ANGALIA LIVE NEWS

Wednesday, June 10, 2026

TFS YAENDELEA KUIMARISHA USTAWI WA WATUMISHI KUPITIA ELIMU YA AFYA YA AKILI, VVU NA MAGONJWA SUGU YASIYOAMBUKIZA


Na Mwandishi Wetu, Dodoma


Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeendelea kutekeleza juhudi za Serikali za kuimarisha afya na ustawi wa watumishi wa umma kwa kutoa mafunzo kuhusu udhibiti wa VVU na UKIMWI, magonjwa sugu yasiyoambukiza, afya ya akili na dhana ya ujumuishaji wa anuai za jamii mahali pa kazi.

Mafunzo hayo yaliyofanyika leo Juni 06,2026 katika Ukumbi wa Mesuma jijini Dodoma yalifunguliwa na Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayesimamia Huduma Saidizi na Utawala wa TFS, DCC Emmanuel Kiboko, na kuwashirikisha jumla ya wahifadhi 116 kutoka Makao Makuu ya TFS na ofisi mbalimbali za Kanda ya Kati.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, DCC Kiboko alisema Serikali imeweka miongozo mbalimbali inayolenga kuimarisha ustawi wa watumishi wa umma, ikiwemo Mwongozo wa Kudhibiti VVU na UKIMWI Mahali pa Kazi, hivyo taasisi zinapaswa kuendelea kutoa elimu na kuhamasisha watumishi kujali afya zao.

Alisema afya ya akili imeendelea kuwa moja ya masuala muhimu yanayohitaji kupewa kipaumbele katika maeneo ya kazi kutokana na mchango wake katika ustawi wa watumishi na ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi.

“Ni muhimu kwa watumishi kuelewa changamoto mbalimbali zinazoweza kuathiri afya ya akili na namna ya kukabiliana nazo. Elimu hii inasaidia kujenga mazingira bora ya kazi na kuimarisha mahusiano mahali pa kazi,” alisema DCC Kiboko.

Aliongeza kuwa mafunzo hayo yanatoa fursa kwa watumishi kupata uelewa kuhusu vihatarishi vya afya ya akili, mbinu za kudhibiti msongo wa mawazo pamoja na umuhimu wa kupata ushauri wa kitaalamu pale inapobidi.

DCC Kiboko alibainisha kuwa mazingira ya kazi na changamoto za kijamii zinazowakabili watumishi zinaweza kuwa chanzo cha msongo wa mawazo, hivyo ni muhimu kwa taasisi kuendelea kuwekeza katika elimu na mifumo ya usaidizi inayolenga kulinda afya ya akili ya watumishi.

Kwa upande wake, Daktari Hafidh Amir kutoka Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) aliwahamasisha watumishi kujitokeza kupima VVU na magonjwa sugu yasiyoambukiza ili kufahamu hali zao za afya na kupata huduma mapema pale inapohitajika.

Alisema TACAIDS imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi na watumishi wa umma kupitia maeneo ya kazi na mikutano mbalimbali ili kuongeza upatikanaji wa huduma za kinga, upimaji na ushauri nasaha.

“Tunawahimiza watumishi kutumia fursa hizi muhimu za kupima afya zao. Utambuzi wa mapema ni hatua muhimu katika kinga na matibabu ya magonjwa mbalimbali,” alisema Dk. Amir.

Awali, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi na Meneja wa Rasilimali Watu wa TFS, SACC Bahati Mtomaye, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Mwongozo wa Serikali wa Kudhibiti VVU, UKIMWI na Magonjwa Sugu Yasiyoambukiza Mahali pa Kazi wa mwaka 2014.

Alifafanua kuwa mafunzo hayo yanalenga kuimarisha afya za watumishi, kuongeza uelewa kuhusu afya ya akili, kudhibiti msongo wa mawazo na kuhamasisha mazingira jumuishi yanayowezesha kila mtumishi kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

“TFS inaendelea kutambua kuwa rasilimali watu ndiyo msingi wa mafanikio ya taasisi. Hivyo, uwekezaji katika afya, ustawi na maendeleo ya watumishi ni sehemu muhimu ya kuhakikisha huduma bora zinaendelea kutolewa kwa wananchi,” alisema Mtomaye.

Kupitia mafunzo hayo, washiriki walipata elimu kuhusu kinga na udhibiti wa VVU na UKIMWI, magonjwa sugu yasiyoambukiza, afya ya akili, usimamizi wa msongo wa mawazo pamoja na umuhimu wa kujenga mazingira ya kazi yenye ushirikiano, heshima na ujumuishaji kwa watumishi wote.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati mpana wa TFS wa kuimarisha ustawi wa watumishi wake, kutambua mchango wao katika uhifadhi na usimamizi endelevu wa rasilimali za misitu na nyuki, na kuhakikisha taasisi inaendelea kuwa na nguvu kazi yenye afya, tija na uwezo wa kutoa huduma bora kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.












WATUMISHI MUHIMBILI WAASWA KUZINGATIA MUDA NA MAADILI YA KAZI ILI KUIMARISHA HUDUMA KWA WANANCHI



Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imeendelea kusisitiza umuhimu wa watumishi wake kuzingatia muda na maadili ya kazi ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Akitoa mada wakati wa Kikao cha 31 cha Baraza la Wafanyakazi wa MNH, Balozi Omary Kashera NDC, amesema matumizi sahihi ya muda ni muhimu katika kupunguza changamoto za kiutendaji na kuongeza tija mahali pa kazi. Pia amewahimiza watumishi kutekeleza majukumu yao kwa weledi, kuzingatia maadili ya utumishi na kulinda usiri wa taarifa za wagonjwa kwa kufuata taratibu zilizowekwa.

Mada hiyo ni sehemu ya kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa MNH linalofanyika chini ya kaulimbiu isemayo, "Pamoja tunajenga Muhimbili Imara, Bunifu na yenye huduma bora kwa kila mwananchi," likitoa fursa kwa watumishi kujifunza na kujengewa uwezo katika maeneo mbalimbali yanayochangia kuboresha utendaji na utoaji wa huduma.







MFAHAMU ZINJANTHROPUS BOISEI /PARANTHROPUS BOISEI



Ukifika Makumbusho ya Taifa la Tanzania jitahidi sana kutana na Zinjanthropus boisei, mmoja wa Zamadamu wanaovutia zaidi ulimwenguni kote, anayejulikana kwa lishe yake maalum na maumbile ya kipekee sana kimwili hasa fuvu  lake la kichwa na taya lake la mdomo wa chini na juu (upper and lower jaw).

Aliishi takriban miaka milioni 2.3 hadi 1.2 iliyopita katika eneo bonde  la Olduvai Tanzania. Zinjanthropus boisei alistawi katika savanna na mazingira ya misitu ya wazi, akitegemea uwezo wake wa ajabu wa kutafuna chakula kigumu kama mbegu na mizizi ili kuishi. 

Magego yake makubwa, na taya lake pana yaliunganishwa na misuli imara (masseter and temporalis muscles) iliyojishikiza kwenye fupa la upanga wa kichwa (suggital crest) ili kusaidia kutafuna chakula kigumu: vyenye nyuzi kama vile mizizi na mbegu ambazo *spishi zingine za Zamadamu* zingeweza kuepukwa. Ikumbukwe kwamba kuna nyakati Mheshimiwa Zinjanthropus boisei aliishi  sambamba na Homo habilis wakiwa pamoja katika mazingira hayo ya Olduvai.

Tofauti na mwenzake Homo habilis, Zinjanthropus boisei huenda hakutegemea sana zana za mawe, badala yake alitegemea viungo vyake vya  kimwili ili kuchakata chakula kwa ufanisi hasa mikono na mdomo. ZINJ  huyu mwenye nguvu thabiti leo amepumzika zake yuko hapa *Makumbusho ya Taifa Dar-es-Salam*, anatunzwa vema na amehifadhiwa kisasa kabisa. Ukimtizama ndani ya *kasha lake la dhahabu* akiwa amevaa *medali yake aliyotunukiwa*,  anaonesha utofauti wake yeye na  Zamadamu wengine wa awali na mageuzi ya njia nyingi alizozichagua yeye katika jitihada za kuendelea kuishi.

Kila kukicha mifupa yake husimulia hadithi ya ustahimilivu na utaalam, inayoonyesha jinsi Zamadamu wa mwanzo walizoea mazingira yao muda mrefu kabla ya ugunduzi moto, uwindaji, au zana za mawe na  chuma kuanza kuenea.

🌍 Kutoka Makumbusho  ya Taifa la Tanzania Muheshimiwa Paranthropus boisei anatukumbusha kwamba mageuzi ya binadamu (human Evolution) si mstari ulionyooka bali ni hadithi ya majaribio mengi, yaliyozaa matawi ya kuishi kwao Kutoka shina moja la mageuzi hadi matawi tofauti. Yapo matawi yaliyotoweka na mengine yalifanikiwa kuwa endelevu. Moja ya tawi lililotoweka ni hili la Babu Zinj. 

Kwa kifupi mifupa ya Zinjanthropus boisei inaongea maneno mengi, siwezi simulia yote nikamaliza. Nawakaribisha sana mtembelee Makubusho ya Taifa la Tanzania muonane naye *Zinj* mwenyewe,  msikilize wenyewe kwakuwa  *mifupa yake huwa inaongea*.

KISA NA MKASA TUKIO LA MKULIMA SAID MWAMWINDI NA RC WA IRINGA DKT. WILBERT KLERUU 1971

 


Ni miaka 55 imepita toka Mnyalukolo, Said Abdallah Siulanga Mwamwindi, ammimimie risasi na kumuua aliyekuwa Mkuu wa mkoa wa Iringa, marehemu Dr. WILBERT KLERUU. Mauaji hayo yaliyokea tarehe 25/12/1971 kijijini Mkungugu, Isimani, Iringa.

Dr. Wilbert Kleruu alikuwa ni mzaliwa wa Mwika, Kilimanjaro ambaye alikuwa ni mmoja wa Watanzania wachache wakati huo waliokuwa na shahada ya uzamivu(PHD) ya uchumi wa kijamaa. 

Dr. Kleruu alikuwa ni kipenzi cha Baba wa Taifa, Mwalimu JK Nyerere, kutokana na weledi na utendaji wake usio na mfano. Mwanazuoni mwa mwaka 1971, DR. Kleruu alikuwaamehamishiwa mkoani Iringa kutokea Mtwara. 

Dr. KLERUU alikuwa ni kiongozi machachari sana na ilikuwa kawaida kwake na alikuwa hana hiana kuwafokea hadharani watumishi wa umma wazembe. Kwa hakika,  Dr. KLERUU alikuwa mbabe sana. Akiwa Iringa, kuna wakati gari yake ilipigwa "overtake" na gari hilo lililompiga"-overtake" likamziba kwa mbele.

Kufumba na kufumbua, Dr. KLERUU alishuka kama komandoo na kwenda kumuwasha vibao dreva wa gari hilo! Dr. KLERUU, mara kwa mara, alipenda kuwafokea watu kwa kuwaambia "Hamnijui Mimi? Kawaulizeni watu wa Mtwara"  na yeye hakuwa mtu wa kukaa ofisini kama viongozi wengi wa wakati huo, bali alijumuika na wananchi na kufanya nao shughuli za maendeleo bega kwa bega ambapo ilikuwa ni kawaida kwake kushika jembe kwa masaa kadhaa bila kula!.

Kipindi hicho kulikuwa na kampeni kubwa ya kuwafanya wananchi walime mashamba ya pamoja na hivyo wakulima waliokuwa na mashamba makubwa walinyang'anywa, kitendo ambacho hakikuwapendeza Wanyalukolo waliokuwa matajiri wenye  mashamba makubwa ya mahindi. 

Dr. KLERUU alihamishiwa Iringa ili akatekeleze mpango huo wa serikali na alipofika tu akatangaza kwamba mashamba yote binafsi yanapaswa kuwa ya ujamaa kufikia Novemba  1971.   

Bw. MWAMWINDI alihamia eneo la  Mkungugu, Isimani mwaka 1954 akitokea Iringa mjini alikokuwa dreva. Alianza kilimo kidogo kidogo hatimaye akawa na mashamba makubwa ya mahindi ya hekari  takriban 160. Akawa analima mashamba yake kwa trekta katika eneo hilo ambalo awali lilikuwa ni pori. Kipindi hicho, hakukuwa na sehemu Tanzania iliyokuwa ikizalisha mahindi mengi kama Isimani.

Jumamosi ya tarehe 24/12/1971, Dr. KLERUU alitembelea mashamba mbalimbali maeneo ya Tarafani, Igulu na Ndolela kuhamasisha kilimo cha pamoja. Kesho yake, Jumapili ya tarehe 25/12/1971, Dr. KLERUU( ambaye hakuwa na  Jumapili wala skukuu) aliendelea na shughuli hizo za kutembelea mashamba ya wakulima.

Muda wa saa 11 jioni, Dr. KLERUU  alifika kwenye shamba la MWAMWINDI  na kumkuta akilima kwa trekta lake. Pamoja nae kulikuwa na mtoto wake(Mohamed) na watu wawili aliowaajiri( Yadi Chaula na Charles Mwamalata), Bw. Joseph Kusava ambaye ni mkwe wake pamoja na wake zake waliokuwa wakishirikiana nae kulima siku hiyo. Dr. KLERUU alifika shambani hapo akiendesha gari lake binafsi aina ya Peugeot 404 rangi ya bluu na ubavuni ikiwa imeandikwa RC-Iringa. 

Baada ya kushuka alimfuata moja kwa moja MWAMWINDI na kuanza kumuhoji maswali mengi kwanini hataki mashamba yake yawe ya ujamaa. Akamwambia "Unafanya nini hapo?"Shuka shenzi we". MWAMWINDI akamuuliza "kwanini unanitukana?" Dr. KLERUU akamjibu "Funga mdomo wako, n'ge n'ge n'ge nini? Kwanini nawaambia hamsikii? Blood fool". 

Katika eneo hilo walikuwa wao wawili tu kwani watu wengine walikuwa mbali kidogo. Dr. KLERUU aliyekuwa na kawaida ya kutembea na kifimbo kidogo akakitumia kumchomachoma nacho MWAMWINDI. 

MWAMWINDI akafura sana hivyo akaanza kwenda ndani kupitia eneo la makaburi ya baba yake na ndugu wengine huku Dr. KLERUU akimfuata na alipoyaona makaburi akasema "Tazama unaendelea kujenga nyumba za kudumu". MWAMWINDI akamjibu "Hizi sio nyumba, ni mahali ninapozika ndugu zangu".  Dr. KLERUU akajibu "Ni mahali unapozikia mirija wenzio, mbwa we!".

Mnyalukolo MWAMWINDI akawaamehamaki sana. Akasema "Swela", akaingia ndani akachukua gobore akatoka nalo nje na kumfyatulia risasi Dr. KLERUU ambaye alianguka na kufariki hapohapo!!! MWAMWINDI aliuchukua mwili wake akauweka kwenye buti ya gari ya Mkuu huyo wa Mkoa, akachukua na kofia ya Pama ya Mkuu wa Mkoa akaivaa yeye na kuanza safari ya kilometa 40 kwenda Iringa mjini.

Mjini Iringa, watu walishangaa kuona gari ya Mkuu wa mkoa inapita upande wa kulia kwa vile mtaa wa Jamatini ulikuwa ni "One way" lakini wakahisi huenda Mkuu wa mkoa ana dharura. Saa 1 jioni, MWAMWINDI akafika kituo kikuu cha polisi akaenda moja kwa moja kaunta akamkuta PC MBETA KASONDA na kukwambia  "Ebu nenda kwenye buti ukaitoe mbwa yenu nimeishaiua" na kumkabidhi bunduki pamoja na funguo za gari. 

PC KASONDA hakuamini macho yake alipouona mwili wa Dr. KLERUU ukiwa umetapakaa damu. Dr. KLERUU alikuwa amevaa ovaroli nyeusi na miwani. Hivyo,  mara moja PC KASONDA akamuweka MWAMWINDI chini ya ulinzi. Mtu mwingine aliyekuwepo kituoni hapo ni mzee DAVID BUTITINI(ambaye alikuwa askari polisi na baadaye kada wa CCM Iringa). 

Tarumbeta likapulizwa na askari wakakusanyika na kupewa rasmi taarifa ya kifo hicho cha Mkuu wao wa mkoa na gari lake likahifadhiwa nyuma ya kituo cha polisi. Askari wanne wakaenda kuleta kitanda cha magurudumu toka hospitali na hatimaye mwili wa Dr. KLERUU ukapelekwa "mortuary". Kesho yake, siku ya jumatatu, mji mzima wa Iringa uligubikwa na simanzi kubwa.

Kuna kundi la watu ambao walikuwa wakimchukia sana Dr. KLERUU kutokana na aina ya uongozi wake hivyo lilipopata tu taarifa za kifo chake wakanunua makreti ya bia usiku huohuo na kuanza kunywa kwa kushangilia hadharani!  Msako ulipoanza  usiku huohuo, jamaa hao walikuwa wa kwanza kukamatwa!.    

Mzee BUTININI ambaye pia alikuwa Mtwara wakati DR. KLERUU alipokuwa Mkuu wa Mkoa, anakiri kuwa ni kweli DR. KLERUU alikuwa mtu wa shoka- "Ni kweli hata kule Mtwara alionekana mtemi sana mwenye kuhimiza mambo kwa nguvu. Lakini lazma muelewe maeneo ya Mtwara yalikuwa ya vita na tulikuwa tukiwasaidia ndugu zetu wa Frelimo hivyo kule kulihitaji mtu kama DR. KLERUU. Mtwara DR. KLERUU hakukumbana na upinzani ila Iringa hali ilikuwa tofauti. Kwa mawazo yangu, Dr. KLERUU alipaswa kwanza kujifunza juu ya mila na desturi za watu wa Iringa. Maana watu wa Iringa ni watu wa Iringa tu."   

Mauaji hayo ya Dr. KLERUU yalimsikitisha sana Mwalimu NYERERE, wakuu wa mikoa na wananchi mbalimbambali. Lilikuwa ni tukio lililoongelewa nchi nzima. Majirani na wazee wengi waliokuwa wakilima pamoja na MWAMWINDI walisombwa na vyombo cha usalama na kumwekea ndani kuisaidia polisi ambapo walikuwa wakikamatwa na kusafirishwa usiku kwa ndege za jeshi.

 Takribani watu 30 walikamatwa wakiwemo wazee maarufu kama IBRAHIM KHALILI, PESAMBIL, MURSALI na wengineo na kupelekwa sehemu mbalimbali za nchi mf Shinyanga, Mwanza na Zanzibar. Cha kusikitisha ni kwamba ndugu zao hawakujua wamepelekwa wapi! Aidha,  nyumbani kwa MWAMWINDI huko Mkungugu kukawa kunalindwa na askari wa FFU muda wote.

Kitendo cha kukamatwa majirani na marafiki wa MWAMWINDI kilileta uhasama mkubwa baina ya ndugu wa majirani hao na familia ya MWAMWINDI.

Ikabidi mwanae (AMANI MWAMWINDI)(21) alazimike kutafuta kibali cha  DC Iringa kwenda gereza la Dodoma alikokuwa anashikiliwa MWAMWINDI. Alipoganikiwa kukipata alikwenda na akamueleza hali hiyo ambayo ilimsukitisha sana Mzee MWAMWINDI. 

AMANI akamshauri baba yake aandike barua kwa Rais NYERERE, nae akafanya hivyo siku hiyohiyo. Katika barua hiyo, MWAMWINDI alimueleza Mwalimu kwamba yeye  ndiye aliyemuua Dr. KLERUU hivyo wengine hawahusiki hivyo waachiwe. Baada ya kupita siku kadhaa,  wazee hao majirani wakaachiwa na kurejea kijijini hapo, Isimani. Hata hivyo, tafrani hiyo iliyokuwaimewakumba ikafanya wengi wahame eneo hilo kwani waliishaona "togwa limeingia nzi"!.

Upelelezi wa mauaji hayo ulienda haraka na MWAMWINDI akafunguliwa kesi ya mauaji ya kukusudia Mahakama kuu. Kesi ilipoanza kusikilizwa, ilivuta hisia za watu wengi na umati wa watu uliokuwa ukitamalaki kila siku mahakamani ulikuwa "si wa nchi hii!. 

Tarehe 2/10/1972, baada ya mashahidi wa pande zote kutoa ushahidi wao akiwemo RPC wa Iringa (Abubakar Hassan) aliyetoa ushahidi upande wa   MWAMWINDI kwamba hakuwa na taarifa kwamba Mkuu huyo wa Mkoa angetembelea eneo hilo ndio maana hakumpa "Police escort",  Jaji GABRIEL CHIKE ONYIUKE toka Nigeria (aliyehudumu Tanzania toka 1970-1973) alimtia MWAMWINDI hatiani na kumuhukumu kunyongwa hadi afe.

 Hii ilikuwa ni baada ya kuukataa utetezi wake kwamba alitenda kosa hilo baada ya kurukwa na akili na pia alikasirishwa "provoked" na marehemu, Mh. Jaji aliona kwamba ingawa ni kweli MNYALUKOLO wa kawaida huwa si mtu wa mchezo-mchezo anapodhihakiwa hasa mbele za wake zake lakini  kitendo cha MWAMWINDI cha kwenda ndani kufuata bunduki kilionesha, pasina shaka, kwamba aliua kwa kudhamiria.

Adhabu hiyo ya kifo ilitekelezwa mara moja kwani Mwalimu NYERERE alisaini hati ya kifo cha MWAMWINDI

. Hayo hiyo, ilikuwa ni moja ya hati tatu za vifo zilizosainiwa na Mwalimu NYERERE kuidhinisha kunyongwa kwa binadamu katika uongozi wake wa miaka 24 katika taifa hili.  

Kesi hii ilikuwa ya aina yake na haikuchukua hata mwaka mmoja toka tukio kutokea na adhabu kutolewa   tofauti na kesi nyingine za mauaji ambazo, kwa kawaida, huchukua miaka mingi kabla ya hukumu kutolewa. Kesi hii ilichukua miezi kumi tu.

Baada ya msiba, familia ya DR. KLERUU ilirudi Kilimanjaro. Hata hivyo, Mwalimu NYERERE na KARUME na baadae ABDU JUMBE walikuwa karibu sana na mjane wa DR. KLERUU na wakawasomesha wanawe nchini Urusi na Bulgaria.  Aidha, viongozi wengine waliwatia moyo na kuwafariji sana mf.  Marehemu Mzee RASHID KAWAWA na mama GETRUDE MONGELA. Dr. KLERUU aliacha watoto wanne ambao ni Eva, Andrew, Carmen na Edwin.

Mwezi Machi 2014, familia ya DR. KLERUU na ya MWAMWINDI zilikutana kwa furaha ili kusameheana kwa tukio hilo. Bi. EVA KLERUU(60) ambaye ni mtoto mkubwa wa Dr. KLERUU na Bw. AMAN MWAMWINDI(67) (aliyekuwa Meya wa mji wa Iringa) walifanya jambo hilo la kihistoria na hivyo kuyaishi kivitendo maandiko ya vitabu vitakatifu yatutakayo wanadamu kusameheana. Picha hii chini inawaonesha wawili hao wakiwa na bashasha baada ya tendo hilo la kihistoria na lisilo la kawaida. 

Mnara wa DR. KLERUU umejengwa kwenye "mji" wa MWAMWINDI mahali ambapo alipigwa risasi . Nyumba ya Mkuu wa Mkoa  DR. KLERUU bado ipo. Picha hizi hapa chini zinamuonesha Mnyalukolo MWAMWINDI baada ya kujisalimisha polisi pamoja na nyumba ya DR. KLERUU.


REST IN PEACE:


1. Dr. W. KLERUU

2. S. A. MWAMWINDI

(Makala hii ni kwa hisani ya mtandao)







Inavyoonekana kwa sasa:

 Ikulu Ndogo Ya RC Kleruu Aliyepigwa Risasi Na Mkulima Mwamwindi...

Ni nyumba namba moja Iringa, eneo la Gangilonga. Haijapata kukaliwa tena na Mkuu wa Mkoa au hata DC tangu auawe RC Dr. Kleruu.

Nimefika tena kwenye nyumba hiyo jana Jumatatu. Imejengwa mwaka 1906 na Wajerumani. Bado iko kwenye ubora wa Mjerumani.

Maggid

Jengo lilioezuliwa paa ni iliyokuwa nyumba ya mtumishi wa RC (Picha kwa hisani ya Magidi Mjengwa.


DKT. KIMAMBO AFUNGUA KIKAO CHA 31 CHA BARAZA LA WAFANYAKAZI MUHIMBILI

 


Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (Upanga na Mloganzila), Dkt. Delilah Kimambo, leo Juni 10, 2026, amefungua rasmi Kikao cha 31 cha Baraza la Wafanyakazi kinachowakutanisha wawakilishi wa watumishi kutoka idara na vitengo mbalimbali vya hospitali kujadili masuala ya maendeleo ya taasisi na ustawi wa watumishi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Dkt. Kimambo amewataka wajumbe kutumia jukwaa hilo kutoa mawazo na mapendekezo yatakayosaidia kuimarisha utendaji wa hospitali na kuboresha huduma za afya kwa wananchi na kusisitiza kuwa mafanikio ya Muhimbili yanategemea mshikamano, uwajibikaji na ushirikiano wa watumishi katika kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujituma.

Baraza la Wafanyakazi Muhimbili hufanyika kila mwaka kwa lengo la kujadili na kutathmini utekelezaji wa shughuli za hospitali, kupitia mipango na bajeti ya taasisi pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya menejimenti na watumishi ili kuongeza ufanisi wa kazi na kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi.











WILLIAM PETER KISAKA WA SIMBA WANYIKA



William Peter Kisaka pia ujulikana Kwa jina la William Kinyonga, alikuwa mpiga drumz wa zamani na mmoja wa waasisi wa bendi ya Simba Wanyika, bwana huyu amekuwa akiteseka na maradhi Nchini Kenya

William,  kwa muda alikuwa akiishi maisha magumu ya kuokota vitu na kujikimu mitaani, ni ndugu wa Wilson Peter na George Peter, ambao walikuwa pamoja naye wakiwa wanamuziki mahiri nchini Kenya .kuanzia miaka ya 1970. 

Kaka zake Wote wawili walisha fariki dunia miaka mingi iliyopita.

Kwa jitihada za bwana Geoffrey Mosira sasa hivi yupo katika.makazi ya wazee jijini NAIROBI

Kulikuwa na habari nyingi hapa Tanzania kuwa Kuna mpango wa kumleta nyumbani Kwa matibabu LAKINI jambo hilo halikufanyika 

Kwa mujibu wa taarifa William amekuwa akikabiliwa na changamoto za afya ya akili.


Geoffrey Mosira akiwa na William Kinyonga katika Jiji la Nairobi. Picha za juu na chini katika hali ya sasa.



Tuesday, June 9, 2026

KONGAMANO LA TANZANIA NA MISRI LAFUNGUA FURSA MPYA ZA BIASHARA, UWEKEZAJI NA UTALII



Na Mwandishi Wetu, Misri


Mahusiano ya muda mrefu kati ya Tanzania na Misri yameendelea kupata nguvu mpya kufuatia kufanyika kwa Kongamano la Biashara, Uwekezaji na Utalii la Tanzania na Misri, ambalo limewakutanisha viongozi wa serikali, wafanyabiashara, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka mataifa hayo mawili.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara Ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi wakati wa kuhitimisha Kongamano hilo ambalo limetoa fursa za ushirikiano wa kiuchumi na kuimarisha mahusiano ya kibiashara kati ya Tanzania na Misri. 

Amesema Katika miaka ya hivi karibuni, Tanzania imeendelea kutekeleza mageuzi mbalimbali yaliyolenga kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

Mageuzi hayo yameongeza imani ya wawekezaji wa ndani na nje ya nchi na kuifanya Tanzania kuwa moja ya vituo vinavyoongoza kwa kuvutia uwekezaji barani Afrika.

Ametumia  wasaa huo kuwakaribisha wawekezaji kutoka Misri kutumia fursa zilizopo kwa kuwekeza katika hoteli, vituo vya burudani, miundombinu ya utalii wa baharini, taasisi za mafunzo ya ukarimu na huduma za kidijitali zinazohusiana na utalii.

“Ninawakaribisha kuja kutalii Tanzania kwakuwa kwa sasa kuna safari za moja kwa moja za ndege kati ya Cairo na Dar es Salaam, amesema Dkt. Abbasi”.

Naye Naibu Waziri wa Utalii na Mambokale Misri, Mhe. Yomna El Bahar amesema Kuwa Misri ipo tayari kuendeleza mashirikiano baina ya nchi hizo mbili ikiwemo kubadilishana uzoefu kwani Misri imeweza kufikisha watalii milioni 16 hivyo kama Tanzania tuna mengi ya kujifunza ikiwemo namna ya kuendeleza utalii wa utamaduni na kujifunza jinsi wanavyoyatumia kimkakati historia yao kujitangaza.

Kongamano hilo lililoanza Juni 8, 2026 limehitimishwa leo Juni 9, 2026 katika Hoteli ya Sofitel jijini Cairo, Misri.