ANGALIA LIVE NEWS

Saturday, June 6, 2026

ADVANCING WILDLIFE CONSERVATION THROUGH SCIENCE: TAWIRI AT KILI FAIR 2026


Arusha  


The Tanzania Wildlife Research Institute (TAWIRI) warmly welcomes visitors to its exhibition booth and is pleased to share scientific knowledge and innovations in wildlife conservation.  

TAWIRI's core mandate is to conduct, coordinate, and supervise wildlife research throughout Tanzania, where is  responsible for disseminating timely, high-quality scientific information to support evidence-based management and sustainable utilization of the country's wildlife resources. 

As the custodian of wildlife research, TAWIRI is responsible for wildlife population monitoring in various ecosystems.

The Institute also conducts surveillance on wildlife diseases, supports wildlife disease control initiatives, and monitors wildlife health across Tanzania's ecosystems.

In addition, TAWIRI promotes and facilitates the training and capacity building of Tanzanians in wildlife science and conservation.

Furthermore, the Institute plays a key advisory role by providing research-findings to the Government, wildlife management authorities, and the general public on effective strategies for conserving Tanzania's wildlife resources.




Wildlife research for Sustainable Conservation and Tourism development🇹🇿_

Friday, June 5, 2026

MAKAMU WA RAIS ASISITIZA NAFASI YA TFS KATIKA KUFANIKISHA KAMPENI ZA UPANDAJI MITI



Na Mwandishi Wetu, Dodoma


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi, ameuagiza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuhakikisha unaandaa miche ya miti ya kutosha ili kuimarisha utekelezaji wa kampeni za upandaji miti na juhudi za uhifadhi wa mazingira nchini.

Dkt. Nchimbi alitoa agizo hilo Juni 5, 2026, wakati akihitimisha kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre jijini Dodoma kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Alisema upatikanaji wa miche ya miti kwa wingi ni moja ya nguzo muhimu katika kufanikisha azma ya Serikali ya kuongeza uoto wa asili, kulinda vyanzo vya maji na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Sambamba na hilo, Makamu wa Rais amezielekeza Sekretarieti za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa na TFS kuimarisha usimamizi wa maeneo yanayopandwa miti ili kuzuia uharibifu na kuhakikisha miti inayopandwa inatunzwa hadi ikue.

“Ni muhimu kuhakikisha juhudi za upandaji miti haziishii kwenye kupanda pekee, bali zinahusisha pia ulinzi na matunzo ya miti hiyo ili iweze kukua na kutoa mchango unaotarajiwa katika uhifadhi wa mazingira,” alisema Dkt. Nchimbi.

Katika hatua nyingine, ameiagiza Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC), kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, kubainisha na kusajili misitu inayofaa kuingizwa katika miradi ya biashara ya kaboni kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuongeza mchango wa sekta ya misitu katika kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, kuimarisha uhifadhi wa mazingira na kufungua fursa zaidi za kiuchumi kwa wananchi kupitia biashara ya kaboni.

Dkt. Nchimbi alibainisha kuwa biashara ya kaboni ni moja ya maeneo yenye uwezo mkubwa wa kuleta manufaa kwa jamii zinazoshiriki katika uhifadhi wa misitu huku ikichangia utekelezaji wa malengo ya Taifa ya maendeleo endelevu.

Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka huu yamewakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za umma na binafsi, wadau wa mazingira pamoja na wananchi kwa lengo la kuhamasisha usimamizi endelevu wa mazingira na matumizi bora ya rasilimali za asili.

Katika maadhimisho hayo, TFS ilikuwa miongoni mwa taasisi zilizoshiriki kikamilifu kwa kuonesha mafanikio ya shughuli zake za uhifadhi wa misitu, urejeshaji wa mazingira, uzalishaji wa miche ya miti na utekelezaji wa programu mbalimbali za kukuza uchumi wa kijani nchini.








UTALII WA MISITU WA TANZANIA WAPATA JUKWAA KOREA KUSINI



Na Mwandishi Wetu, Seoul


Fursa za utalii wa misitu na uwekezaji katika miundombinu ya utalii ndani ya misitu ya hifadhi inayosimamiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) zimetangazwa katika Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Seoul International Travel Fair (SITF) 2026 yanayoendelea jijini Seoul, Korea Kusini.

Ushiriki huo ni sehemu ya juhudi za Serikali kupitia Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) za kupanua masoko ya utalii katika eneo la Mashariki ya Mbali na bara la Asia, ambalo linaendelea kuwa miongoni mwa masoko yenye ukuaji mkubwa wa watalii duniani.

Akizungumza katika maonesho hayo, Mhifadhi Someni Mteleka wa TFS alisema ushiriki wa Tanzania unatoa fursa ya kutangaza vivutio vya utalii wa misitu vilivyopo nchini pamoja na kujifunza mahitaji na matarajio ya watalii wa kimataifa.

Alisema idadi kubwa ya washiriki wa maonesho hayo wameonesha kuvutiwa na utalii wa mazingira asilia na kueleza nia ya kutembelea maeneo mbalimbali ya vivutio vya misitu nchini.

“Tumeshuhudia watu wengi wakivutiwa na utalii wa mazingira asilia na kuonesha hamu ya kutembelea maeneo mbalimbali ya misitu nchini Tanzania, ikiwemo Mlima Rungwe, Maporomoko ya Kalambo, Hifadhi ya Mazingira Asilia ya Amani, Milima ya Magamba, Msitu wa Chome na Mlima Hanang. Fursa hii pia inatuwezesha kujifunza matarajio yao ili tuendelee kuboresha huduma na miundombinu ya utalii ikolojia,” alisema.



Kwa mujibu wa Mteleka, Korea Kusini ni miongoni mwa nchi zilizofanikiwa kuendeleza utalii wa mazingira asilia unaojumuisha misitu, milima, maziwa, mito, mabwawa na maporomoko ya maji, hali inayofanana kwa kiasi kikubwa na utajiri wa vivutio vilivyopo Tanzania.

Alisema uzoefu unaopatikana kupitia maonesho hayo utaisaidia Tanzania kuimarisha mipango ya kuendeleza utalii wa misitu kama zao jipya la utalii lenye mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi na ajira.

“Tutatumia uzoefu huu kujenga uwezo wetu katika kuendeleza miundombinu na huduma zinazowezesha utalii wa misitu kukua na kuchangia zaidi katika uchumi wa nchi. Hii itasaidia kufanikisha azma ya Serikali ya kufikia watalii milioni nane ifikapo mwaka 2030 sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” alisema.

Korea Kusini imeendelea kuwa mfano wa mafanikio katika maendeleo ya utalii wa mazingira asilia, jambo linalofungua fursa kwa Tanzania kujifunza mbinu bora za usimamizi wa vivutio, huduma za wageni na uwekezaji katika miundombinu ya utalii wa ikolojia.

Maonesho ya SITF 2026 huwakutanisha wadau wa sekta ya utalii kutoka mataifa mbalimbali duniani, wakiwemo wawekezaji, waendeshaji wa biashara za utalii, wanunuzi na wauzaji wa huduma za utalii, kwa lengo la kukuza ushirikiano na biashara katika sekta hiyo.




KILOMBERO YAPANDA MITI 1,000 KUADHIMISHA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI



Na Mwandishi Wetu, Kilombero


Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Kilombero umeadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kwa kupanda miti 1,000 katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo, huku wananchi wakihimizwa kuacha shughuli zinazoharibu mazingira na kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wa rasilimali za asili.

Shughuli hiyo ilifanyika chini ya kampeni ya kitaifa ya “Dira ya 2050: Tunakijanisha Tanzania” na kuongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Wakili Dunstan Kyobya, aliyekuwa mgeni rasmi.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mhe. Kyobya alisema mazingira ni msingi wa maendeleo ya taifa na ustawi wa jamii, hivyo ni wajibu wa kila mwananchi kushiriki katika kuyatunza kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Alisema vitendo vya uharibifu wa mazingira vinaendelea kuchangia kupungua kwa vyanzo vya maji, kuongezeka kwa athari za mabadiliko ya tabianchi na kuhatarisha shughuli muhimu za kiuchumi, hususan kilimo na ufugaji.

“Ni wajibu wa kila mmoja wetu kushiriki katika kulinda mazingira kwa kupanda miti, kutunza vyanzo vya maji na kuacha shughuli zinazochangia uharibifu wa mazingira. Haya ni maeneo muhimu kwa maisha ya sasa na ya baadaye,” alisema.





Mhe. Kyobya aliwataka wananchi kuepuka shughuli za kibinadamu katika maeneo yaliyohifadhiwa na kandokando ya mito, akieleza kuwa maeneo hayo yana mchango mkubwa katika kulinda mifumo ikolojia na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji.

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuongeza uoto wa asili kupitia kampeni mbalimbali za upandaji miti zinazolenga kuifanya Tanzania kuwa ya kijani zaidi ifikapo mwaka 2050.

Kwa mujibu wa Mhifadhi waTFS Wilaya ya Kilombero, SCO Zarina Haridi, miti 1,000 iliyopandwa ni sehemu ya mchango wa wilaya hiyo katika utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya kuimarisha uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Siku ya Mazingira Duniani huadhimishwa kila mwaka kwa lengo la kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira na kuhamasisha hatua za uhifadhi wa rasilimali za asili kwa maendeleo endelevu.

Maadhimisho ya mwaka huu nchini yamefanyika chini ya kaulimbiu ya “Dira ya 2050: Tunakijanisha Tanzania,” inayolenga kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika urejeshaji wa mifumo ikolojia, utunzaji wa mazingira na kuongeza uoto wa asili nchini.







DKT. MUGOBI: KARIBU-KILIFAIR NI JUKWAA MUHIMU LA KUTANGAZA UTALII WA TANZANIA



Na Timothy Mwakyenda, Arusha


Mkurugenzi wa Idara ya Utalii kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Thereza Mugobi, amesema Maonesho ya Kimataifa ya Karibu-KiliFair 2026 yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii barani Afrika, huku yakitoa nafasi ya kuonesha vivutio mbalimbali vya utalii ikiwemo utalii wa misitu, kuimarisha ushirikiano wa wadau na kuvutia uwekezaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa maonesho hayo uliofanyika Juni 5, 2026 katika Viwanja vya Magereza mkoani Arusha, Dkt. Mugobi alisema Karibu-KiliFair imekuwa nyenzo muhimu ya kutangaza utajiri wa rasilimali za utalii zinazopatikana nchini na kufungua masoko mapya ya sekta hiyo.

Alisema maonesho hayo yanatoa fursa kwa taasisi za umma na sekta binafsi kuonesha bidhaa na huduma zao, kujenga mitandao ya kibiashara na kuimarisha ushirikiano unaochochea ukuaji wa sekta ya utalii.

“Karibu-KiliFair si maonesho ya kawaida bali ni uwekezaji wa kimkakati unaosaidia kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Tanzania, kuvutia wawekezaji wapya na kufungua masoko mapya ya bidhaa na huduma za utalii,” alisema Dkt. Mugobi.

Aliongeza kuwa maonesho hayo yanaendelea kuwakutanisha wadau wa utalii kutoka ndani na nje ya nchi, jambo linalochangia kuongeza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Dkt. Mugobi alisema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya utalii ikiwemo barabara, viwanja vya ndege na huduma za malazi ili kuongeza urahisi wa kufikia maeneo ya vivutio na kuboresha uzoefu wa watalii.

Pia alisisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia za kidijitali katika kuitangaza Tanzania kwenye masoko ya kimataifa, akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza mwonekano wa vivutio vya nchi na kuwafikia watalii wengi zaidi duniani.

Katika maonesho hayo, taasisi mbalimbali za umma na binafsi, ikiwemo Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), zinashiriki kutangaza huduma na fursa za uwekezaji zilizopo katika maeneo ya utalii wa mazingira na misitu ya hifadhi.

Karibu-KiliFair 2026 inaendelea kuthibitisha nafasi yake kama moja ya maonesho makubwa ya biashara ya utalii Afrika Mashariki, ikitoa jukwaa la kukuza ushirikiano, uwekezaji na utangazaji wa vivutio vinavyoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa utalii barani Afrika.





NI TANAPA TENA: YANG’ARA KITAIFA, YABEBA TUZO YA UBORA WA HUDUMA ZA UMMA



Na. Catherine Mbena - Dar es Salaam.


Ubora wa huduma, utekelezaji wa *ISO 9001:2015* na kuridhika kwa wateja vyaiwezesha TANAPA kushika nafasi ya pili kitaifa katika Tuzo za Ubora wa Taifa (National Quality Award 2025/2026).

*DAR ES SALAAM*: Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limeandika historia nyingine mjarabu baada ya kutunukiwa Cheti cha Ushindi wa Pili (First Runner-Up) katika Tuzo za Ubora wa Taifa 2025/2026, tuzo zinazoratibiwa na kutolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kwa lengo la kutambua taasisi zinazofanya vizuri katika utoaji wa huduma na kuzingatia viwango vya ubora.

Tuzo hiyo iliyotolewa leo juni 5, 2026 katika Jukwaa la Biashara la Viwango (Standards Business Forum) lililofanyika jijini Dar es Salaam katika Ukumbi wa Mlimani City, ambapo TANAPA iling’ara katika kipengele cha “Mtoa Huduma Bora wa Umma wa Mwaka”, ikiibuka mshindi wa pili miongoni mwa taasisi zilizofanya vizuri zaidi nchini katika utoaji wa huduma kwa watalii na wageni mbalimbali wanaotembelea maeneo yao yenye tunu za Taifa.

Mafanikio hayo yanaonesha hatua kubwa iliyofikiwa na TANAPA katika kuimarisha ubora wa huduma, kuongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuhakikisha wateja wake ambao ni watalii, wanapata huduma zinazokidhi viwango vya kitaifa na  kimataifa. 

Tangu mwaka 2022, TANAPA imekuwa ikitekeleza Mfumo wa Usimamizi wa Ubora wa ISO 9001:2015, ambao umechangia kuimarisha usimamizi wa shughuli zake, kuongeza uwajibikaji na kujenga utamaduni wa maboresho endelevu kwa kila huduma inayotoa ndani ya Hifadhi za Taifa 21 inayozisimamia.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi TANAPA baada ya kupokea tuzo hiyo, Afisa Mhifadhi Mkuu Eunice Msangi, alisema kuwa ushindi huo ni matokeo ya juhudi za pamoja za Menejimenti na watumishi wa TANAPA katika kuhakikisha huduma zinazotolewa zinakizi matarajio na matamanio ya wateja na wadau wake.

Aidha, Mhifadhi huyo aliongeza; “Ushirikiano mkubwa kutoka kwa wadau wa sekta ya Uhifadhi na Utalii pia wamechangia kwa kiasi kikubwa mafanikio hayo. Tuwaahidi wateja wetu na wadau mbalimbali TANAPA itaendelea kuboresha huduma zake ili kuongeza uzoefu mzuri kwa wageni na kuchochea ukuaji wa sekta ya utalii nchini”.

Ushindi huo unaongeza hadhi ya TANAPA kama taasisi ya umma iliyojizatiti kutoa huduma bora na kuendeleza dhamira yake ya kusimamia kwa weledi rasilimali za Taifa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.







FURSA ZA KIUCHUMI TANZANIA NA URUSI, AIR TANZANIA KUANZA SAFARI ZA MOJA KWA MOJA DAR/ZANZIBAR -MOSCOW



RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye yupo nchini Urusi kwa ziara maalum, amebainisha kuwa, kuanzia Julai 2026, Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL) itaanza safari za moja kwa moja kati ya Dar es Salaam, Zanzibar na Moscow. 

Ambapo amesema hatua hio muhimu itaimarisha zaidi utalii, biashara na uwekezaji, na kufungua ukurasa mpya katika historia ya uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi.

Amesema:

"Nikihitimisha ziara yangu ya Kitaifa katika Shirikisho la Urusi, leo pamoja na mambo mengine nimepata fursa ya kuhutubia Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Urusi pamoja na Jukwaa la 29 la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg (SPIEF), ambayo yamekutanisha viongozi, wataalamu wafanyabiashara na wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali.

Nimewahakikishia wawekezaji kuwa Tanzania ni sehemu salama na bora kwa mitaji yao, tukijivunia mazingira wezeshi ya kisheria, amani na utulivu, miundombinu bora, ukuaji imara wa uchumi, uwepo wa nguvu kazi na fursa ya kufikia soko la zaidi ya watu milioni 500 ukanda wa Mashariki na Kusini mwa Afrika.

Pia, nimebainisha sekta za kimkakati ambazo ni kipaumbele katika uwekezaji zikijumuisha madini, kilimo, nishati safi, mafuta na gesi, afya pamoja na usafiri na usafirishaji." Amesema.





WIZARA YA AFYA MIKOA NA HALMASHAURI NCHINI KUIMARISHA HUDUMA ZA CHANJO



Na Mvuda Jaffer,WAF:Dar-es-Salaam


Wizara ya Afya imezitaka Mikoa na Halmashauri nchini kuimarisha huduma za chanjo kwa kubuni mbinu mpya za kuwafikia watoto ambao hawajapata chanjo kabisa (zero-dose) au ambao hawajakamilisha ratiba za chanjo, ili kuongeza kinga dhidi ya magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.

Maelekezo hayo yametolewa na Mkurugenzi wa Huduma za Tiba, Dkt. Hamad Nyembea, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif  Shekalaghe, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Tathmini ya Utekelezaji wa Huduma za Chanjo nchini unaofanyika jijini Dar es Salaam.

Dkt.Nyembea amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa huduma za chanjo kwa zaidi ya miaka mitano mfululizo ambapo walengwa zaidi ya asilimia 80 wameendelea kufikiwa, bado kuna makundi ya watoto katika jamii za wafugaji, wavuvi, maeneo ya migodini pamoja na baadhi ya maeneo ya mijini ambayo hayajafikiwi kikamilifu na huduma hizo.





“Serikali imeandaa Mpango Mkakati wa Taifa wa Chanjo wa mwaka 2026–2030 unaolenga kuhakikisha huduma za chanjo zinawafikia walengwa wote na kujenga jamii yenye kinga dhidi ya magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.”amesema Dkt.Nyembea

Aidha, Dkt.Nyembea ameeleza kuwa bado kuna changamoto ya ufuatiliaji wa magonjwa yanayozuilika kwa chanjo ikiwemo Surua na Polio, hali inayosababisha kushindwa kuwabaini mapema wahisiwa wa magonjwa hayo na kuchukua hatua stahiki za kinga na udhibiti.

“Wizara ya Afya imezitaka Halmashauri na vituo vya kutolea huduma za afya kutumia kikamilifu fursa ya usafirishaji wa sampuli kupitia Shirika la Posta pamoja na kutenga rasilimali kwa ajili ya uibuaji wa wahisiwa, uchukuaji wa sampuli na usafirishaji wake ili kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa hayo.”amesema Dkt. Nyembea

Pia Dkt.Nyembea amesisitiza umuhimu wa kuimarisha huduma za mkoba na huduma tembezi katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa huduma za afya, akieleza kuwa huduma hizo ni nyenzo muhimu ya kuwafikia walengwa ambao hawawezi kufika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.

Sambamba na hilo, Dkt.Nyembea amewaelekeza Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri kuhakikisha huduma za chanjo zinatolewa kila siku katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa mujibu wa miongozo ya Taifa, pamoja na kusimamia matumizi sahihi ya chanjo kwa kuzingatia utaratibu wa kutumia kwanza chanjo zinazokaribia kuisha muda wake.

“Mafanikio ya huduma za chanjo yatategemea zaidi uwezo wa wataalamu wa afya, viongozi wa jamii na wadau mbalimbali kushirikiana katika kuwafikia walengwa mahali walipo na kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa huduma za chanjo kutokana na changamoto za umbali, taarifa au mazingira ya makazi.”amesema Dkt.Nyembea