ANGALIA LIVE NEWS

Tuesday, June 2, 2026

TANAPA YANG’ARA KIMATAIFA YATUNUKIWA TUZO YA UBORA 2026 UBELGIJI

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Nkoba Mabula


Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limeendelea kuipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa. Hii ni baada ya kutunukiwa Tuzo ya Mafanikio katika Ubora ya mwaka 2026 (Quality Achievement Award 2026) tarehe 31 Mei 2026 jijini Brussels, Ubelgiji, inayotolewa na Taasisi ya _European Society for Quality Research_ (ESQR)

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Nkoba Mabula, ameipongeza TANAPA kwa kuendelea kutoa huduma zenye kukidhi  ubora wa viwango vya kimataifa.

Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA, CPA (T) Musa N.K.Juma amesema TANAPA imepokea tuzo hiyo kwa mara ya nane mfululizo, na kwamba huu ni uthibitisho wa ubora wa huduma za TANAPA na jitihada za kimkakati za kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii duniani.

Kamishna wa Uhifadhi CPA (T) Kuji, ameongeza kuwa mafanikio hayo yanaakisi jitihada za Serikali ya awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuimarisha sekta ya utalii na kuitangaza Tanzania katika masoko ya kimataifa.



#ESQR2026 #MNRT #DestinationTanzania #TANAPA #TanzaniaUnforgettable #QualityAchievementAwards

BALOZI WA TANZANIA AWASILISHA HATI ZA UTAMBULISHO KWA MKURUGENZI MKUU WA UNESCO


Paris, Ufaransa


Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika UNESCO, Mhe. Saidi Othman Yakubu, amewasilisha rasmi Hati za Utambulisho kwa Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Profesa Khaled El-Enany, katika Makao Makuu ya Shirika hilo jijini Paris, Ufaransa.

Uwasilishaji huo wa hati unamwezesha Mhe. Balozi Yakubu kuanza rasmi majukumu yake kama Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika UNESCO, shirika la Umoja wa Mataifa linalojihusisha na masuala ya elimu, sayansi, utamaduni na mawasiliano.

Baada ya hafla hiyo, viongozi hao walifanya mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na UNESCO katika sekta za elimu, sayansi, utamaduni, uhifadhi wa urithi wa dunia pamoja na maendeleo ya rasilimali watu.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Balozi Yakubu aliwasilisha salamu za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na kueleza dhamira ya Tanzania ya kuendelea kushirikiana kwa karibu na UNESCO katika kutekeleza ajenda za maendeleo endelevu na kukuza ustawi wa wananchi kupitia elimu, sayansi na utamaduni.

Kwa upande wake, Profesa El-Enany amepongeza mafanikio na hatua za maendeleo zinazopatikana nchini Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na kueleza kufurahishwa kwake na mchango wa Tanzania ndani ya UNESCO. Aidha, ameahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na UNESCO kwa manufaa ya pande zote mbili.

Mkutano huo umeweka msingi mzuri wa kuendeleza ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na UNESCO katika maeneo mbalimbali ya maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiutamaduni.




Monday, June 1, 2026

TANAPA SHINES ON THE GLOBAL STAGE IN BRUSSELS



A proud moment for Tanzania! 🇹🇿


Tanzania National Parks (TANAPA) has been honoured with the prestigious Quality Achievement Award 2026 presented by the European Society for Quality Research (ESQR), a Switzerland-based international organization that, through its annual recognition programme, honours selected companies, institutions, public administrations and organizations representing different sectors from Europe, Asia, the Americas, Africa and Australia that have demonstrated

outstanding commitment, support and efforts to endorse and improve achievements in quality management.

The award was received today, 31 May 2026, during the Quality Achievement Award 2026 Convention held at Le Plaza Hotel in Brussels, marking another milestone for Tanzania on the global stage.

This recognition reflects TANAPA’s continued commitment to delivering quality services and sustainable conservation reinforced by its conformance to ISO 9001:2015 and its requirements.






#ESQR2

Sunday, May 31, 2026

TUME YA TAIFA YA UNESCO INARATIBU UTEKELEZAJI WA MIKATABA INAYOLINDA NA KUHIFADHI BAHARI, MAZIWA, MITO NA MAENEO OEVU



Tume ya Taifa ya UNESCO imekasimiwa mamlaka kisheria pamoja na masuala mengine, kuratibu utekelezaji wa Mikataba ya UNESCO  inayolinda na kuhifadhi bahari, maziwa, mito, na maeneo oevu kupitia mashirika yake teule kama vile Tume ya Kiserikali ya Bahari (IOC),  Mkataba wa Kimataifa wa Maeneo Oevu (Ramsar) na Mpango wa Hifadhi ya Mazingira na Binadamu.

Majukumu ya Tume ni pamoja na:

Hifadhi ya Bahari: Kuratibu mtandao wa urithi wa dunia na kupitia Tume ya Kiserikali ya Bahari inaratibu utafiti na uhifadhi wa viumbe vya baharini na kupunguza uchafuzi.

Maeneo Oevu (Ramsar): Tume inaratibu ulinzi na uhifadhi wa maeneo oevu yenye umuhimu wa kimataifa ili kuzuia uharibifu wa vyanzo vya maji na makazi ya viumbe.

Maziwa na Mito: Tume inaratibu ulinzi wa mifumo ya ikolojia ya maji baridi kupitia mpango wa Maji Duniani (IHP) na usimamizi wa hifadhi za viumbe (Biosphere Reserves).

UNESCO ina mikataba na programu muhimu zinazolenga kulinda na kuhifadhi bahari, maziwa, mito, na maeneo oevu.

Mikataba hii inasaidia katika usimamizi endelevu wa rasilimali za maji na kulinda viumbe hai.

Mkataba wa Ramsar (The Ramsar Convention): Huu ni mkataba wa kimataifa unaohusu uhifadhi na matumizi endelevu ya maeneo oevu (wetlands) na rasilimali zake.

Mkataba wa Urithi wa Dunia (World Heritage Convention): Unalinda na kuhifadhi maeneo yenye umuhimu wa kipekee kwa binadamu, ikiwa ni pamoja na maeneo ya bahari (kama vile miamba ya matumbawe) na mifumo ya maji safi ambayo imetambuliwa kuwa na thamani ya kiulimwengu.

Programu ya Biolojia na Binadamu (MAB - Man and the Biosphere Programme): Inajenga mtandao wa hifadhi za viumbe hai (Biosphere Reserves) ambazo mara nyingi hujumuisha maziwa, mito, na maeneo oevu ili kuoanisha uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya kijamii.

Tume ya Kimataifa ya Kiserikali ya Bahari (IOC-UNESCO): Hiki ni chombo pekee cha UNESCO kinachoratibu sayansi ya bahari, uchunguzi wa bahari, na mipango ya kuzuia majanga na kulinda afya ya bahari duniani.


ZAIDI YA WASAFIRI 75,000 WAFANYIWA UCHUNGUZI NA HAKUNA KISA CHA EBOLA KILICHOBAINIKA TANZANIA HADI SASA

 


Na Hassan Kimweri, WAF - Kagera 


Tanzania imeendelea kuimarisha udhibiti dhidi ya ugonjwa wa Ebola kwa kushirikiana na nchi jirani ikiwemo Uganda, Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Burundi na Kenya kupitia  ushirikiano wa kikanda ili kudhibiti kusambaa kwa maambukizi ya Ebola.

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amesema Hayo  Mei 30, 2026 akiwa katika ziara mkoani Kagera kwa lengo la kukagua udhibiti na utayari wa kukabiliana na ugonjwa huo mipakani pamoja na vituo vya afya vya kutolea huduma za dharula akiambatana na timu kutoka Wizara ya Afya, OWM- TAMISEMI na Mkoa wa Kagera. 

"Zaidi ya wasafiri elfu 75,000 wamefanyiwa uchunguzi katika mipaka mbalimbali nchini tangu kuongezeka kwa tahadhari za Ebola, huku takribani watu 45,000 wakifanyiwa tathmini ya kina zaidi kutokana na kuhisiwa lakini hakuna aliyebainika na ugonjwa wa Ebola," amesema Dkt. Magembe

Amesema, Serikali imeweka mifumo ya ufuatiliaji katika mipaka yote ya nchi ikiwemo mipaka ya nchi kavu, viwanja vya ndege, bandari na maeneo mengine ya kuvukia, ambapo wasafiri wote wanaingia nchini hupimwa na kufanyiwa uchunguzi wa afya.

Aidha, Dkt. Magembe amesema kuwa wahisiwa hao walitambuliwa kwa kuzingatia vigezo vya kitaalamu vya uchunguzi wa Ebola vya kitaifa na kimataifa kama inavyoelekezwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) ikiwemo historia ya kusafiri kutoka maeneo yenye maambukizi, kuwasiliana na watu wenye dalili zinazofanana na Ebola au kuwa na baadhi ya dalili zinazohusishwa na ugonjwa huo.

“Tumefanya vipimo na uchunguzi kwa watu wote waliotiliwa shaka, lakini hadi sasa hakuna hata mtu mmoja aliyebainika kuwa na maambukizi ya ugonjwa wa Ebola nchini Tanzania,” amesema Dkt. Magembe.

Amefafanua kuwa dalili za Ebola zinaweza kufanana na magonjwa mengine , hivyo amewataka wataalamu wa afya katika vituo vya kutolea huduma kuendelea kuwahoji na kuwachunguza wagonjwa wote wenye dalili zinazoweza kuashiria magonjwa ya mlipuko huku wakichukua tahadhari zote muhimu kujikinga ili wasipate maambukizi.

Mwisho, Dkt. Magembe amewataka wananchi kuendelea kutoa taarifa kupitia namba ya dharura 199 , ofisi za serikali za vijiji na mitaa na  vituo vya afya vilivyo karibu nao pindi wanapobaini mtu mwenye dalili zinazotia shaka, akisisitiza kuwa watumishi wa afya wanaendelea kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa salama dhidi ya ugonjwa wa Ebola.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa huduma za Kinga Wizara ya Afya Dkt. Otilia Gowelle amesema mwananchi yeyote anaefika katika kituo cha kutolea huduma anapata elimu sahihi ya namna ya kujikinga na ugonjwa huo ikiwemo kutoa elimu kupitia TV, vipeperushi pamoja na watoa huduma za afya.










BALOZI YAKUBU ATETA NA VIONGOZI WAPYA WA DIASPORA TANZANIA FRANCE, ATOA WITO WA KUCHANGIA MAENDELEO YA TAIFA

 


Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe. Saidi Othman Yakubu, amezungumza na viongozi wapya wa Chama cha Watanzania Waishio Ufaransa (Diaspora Tanzania France) kujadili nafasi ya diaspora katika kuchangia maendeleo ya taifa.

Akizungumza na viongozi hao katika mazungumzo yaliyofanyika katika Ubalozi wa Tanzania mjini Paris, Balozi Yakubu amewapongeza kwa kuaminiwa kuongoza jumuiya hiyo na kusisitiza kuwa Serikali inathamini mchango wa diaspora katika maendeleo ya taifa. Amesema utaalamu na uzoefu wa Watanzania waishio nje ya nchi ni rasilimali muhimu katika kukuza uwekezaji, biashara, utalii na uhamishaji wa maarifa.

Aidha, Balozi Yakubu amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi yatakayochochea ushiriki wa diaspora katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Pia amewahimiza kutumia nafasi zao za kitaaluma, kijamii na kiuchumi kuitangaza Tanzania kimataifa, sambamba na kuhamasisha fursa za uwekezaji, biashara na utalii zilizopo nchini.

Vilevile, amesema Ubalozi utaendelea kuwa kiungo muhimu kati ya Serikali na diaspora katika kuimarisha mawasiliano, uratibu na ushirikiano wenye tija. Ameongeza kuwa Ubalozi utaendelea kuhamasisha matumizi ya lugha ya Kiswahili na kuitangaza Tanzania katika nchi zote zilizo chini ya eneo lake la uwakilishi ambazo ni Ufaransa, Hispania, Ureno na Morocco.

Kwa upande wao, viongozi wa Diaspora Tanzania France wameeleza dhamira yao ya kuimarisha mshikamano wa Watanzania wanaoishi Ufaransa, kuendeleza matumizi na ufundishaji wa lugha ya Kiswahili, pamoja na kuimarisha ushirikiano na taasisi mbalimbali nchini Tanzania katika sekta za maendeleo, elimu, teknolojia na uwekezaji.

Viongozi hao, ambao ni wataalamu katika fani mbalimbali zikiwemo sayansi ya nyuklia, akili mnemba (AI), jiolojia, teknolojia na utafiti, wameahidi kutumia utaalamu na uzoefu wao kuchangia maendeleo ya Tanzania kupitia ushauri wa kitaalamu, uhamishaji wa maarifa na ushiriki katika miradi mbalimbali ya maendeleo.




TANAPA YATINGA BRUSSELS KUELEKEA TUZO ZA KIMATAIFA ZA UBORA



Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ubelgiji, Mhe. Jestas Abuok Nyamanga, amwekaribisha ujumbe kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii ukiongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Nkoba Mabula, pamoja na maafisa kutoka Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), walipotembelea ubalozi huo mara baada ya kuwasili nchini Ubelgiji.

Ujumbe huo upo nchini Ubelgiji kwa ajili ya kushiriki hafla ya utoaji wa “Tuzo ya Kimataifa ya Mafanikio katika utoaji huduma kwa  Ubora kwa mwaka 2026” (Quality Achievement Award 2026), inayotolewa na taasisi ya kimataifa ya European Society for Quality Research (ESQR) 

Hafla hiyo inatarajiwa kufanyika tarehe 31 Mei 2026 katika Hoteli ya Le Plaza, Brussels.

Aidha, Mhe.Balozi Nyamanga amesisitiza kuwa uwepo wa ujumbe huo nchini Ubelgiji ni fursa muhimu ya kuendelea kuitangaza Tanzania, vivutio vyake vya utalii pamoja na kuonesha juhudi za TANAPA katika utoaji wa huduma bora kwenye jukwaa la kimataifa.






#ESQR2026 #QualityAchievementsAward2026 #TANAPA #MNRT #DestinationTanzania #Brussels #TANAPAGOApp

Thursday, May 28, 2026

TMDA YATOA UFAFANUZI WA CHANGAMOTO ZA MFUMO MPYA WA PAMOJA WA UGOMBOAJI WA MIZIGO (TANESW)

Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, Dk Adam Fimbo 


Na. Mwandishi Wetu.

MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) Imetoa ufafanuzi kwa Umma juu ya changamoto za mfumo mpya wa ugomboaji wa mizigo wa pamoja ujulikanao kama Tanzania Electronic Single Window (TANESW).

Kwa mujibu wa taarifa kwa Umma iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, Imebainisha kuwa, ilianza kutumia mfumo huo mpya wa TANESW, mnamo tarehe 1 Mei, 2026, lengo kuu la hatua hii ni kurahisisha ugomboaji wa shehena za mizigo mbalimbali inayoingizwa nchini zikiwemo bidhaa tiba.

Aidha, utaratibu huo unalenga kuhakikisha kuwa, ugomboaji wa shehena hizo unafanyika kwa kutumia mfumo mmoja badala ya kuwa na mifumo mingi, suala ambalo lilikuwa ni usumbufu kwa wateja. 

"Baada ya kuanza kutumika kwa mfumo huu, kumejitokeza changamoto mbalimbali za kimfumo kama ifuatavyo; Wateja kuwa na uelewa mdogo wa namna ambavyo mfumo mpya unavyofanya kazi;

"Kucheleweshwa kwa ugomboaji wa mizigo ambayo ina bidhaa zisizodhibitiwa na TMDA; Kucheleweshwa kwa ugomboaji wa mizigo iliyochanganywa na bidhaa zinazodhibitiwa na TMDA; 

Kucheleweshwa kwa ugomboaji wa mizigo ambayo tayari ilikuwa na vibali vya kuingiza mizigo vilivyotolewa na TMDA kabla ya mfumo mpya kuanza kutumika; na kutoonekana kwa hoja ambazo zimetumwa kwa wateja kupitia mfumo wa TANESW na hivyo mteja kushindwa kujibu hoja hizo kwa wakati.

"Ili kutatua changamoto hizo, katika kipindi hiki cha mpito, TMDA inafanya yafuatayo: -  Kuruhusu mizigo yote ambayo haidhibitiwi na TMDA igombolewe kupitia mfumo wa TANOGA; 

Kuruhusu mizigo yote yenye vibali vilivyotolewa kabla ya kuanza kutumika kwa mfumo huu mpya, kuingizwa nchini bila kulazimika kutumia mfumo mpya wa TANESW; 

Kushirikiana na TRA kutatua changamoto ya kutoonekana kwa hoja zinazotumwa kwa baadhi ya wateja; na Kuweka dawati la msaada kwa wateja (help desk) katika vituo vya forodha vya uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere na ofisi za bandari zilizopo TPA Tower - ghorofa ya 3, ili kusaidia kutatua changamoto za kimfumo. 

"Wito unatolewa kwa wateja wetu kuwasiliana na TMDA pale wanapokumbana na changamoto za matumizi ya mfumo huu mpya kupitia namba 0784 227 069 (Meneja, Udhibiti na Ukaguzi wa Vifaa Tiba), 0782 119 437 (Meneja, Udhibiti na Ukaguzi wa Dawa) na 0784 040 655 (Meneja, TMDA, Kanda ya Mashariki)." Imebainisha taarifa hiyo.


Mwisho.

MIAKA 40 YA NEMC, JET YAPEWA TUZO YA HESHIMA

 


Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) leo Mei 28, 2026 limetambua mchango mkubwa wa Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) katika kuandika na kuhabarisha umma kuhusu masuala ya utunzaji wa mazingira kwa weledi na umahiri mkubwa.

Utambuzi huo umetolewa kupitia tuzo maalum ya umahiri iliyokabidhiwa kwa Mkurugenzi wa JET, John Chikomo, ikiwa ni sehemu ya kuthamini kazi kubwa inayofanywa na waandishi wa habari za mazingira nchini katika kuelimisha jamii kuhusu uhifadhi na utunzaji wa mazingira.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Chikomo amesema tuzo hiyo ni heshima kubwa kwa wanachama wote wa JET na ni uthibitisho kuwa kazi inayofanywa na waandishi wa habari za mazingira inatambuliwa na serikali pamoja na wadau wa mazingira nchini.

“Leo tumetunukiwa tuzo ya umahiri kutoka NEMC kwa kutambua mchango mkubwa ambao JET imekuwa ikiutoa tangu kuanzishwa kwake. 

Hii inaonesha kuwa mchango wa waandishi wa habari za mazingira katika kuhamasisha na kuhabarisha umma kuhusu uhifadhi na utunzaji wa mazingira unatambuliwa,” amesema Chikomo.

Ameeleza kuwa tangu miaka ya mwanzo ya uanzishwaji wa sera za mazingira nchini, JET imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha taarifa za mazingira zinawafikia wananchi kupitia magazeti, redio na televisheni.

Kwa mujibu wa Chikomo, tuzo hiyo haipaswi kuchukuliwa kwa wepesi kwani ni matokeo ya kazi kubwa iliyofanywa kwa muda mrefu na wanachama wa JET kwa kushirikiana na sekretarieti ya chama hicho.

“Tuzo hii si ya ofisi pekee, bali ni ya wanachama wote wa JET ambao wamekuwa bega kwa bega kuhakikisha habari za mazingira zinaandikwa kwa weledi mkubwa.

"Kazi yao haiendi bure kwa sababu serikali na wadau mbalimbali wametambua mchango wao,” amesema.

Aidha, amesema kutambuliwa huko kunapaswa kuwa chachu ya kuongeza juhudi zaidi katika kuandika habari za mazingira kwa umakini na weledi ili kuendelea kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kulinda mazingira.

Chikomo amesema JET, ambayo sasa inaelekea kutimiza miaka 40 tangu kuanzishwa kwake, inaona hatua hiyo kama mwanzo mpya wa mafanikio makubwa zaidi katika sekta ya habari za mazingira.

“Wanasema maisha yanaanza miaka 40. Sisi JET tunaona sasa ndiyo tunaanza upya kwa nguvu kubwa zaidi katika kuhakikisha tunasogeza mbele gurudumu la uhifadhi wa mazingira nchini,” amesema.

JET ambayo imekabidhiwa tuzo hiyo na Waziri Mkuu wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba kwenye siku ya kwanza ya maadhimisho ya kilele cha miaka 40 ya NEMC, imeendelea kuwa taasisi muhimu inayowaunganisha waandishi wa habari za mazingira nchini huku ikichangia kwa kiasi kikubwa kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu changamoto za mazingira, mabadiliko ya tabianchi na umuhimu wa matumizi endelevu ya rasilimali za asili.







UONGOZI WA TAGCO MGUU SAWA MAANDALIZI YA TAGCO AGM 2026

 


Uongozi wa Chama cha Maafisa Mawasiliano wa Serikali (TAGCO) ukiongozwa na Mwenyekiti wake Bw. Karimu Meshack umewasili jijini Mwanza kwa ajili ya maandalizi ya Mkutano mkuu wa Mwaka wa TAGCO unaotarajiwa kufanyika Jijini Mwanza kuanzia tarehe 1-5 Juni, 2026.

Ukiwa Jijini Mwanza uongozi huo umemtembelea mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda kwa lengo la kujitambulisha na kumuelezea ratiba ya mkutano huo ambapo maafisa Mwasiliano wa Serikali watapata wasaa wa kubadilishana uzoefu, mbinu mbalimbali za kuimarisha utendaji kazi, mafunzo, kuhamasisha shughuli za kijamii, kushiriki michezo na kuhamasisha utalii wa ndani ambapo zaidi ya wanachama 500 wanatarajiwa kuhudhuria mkutano huo.







Wednesday, May 27, 2026

HOSPITALI YA KANDA MBEYA YAONYESHA UFANISI HUDUMA ZA KIBINGWA MAONESHO YA MBEYA CITY EXPO 2026



MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica Yegela, ametembelea banda la Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (MZRH) katika Maonesho ya Nne ya Biashara na Kilimo (Mbeya City Expo 2026) yanayofanyika kwenye viwanja vya lililokuwa Soko la Zamani la Uhindini Jijini Mbeya.

Akiwa bandani hapo, Bi. Yegela amejionea namna wataalamu wa afya wanavyotoa huduma mbalimbali za kibingwa na kibobezi bila malipo kwa wananchi wanaofika kujitokeza kwenye maonesho hayo makubwa Nyanda za Juu Kusini.

Bi. Yegela ameupongeza Uongozi wa hospitali hiyo chini ya Mkurugenzi Mtendaji, Dkt. Godlove Mbwanji, kwa kusogeza huduma za kisasa na vipimo vya kibingwa karibu na jamii, hatua inayookoa muda na gharama kwa wananchi wa mkoa wa Mbeya na mikoa jirani.

"Nimefarijika sana kuona namna hospitali yetu ya kanda ilivyojipanga vizuri kusogeza huduma hizi kubwa na muhimu hapa kiwanjani. Wananchi wasisubiri hadi wawe wagonjwa sana, waje sasa hivi kupata ushauri na vipimo kutoka kwa madaktari bingwa," alisema Bi. Yegela.

Aidha, ametoa wito kwa wakazi wote wa Mbeya na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo kuanzia sasa hadi yatakapotamatika tarehe 30 Mei 2026, ili kupata huduma bora za afya pamoja na kujifunza fursa mbalimbali za biashara na kilimo zilizopo mkoani hapo.

Amesema kuwa uwepo wa huduma hizo bure ni fursa ya kipekee ambayo haipaswi kuachwa hivi hivi na wananchi wanaojali afya zao.

Maonesho hayo ya Mbeya City Expo yameandaliwa na Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) kwa ushirikiano na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, yakiwa na lengo la kukuza uchumi, biashara, kilimo, na uwekezaji mkoani humo.

Hadi sasa, maonesho hayo yamevutia taasisi nyingi za kiserikali na binafsi zinazotoa elimu na huduma mbalimbali kwa umma.







Friday, March 27, 2026

MAZIKO YA MPENDWA WETU HASSAN NG'ANZO

Ndugu, jamaa na marafiki wakijumuika pamoja katika siku ya msiba wa mpendwa wetu Hassan Ng'anzo nyumbani kwa marehemu Sinza Mori mapema siku ya Ijumaa March 27, 2026 kabla ya kuelekea makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam yalikofanyika maziko yake. Marehemu alifariki siku ya Jumatau asubuhi katika ajali ya gari march 23, 2027 jijini Dodoma. Marehemu alikua na wenzake wawili katika ajali hiyo lakini ni yeye pake yake aliyafariki na wenzake kukimbizwa hospitali ya Dodoma kwa matibabu zaidi. Hassan Ng'anzo alikua mkaaz inchini Norway. Picha zote kwa hisani ya Mayor Mlima.
Kwa picha zaidi bofya soma zaidi