ANGALIA LIVE NEWS

Monday, August 10, 2026

MUHIMBILI YAWEKA HISTORIA, YAFANIKISHA UPASUAJI WA KWANZA WA KUTENGANISHA MAPACHA WALIOUNGANA AINA YA PARASITIC CONJOINED TWINS

 

 

Madaktari bingwa wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) leo, Agosti 10, 2026, wamefanikiwa kufanya upasuaji wa kwanza wa kutenganisha mapacha walioungana aina ya parasitic conjoined twins, ambapo mmoja wa mapacha hakukua kikamilifu na alikuwa akimtegemea mwenzake kwa ukuaji na uhai.

Akizungumza mara baada ya upasuaji huo, Dkt. Victor Ngotta, Bingwa wa Upasuaji wa Watoto wa MNH, amesema mafanikio hayo yanaonyesha uwezo wa hospitali kushughulikia kesi ngumu na adimu zinazohitaji utaalamu wa hali ya juu, na ni hatua muhimu katika kuendelea kuimarisha huduma za upasuaji wa kibingwa nchini.

Dkt. Ngotta amesema upasuaji huo ulihitaji maandalizi ya kina na ushirikiano wa wataalamu kutoka fani mbalimbali kutokana na hali ya kipekee ya mtoto huyo, ambaye alikuwa na pacha aliyekuwa na mikono, miguu na sehemu ya kiuno pekee huku akimtegemea mwili wa mwenzake kwa ukuaji na uhai.

Mafanikio ya upasuaji huo yanaendelea kuimarisha nafasi ya Hospitali ya Taifa Muhimbili kama kituo kinachoongoza nchini katika utoaji wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi. Mtoto anaendelea vizuri na yupo chini ya uangalizi wa karibu wa madaktari.








  



RAIS DKT. MWINYI: KAMERA ZA USALAMA BARABARANI KUDHIBITI AJALI ZANZIBAR

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali imeanza kuweka mfumo wa kamera za usalama barabarani ili kuimarisha utii wa sheria, kurejesha nidhamu na kudhibiti ajali zinazotokana na ukiukwaji wa sheria za usalama barabarani.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 10 Agosti 2026, alipokutana na Kamati ya Baraza la Wawakilishi ya Kusimamia Viongozi Wakuu wa Kitaifa, iliyoongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Machano Othman Said, Ikulu Zanzibar.

Amesema utekelezaji wa mfumo huo umeanza katika Mkoa wa Mjini Magharibi na utaendelea kuimarishwa na kupanuliwa katika maeneo mbalimbali ya mijini na vijijini, kwa lengo la kuongeza usalama wa madereva, waendesha vyombo vya usafiri pamoja na watembea kwa miguu.

Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali itaendelea kuimarisha vituo vya mafunzo ya amali na kufanya mageuzi katika elimu ya ufundi ili kuwapatia vijana ujuzi na maarifa yatakayowawezesha kujiajiri, kuajiriwa na kuwa na ushindani katika soko la ajira.

Kuhusu kupanda kwa bei za bidhaa, amesema Serikali inaendelea kuweka bei elekezi na kusimamia utekelezaji wake, huku akiwataka wafanyabiashara kuzingatia viwango vilivyowekwa kwa lengo la kulinda maslahi ya wananchi na kupunguza gharama za maisha.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amewataka wakandarasi na wasimamizi wa ujenzi kuhakikisha mahitaji ya watu wenye ulemavu yanazingatiwa katika majengo ya umma na binafsi, ili kuwawezesha kupata huduma kwa urahisi na bila vikwazo.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Machano Othman Said, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa maono na utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo, na kueleza kuwa Kamati itaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuimarisha maendeleo na kukuza uchumi wa Zanzibar.













Thursday, August 6, 2026

TFS YAANDIKA HISTORIA KWA KUSHIRIKI MAONESHO YA KILIMO ZANZIBAR KWA MARA YA KWANZA, YAPOKELEWA KWA KISHINDO

  



Na Mwandishi Wetu, Dole Kizimbani, Zanzibar

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeandika historia kwa kushiriki kwa mara ya kwanza Maonesho ya Kilimo Zanzibar, hatua iliyopokelewa kwa pongezi na viongozi pamoja na wananchi kutokana na kupeleka elimu na fursa za kiuchumi zinazotokana na uhifadhi wa misitu na nyuki visiwani humo.

Mafanikio hayo yalidhihirika Agosti 5, 2026, baada ya Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar, Haroun Ally Suleiman, kutembelea banda la TFS katika Viwanja vya Dole, Kizimbani na kupongeza uamuzi wa wakala huo kuvuka bahari na kuwaletea Wazanzibari huduma za elimu ya uhifadhi pamoja na fursa za uwekezaji.

    "Niwapongeze sana TFS kwa kuona umuhimu wa kutangaza fursa za uhifadhi hapa Zanzibar. Ni hatua nzuri ambayo itawanufaisha wananchi kwa kuwawezesha kuibua vyanzo vipya vya mapato kupitia uhifadhi wa misitu," alisema Waziri Haroun.

Alisema ushiriki wa TFS katika maonesho hayo unafungua milango mipya ya ushirikiano kati ya Tanzania Bara na Zanzibar katika kukuza uchumi kupitia matumizi endelevu ya rasilimali za misitu na nyuki, huku akiitaka taasisi hiyo kuendelea kushiriki maonesho na kampeni za uelimishaji visiwani humo.

Kwa upande wake, Mhifadhi Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Francis Kiondo, alisema ushiriki huo wa kwanza Zanzibar ni sehemu ya mkakati wa TFS wa kusogeza huduma karibu na wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuhakikisha fursa za uhifadhi zinawafikia Watanzania bila kujali walipo.

Alisema kupitia maonesho hayo, wananchi wanapata elimu kuhusu uhifadhi wa misitu na nyuki, uzalishaji wa mbegu bora za miti na miche, ufugaji nyuki, fursa za uwekezaji katika sekta ya misitu pamoja na utalii wa ikolojia, ambao unazidi kuwa chanzo muhimu cha ajira na mapato.

Maonesho ya Kilimo Zanzibar yanaendelea katika Viwanja vya Dole, Kizimbani kuanzia Agosti 1 hadi 14, 2026, ambapo TFS imewahimiza wananchi kutembelea banda lake ili kujifunza na kutumia fursa mbalimbali zinazotokana na uhifadhi endelevu wa rasilimali za misitu.

UONI HAFIFU WAONGOZA CHANGAMOTO KWA WANAOPIMA MACHO BANDA LA MUHIMBILI NANE NANE



Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imesema tatizo la uoni hafifu linaongoza miongoni mwa changamoto zinazobainika kwa wananchi wanaofika kupima afya ya macho katika Maonesho ya Wakulima (Nanenane) yanayoendelea katika viwanja vya Dk. Samweli Malechela, jijini Dodoma, ambapo huduma za uchunguzi wa macho, elimu na ushauri wa kitaalamu zinatolewa bure. 

Akizungumza Dkt. Bingwa wa Magonjwa ya Macho kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Johannes Mafwili, amesema wananchi wengi wanaofika katika banda la hospitali hiyo hupatikana na tatizo la uoni hafifu, huku wakifanyiwa uchunguzi wa kina na kupatiwa ushauri wa kitaalamu kulingana na hali zao. 

Amesema uchunguzi wa mapema husaidia kubaini magonjwa mbalimbali ya macho kabla hayajasababisha madhara makubwa, hivyo amewahimiza wananchi kutumia fursa ya maonesho hayo kupima afya ya macho bila kusubiri dalili kuwa mbaya. 

Dkt. Mafwili amewataka wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nane Nane kufika katika banda la Hospitali ya Taifa Muhimbili ili kunufaika na huduma hizo za bure na kupata elimu itakayowasaidia kulinda afya zao.











Wednesday, August 5, 2026

NCAA, BODI YA MIKOPO WAPELEKA TABASAMU JIPYA KWA WANAFUNZI KUTOKA HIFADHI YA NGORONGORO


Serikali kupitia Mamlaka ya hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) kwa kushirikiana na Bodi ya Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu (HESLB), imeanzisha mfuko wa  Ngorongoro Scholarship Fund  kwa lengo la kuwezesha wanafunzi wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kupata fursa ya masomo ya elimu ya juu kupitia ufadhili Ngorongoro Fund.  

Akizungumza wakati wa mkutano wa waandishi wa Habari Jijini Dar es salaam kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi, Kamishna msaidizi mwandamizi wa uhifadhi anayesimamia idara ya Maendeleo ya Jamii Gloria Bideberi ameeleza kuwa, Program hiyo inalenga  kuboresha maisha ya jamii zinazoishi ndani ya hifadhi,  ambapo kwa kushirikiana na bodi ya mikopo ya elimu ya juu watahakikisha kila mtoto anayeishi ndani ya hifadhi  hiyo anayekidhi vigezo anapata nafasi ya kupata ufadhili wa elimu ya juu.

“Kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ufadhili huu utasaidia kuondoa malalamiko ya upendeleo, taratibu zote za ufadhili wa vijana wetu zitakuwa wazi kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa tukitambua kuwa elimu ndiyo msingi wa kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na mazingira” amesema kamishna Bideberi.

Ameongeza kuwa Ngorongoro Fund inaongozwa na kauli mbiu isemayo "Elimu Endelevu kwa Maendeleo ya Jamii na Uhifadhi" itakwenda  kufadhili watoto wa kitanzania waliodahiliwa katika vyuo vilivyopo ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kunufaisha vijana watakaojikita katika masomo ya uhifadhi  wa Wanyamapori na misitu, Malikale na utalii na hapo baadaye wigo utaendelea kutanuliwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji  wa HESLB Dkt. Bill Kiwia amesema kuanzia mwaka wa masomo 2026/2027, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), kwa kushirikiana Ngorongoro, itaanza kutoa ufadhili huo maalum kwa wanafunzi kutoka eneo la Hifadhi ya Ngorongoro watakaosoma fani zinazohusiana na uhifadhi wa maliasili, usimamizi wa wanyamapori, pamoja na taaluma nyingine zitakazoainishwa katika Mwongozo wa Utoaji wa Scholarship hiyo.

Dkt. Kiwia ameeleza kuwa hatua ya kwanza ya utekelezaji wa mpango huu utaanza kwa kutoa ufadhili kwa wanafunzi 15, ambapo Ngorongoro imetenga shilingi milioni 99 kugharamia masomo ya ufadhili na kuwawezesha vijana hao kupata elimu ya juu, kujenga wataalamu watakaosaidia kuhifadhi rasilimali za Taifa, na kuchochea maendeleo endelevu ya jamii zinazozungukaHifadhi ya Ngorongoro.

Kwa ushirikiano wa karibu kati ya HESLB na NCAA, tayari tumekamilisha Mwongozo Maalum wa Utoaji wa Scholarship ya NCAA ambapo mwongozo huo umeweka vigezo, taratibu na masharti ya utoaji wa ufadhili huo kwa wanafunzi wanaotoka katika jamii zinazoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kutambua programu mahususi zitakazopewa kipaumbele, hususan zile zinazohusiana na uhifadhi wa maliasili, usimamizi wa wanyamapori na taaluma nyingine zinazochangia maendeleo endelevu ya eneo la Ngorongoro na Taifa kwa ujumla.

Sambamba na mwongozo huo, HESLB imekamilisha maandalizi ya mfumo wa kidijitali wa kupokea na kuchakata maombi ya scholarship ambapo hii dirisha la kupokea maombi litafunguliwa tarehe 15 Agosti, 2026, kwa sasa Ngorongoro na bodi ya mikopo zinaendelea kutoa elimu na uhamasishaji kwa waombaji watarajiwa ili kuwawezesha kuelewa vigezo vya scholarship hii na kujaza maombi yao kwa usahihi na kwa wakati.

Kabla makubaliano haya ya leo, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ilikuwa ikitekeleza  ufadhili huu kupitia Baraza la Wafugaji ambapo mpaka mwaka wa fedha uliopita 2025/2026 zaidi ya watu elfu kumi na tano kutoka ndani ya hifadhi wamepatiwa ufadhili katika  nyanja mbalimbali ikiwemo ualimu, udaktari, uhandisi, uhasibu, wataalamu wa uhifadhi na kada nyingine nyingi zinazochangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.




NAIBU WAZIRI AVUTIWA NA TEKNOLOJIA YA DRONE KATIKA UHIFADHI WA MISITU

 


Na Mwandishi Wetu, Lindi


LINDI: Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Kaspar K. Mmuya, ametembelea banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Kusini katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Kusini yanayoendelea Viwanja vya Ngongo, Manispaa ya Lindi, na kujionea teknolojia na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na TFS katika uhifadhi wa rasilimali za misitu.

Katika ziara hiyo iliyofanyika leo Agosti 4, 2026, Mmuya alijionea matumizi ya teknolojia ya drone katika uhifadhi wa misitu, shamba darasa la miti, elimu na fursa za ufugaji wa nyuki pamoja na bidhaa na huduma zinazotokana na mazao ya misitu.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi Manyisye K. Mpokigwa, ambaye ni Kamanda wa TFS Kanda ya Kusini, alisema banda hilo pia limewakutanisha wadau mbalimbali wa mazao ya misitu wakiwemo wajasiriamali wa vikapu, watengenezaji wa samani za ndani kama vitanda na milango, pamoja na wauza maua na miche ya matunda.

Alisema ushiriki wa wadau hao unalenga kuwaonesha wananchi na washiriki wa maonesho fursa zilizopo katika sekta ya misitu, huku ukihamasisha matumizi endelevu ya rasilimali za misitu kwa ajili ya kuongeza kipato na kuchochea maendeleo ya uchumi.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri alipata fursa ya kukata keki na kuonja asali safi inayozalishwa na wafugaji nyuki wanaoshirikiana na TFS kabla ya kukabidhiwa zawadi ya Asali ya Nyuki Wadogo na Kamanda wa TFS Kanda ya Kusini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Manyisye K. Mpokigwa.

Maonesho ya Nanenane Kanda ya Kusini yanaendelea Viwanja vya Ngongo, Manispaa ya Lindi, yakibeba kaulimbiu isemayo, “Tambua Soko: Ongeza Tija Kutekeleza Dira ya 2050,” huku yakitarajiwa kuendelea kuvutia washiriki na wadau kutoka sekta mbalimbali za uzalishaji nchini.







TANZANIA YAITAKA DUNIA KUONGEZA NGUVU KULINDA BIOANUWAI



NAIROBI: Tanzania imezitaka nchi duniani kuimarisha ushirikiano, kuongeza fedha na kuharakisha uhamishaji wa teknolojia ili kufanikisha  Muundo wa utekelezaji wa Kunming-Montreal wa Baioanuai (KMGBF), ikisema hatua hizo ni muhimu kuzuia kuendelea kwa uharibifu wa baioanuai ifikapo mwaka 2030.

Msimamo huo uliwasilishwa na Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi kwa niaba ya jopo la wataalam wa Mazingira wa Tanzania Fandey H. Mashimba, katika Mkutano wa Saba wa Chombo Tanzu cha Utekelezaji (SBI-7) chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Baioanuai (CBD), unaofanyika Nairobi, Kenya. Tanzania pia iliunga mkono tamko la Ghana lililotolewa kwa niaba ya Kundi la Afrika (African Group).

Mashimba alisema Tanzania imeendelea kutekeleza malengo ya KMGBF kupitia Mkakati na Mpango wa Taifa wa Baioanuai (NBSAP), huku ikiimarisha uhifadhi wa misitu na maeneo yenye utajiri mkubwa wa baioanuai (biodiversity hotspot), wanyamapori, bahari na ukanda wa pwani, pamoja na kurejesha mifumo ya ikolojia kwa kushirikisha jamii.

Alisema juhudi hizo zinafanyika Tanzania Bara na Zanzibar, zikihusisha maeneo yenye mifumo muhimu ya kiikolojia kama vile misitu ya Miombo na mbuga (savannah) maeneo oevu, mikoko, miamba ya matumbawe, milima na visiwa vyenye utajiri mkubwa wa baioanuai.

Hata hivyo, Tanzania ilisema mafanikio ya utekelezaji wa muundo huo yatategemea upatikanaji wa fedha za uhakika, ushirikiano wa kisayansi, ujenzi wa uwezo na kuboreshwa kwa mifumo ya ukusanyaji na usimamizi wa taarifa za baioanuai.

Aidha, ilizitaka taasisi za kimataifa kuongeza msaada kwa nchi zinazoendelea kupitia Mfuko wa Muundo wa utekelezaji wa Kimataifa wa Baioanuai (Global Biodiversity Framework Fund–GBFF) pamoja na Mfuko wa Mazingira wa Dunia (Global Environment Facility–GEF) ili ziweze kutekeleza kwa ufanisi malengo ya mkataba huo.

Tanzania pia ilisisitiza kuwa tathmini za kimataifa zinapaswa kuzingatia mazingira na uwezo wa kila nchi, badala ya kutafsiri upungufu wa takwimu kuwa ushahidi wa utekelezaji dhaifu.

Akihitimisha tamko hilo, Mashimba alisema Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama wa Mkataba wa Baioanuai kuhakikisha malengo ya Muundo wa Kunming-Montreal yanafikiwa ifikapo mwaka 2030.



Sunday, August 2, 2026

KATIBU MKUU WA BARAZA LA MAWAZIRI ZAMBIA APONGEZA HUDUMA ZA HOSPITALI YA RUFAA YA KANDA MBEYA

 



Diplomasia ya kiuchumi na sekta ya utalii wa matibabu (Medical Tourism) katika ukanda wa Kusini mwa Afrika (SADC) umezidi kuimarika. Hii ni kufuatia ziara ya Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Baraza la Mawaziri nchini Zambia, Ndugu Patrick Kangwa, alipotembelea banda la Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya na Taasisi ya Mifupa na Ubongo MOI ililopo chini ya Banda la Tanzania katika Maonyesho ya 98 ya Kilimo na Biashara yanayoendelea jijini Lusaka. 

Ndugu Kangwa amepongeza namna hospitali inavyotekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya maonyesho ya mwaka huu inayosema "Fostering Trade and Investment" (Kukuza Biashara na Uwekezaji). 

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Ndugu Kangwa alieleza kuvutiwa kwake na ubora wa huduma za kibingwa zinazotolewa na Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, ikiwemo matibabu ya magonjwa ya moyo, mifupa, upasuaji wa mgongo, pamoja na huduma za kibingwa za uzazi na utatuzi wa changamoto za kushika ujauzito. 

Alibainisha kuwa uwezo huo mkubwa wa kitabibu ni fursa adhimu kwa raia wa Zambia na nchi jirani kupata matibabu ya uhakika bila kusafiri umbali mrefu. Mbali na viongozi wa kitaifa, banda la MZRH limeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa raia na wadau wa afya nchini Zambia waliomiminika kujionea, kujifunza, na kupata ushauri wa kitaalamu.







Saturday, August 1, 2026

HIKE 4 GIRLS UGANDA TEAMS DEPART FOR MT. MGAHINGA MENSTRUAL HEALTH TREK


TEAMS from Raising Teenagers Uganda (RTU) and partners kicked off the ninth Hike4GirlsUg today, heading to Kisoro District for a trek up Mt. Mgahinga to spotlight menstrual health, dignity, and girls' education. 

The annual event fights period poverty and stigma that sideline girls from school, with participants flashing peace signs and exchanging items amid an upbeat mood. Past hikes have reached thousands with pads and education, and this year builds on that by blending the physical challenge with community advocacy.