ANGALIA LIVE NEWS

Sunday, June 28, 2026

TIMU SABA KUCHUANA RESI ZA NGALAWA ZIFF2026



Ngalawa saba zitachuana vikali katika mbio za kasi na ufundi zinazotarajiwa kufanyika kwenye Ufukwe wa Serena. 

Mbio hizo za ngalawa zinabeba msisimko mkubwa wa kuhitimisha Tamasha la 29 la Kimataifa la Filamu la Nchi za Jahazi (ZIFF) kwa mwaka huu wa 2026. 

Mtendaji Mkuu wa ZIFF, Joseph Mwale, amethibitisha kuwa ushindani huo utazikutanisha ngalawa zenye majina makubwa ikiwemo Azam Media, UNICEF, UN WOMEN, Fish Market, BATISTA, WIOMSA, na COMNET, ambapo mabaharia watachuana kuanzia ufukweni hapo, kuzunguka baharini na kurejea nchi kavu huku washindi wakiondoka na zawadi nono za fedha taslimu.

Kihistoria na kitamaduni, mbio za ngalawa zimekuwa kielelezo kikuu cha maisha, ukakamavu na urithi wa Waswahili wa mwambao ambao wametumia vyombo hivi kwa karne nyingi katika uvuvi na usafiri. 

Kuingizwa kwa mashindano haya kama kilele cha tamasha kupitia jukwaa la Wanawake na Vijijini (Women Panorama) kunalenga kuhuisha mchezo huu wa asili na kuupa sura ya kisasa inayovutia watalii na wenyeji. 

Tukio hili la kasi na ufundi majini halimalizi tu tamasha kwa burudani, bali linaweka msisitizo mkubwa katika agenda ya mashindano yenyewe kama nguzo inayounganisha jamii, huku ufukwe wa Serena ukigeuka kuwa uwanja wa mayowe, shangwe na ushindani wa kweli wa baharini.





WANAWAKE 30 VINARA WATUNUKIWA TUZO ZA MALKIA WA ARUSHA 2026



Tuzo za Malkia wa Arusha 2026 zimewakutanisha wanawake zaidi ya 300 kutoka sekta mbalimbali nchini kwa lengo la kutambua na kuenzi mchango wao katika maendeleo ya jamii na uchumi. Katika hafla hiyo, wanawake 30 vinara walitunukiwa tuzo kwa umahiri wao katika sekta mbalimbali ikiwemo Ujasiriamali, Biashara, Kilimo, Utalii, Afya, Elimu, Teknolojia, Maendeleo ya jamii, Sanaa na Utamaduni. Hafla hiyo ilifanyika tarehe 27 Juni 2026 katika Hoteli ya Gran MeliĆ” Arusha.

Akimwakilisha Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), Mgeni Rasmi ambaye ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Witness Shoo, Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Arusha, aliwapongeza wanawake wote walioshiriki na waliotambuliwa kwa mchango wao katika jamii.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mgeni Rasmi alisema ongezeko la watalii nchini linafungua fursa nyingi za kiuchumi kwa watanzania hususan wanawake na kuwataka kujipanga kunufaika na matukio makubwa yanayotarajiwa kufanyika nchini, ikiwemo Mkutano wa 153 wa Umoja wa Mabunge Duniani (Inter-Parliamentary Union - IPU)2026, World Travel Awards Grand Finale 2026 na AFCON 2027, kwa kujiandaa kutoa huduma zenye viwango vya kimataifa ili kuongeza mapato na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Vilevile, aliwahimiza wanawake kuendelea kudumisha nidhamu, uadilifu, ushirikiano na kujituma, akieleza kuwa misingi hiyo ndiyo nguzo ya kujenga viongozi bora, jamii yenye maadili na uchumi imara.

Kupitia jukwaa hilo, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) liliendelea kuhamasisha Utalii wa ndani pamoja na kutangaza fursa mbalimbali za Utalii na uwekezaji zinazopatikana ndani ya Hifadhi za Taifa Tanzania.
















#MalkiaWaArusha #TuzoZaWanawake #TanzaniaParks #ATM2030 #UtaliiNiMaisha #DestinationTanzania

WAHADZABE KWA MARA YA KWANZA KATIKA HISTORIA JUKWAA LA ZIFF2026


Uchezaji na burudani ya kipekee kutoka kwa jamii ya asili ya Wahadzabe ilikuwa moja ya vionjo vilivyoteka hisia za watazamaji zaidi ya 300 katika ufunguzi wa msimu wa 29 wa Tamasha la Kimataifa la Filamu la Zanzibar (ZIFF 2026).

Onyesho lao lilianza kwa namna ya kipekee ambapo, kabla ya kuingia kwenye ngoma yenyewe, waligubika jukwaa kwa mchezo wa kuigiza ulioonesha uhalisia wa maisha yao ya kila siku ya nyumbani na uwindaji. 

Taswira hiyo ya asili ilivutia mno na kuwafanya watazamaji kubaki vinywa wazi kwa mshangao na msisimko mkubwa.  

Baada ya kuonesha tamaduni hizo za maisha ya kila siku, burudani hiyo iligeuka kuwa sherehe kubwa pale walipoanza kushangilia maisha yao kupitia ngoma ya jadi yenye miondoko ambayo ni nadra sana kuikuta nje ya mazingira yao ya asili. 





Ilikuwa ni midundo ya kusisimua iliyosababisha jukwaa zima kutikisika kwa nguvu ya miguu yao na hewa kujazwa na mikono iliyokuwa ikitinga kwa madaha. 

Shangwe hiyo ilipamba moto kiasi cha kumfanya Balozi wa Italia nchini Tanzania, Mheshimiwa Giuseppe Sean Coppola, pamoja na viongozi wakuu wa ZIFF, kushindwa kuzuia hisia zao na kujumuika nao jukwaani kucheza na kushangilia pamoja midundo hiyo adhimu ya kitamaduni.  

Tamasha la ZIFF2026 mwaka huu linafanyika Juni 24-28, 2026.

Kwa hisani ya BSKY media, Zanzibar.










STORI YA LIONEL MESSI, KIJANA ALIYEJISHINDA YEYE MWENYEWE

 


Na. Elisa Niarira Mrutu 

0787356060


Mtoto wa "Dwarf, Kutoka Rosario 

Lionel AndrƩs Messi alizaliwa 24 Juni 1987 huko Rosario, Argentina. Alikuwa mtoto wa 3 kati ya 4. Familia ya kawaida tu baba yake alifanya kazi kiwandani, mama yake alifua nguo.

Umri wa miaka 11 daktari akagundua ana ugonjwa: Growth Hormone Deficiency [GHD]. Maana yake mwili wake haukutoa homoni ya kukua. Kama hangepewa sindano kila siku, asingekuwa mkubwa zaidi ya futi 4'3. Gharama ya sindano ilikuwa dola $900 kwa mwezi. Familia yake haikuwa na hizo pesa.

Vilabu vya Argentina vikasema ,Tunapenda kipaji chake, lakini hatuwezi kulipia matibabu yake. Ndoto yake ya kuwa mchezaji ilikuwa inaisha kabla hata haijaanza.


Safari ya Barcelona na  Sindano 1000

Akiwa na miaka 13, msimamizi wa talenti wa Barcelona alimwona akicheza kwao Argentina. Barcelona wakasema tutakuchukua, tutakulipia matibabu yako yote, Shida? Messi alikuwa Argentina, Barcelona Uhispania.

Baba yake Jorge akaacha kila kitu. Akamchukua Messi na ndugu zake, wakapanda ndege kwenda Spain bila kujua Kihispania vizuri. Messi kila siku kwa miaka 3 alichomwa sindano mguuni. Alilia, aliogopa, lakini hakuwahi kukosa Alisema, "Nilichagua kuumia kwa sindano ili nisiume kwa majuto maisha yangu yote".

Alipona. Urefu wake ukafika futi 5'7". Leo hii bado ni mfupi kama mchezaji, lakini ndio "urefu kamili" wa dribbling yake.


Alifanya Nini Kwenye Maisha Yake - Mafanikio


Klabu Barcelona 2004-2021,  

Alivunja rekodi zote. Magoli 672 kwa Barcelona rekodi ya mchezaji 1 klabu 1 duniani. Akatwaa Ballon d'Or mara 8 - mtu pekee kuwahi kufika hapo. Akawaongoza Barcelona kuchukua Champions League mara 4.

Staili yake ni tofauti, hajisumbui kukimbia sana, lakini mpira ukiwa miguuni mwake unashikamana kama gundi. Watu humwita "Mchawi mdogo".



Timu ya Taifa Argentina

Hapa ndio watu walimkosoa sana. Miaka 16 alicheza finali 4 na kupoteza zote. Watu wa Argentina wakasema ,Haipendi nchi yake kama Maradona, Mwaka 2016 hata alistaafu kwa hasira baada ya kupoteza fainali ya Copa America. 

Lakini akarejea. Mwaka 2021 alitwaa Copa America - kombe lake la kwanza na Argentina. 2022 akatimiza ndoto, Akatwaa Kombe la Dunia Qatar 2022, Alifunga magoli 7, akawa mchezaji bora wa mashindano yote. Watu wote wakakubali,Sasa Messi ni GOAT kamili.


Nje ya Uwanja

1. Mfadhili ana foundation yake ,Leo Messi Foundation inayosaidia watoto 200,000+ kupata elimu na matibabu duniani kote. Yeye mwenyewe alikuwa mtoto mgonjwa, hivyo anajua maumivu ya wazazi.

2.Mnyenyekevu, Hapendi kelele, hapendi maneno mengi. Baada ya kushinda Kombe la Dunia, alisema tu: "Nilikuwa nina deni kwa nchi yangu, Leo nimelipa.

3. Mwaminifu, Ameoa mpenzi wake wa utotoni Antonella. Hana skendo, hana matatizo. Alisema ,Familia yangu ndio tuzo yangu kubwa kuliko Ballon d'Or na alimweka baba yake kuwa meneja wake kwa kutambua mchango wa baba yake.


MAFUNZO  MAKUBWA 4 KUBWA KUTOKA MAISHA YA MESSI



1. Udogo sio kikwazo Watu walimwambia we ni mfupi, huwezi. Leo ni mfupi zaidi kuwahi kushinda Ballon d'Or. Akatumia udogo wake kama silaha  ni mgumu kumshika kwa sababu kituo chake cha mvuto ni chini, na hakutishwa na kelele za watu.

2. Baada ya maumivu huja furaha,


 Sindano 1000 kwa miaka 3. Hakuna talenti bila maumivu. Talenti na nidhamu  zimempa historia.

3. Usiache wakati watu wanacheka, Argentina ilimcheka kwa 16 miaka. 2022 akawanyamazisha wote. Kombe la Dunia ndio jibu lake.

4. Mshinde kimya, Messi hana kelele  Anafanya kazi, anafunga, anarudi nyumbani kwa familia. Alionyesha unaweza kuwa bora bila kupiga kelele.

Nukuu yake maarufu ya Messi.

"Utalazimika kujitahidi mara 10 zaidi ya wengine kama unataka kufanikiwa. Nilifanya hivyo nikawa mdogo, na bado nafanya hivyo leo".



Tuesday, June 23, 2026

TEMBO: MHANDISI WA ASILI ANAYEWAWEZESHA WENGINE KUISHI


šŸ“Je, akitoweka nani ataendeleza kazi yake?


Na. Beatus Maganja,

+255 676 475 541.

Tembo ni mnyama wa aina gani?! Je mnyama huyu ana faida gani katika sayari hii tuliyomo?!  Kwanini Tanzania inajivunia kuwa na tembo?!  Kwanini mikataba ya kimataifa inamlinda tembo?!! Kwanini tembo, kwanini? Nauliza kwanini ?!!

Haya ni maswali, maswali yanayosumbua fikra za binadamu, ambapo  Kwa wengi wetu tukimtazama tembo, tunamwona ni mnyama mkubwa mwenye nguvu nyingi, anayepita porini aking'oa miti na wakati mwingine kuingia mashambani kusababisha uharibifu na hata kuleta madhara kwa binadamu. Lakini kuna swali ambalo wengi wetu hatujawahi kujiuliza, kwamba Je, nyuma ya ukubwa wake huo, athari zake kuna kazi gani kubwa anayoifanya kwa manufaa ya viumbe wengine na hata binadamu? 

Ukweli ni kwamba tembo si mnyama wa kawaida. Ni mnyama mwenye maajabu mengi ambayo watafiti walitumia miongo kadha wa kadha kuvumbua . Hivi umewahi kujua  kuwa tembo ni mhandishi kwa asili yake?!! Naam, tembo ni mhandisi wa mazingira ambaye kazi zake zinawezesha maisha ya maelfu ya viumbe kuendelea kuwepo kila siku katika sayari ya dunia.

Fikiria msitu mkubwa uliokauka wakati wa kiangazi. Mito imepungukiwa  maji, mabwawa yamekauka na viumbe wengi wako katika hatari ya kufa kwa kiu. Katika mazingira hayo magumu, anaibuka mnyama tembo ambaye kwa kutumia meno na miguu yake anachimba maeneo yenye unyevunyevu hadi maji yatoke ardhini. Anapomaliza kunywa na kuondoka, swala, pundamilia, nyani, ndege na viumbe wengine wengi huja kutumia maji hayo. Bila kujua, tembo huwa ameokoa maisha ya mamia ya viumbe ambao hawana uwezo wa kufanya kazi hiyo.

Si hivyo tu. Tembo anapotembea mamia ya kilomita kutafuta chakula, hubeba mbegu za miti mingi kupitia kinyesi chake na kuzisambaza maeneo mbalimbali. Mbegu hizo huota na kuwa miti mipya. Miaka inapopita, miti hiyo hugeuka kuwa misitu inayovutia mvua, kuhifadhi maji na kutoa hewa safi tunayovuta kila siku. Kwa lugha rahisi, tembo ni mpandaji miti wa asili ambaye hafanyi kampeni wala kutafuta sifa wala kutambuliwa, lakini matokeo ya kazi yake yanaonekana kwa vizazi vingi.

Katika misitu minene, tembo amekuwa akifungua njia kwa kuvunja matawi na kusafisha mapito. Njia hizo hutumiwa na wanyama wengine kutafuta chakula, maji na maeneo salama ya kuishi. Hata mbegu zinazoota ardhini hupata nafasi ya kukua kwa sababu mwanga wa jua hupenya kwenye maeneo aliyopita. Hivyo, tembo si mnufaika wa mazingira pekee; bali ni mmoja wa watengenezaji wakuu wa mazingira hayo.

Jambo ambalo wengi hatulioni ni kwamba faida za tembo hazibaki porini tu. Maelfu ya watalii kutoka duniani kote huja Tanzania kushuhudia uzuri wake. Wageni hao huacha fedha zinazochangia uchumi wa Taifa, kuongeza ajira kwa vijana na kusaidia ukuaji wa biashara mbalimbali katika jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi. Kwa namna hiyo, tembo anageuka kuwa daraja linalounganisha uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya wananchi.

Sasa, hebu tufikirie kwa undani zaidi. Kama tembo wote wangetoweka leo, nani angechimba visima vya asili wakati wa ukame? Nani angesambaza mbegu za maelfu ya miti kwa umbali mkubwa kiasi hicho? Nani angeendelea kufungua njia za asili zinazotumiwa na viumbe wengine porini? Ukweli ni kwamba baadhi ya kazi anazozifanya tembo haziwezi kufanywa kwa ufanisi uleule na mnyama mwingine yeyote.

Ndiyo maana tunapomtazama tembo, tusione ukubwa wake pekee wala tusikumbuke madhara yake pekee. Tumuone kama mhandisi wa mazingira/ikolojia, mzalishaji wa misitu, mtoa maji kwa viumbe wengine na mshirika muhimu wa maisha duniani. Kadiri tunavyozidi kumwelewa, ndivyo tutakavyogundua kuwa tembo si mzigo wa mazingira, bali ni moja ya zawadi kubwa ambazo asili imeikabidhi Tanzania, na Mungu ameitunuku  dunia kwa ujumla wake 

Endelea kubaki katika kurasa za TAWA  ujifunze mengi kuhusu wanyamapori na faida zao kwetu. Tchao!!

#tawatzanzania #tumerithishwa #tuwarithishe

Monday, June 22, 2026

ZAIDI YA WANANCHI 300 WATEMBELEA BANDA LA TARURA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA

 


# Wananchi wa Kimara kunufaika na ujenzi wa barabara ya TRA - King'ongo


Dodoma:

ZAIDI ya wananchi 300 wametembelea banda la Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) tangu kuanza kwa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, wakipata elimu na ufafanuzi kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya barabara za wilaya katika maeneo yao.

Hatua hiyo imeendelea kuimarisha uhusiano kati ya wananchi na taasisi hiyo, huku ikitoa fursa ya kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi moja kwa moja.

Akizungumza katika maonesho hayo, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma Bi. Catherine Sungura amesema  wananchi wanaowasilisha kero zao huunganishwa moja kwa moja na mameneja wa maeneo husika ili kupata maelezo ya kina na ufumbuzi wa haraka.

“Tunawapokea wananchi wengi kutoka maeneo tofauti ya Tanzania ambao wengi wanataka kufahamu ujenzi au matengenezo ya barabara katika maeneo yao na hivyo wengi wao wanapata majibu hapo hapo kwani wanazungumza moja kwa moja na mameneja wa mkoa au wilaya husika”.

Amesema  lengo la TARURA ni kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu miradi inayotekelezwa pamoja na hatua mbalimbali za maendeleo yake.

Bi. Sungura ametolea mfano wa mwananchi mmoja kutoka Kimara jijini Dar es Salam Bi. Sarah James Joseph ambaye amefika katika banda na kutaka kujua ujenzi wa barabara ya Kimara mwisho hadi king’ongo ujenzi wake umefikia wapi ambapo mwananchi huyo ameweza kuwasiliana na Meneja wa Wilaya ya Ubungo na kupata ufafanuzi na hivyo kupokea majibu kwa furaha na kuridhika na huduma aliyoipata kwenye banda la TARURA.

Akizungumzia maendeleo ya ujenzi wa barabara ya King'ongo iliyopo Kimara, Wilaya ya Ubungo mkoani Dar es Salaam, Bi. Sungura amesema  barabara hiyo inajengwa kwa kiwango cha zege kuanzia TRA kuelekea King'ong'o ambapo kilomita 1.6 pekee zimebaki na kati ya hizo, mita 800 zinatarajiwa kujengwa kuanzia Julai mwaka huu, huku sehemu iliyobaki ikikamilishwa katika awamu inayofuata.

Bi. Sungura amesisitiza kuwa TARURA itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara ili kurahisisha usafiri na mawasiliano kwa wananchi na kwamba barabara bora huchochea upatikanaji wa huduma za kijamii, biashara na shughuli nyingine za maendeleo, hatua inayochangia kuinua ustawi wa jamii na kukuza uchumi wa maeneo mbalimbali nchini.

Kwa upande wake Bi. Sarah James Joseph mkazi wa King'ongo, Kimara jijini Dar es Salaam ameishukuru TARURA kwa kazi zao na juhudi kubwa wanazozifanya kila siku kwaajili ya kuwasaidia   wananchi katika suala la mawasiliano ya barabara nchini.






Katambi Awaonya Wahalifu na Maandamano haramu ya Tarehe 7



Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi amewaasa watu wanaotoa kauli za kichochezi katika mitandao ya kijamii,majukwaa ya kisiasa na maeneo mbalimbali ambapo kauli hizo za kibaguzi na kichochezi zinahusu  Muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Viongozi mbalimbali wa serikali au wa dini.


Waziri Katambi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waumini wa Msikiti wa Mukadam uliopo  Kata ya Chang’ombe iliyopo wilaya ya Dodoma Mjini ambapo kumefanyika Mashindano ya Quran na Harambee ya Ujenzi wa Msikiti huo.


“Taifa hili limejengwa kwa maumivu makubwa ya waasisi,limejengwa kwa jasho na hata damu ilipobidi ili Taifa Tanzania liwepo,nitumie fursa hii kuwaomba sana na kuwaasa wale wote ambao wanatumia majukwaa ya kisiasa kuchonganisha wananchi,kuwajaza chuki,kuchochea lakini pia kuhamasisha kufanya uhalifu na wanaounda magenge ya uhalifu yanayolenga kuharibu taifa letu,niwasihi na kuwaomba waache mara moja kwasababu kufanya hivyo hakuna ambae atabaki salama tutaathirika sisi Watanzania wote na athari hii italiathiri taifa kisiasa,kiuchumi na kiutamaduni.” amesema Waziri Katambi


“Tutarudi nyuma kimaendeleo,tutashindwa kuswali,tutashindwa kwenda kanisani,tutashindwa kufanya kazi za kiuchumi,tutashindwa kujenga nchi yetu,tutashindwa kujenga uchumi wa mtu mmoja mmoja ,tuwakanye na kuwaelekeza vijana wetu wakaishi mwenendo mwema na uzalendo kwa taifa lao na pale yanapotolewa maonyo na maelekezo ya vyombo vya ulinzi na usalama wasikaidi kwani kwenda kinyume ni kuvunja sheria,katiba na taratibu.” aliongeza Waziri Katambi

Ukaguzi wa Leseni za Madini Waimarisha Uzingatiaji wa Sheria Nchini

 


šŸ“DODOMA


Tume ya Madini imeendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa leseni za madini nchini kwa lengo la kufuatilia maendeleo ya leseni hizo na kuhakikisha shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini zinafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Akizungumza katika Banda la Tume ya Madini kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park mkoani Dodoma, Mtakwimu kutoka Kurugenzi ya Leseni ya Tume ya Madini, Azihar Kashakara, amesema ukaguzi huo ni muhimu katika kuhakikisha wamiliki wa leseni wanatimiza masharti na wajibu unaotokana na leseni walizopewa.

Amesema kuwa, pamoja na kufuatilia maendeleo ya leseni, Kurugenzi ya Leseni ina jukumu la kutoa na kusimamia leseni za madini, kutafsiri na kusambaza takwimu za leseni, pamoja na kuwezesha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali yatokanayo na umiliki wa leseni hizo.

Kashakara ameeleza kuwa utoaji wa leseni za madini unazingatia masharti na vigezo vilivyowekwa kisheria, hivyo waombaji wanapaswa kuyatimiza ili kuwezesha upatikanaji wa leseni kwa wakati. 

Aidha, ametoa ufafanuzi kuhusu ada na tozo mbalimbali zinazohusiana na leseni za madini, sambamba na kueleza tofauti kati ya umiliki wa ardhi (Surface Rights) na umiliki wa haki za madini (Mineral Rights).

Tume ya Madini ni miongoni mwa taasisi zinazoshiriki Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma chini ya kaulimbiu isemayo, “Kuchochea Uwajibikaji kwa Huduma Endelevu.” 

Kupitia maonesho hayo, wananchi na wadau wa sekta ya madini wanapata fursa ya kuelimishwa kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na Tume ya Madini pamoja na mchango wake katika usimamizi endelevu wa rasilimali za madini kwa maendeleo ya taifa.





West Kili Forest Tour Challenge 2026 Yavutia Washiriki Zaidi ya 350

 


Zaidi ya washiriki 350 kutoka ndani na nje ya Tanzania wamejitokeza kushiriki mashindano ya West Kili Forest Tour Challenge 2026 yaliyofanyika katika Shamba la Miti West Kilimanjaro, Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro, yakilenga kuhamasisha uhifadhi wa mazingira, utalii wa misitu na afya kupitia michezo.

Mashindano hayo yaliyoandaliwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) chini ya kaulimbiu ya “Experience the Difference, Explore Life in Nature” yalihusisha mbio za kilomita 5, 10 na 21, mashindano ya baiskeli, pikipiki, matembezi ya misituni pamoja na shughuli mbalimbali za utalii wa mazingira.

Akizungumza wakati wa kufunga mashindano hayo Leo Juni 21,2026, Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka, alisema tukio hilo limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza Siha kama kitovu cha utalii wa asili na michezo huku likichochea shughuli za kiuchumi kwa wananchi kupitia biashara mbalimbali zinazohusiana na utalii.

Dkt. Timbuka aliipongeza TFS kwa kuendelea kuandaa mashindano hayo na kusema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha yanaendelea kukua na kuvutia washiriki wengi zaidi kutoka ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Siha, Hellen Mwambeta, alisema mashindano hayo yamechangia kuhamasisha wananchi kufanya mazoezi, kuimarisha afya na wakati huo huo kuongeza mzunguko wa fedha kupitia huduma zinazotolewa kwa wageni wanaofika kushiriki tukio hilo.

Mratibu wa mashindano hayo, Mensieur Elly, alisema washiriki wa mwaka huu walitoka katika maeneo mbalimbali ya Tanzania pamoja na Kenya na Uganda, huku wageni wengine wakitokea Ujerumani na Scotland, jambo linaloonesha kuongezeka kwa umaarufu wa mashindano hayo kimataifa.

Naye Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti West Kilimanjaro, PCO. Robert Faida, alisema West Kili Forest Tour Challenge ni sehemu ya juhudi za TFS za kuhamasisha uhifadhi wa mazingira kupitia michezo na utalii endelevu, huku ikitoa fursa kwa washiriki kujifunza kuhusu umuhimu wa kulinda mfumo wa ikolojia wa Kilimanjaro.

Mwisho wa mashindano hayo, washiriki wote walitunukiwa medali za kumbukumbu kwa kutambua mchango wao katika kuhamasisha michezo, utalii wa misitu na uhifadhi wa mazingira,na washindi mbalimbali walipewa zawadi huku TFS ikiahidi kuendelea kuimarisha tukio hilo ili liwe moja ya matukio makubwa zaidi ya michezo na utalii nchini.