 |
| Pichani ni mpiga rithim wa jamhuri Harisoni Siwale na mkewe |
Peter Toll anaendelea
Philps to Plydor
"Mwaka 1973 ndiyo mwaka ambao Philips Kenya ilibadilika na kuwa Polygram (Polydor)."
"Polygram ilipoanza kutoa albamu za LP zilizokusanywa kutoka rekodi za 45 RPM, mara nyingi waliandika 'Original Recording – Polygram Studios 1973', kama ilivyo kwenye LP Dunia Haina Wema."
"Lakini hilo lilitokana na ukweli kwamba Polygram haikujali sana au haikuweza kubaini nyimbo hizo zilikuwa zimetolewa lini kwa mara ya kwanza."
Ziara ulaya
Katika makala yake “Wanyika Memories” (The Beat, Vol. 12, No. 4, 1993), Peter Toll anasimulia kuwa wakati Simba Wanyika walipokuwa wakijiandaa kuanza ziara yao ya kwanza Ulaya mwezi Novemba 1989, walikumbana na tatizo kubwa: ndugu Wilson Kinyonga na George Kinyonga pekee ndiyo waliokuwa na pasi za kusafiria.
Africa jambo jambo
Ili kuziba pengo la wanamuziki wengine watatu waliokosekana, waliajiri wanachama watatu kutoka bendi nyingine iliyoitwa Africa Jambo Jambo. Miongoni mwao alikuwa Muitikanda kutoka Uganda aitwaye Sammy Kasule, ambaye alikuwa amewahi kupiga katika makundi mbalimbali na pia kurekodi kazi zake binafsi.
Les Mangelepa
Wengine wawili walikuwa Wakongo Coco Kanyinda na Micky Jaga Jaga, ambao hapo awali walikuwa wanamuziki wa Orchestra Les Mangalepa.
Peter Toll anaendelea
"Ingawa kundi lililosafiri kwenda Ulaya mwaka 1989 halikuwa Simba Wanyika halisi ya Wilson Peter, walipiga muziki wa Kinyonga pekee, na waliufanya kwa ustadi mkubwa na nguvu nyingi."
"Maonesho yao yalipokelewa kwa sifa nyingi, na kabla ya kurudi Nairobi walirekodi mchanganyiko (medley) wa nyimbo maarufu za Simba Wanyika ambao ulitumika kutangaza ziara kubwa ya Ulaya iliyopangwa kufanyika kipindi cha kiangazi."
Peter anaendelea kueleza kuwa kutokana na mgogoro wa kimkataba kati yake na Polygram Records ya Nairobi, alishindwa kuachia rasmi mkanda huo wa “Wanyika Medley Tape” kama ilivyokuwa imepangwa.
Hata hivyo, mkanda huo ulihamasisha kutolewa kwa albamu ya medley ya Les Wanyika mwaka 1990 iliyoitwa Les Les Non Stop '90 (Polydor POLP 606).
Peter Toll alieleza matumaini yake kwamba siku moja rekodi ya “Live in Europe” itaweza kutolewa rasmi.
Lakini tayari ipo YouTube na aloyeiweka jina linahifadhiwa
NYIMBO ZA ZIARA YA DUNIA YA 1991
Nyimbo zilizorekodiwa nchini Uholanzi wakati wa ziara ya dunia ya Simba Wanyika mwaka 1991 ni:
Mwongele, Wenzako, Pamela
Sikujua Utabadilika, Nakupenda Cherie, Pole Pole, Maria
Wanamuziki waliorekodi pamoja na Wilson na George Kinyonga (waliokuwa waimbaji pamoja na wapiga solo na rhythm guitar) walikuwa, Maneno Shaban Ally percussion na ngoma, Mike Beche ngoma, Victor Boniface – gitaa la besi
Peter Toll pia aliwahi kusema kuhusu mkanda mmoja uliojitokeza baada ya kifo cha Wilson.........
"Hii si Simba Wanyika halisi. Ni kijana mmoja kutoka Tanzania aliyeniandikia baada ya Wilson kufariki. Alidai kuwa alikuwa ndugu yao (?) na kwamba angeendelea na Simba Wanyika.
Alinitumia kaseti hiyo, lakini sikuwahi kusikia tena habari zake."
LES WANYIKA
Mpiga rhythm guitar Omar Shabani, aliyefahamika kama “Professor Omar”, aliondoka Simba Wanyika mwaka 1978 pamoja na:
Tom Malanga (besi) Rashid Juma (ngoma) Elias John (saxophone)
na kwa kushirikiana na Watanzania John Ngereza na mwimbaji Issa Juma, wakaanzisha bendi ya Les Wanyika.
Muda mfupi baada ya kutoa wimbo wao maarufu “Sina Makosa” mwaka 1979, Issa Juma alijitenga na kuanza shughuli zake binafsi.
Katika miaka ya 1980, Les Wanyika walikuwa na mafanikio makubwa sawa na Simba Wanyika. Walitoa nyimbo nyingi zilizotikisa Afrika Mashariki, zikiwemo vibao vikubwa:.......Nilipi la Ajabu (1988)
Nimaru (1989)
Ingawa Omar Shabani ni mmoja wa mwanzilishi wa Les Wanyika na mtunzi wa nyimbo nyingi za bendi hiyo, kufikia mwaka 1990 ilionekana wazi kuwa ushawishi wake ulikuwa unapungua.
Peter Toll anaandika:
"Katika miaka ya 1980 kulikuwa na mvutano wa madaraka kati ya Ngereza na Shabani. Nafikiri Ngereza ndiye aliyeshinda baada ya Polygram kuamua kwamba yeye ndiye mtu ambaye walitaka kufanya naye kazi."
"Nyimbo zake pia zilikuwa zinauza zaidi."
Kutokana na hali hiyo, Omar Shabani alifukuzwa Les Wanyika mwaka 1990 na kujiunga na Everest Kings, kabla ya kurejea tena Les Wanyika miaka michache baadaye.
Kwa masikitiko, Omar Shabani alifariki mwaka 1997, na John Ngereza akafariki mwaka 2002.
SIRI YA WIMBO “SINA MAKOSA”
Katika makala ya Wanyika Memories, Peter Toll anaeleza:
"Ingawa Professor Omar amekuwa akitajwa kama mtunzi wa 'Sina Makosa' na hivyo kupata manufaa ya kifedha kutokana na wimbo huo, ukweli ni kwamba uliandikwa kwa ushirikiano na George Kinyonga walipokuwa bado Simba Wanyika."
"Mstari wa sauti unaonyesha wazi kabisa alama ya George Kinyonga, huku mpangilio wa rhythm na progression ya chords ukifanana sana na wimbo 'Daina' ambao George alikuwa ameutunga hapo awali."
"Huenda kutokana na kufanana huko, ndugu wa Kinyonga waliamua kutourekodi wimbo huo."
"Lakini wanamuziki wao walipoondoka na kuanzisha Les Wanyika, waliuchukua kama mojawapo ya nyimbo zao za kwanza kurekodi."
"Kwa mshangao na huzuni ya George, rekodi hiyo ikawa mafanikio makubwa sana ndani na nje ya Kenya."
LES MOTO MOTO
Nchini Kenya mikataba ya kurekodi haikusainiwa kwa jina la bendi nzima, bali kwa jina la kiongozi wa bendi.
Kwa sababu hiyo, wakati Les Wanyika walipoongozwa na Omar Shabani, John Ngereza hakuwa akipata mirabaha (royalties) za nyimbo alizokuwa akiandika.
Ili kutatua tatizo hilo, Ngereza akaanzisha Les Moto Moto, ambayo kimsingi ilikuwa ni Les Wanyika wakirekodi kwa jina tofauti.
Mpangilio huu ulikuwa sawa kabisa na ule uliotumika kati ya Simba Wanyika na Orchestra Jobiso.
ORCHESTRA JOBISO
Mwaka 1980, George Kinyonga aligombana na ndugu yake Wilson Kinyonga na kuondoka Simba Wanyika.
Wanachama wote wa bendi, isipokuwa William Kinyonga, waliondoka pamoja naye na kuanzisha Orchestra Jobiso, jina lililotokana na mtindo wa dansi ulioonekana kwenye rekodi za Simba Wanyika miaka ya 1970.
Wanamuziki wengine waliojiunga walikuwa:.......Mike Beche (percussion) Saidi Makelele (tarumbeta) ambao wote walikuwa wametoka katika bendi ya Super Volcano ya Mbaraka Mwinshehe.
Bendi hiyo mpya ilipata mafanikio ya haraka kupitia vibao:
Nakupenda Sherry, Pole Jobiso
Mwisho wa mwaka huo, Wilson na George walipatana na George akarudi Simba Wanyika.
Wanachama waliobaki wa Jobiso walijiunga na Issa Juma kuunda Super Wanyika Stars.
Hata hivyo Orchestra Jobiso haikufa.
Peter Toll anaandika:
"Baada ya George kurejea Simba Wanyika, ndugu hao walitatua tatizo la zamani la mkataba wa kurekodi kuwa kwa jina la Wilson pekee."
"Suluhisho lilikuwa kumpa George nafasi ya kurekodi nyimbo zake mwenyewe akiwa na wanamuziki wa Simba Wanyika na kuzitoa chini ya mkataba wake binafsi kama Orchestra Jobiso."
Kwa utaratibu huo zilirekodiwa nyimbo kama:........
.Natafuta Mwali, Tatizo la Pesa
Epuka Kizai-Zai (1984)
SUPER WANYIKA STARS
Baada ya kuimba kwa mafanikio makubwa wimbo “Sina Makosa” mwaka 1979, mwimbaji Mtanzania Issa Juma alijitenga na kuanzisha kundi lake mwenyewe akishirikiana na wanachama waliobaki wa Orchestra Jobiso.
Kundi hilo lilijulikana kwa majina mbalimbali, Waanyika, Wanyika Stars, Super Wanyika na Wanyika Super Les Les
lakini kwa pamoja lilijulikana kama Super Wanyika Stars.
Kwa kipindi fulani waliweza kushindana na makundi mengine ya Wanyika kupitia nyimbo maarufu kama....Ateka, Sigalame
Mwishoni mwa miaka ya 1980 Issa Juma alipitia matatizo mengi binafsi, yakiwemo kufungwa jela kwa miezi sita kwa kufanya kazi bila kibali halali.
Baadaye alihamia Kericho, magharibi mwa Kenya, na kuacha muziki.
Ni katika kipindi hicho alipata kiharusi kilichopooza upande mmoja wa mwili wake.
Issa Juma alifariki mwanzoni mwa miaka ya 1990.
EVEREST KINGS
Mkongwe wa muziki wa Wanyika Abdul Muyonga, akishirikiana na Mohamed Tika na Mahmood Hussein Yassin, aliondoka Mavalo Kings mwishoni mwa miaka ya 1980 na kuanzisha Everest Kings.
Tangu kifo cha John Ngereza mwaka 2002, Everest Kings wamekuwa walinzi wakuu wa urithi wa muziki wa Wanyika nchini Kenya.
Makao yao yamekuwa yakihama kati ya Machakos na Nairobi.
Kwa miaka mingi bendi hiyo imehifadhi sauti ya Wanyika huku pia ikiwakusanya wanamuziki waliotoka katika makundi mbalimbali ya Wanyika.
Miongoni mwa waliowahi kujiunga nayo ni....Omar Shabani, Tom Malanga, Freshley Mwamburi
Mwaka 2003, Freshley Mwamburi na wanachama wengine waliondoka na kujiunga na Great Sounds Band.
Gazeti la Daily Nation la Nairobi liliripoti kuwa baadhi ya waanzilishi wa awali wa Everest Kings, akiwemo Mohammed Hussein, Pius Indimuli na Richard Bangalala, walirejea tena kundini.
Mwaka 2000 Everest Kings walitoa CD Nivishe Pete, iliyokuwa na nyimbo: Nivishe Pete Boaz Olao
Wambua, Panga Mipango
Mwaka 2004 walitoa albamu Stella Wangu, iliyokuwa na nyimbo maarufu: Stella Wangu, Njiwa
Simoni
Albamu hiyo ilichanganya mitindo ya rumba na hip hop.
GREAT SOUNDS BAND
Kwa mujibu wa gazeti la Daily Nation la tarehe 13 Machi 2004, Tom Malanga, Freshley Mwamburi na mpiga rhythm guitar Rashid Athman waliondoka Everest Kings mwaka 2003 na kuanzisha Great Sounds Band.
Hata hivyo, haijulikani kwa uhakika bendi hiyo ilikuwa na uhusiano gani rasmi na makundi ya Wanyika, wala kama iliwahi kutoa rekodi zozote rasmi.
Itaendelea.............
Makala haya kwa hisani ya : BARIKI NGOWO -MUZIKI HALISI