ANGALIA LIVE NEWS

Thursday, August 6, 2026

TFS YAANDIKA HISTORIA KWA KUSHIRIKI MAONESHO YA KILIMO ZANZIBAR KWA MARA YA KWANZA, YAPOKELEWA KWA KISHINDO

  



Na Mwandishi Wetu, Dole Kizimbani, Zanzibar

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeandika historia kwa kushiriki kwa mara ya kwanza Maonesho ya Kilimo Zanzibar, hatua iliyopokelewa kwa pongezi na viongozi pamoja na wananchi kutokana na kupeleka elimu na fursa za kiuchumi zinazotokana na uhifadhi wa misitu na nyuki visiwani humo.

Mafanikio hayo yalidhihirika Agosti 5, 2026, baada ya Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar, Haroun Ally Suleiman, kutembelea banda la TFS katika Viwanja vya Dole, Kizimbani na kupongeza uamuzi wa wakala huo kuvuka bahari na kuwaletea Wazanzibari huduma za elimu ya uhifadhi pamoja na fursa za uwekezaji.

    "Niwapongeze sana TFS kwa kuona umuhimu wa kutangaza fursa za uhifadhi hapa Zanzibar. Ni hatua nzuri ambayo itawanufaisha wananchi kwa kuwawezesha kuibua vyanzo vipya vya mapato kupitia uhifadhi wa misitu," alisema Waziri Haroun.

Alisema ushiriki wa TFS katika maonesho hayo unafungua milango mipya ya ushirikiano kati ya Tanzania Bara na Zanzibar katika kukuza uchumi kupitia matumizi endelevu ya rasilimali za misitu na nyuki, huku akiitaka taasisi hiyo kuendelea kushiriki maonesho na kampeni za uelimishaji visiwani humo.

Kwa upande wake, Mhifadhi Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Francis Kiondo, alisema ushiriki huo wa kwanza Zanzibar ni sehemu ya mkakati wa TFS wa kusogeza huduma karibu na wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuhakikisha fursa za uhifadhi zinawafikia Watanzania bila kujali walipo.

Alisema kupitia maonesho hayo, wananchi wanapata elimu kuhusu uhifadhi wa misitu na nyuki, uzalishaji wa mbegu bora za miti na miche, ufugaji nyuki, fursa za uwekezaji katika sekta ya misitu pamoja na utalii wa ikolojia, ambao unazidi kuwa chanzo muhimu cha ajira na mapato.

Maonesho ya Kilimo Zanzibar yanaendelea katika Viwanja vya Dole, Kizimbani kuanzia Agosti 1 hadi 14, 2026, ambapo TFS imewahimiza wananchi kutembelea banda lake ili kujifunza na kutumia fursa mbalimbali zinazotokana na uhifadhi endelevu wa rasilimali za misitu.

UONI HAFIFU WAONGOZA CHANGAMOTO KWA WANAOPIMA MACHO BANDA LA MUHIMBILI NANE NANE



Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imesema tatizo la uoni hafifu linaongoza miongoni mwa changamoto zinazobainika kwa wananchi wanaofika kupima afya ya macho katika Maonesho ya Wakulima (Nanenane) yanayoendelea katika viwanja vya Dk. Samweli Malechela, jijini Dodoma, ambapo huduma za uchunguzi wa macho, elimu na ushauri wa kitaalamu zinatolewa bure. 

Akizungumza Dkt. Bingwa wa Magonjwa ya Macho kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Johannes Mafwili, amesema wananchi wengi wanaofika katika banda la hospitali hiyo hupatikana na tatizo la uoni hafifu, huku wakifanyiwa uchunguzi wa kina na kupatiwa ushauri wa kitaalamu kulingana na hali zao. 

Amesema uchunguzi wa mapema husaidia kubaini magonjwa mbalimbali ya macho kabla hayajasababisha madhara makubwa, hivyo amewahimiza wananchi kutumia fursa ya maonesho hayo kupima afya ya macho bila kusubiri dalili kuwa mbaya. 

Dkt. Mafwili amewataka wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nane Nane kufika katika banda la Hospitali ya Taifa Muhimbili ili kunufaika na huduma hizo za bure na kupata elimu itakayowasaidia kulinda afya zao.











Wednesday, August 5, 2026

NCAA, BODI YA MIKOPO WAPELEKA TABASAMU JIPYA KWA WANAFUNZI KUTOKA HIFADHI YA NGORONGORO


Serikali kupitia Mamlaka ya hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) kwa kushirikiana na Bodi ya Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu (HESLB), imeanzisha mfuko wa  Ngorongoro Scholarship Fund  kwa lengo la kuwezesha wanafunzi wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kupata fursa ya masomo ya elimu ya juu kupitia ufadhili Ngorongoro Fund.  

Akizungumza wakati wa mkutano wa waandishi wa Habari Jijini Dar es salaam kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi, Kamishna msaidizi mwandamizi wa uhifadhi anayesimamia idara ya Maendeleo ya Jamii Gloria Bideberi ameeleza kuwa, Program hiyo inalenga  kuboresha maisha ya jamii zinazoishi ndani ya hifadhi,  ambapo kwa kushirikiana na bodi ya mikopo ya elimu ya juu watahakikisha kila mtoto anayeishi ndani ya hifadhi  hiyo anayekidhi vigezo anapata nafasi ya kupata ufadhili wa elimu ya juu.

“Kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ufadhili huu utasaidia kuondoa malalamiko ya upendeleo, taratibu zote za ufadhili wa vijana wetu zitakuwa wazi kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa tukitambua kuwa elimu ndiyo msingi wa kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na mazingira” amesema kamishna Bideberi.

Ameongeza kuwa Ngorongoro Fund inaongozwa na kauli mbiu isemayo "Elimu Endelevu kwa Maendeleo ya Jamii na Uhifadhi" itakwenda  kufadhili watoto wa kitanzania waliodahiliwa katika vyuo vilivyopo ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kunufaisha vijana watakaojikita katika masomo ya uhifadhi  wa Wanyamapori na misitu, Malikale na utalii na hapo baadaye wigo utaendelea kutanuliwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji  wa HESLB Dkt. Bill Kiwia amesema kuanzia mwaka wa masomo 2026/2027, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), kwa kushirikiana Ngorongoro, itaanza kutoa ufadhili huo maalum kwa wanafunzi kutoka eneo la Hifadhi ya Ngorongoro watakaosoma fani zinazohusiana na uhifadhi wa maliasili, usimamizi wa wanyamapori, pamoja na taaluma nyingine zitakazoainishwa katika Mwongozo wa Utoaji wa Scholarship hiyo.

Dkt. Kiwia ameeleza kuwa hatua ya kwanza ya utekelezaji wa mpango huu utaanza kwa kutoa ufadhili kwa wanafunzi 15, ambapo Ngorongoro imetenga shilingi milioni 99 kugharamia masomo ya ufadhili na kuwawezesha vijana hao kupata elimu ya juu, kujenga wataalamu watakaosaidia kuhifadhi rasilimali za Taifa, na kuchochea maendeleo endelevu ya jamii zinazozungukaHifadhi ya Ngorongoro.

Kwa ushirikiano wa karibu kati ya HESLB na NCAA, tayari tumekamilisha Mwongozo Maalum wa Utoaji wa Scholarship ya NCAA ambapo mwongozo huo umeweka vigezo, taratibu na masharti ya utoaji wa ufadhili huo kwa wanafunzi wanaotoka katika jamii zinazoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kutambua programu mahususi zitakazopewa kipaumbele, hususan zile zinazohusiana na uhifadhi wa maliasili, usimamizi wa wanyamapori na taaluma nyingine zinazochangia maendeleo endelevu ya eneo la Ngorongoro na Taifa kwa ujumla.

Sambamba na mwongozo huo, HESLB imekamilisha maandalizi ya mfumo wa kidijitali wa kupokea na kuchakata maombi ya scholarship ambapo hii dirisha la kupokea maombi litafunguliwa tarehe 15 Agosti, 2026, kwa sasa Ngorongoro na bodi ya mikopo zinaendelea kutoa elimu na uhamasishaji kwa waombaji watarajiwa ili kuwawezesha kuelewa vigezo vya scholarship hii na kujaza maombi yao kwa usahihi na kwa wakati.

Kabla makubaliano haya ya leo, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ilikuwa ikitekeleza  ufadhili huu kupitia Baraza la Wafugaji ambapo mpaka mwaka wa fedha uliopita 2025/2026 zaidi ya watu elfu kumi na tano kutoka ndani ya hifadhi wamepatiwa ufadhili katika  nyanja mbalimbali ikiwemo ualimu, udaktari, uhandisi, uhasibu, wataalamu wa uhifadhi na kada nyingine nyingi zinazochangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.




NAIBU WAZIRI AVUTIWA NA TEKNOLOJIA YA DRONE KATIKA UHIFADHI WA MISITU

 


Na Mwandishi Wetu, Lindi


LINDI: Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Kaspar K. Mmuya, ametembelea banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Kusini katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Kusini yanayoendelea Viwanja vya Ngongo, Manispaa ya Lindi, na kujionea teknolojia na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na TFS katika uhifadhi wa rasilimali za misitu.

Katika ziara hiyo iliyofanyika leo Agosti 4, 2026, Mmuya alijionea matumizi ya teknolojia ya drone katika uhifadhi wa misitu, shamba darasa la miti, elimu na fursa za ufugaji wa nyuki pamoja na bidhaa na huduma zinazotokana na mazao ya misitu.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi Manyisye K. Mpokigwa, ambaye ni Kamanda wa TFS Kanda ya Kusini, alisema banda hilo pia limewakutanisha wadau mbalimbali wa mazao ya misitu wakiwemo wajasiriamali wa vikapu, watengenezaji wa samani za ndani kama vitanda na milango, pamoja na wauza maua na miche ya matunda.

Alisema ushiriki wa wadau hao unalenga kuwaonesha wananchi na washiriki wa maonesho fursa zilizopo katika sekta ya misitu, huku ukihamasisha matumizi endelevu ya rasilimali za misitu kwa ajili ya kuongeza kipato na kuchochea maendeleo ya uchumi.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri alipata fursa ya kukata keki na kuonja asali safi inayozalishwa na wafugaji nyuki wanaoshirikiana na TFS kabla ya kukabidhiwa zawadi ya Asali ya Nyuki Wadogo na Kamanda wa TFS Kanda ya Kusini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Manyisye K. Mpokigwa.

Maonesho ya Nanenane Kanda ya Kusini yanaendelea Viwanja vya Ngongo, Manispaa ya Lindi, yakibeba kaulimbiu isemayo, “Tambua Soko: Ongeza Tija Kutekeleza Dira ya 2050,” huku yakitarajiwa kuendelea kuvutia washiriki na wadau kutoka sekta mbalimbali za uzalishaji nchini.







TANZANIA YAITAKA DUNIA KUONGEZA NGUVU KULINDA BIOANUWAI



NAIROBI: Tanzania imezitaka nchi duniani kuimarisha ushirikiano, kuongeza fedha na kuharakisha uhamishaji wa teknolojia ili kufanikisha  Muundo wa utekelezaji wa Kunming-Montreal wa Baioanuai (KMGBF), ikisema hatua hizo ni muhimu kuzuia kuendelea kwa uharibifu wa baioanuai ifikapo mwaka 2030.

Msimamo huo uliwasilishwa na Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi kwa niaba ya jopo la wataalam wa Mazingira wa Tanzania Fandey H. Mashimba, katika Mkutano wa Saba wa Chombo Tanzu cha Utekelezaji (SBI-7) chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Baioanuai (CBD), unaofanyika Nairobi, Kenya. Tanzania pia iliunga mkono tamko la Ghana lililotolewa kwa niaba ya Kundi la Afrika (African Group).

Mashimba alisema Tanzania imeendelea kutekeleza malengo ya KMGBF kupitia Mkakati na Mpango wa Taifa wa Baioanuai (NBSAP), huku ikiimarisha uhifadhi wa misitu na maeneo yenye utajiri mkubwa wa baioanuai (biodiversity hotspot), wanyamapori, bahari na ukanda wa pwani, pamoja na kurejesha mifumo ya ikolojia kwa kushirikisha jamii.

Alisema juhudi hizo zinafanyika Tanzania Bara na Zanzibar, zikihusisha maeneo yenye mifumo muhimu ya kiikolojia kama vile misitu ya Miombo na mbuga (savannah) maeneo oevu, mikoko, miamba ya matumbawe, milima na visiwa vyenye utajiri mkubwa wa baioanuai.

Hata hivyo, Tanzania ilisema mafanikio ya utekelezaji wa muundo huo yatategemea upatikanaji wa fedha za uhakika, ushirikiano wa kisayansi, ujenzi wa uwezo na kuboreshwa kwa mifumo ya ukusanyaji na usimamizi wa taarifa za baioanuai.

Aidha, ilizitaka taasisi za kimataifa kuongeza msaada kwa nchi zinazoendelea kupitia Mfuko wa Muundo wa utekelezaji wa Kimataifa wa Baioanuai (Global Biodiversity Framework Fund–GBFF) pamoja na Mfuko wa Mazingira wa Dunia (Global Environment Facility–GEF) ili ziweze kutekeleza kwa ufanisi malengo ya mkataba huo.

Tanzania pia ilisisitiza kuwa tathmini za kimataifa zinapaswa kuzingatia mazingira na uwezo wa kila nchi, badala ya kutafsiri upungufu wa takwimu kuwa ushahidi wa utekelezaji dhaifu.

Akihitimisha tamko hilo, Mashimba alisema Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama wa Mkataba wa Baioanuai kuhakikisha malengo ya Muundo wa Kunming-Montreal yanafikiwa ifikapo mwaka 2030.



Sunday, August 2, 2026

KATIBU MKUU WA BARAZA LA MAWAZIRI ZAMBIA APONGEZA HUDUMA ZA HOSPITALI YA RUFAA YA KANDA MBEYA

 



Diplomasia ya kiuchumi na sekta ya utalii wa matibabu (Medical Tourism) katika ukanda wa Kusini mwa Afrika (SADC) umezidi kuimarika. Hii ni kufuatia ziara ya Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Baraza la Mawaziri nchini Zambia, Ndugu Patrick Kangwa, alipotembelea banda la Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya na Taasisi ya Mifupa na Ubongo MOI ililopo chini ya Banda la Tanzania katika Maonyesho ya 98 ya Kilimo na Biashara yanayoendelea jijini Lusaka. 

Ndugu Kangwa amepongeza namna hospitali inavyotekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya maonyesho ya mwaka huu inayosema "Fostering Trade and Investment" (Kukuza Biashara na Uwekezaji). 

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Ndugu Kangwa alieleza kuvutiwa kwake na ubora wa huduma za kibingwa zinazotolewa na Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, ikiwemo matibabu ya magonjwa ya moyo, mifupa, upasuaji wa mgongo, pamoja na huduma za kibingwa za uzazi na utatuzi wa changamoto za kushika ujauzito. 

Alibainisha kuwa uwezo huo mkubwa wa kitabibu ni fursa adhimu kwa raia wa Zambia na nchi jirani kupata matibabu ya uhakika bila kusafiri umbali mrefu. Mbali na viongozi wa kitaifa, banda la MZRH limeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa raia na wadau wa afya nchini Zambia waliomiminika kujionea, kujifunza, na kupata ushauri wa kitaalamu.







Saturday, August 1, 2026

HIKE 4 GIRLS UGANDA TEAMS DEPART FOR MT. MGAHINGA MENSTRUAL HEALTH TREK


TEAMS from Raising Teenagers Uganda (RTU) and partners kicked off the ninth Hike4GirlsUg today, heading to Kisoro District for a trek up Mt. Mgahinga to spotlight menstrual health, dignity, and girls' education. 

The annual event fights period poverty and stigma that sideline girls from school, with participants flashing peace signs and exchanging items amid an upbeat mood. Past hikes have reached thousands with pads and education, and this year builds on that by blending the physical challenge with community advocacy.


















Thursday, July 30, 2026

KATIBU MKUU WIZARA YA AFYA NA MKURUGENZI MTENDAJI MUHIMBILI WAWEKA MIKAKATI MADHUBUTI KUBORESHA MFUMO WA MALIPO YA HUDUMA ZA AFYA



Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Dellilah Kimambo, kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za afya na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha mfumo wa malipo ya huduma ili kuwawezesha wananchi kupata huduma kwa urahisi, haraka, kwa ufanisi na kuondoa malalamiko ya wananchi.

Katika kikao hicho, Dkt. Magembe amesisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma za afya, akimtaka Mkurugenzi Mtendaji kuhakikisha mifumo ya TEHAMA ya hospitali inaendelea kuimarishwa ili kurahisisha mchakato wa malipo ya huduma, kuongeza uwazi kwa wananchi, kupunguza usumbufu na muda wa kusubiri kwa wagonjwa, pamoja na kuondoa udanganyifu.

“Mwananchi apate taarifa za malipo anayotakiwa kufanya kiganjani mwake kupitia simu ili kabla ya kulipa ajihakikishie kama malipo hayo ni sahihi au hapana”, amesema Dr Grace. 

Amemwelekeza Mkurugenzi wa Muhimbili kuimarisha usimamizi wa huduma za afya kupitia viongozi walioko chini yake wakiwemo wakurugenzi, mameneja na wasimamizi wote na endapo kutakuwa na watumishi wowote wasiowajibika achukue hatua zilizo chini ya mamlaka yake na mengine yanayohitaji Wizara kufanyia kazi, ayawasilishe ili hatua stahiki zichukuliwe. 

Amepongeza maboresho yanayoendelea kufanyika ikiwemo watumishi wanaofanya kazi kwa kujituma na weledi mkubwa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe (kushoto) akifanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Dellilah Kimambo


DC KYOBYA MGENI RASMI TUKIO LA KIHISTORIA "HIKE FOR A GIRL CHILD" UDZUNGWA AGOSTI 2

Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Wakili Msomi Dkt. Dunstan Kyobya


KILOMBERO - 

Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Wakili Msomi Dkt. Dunstan Kyobya anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi kwenye tukio la kihistoria la Matembezi ya Vilimani ili kupaza Sauti kwa Ajili ya Mtoto wa Kike, _"Hike for A Girl Child"_.

Tukio hilo lenye lengo la kuvunja ukimya na unyanyapaa masuala ya Hedhi Salama kwa Watoto wa Kike, litafanyika tarehe 2 Agosti 2026, katika Hifadhi ya Taifa ya Milima ya Udzungwa, Wilaya ya Kilombero, Mkoa wa Morogoro.

Kwa mujibu wa Waratibu wa kampeni hiyo kutoka The Brighter Binti Foundation (TBBF) kwa Kushirikiana na Tanzania Save the Community Initiatives (TASACI),  Dkt. Kyobya anatarajiwa kuzindua daraja la Utalii katika njia ya Sonjo Route tayari kwa matembezi ya vilimani.

"Agosti 2, saa 1:00 Asubuhi, Mkuu wa Wilaya Dkt. Kyobya atazindua rasmi daraja la Utalii, kisha kufanya 'Hike' njia ya maporomoko ya maji ya Sanje ambapo washiriki wote tutajumuika," wamesema waratibu hao.

Mchana, matukio mengine yatafanyika Shule ya Sekondari Sanje ambapo kutakuwa na shughuli mbalimbali zikiwemo: Mawasilisho mafupi juu ya Mwongozo wa Hedhi Salama, Elimu ya Malezi ya Familia, Afya ya Akili na Saikolojia.

Pia kutakuwa na Clinic ya Hedhi Salama kwa Jamii, Wanafunzi na Walimu, Maonesho ya bidhaa za Hedhi, Hotuba fupi ya Dkt. Kyobya kwa Wananchi, Wanafunzi na Wadau, sambamba na Utoaji wa Taulo za Hedhi kwa Shule ya Sekondari Sanje na zile za karibu kuzunguka Hifadhi ya Udzungwa.

The Brighter Binti Foundation wanasema wanaamini mabadiliko huanza na Jamii, hivyo matembezi hayo ya vilimani yataongeza umuhimu wa jamii kwa ujumla katika kuelewa na kuondoa unyanyapaa wa hedhi hapa nchini.

_"Mabadiliko huanza pale jamii inapopata uelewaji sahihi na kuondoa unyanyapaa wa hedhi. Tunapanda mlima huu sio kwa raha tu. Tunapanda kwa ajili ya Mtoto wa Kike"._

The Brighter Binti Foundation imewashukuru wadau wote wakiwemo: Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Halimashauri ya Wilaya ya Kilombero, Hifadhi ya Taifa ya Udzungwa - TANAPA, TASACI, RTU, Wizara ya Afya, SAFEPAD, She Foundation Tanzania, ICON, FOCAYO, Next Fox Adventures, ARQ, PEPAIN, ToneHai, ONE DRAIN, SAWA na wadau wengine.



Wednesday, July 29, 2026

SIMBA SC ELIMINATED CECAFA KAGAME CUP 2026

Simba SC are officially out of the competition. 🇹🇿❌

The Tanzanian giants have collected just 2 points from 2 games, with one match remaining against Singida Black Stars.

Even if Simba win their final game, they can only reach 5 points.

That won’t be enough to finish as the best 2nd-placed team and qualify for the semi-finals, with Al Hilal and Rayon Sports already on 6 points.

A disappointing campaign for Simba. 

#CECAFAKagameCup2026 #AfricanFootball

#NguvuMoja

JE KUMBUKUMBU HII INA KUKUMBUSHA NINI?.


Na. Bariki Ngowo, Tanzania.

Baada ya Tanzania kupata uhuru mwaka 1961, serikali ilianza kujenga uchumi unaotegemea umiliki wa umma kupitia sera za Ujamaa na Kujitegemea. 

Sekta ya utalii ilitambuliwa kuwa chanzo muhimu cha mapato ya taifa, hivyo serikali ikaamua kuanzisha taasisi mbalimbali za kusimamia hoteli, safari na huduma za watalii.

Miongoni mwa taasisi hizo ilikuwa State Travel Services Ltd. (STS), iliyoanzishwa mwaka 1970 ikiwa kampuni tanzu ya Tanzania Tourist Corporation (TTC). 

Jukumu lake lilikuwa kutoa huduma za uwakala wa safari, kuhifadhi tiketi za ndege, kupanga safari za watalii, pamoja na kuhudumia serikali, mashirika ya umma na wananchi.

Katika kipindi hicho, TTC ilisimamia mtandao mpana wa hoteli na kampuni za utalii nchini. 

Mbali na STS, ilisimamia Kilimanjaro Hotel, New Africa Hotel, New Safari Hotel, Mwanza Hotel, Mount Meru Hotel pamoja na malazi na lodges nyingi za mbugani. 

Mfumo huu uliifanya serikali kuwa mdau mkuu wa sekta ya utalii nchini.

Ili kuimarisha utalii katika Kanda ya Kaskazini, serikali ilianzisha Mount Meru Hotels Ltd. mwaka 1973, kampuni iliyokuwa chini ya TTC kwa umiliki wa asilimia 80. 

Kampuni hiyo ilisimamia ujenzi na uendeshaji wa Mount Meru Hotel mjini Arusha, ambayo ilikamilika mwishoni mwa miaka ya 1970 na kuwa hoteli muhimu kwa watalii na mikutano ya kimataifa.

Ingawa kuna simulizi zinazodai kuwa Mount Meru Hotel ilijengwa na kampuni ya Israel, hadi sasa hakuna nyaraka rasmi zilizopatikana zinazotaja jina la mkandarasi wa awali. 

Tofauti na Kilimanjaro Hotel, historia ya ujenzi wa Mount Meru Hotel haijawekwa wazi katika kumbukumbu za umma zinazopatikana.

Katika miaka ya 1980, sekta ya utalii ilikumbwa na changamoto za kiuchumi, hivyo serikali ilianza kushirikisha kampuni za kimataifa katika usimamizi wa baadhi ya hoteli zake ili kuboresha huduma na kuongeza ushindani. 

Hatua hizi zilikuwa sehemu ya maandalizi ya mageuzi ya uchumi yaliyofuata.

Kuanzia mwishoni mwa miaka ya 1980 na hasa miaka ya 1990, Tanzania ilianza kutekeleza sera za ubinafsishaji. 

Mashirika mengi ya umma yalivunjwa, kuuzwa au kubadilishwa mfumo wa uendeshaji. 

Hali hiyo iliathiri pia STS, ambayo ilipoteza nafasi yake baada ya kampuni binafsi za usafiri na uwakala wa safari kuingia kwa wingi sokoni.

Mount Meru Hotel nayo iliendelea kupitia mabadiliko hayo. 

Hatimaye kampuni ya Mount Meru Hotel Ltd. ilibinafsishwa mwaka 2004, na baadaye hoteli ikafanyiwa ukarabati mkubwa na kurejea katika hadhi yake kama moja ya hoteli bora za Arusha zinazohudumia utalii na mikutano ya kimataifa.

Historia ya Kilimanjaro Hotel ni ya kipekee. Hoteli hiyo ilifunguliwa mwaka 1965 ikiwa hoteli kuu ya serikali kwa ajili ya kupokea wageni wa kimataifa. 

Mradi huo ulifadhiliwa na Israel na Uingereza, ukajengwa na kampuni ya Israel Solel Boneh, huku usimamizi wa mwanzo ukifanywa na kampuni ya Israel Mlonot. 

Mwaka 1972, hoteli hiyo ilitaifishwa na kuhamishiwa chini ya TTC.

Kwa ujumla, historia ya STS, Mount Meru Hotel na Kilimanjaro Hotel inaonyesha namna serikali ya Tanzania ilivyowekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya utalii baada ya uhuru. 

Taasisi hizo zilikuwa nguzo muhimu za maendeleo ya utalii wakati wa Ujamaa, kabla ya mageuzi ya uchumi na ubinafsishaji kubadilisha kabisa mfumo wa umiliki na uendeshaji wa sekta hiyo nchini.