitiza umuhimu wa kutunza mazingira, akieleza kuwa ardhi ndiyo msingi wa maisha na nguzo muhimu ya maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Vyanzo vya Mbegu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Dkt. Fortunata Senya, amesema ushirikishwaji wa wadau, taasisi na mashirika mbalimbali ni nguzo muhimu katika kuhakikisha lengo la kurejesha ardhi iliyoharibiwa linafikiwa kwa ufanisi na kwa matokeo endelevu.

Naye Mkurugenzi wa Uzalishaji wa Mbegu za Miti wa TFS, Dkt. Hamza Katety, amesema kikao kazi hicho kinatarajiwa kutoa majawabu na mapendekezo yatakayosaidia kuimarisha utekelezaji wa mpango wa urejeshaji wa ardhi ya misitu na kuhifadhi bayonuai nchini.











RAIS DKT. MWINYI: TAMKO LA PAMOJA CCM NA ACT-WAZALENDO LAFUNGUA NJIA YA UTEKELEZAJI WA SERIKALI YA UMOJA WA KITAIFA



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Tamko la Pamoja kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo linafungua njia ya utekelezaji wa uundaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa na kuimarisha amani, umoja, mshikamano na maendeleo ya Zanzibar.

Rais Dkt.Mwinyi ameyasema hayo baada ya kushuhudia utiaji wa saini wa ajenda zilizokubaliwa kwa pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi kufuatia Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa Zanzibar baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo katika Viwanja vya Ikulu Zanzibar leo tarehe 09 Julai, 2026.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema maridhiano hayo yanaonesha dhamira ya viongozi kuweka mbele maslahi ya taifa, huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote kuhakikisha mchakato huo unadumisha utulivu, utawala bora na maendeleo endelevu.


Halikadhalika, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongeza hatua hiyo akieleza kuwa maridhiano hayo yanafungua ukurasa mpya wa kuimarisha umoja, utulivu na mshikamano miongoni mwa Wazanzibari, na ni ishara ya ukomavu wa kisiasa na dhamira ya kujenga mazingira ya amani na maendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Taifa, Mhe. Othman Masoud Othman, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa kuendeleza mchakato wa maridhiano, akisema umefungua njia ya kupatikana kwa ufumbuzi wa kudumu wa changamoto za kisiasa Zanzibar.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi; Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume na Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein; Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla; Viongozi wa vyama vya siasa, Viongozi wa dini, Viongozi wa Serikali za SMT na SMZ, Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Mabalozi, Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa pamoja na wananchi mbalimbali.


















KAMISHNA WA UHIFADHI TANAPA AANZA KAZI KWA MAAGIZO SITA YA WAZIRI KIJAJI

 

Na. Calvin Katera - Arusha.


Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) ametoa maagizo sita kwa Kamishna wa Uhifadhi TANAPA Massana Mwishawa leo Julai 09, 2026, jijini Arusha alipokuwa akiongoza zoezi la uapisho kwa aliyekuwa Naibu Kamishna wa Uhifadhi baada ya kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan Julai 02, 2026 kuchukua nafasi ya Kamishna wa Uhifadhi (Mstaafu) CPA Musa Nassoro Kuji aliyemaliza muda wake.

Akizungumza katika hafla ya uapisho huo Waziri Kijaji amemwelekeza Kamishna Mwishawa kusimamia miundombinu ya hifadhi, kuvutia wawekezaji, kubuni bidhaa mpya za utalii, kusimamia mapato, kuimarisha uhusiano na jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi bila kusahau nidhamu, uadilifu, weledi, ustawi wa watumishi na kusimamia maslahi yao kwa wakati.

Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini TANAPA, Mkuu wa Majeshi (Mst.) Jenerali George Waitara alieleza kuwa Bodi itaendelea kutoa ushirikiano wa dhati na ushauri wakati wote ili kufanikisha adhma ya kuendeleza sekta ya maliasili na utalii.

Pia alisisitiza kuwa uendeshaji wa shughuli za Shirika zifanywe kwa uwazi na utoaji wa mrejesho uwahusishe maafisa na askari ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi Massana Gibril Mwishawa alibainisha kuwa Hifadhi za Taifa ni hazina kubwa ya kiikolojia, kiuchumi, na kijamii na zinachangia kwa kiasi kikubwa katika mapato ya serikali na miradi ya kimkakati kama uzalishaji wa umeme.

Akimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini na kumpa dhamana hiyo, Kamishna Mwishawa aliahidi kutekeleza majukumu yake kwa uzalendo, uadilifu, uwajibikaji, nidhamu, na weledi akishirikiana na watumishi wenzake.

Hafla hii imehudhuriwa na wakuu wa taasisi za uhifadhi ikiwemo NCAA, TFS na wawakilishi kutoka TAWA, viongozi wa Serikali, wadau wa uhifadhi na utalii, viongozi wa dini, Maafisa na Askari wa TANAPA.











Tuesday, July 7, 2026

DIB YALETA UNAFUU KWA MABENKI

  

Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano ya Umma wa DIB, Lwaga Mwambande pichani.


Na Hellen Ngoromera


BODI ya Bima ya Amana nchini (DIB) imeanzisha utaratibu mpya wa kuzipunguzia hasara benki zinazoingia kwenye migogoro au changamoto za kiuendeshaji.

Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano ya Umma wa bosi hiyo Lwaga Mwambande amesema hayo Julai 6 Jijini Dar es Salaam katika Maonyesho ya Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya Sabasaba yanayoendelea katila viwanja vya  Sabasaba.

Amesema badala ya kusubiri mpaka benki ife ndipo bodi yake ilipe fidia wameona ianzishe utaratibu huo ambao ni mzuri na wenye manufaa makubwa.

"Badala ya kusubiri mpaka benki ife ndipo tulipe fidia sasa tuna jukumu la kupunguza hasara kwa benki zinazopita changamoto hizo," amesema Lwaga.

Ameeleza kwamba utaratibu huo umeanza katika mwaka mpya wa fedha ulioanza Julai na kwamba Benki Kuu ya Tanzania(BoT) ndiyo yenye jukumu la kushughulikia jambo hilo. Hata hivyo ameweka wazi kwamba hadi sasa hakuna benki iliyofikia katika hali hiyo.

"Mpango huo ni mzuri na wenye manufaa kwani ni nafuu kuliko kulipia fidia. "Wataalamu wanasema kupunguza hasara wakati mwingine ni nafuu kuliko kulipa fidia, unaweza kukuta benki inahitaji Shs.mlioni 500 ili irejee kwenye utendeji wa kawaida na mkiiacha ikafa mnaweka mkakuta fidia inakuwa hadi milioni 2," amesema Lwaga.

Amebainisha kuwa katika vitu ambavyo bodi hiyo inajitahidi  ni kuwa mwangalifu katika mfuko wa amana. 

Bodi ya amana imeanzishwa kwa lengo la kukinga amana za wananchi katika benki na taasisi za kifedha na inapotokea benki ambazo wananchi hao wanaweka fedha zao zinafilisika amana zao zingawiwa  kikamilifu.

Monday, July 6, 2026

TAMASHA LA SANJO YA BUSIYA 2026 LAZINDULIWA RASMI, WATANZANIA WAHIMIZWA UPENDO NA AMANI

 


Na. Matukio Daima Media App, Kishapu, Shinyanga.


MTEMI wa Busiya Ntemi Makwaia wa iii amezindua rasmi tamasha la Sanjo ya Busiya  maarufu kama  Sabasaba (7-7) huku Wananchi wakihimizwa upendo na Amani.

Uzinduzi huo umefanyika jioni ya Julai 5,2026  umefanyika katika eneo la Ikulu ya Busiya  na Mtemi wa Busiya Ntemi Makwaia wa iii pamoja na Machifu wengine kutoka meeneo mbalimbali ikiwemo: Kilimanjaro, Morogoro, Dodoma, Tabora, Mara, Mwanza, Ruvuma, Mkoa mwenyeji wa Shinyanga na Taifa la  Afrika Kusini, ambao kwa pamoja walipata pia kutoa neno la Shukrani.

Awali, Ntemi Makwaia iii alishuhudia matukio mbalimbali ya tamasha hilo ikiwemo ngoma za asili kutoka Jamii ya Wasukuma.



Mtemi wa Busiya Ntemi Makwaia wa iii  akivikwa mavazi maalum ya kiutawala


Aidha, amewatakia Wananchi kuendelea kupendana na kudumisha amani sambamba na kuendeleza utamaduni.

Tamasha hilo limekuwa likikusanya umati mkubwa kutoka ndani na nje ya Nchi wakifika kwa wingi kushuhudia matukio ya Ngoma za asili na kila za Jamii ya Wasukuma kutoka Busiya na maeneo jirani.

Ambapo pia Wananchi wanapata fursa za  huduma za afya ikiwemo kupimwa Afya zao bure kutoka kwa Watalaam na Madaktari wa Afya Check, pamoja na Hospitali ya jirani.

Tamasha hilo linatarajiwa kufika kilele chake Julai 7, 2026 ambapo shughuli za Ngoma , vyakula vya asili na manunuzi ya bidhaa mbalimbali zinaendelea kunogesha tamasha hilo kila mwaka tokea kuanzishwa kwake miaka 16 iliyopita.