ANGALIA LIVE NEWS

Tuesday, June 16, 2026

TUME YA TAIFA YA UNESCO YASHIRIKI KIKAMILIFU KATIKA TAMASHA LA UTAMADUNI LA BULABO 2026



Mwanza, Tanzania


Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilikuwa miongoni mwa taasisi zilizoshiriki kikamilifu katika Tamasha la Utamaduni la Bulabo 2026 lililofanyika kuanzia tarehe 7 hadi 14 Juni 2026 katika Viwanja vya Ngomeni, Kisesa, Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza.

Tamasha hilo lililobeba kaulimbiu ya “Maridhiano kwa Njia ya Amani Ndiyo Jadi Yetu, Linda Maadili ya Mtanzania” lilikusanya pamoja viongozi wa Serikali, viongozi wa kimila, taasisi mbalimbali na wananchi kutoka maeneo tofauti ya nchi kwa lengo la kuenzi urithi wa utamaduni wa Tanzania, kuimarisha mshikamano wa kijamii na kukuza maadili yanayochangia maendeleo ya Taifa.

Miongoni mwa washiriki wa tamasha hili alikuwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na maafisa wa Tume ya Taifa ya UNESCO, walioshiriki katika shughuli mbalimbali zilizofanyika katika kipindi chote cha tamasha. Ushiriki huo ulitoa fursa ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kushuhudia namna utamaduni unavyoendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuimarisha umoja, amani na utambulisho wa Taifa.

Kilele cha tamasha hilo kilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa Said Mtanda, aliyemwakilisha Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Akizungumza katika hafla hiyo, Mheshimiwa Mtanda aliwapongeza machifu wa jadi kwa juhudi zao za kuendelea kuhifadhi na kurithisha mila, desturi na maadili mema ambayo yameendelea kuwa msingi wa mshikamano na amani nchini.

Alieleza kuwa utamaduni wa Kitanzania una mchango mkubwa katika kujenga jamii inayoheshimiana, inayosikilizana na inayoweza kutatua changamoto zake kwa njia ya mazungumzo. Alisisitiza kuwa maadili na tamaduni zetu ni hazina muhimu inayopaswa kulindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.



Tamasha la Bulabo limeendelea kujidhihirisha kuwa jukwaa muhimu la kuenzi na kutangaza urithi wa utamaduni wa Tanzania. Kupitia maonesho ya mila na desturi, ngoma za asili, sanaa za jadi na mijadala mbalimbali kuhusu nafasi ya utamaduni katika maendeleo ya jamii, washiriki walipata fursa ya kutambua mchango wa urithi wa kitamaduni katika kujenga Taifa lenye umoja na mshikamano.

Ushiriki wa Tume ya Taifa ya UNESCO katika Tamasha la Bulabo 2026 unaendana na dhamira ya UNESCO ya kulinda na kuendeleza urithi wa utamaduni duniani, pamoja na kutambua nafasi ya utamaduni katika kujenga amani na maendeleo endelevu. Kwa kutekeleza majukumu yake nchini, Tume ya Taifa ya UNESCO inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuhifadhi na kuhamasisha matumizi ya urithi wa utamaduni kama nyenzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Tamasha hilo pia limetoa ujumbe muhimu kuhusu umuhimu wa maridhiano, uvumilivu na kuheshimu tofauti zilizopo katika jamii. Kaulimbiu ya mwaka huu imewakumbusha Watanzania kuwa amani na umoja ni tunu za Taifa zinazopaswa kuendelezwa na kulindwa wakati wote.

Kadiri dunia inavyobadilika, umuhimu wa kuhifadhi utamaduni na maadili ya jamii unaendelea kuwa mkubwa zaidi. Matukio kama Tamasha la Bulabo yanaendelea kuwa sehemu muhimu ya juhudi za kuimarisha utambulisho wa Taifa, kukuza mshikamano wa wananchi na kuhamasisha ushiriki wa jamii katika maendeleo endelevu.

Tume ya Taifa ya UNESCO itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuhifadhi, kuendeleza na kutangaza urithi wa utamaduni wa Tanzania kama nguzo muhimu ya amani, umoja na maendeleo ya Taifa.


SIMULIZI YA KISHERIA: KESI YA REGINALD MENGI VS YUSUF MANJI (2011) MAPAMBANO YA VIGOGO WAWILI.

 


​​Imeandaliwa na Karim Gabriel Mussa

Mwanasheria & Mchambuzi wa Sheria (KGM Attorneys) 0755 395 572.


​Leo tunatupa jicho kwenye moja ya mivutano ya kisheria iliyovuta hisia za kipekee nchini Tanzania mapema miaka ya 2010. Hili lilikuwa ni pambano la kisheria kati ya miamba miwili ya biashara: Aliyekuwa Mwenyekiti wa IPP Media, Marehemu Dr. Reginald Mengi (pamoja na Independent Television - ITV Tanzania), dhidi ya mfanyabiashara na aliyekuwa Mwenyekiti wa klabu ya Young Africans Sports Club, Marehemu Yusuf Manji.


​Kesi hii haikutikisa tu kwa sababu ya majina ya wahusika, bali iliacha funzo kubwa la kiutaratibu wa kisheria (Procedural Law) katika shauri la madai ya kuchafuliwa jina (Civil Defamation) na matumizi ya rungu la Marejeo (Civil Revision) chini ya Kifungu cha 79 cha Sheria ya Mwenendo wa Madai (CPC, 2002).


↘️ SAKATA LILIVYOANZA: Tuhuma za "Mafisadi Papa" na Dai la Fidia ya Shilingi Moja!


​Sakata hili lilianza mnamo mwaka 2009 baada ya Dr. Reginald Mengi kuitisha mkutano na waandishi wa habari na kuwataja baadhi ya wafanyabiashara akizungumzia kile alichokiita "Mafisadi Papa" wanaohujumu uchumi wa nchi. Katika orodha hiyo, jina la Yusuf Manji lilitajwa.


​Yusuf Manji akahisi jina na hadhi yake kama mfanyabiashara mkubwa wa ndani na kimataifa vimechafuliwa vibaya, alifungua kesi ya madai ya kashfa (Civil Case No. 85 of 2009) katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu dhidi ya Dr. Mengi na ITV.


​Lakini Manji alitega mtego wa kipekee na wa kisaikolojia wa kisheria: Katika madai yake ya fidia, tofauti na kesi nyingine ambapo watu huomba mabilioni kwa mabilioni, Manji aliomba kulipwa Fidia ya Jumla (General Damages) ya Shilingi Moja tu ya Kitanzania (TZS 1/=)!


​Hoja ya Manji ilikuwa rahisi: "Jina na heshima yangu havina thamani ya kifedha inayoweza kununulika. Sihitaji fedha za Mengi; ninachohitaji ni Mahakama ya Tanzania isafishe jina langu na kutamka kuwa nimesingiziwa."


↘️ MTIFUANO MAHAKAMANI: Mapambano ya Nyaraka na Pingamizi la Awali


​Kesi ilianza kusikilizwa mwaka 2011 mbele ya Hakimu Mkazi Katemana pale Yusuf Manji (PW1) alipoanza kutoa ushahidi wake. Katika kujihami, mawakili wa akina Dr. Mengi waliwasilisha mahakamani orodha ya nyaraka (List of Documents) zilizolenga kutumika kumng'oa Manji kwenye ushahidi wake.


​Hapo ndipo dhoruba ya kiutaratibu ilipolipuka. Mawakili wa Manji waliweka pingamizi wakidai kuwa uwasilishaji wa nyaraka hizo ulifanyika nje ya utaratibu na kanuni za mwenendo wa madai. 


Baada ya malumbano ya siku mbili, Hakimu Katemana alikubaliana na upande wa Manji na akazitupa nje nyaraka zote za akina Mengi, lakini akawapa nafasi ndogo ya kwenda kuomba kibali rasmi cha kuziwasilisha upya.


​Dr. Mengi na ITV, wakaona kuwa kutupwa nje kwa nyaraka zao kungezuwia utetezi wao kusikika kikamilifu, walisikitika na kukimbilia Mahakama Kuu ya Tanzania kupitia maombi ya marejeo (Civil Revision No. 38 of 2011) chini ya Mheshimiwa Jaji Dr. Fauz Twaib.


↘️ ​MBELE YA MAHAKAMA KUU: Pambano Linalohamia Kwenye "Ufundi wa Sheria"


​Mbele ya Jaji Dr. Fauz Twaib, pambano halikuwa tena kuhusu "Nani fisadi au nani amesingiziwa", bali lilihama kabisa na kuwa pambano la ufundi wa sheria (Technicalities of Procedure). Mawakili wa Yusuf Manji waliweka mapingamizi makali ya awali (Preliminary Objections) wakitaka maombi ya Dr. Mengi yatupiliwe mbali bila hata kusikilizwa.


Maombi hayo yaliwasilishwa Mahakama Kuu yakitaka kufutwa kwa mwenendo mzima wa kesi iliyokuwa ikiendelea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi na kuamriwa ianze upya (de novo). 


Waombaji Dr. Mengi na mwenzake walidai kuwa kulikuwa na mazingira maalumu yaliyohitaji Mahakama Kuu kutumia mamlaka yake ya marejeo ili kurekebisha makosa yaliyokuwa yametokea katika mwenendo wa shauri hilo.


Miongoni mwa malalamiko yao kulikuwa na namna masuala ya kesi yalivyopangwa (framing of issues), kuondolewa kwa baadhi ya nyaraka zao katika kumbukumbu za mahakama, kujiondoa kwa hakimu aliyekuwa akisikiliza shauri bila kutoa sababu, pamoja na amri iliyozuia vyombo vya habari kufuatilia mwenendo wa kesi hiyo.


Hata hivyo, kabla ya kuingia katika kiini cha hoja hizo, Mahakama ilikabiliwa na pingamizi la awali kutoka kwa mawakili wa Yusuf Manji. 

Pingamizi hilo lilihusu mambo mawili makubwa: 

1️⃣ kwanza, kwamba baadhi ya maamuzi yaliyolalamikiwa yalikuwa yamepitwa na muda wa kuombewa marejeo; na 

2️⃣ Pili, kwamba maamuzi hayo hayakuwa ya aina inayoweza kurejelewa kwa njia ya revision.


Mahakama ilikubaliana na hoja kwamba baadhi ya maamuzi yaliyokuwa yanalalamikiwa yalikuwa yamepitwa na muda kwa mujibu wa Sheria ya Ukomo wa Madai. Ilisisitiza kuwa pale ambapo upande binafsi ndiye anayeliomba Mahakama itumie mamlaka yake ya marejeo, maombi hayo lazima yawasilishwe ndani ya muda unaotakiwa na sheria. 


Lakini somo kubwa zaidi lilitokana na hoja ya pili. Mahakama ilieleza kuwa si kila uamuzi wa kati unaotolewa wakati kesi inaendelea unaweza kuwa msingi wa marejeo. Kimsingi, sheria imeweka kanuni kwamba maamuzi ya awali au ya muda (interlocutory decisions) hayawezi kukatiwa rufaa wala kuombewa marejeo isipokuwa kama yana athari ya kuamua kwa mwisho haki za wahusika katika shauri husika. 


Mahakama ilikumbusha kuwa mamlaka ya marejeo ni mamlaka ya kipekee yanayotumiwa kwa tahadhari kubwa. Ili Mahakama iingilie kati, lazima kuwe na kosa la msingi linaloweza kusababisha dhuluma au kuathiri haki za mhusika kwa kiwango kikubwa. Si kila kutokuridhishwa na uamuzi wa hakimu kunatosha kuhalalisha matumizi ya mamlaka hayo. 


Katika kuchambua malalamiko yaliyowasilishwa, Mahakama iliona kuwa baadhi ya maamuzi yaliyolalamikiwa yalikuwa ndani ya mamlaka ya mahakama ya chini na hayakuonyesha uwepo wa dhuluma au kosa kubwa kiasi cha kuhitaji kuingiliwa na Mahakama Kuu. Kwa mfano, kuhusu suala la kuanza kesi upya baada ya hakimu mwingine kuchukua usikilizaji wa shauri, Mahakama ilieleza kuwa uamuzi huo ni wa hiari ya hakimu anayesikiliza shauri kwa mujibu wa sheria, hivyo haukuwa msingi wa marejeo. 


Baada ya kusikiliza maombi hayo Mahakama kuu, maombi hayo ya marejeo ya Dr. Mengi yalitupiliwa mbali.


Uamuzi huu unafundisha jambo muhimu sana katika mfumo wa haki. Mahakama za juu hazipo kwa ajili ya kurekebisha kila hatua au kila uamuzi mdogo unaotolewa wakati wa usikilizaji wa kesi. Badala yake, huingilia pale tu ambapo kuna kosa la msingi la kisheria, ukiukwaji mkubwa wa haki, au mazingira maalumu yanayoonyesha kuwa kuendelea kwa mwenendo wa shauri kunaweza kusababisha dhuluma. 


Kwa hiyo, kabla ya kukimbilia kuomba revision dhidi ya uamuzi wa kati uliotolewa na mahakama ya chini, ni muhimu kujiuliza swali moja muhimu: 


Je, uamuzi huo umeamua mwisho haki zangu au umesababisha dhuluma kubwa inayohitaji Mahakama ya Juu iingilie kati? Kama jibu ni hapana, basi mara nyingi sheria itahitaji usubiri shauri likamilike ndipo hatua nyingine za kisheria zichukuliwe.


Uamuzi katika kesi ya Reginald Abraham Mengi & IPP Limited v. Yusuf Manji (Miscellaneous Civil Cause No. 45 of 2011, High Court of Tanzania, Dar es Salaam Registry, 20 December 2011) umeendelea kuwa rejea muhimu katika kuelewa mipaka ya mamlaka ya marejeo na umuhimu wa kutofautisha kati ya uamuzi wa kawaida wa mwenendo wa kesi na kosa la kisheria linalostahili kuingiliwa na Mahakama ya Juu. Na ​​Sakata hili la Mengi na Manji linabaki kuwa shule tosha kwa wanafunzi na watendaji wa sheria nchini;


1️⃣ ​Fidia Si Utajiri, Ni Heshima: 

Manji alionyesha mfano wa kipekee kuwa kwenye kesi ya kashfa, lengo kuu la mdai linapaswa kuwa kusafisha jina (vindication of reputation) na sio fursa ya kujipatia ukwasi wa haraka; ndio maana dai la "Shilingi Moja" lilikuwa na uzito wa kimaadili kuliko madai ya mabilioni.


2️⃣ ​Utaratibu Usiue Haki (Substantive Justice): Mahakama Kuu ilikumbusha kuwa ufundi wa kisheria na mapingamizi (technicalities) yasitumike kama mtego wa kuwaziba mdomo wadau wasiweze kupata haki yao ya kusikilizwa.


​Je, unaoni gani kuhusu mkakati wa Yusuf Manji kudai fidia ya Shilingi Moja tu ili kulinda heshima yake?  Tukutane kwenye maoni!


​⚠️ DISCLAIMER: Makala hii ni kwa ajili ya kutoa elimu ya kisheria, kihistoria na kijamii pekee kulingana na kumbukumbu rasmi za uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (2011).

#kgmupdates #sheria #tanzania #LegalEducation

MFAHAMU: CELINA KOMBANI: MWANAMKE SHUPAVU ALIYETUMIKIA ULANGA NA TAIFA KWA UZALENDO.



Mwandishi: Akwisuss Chabruma

Student University of Dar es Salaam, College of social science ( CoSS), 0616438250

UTANGULIZI

✍🏼Katika historia ya siasa za Tanzania, wapo viongozi ambao mchango wao unaendelea kukumbukwa hata baada ya kuondoka duniani..✍🏼

 Miongoni mwa viongozi hao ni marehemu Selina (Celina) Ompeshi Kombani, mwanamke jasiri, mchapakazi na kiongozi aliyetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Wilaya ya Ulanga na Taifa la Tanzania kwa ujumla... ✍🏼

Kwa miaka mingi ya utumishi wake, Selina Kombani alijijengea heshima kubwa kutokana na uadilifu, bidii na uwezo wake wa kusimamia masuala ya wananchi. ... ✍🏼

Selina Kombani alikuwa mfano wa mwanamke aliyethibitisha kuwa uongozi si suala la jinsia bali ni uwezo, maono na uzalendo... ✍🏼


HISTORIA YAKE KWA UFUPI

🍼Selina Ompeshi Kombani alizaliwa tarehe 19 Juni 1959 katika Wilaya ya Ulanga, Mkoa wa Morogoro. 

👨🏼‍🎓Alipata elimu yake ya juu katika Chuo Kikuu cha Mzumbe ambako alihitimu shahada zake kabla ya kuingia kikamilifu katika utumishi wa umma na siasa.

🟩Selina Kombani alikuwa mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na alichaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ulanga Mashariki mwaka 2005, nafasi aliyoiendelea kuitumikia hadi mwaka 2015... ✍🏼



SAFARI YAKE YA UONGOZI

Baada ya kuingia Bungeni, uwezo wake wa kiuongozi ulionekana mapema na kuaminiwa na Rais Jakaya Kikwete ( Raisi wa Tanzania awamu ya nne)kushika nyadhifa mbalimbali serikalini.

Miongoni mwa nafasi alizowahi kushika ni:

1.Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI (2006–2008)

2.Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI (2008–2010)

3.Waziri wa Katiba na Sheria (2010–2012)

4.Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma (2012–2015)

🫂Katika nafasi hizo, alijulikana kwa kusimamia uwajibikaji, nidhamu katika utumishi wa umma na kuhimiza utoaji bora wa huduma kwa wananchi.


MCHANGO WAKE KATIKA ULANGA

Kwa wananchi wa Ulanga, Selina Kombani alikuwa zaidi ya Mbunge. Alikuwa mlezi, mshauri na mtetezi wa maendeleo yao.

Wananchi wengi wanakumbuka kwa:

1.Kusukuma mbele maendeleo ya miundombinu ya barabara.

2.Kusaidia wanafunzi kupata ada na fursa za elimu.

3.Kuwezesha vijana na wajasiriamali wadogo.

4.Kutetea huduma za afya na maendeleo ya jamii.

Mchango wake ulifanya wananchi wengi wa Ulanga kumwona kama kiongozi aliyekuwa karibu nao na aliyegusa maisha yao moja kwa moja. 😭😭


🏥URITHI WAKE KATIKA SEKTA YA AFYA

Mbali na siasa, Selina Kombani alihusika katika juhudi za kuimarisha huduma za afya, hususan katika Wilaya ya Ulanga. 

Selina Kombani anatajwa kuwa ni mmoja wa viongozi waliochangia kuhamasisha ajira za wahudumu wa afya ngazi ya jamii, hatua iliyosaidia kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa maeneo ya vijijini.... ✍🏼



🪦KIFO CHAKE NA MAOMBOLEZO YA TAIFA

Tarehe 24 Septemba 2015, Taifa la Tanzania lilipokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo cha Selina Kombani. ...

Umauti ulimkuta akiwa nchini India alipokuwa akipatiwa matibabu akiwa na umri wa miaka 56... ✍🏼

Kifo chake kilizua huzuni kubwa miongoni mwa wananchi wa Ulanga, viongozi wa serikali na Watanzania kwa ujumla. ... 😭😭

Katika Msiba wake watu wengi walimwelezea kama kiongozi mchapakazi, mwenye ushirikiano na aliyejitolea kwa dhati kuwatumikia wananchi wake... ✍🏼

HITIMISHO

Maisha ya Selina Kombani ni somo muhimu kwa kizazi cha sasa na kijacho. Alionyesha kuwa uongozi bora unahitaji kujitoa, kufanya kazi kwa bidii na kuweka maslahi ya wananchi mbele... ✍🏼

Ingawa ameondoka duniani, mchango wake katika maendeleo ya Ulanga na Tanzania utaendelea kukumbukwa kwa miaka mingi ijayo. 

Jina lake limebaki kuwa sehemu ya historia ya viongozi wanawake waliolipigania Taifa kwa moyo wote.

"Viongozi huondoka, lakini matendo yao mema huendelea kuishi katika mioyo ya watu."

@ Wewe Msomaji wangu utamkumbuka SELINA OPESHI KOMBANI kwa lipi???



DKT. KIMAMBO AWAASA WAFAMASIA KUWA VINARA WA MABADILIKO KUELEKEA MUHIMBILI MPYA



Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Delilah Kimambo, amewataka wafamasia wa hospitali hiyo kuendana na kasi ya mabadiliko yanayoendelea kufanyika katika taasisi hiyo na kushiriki kikamilifu katika safari ya kuelekea Muhimbili mpya yenye huduma bora na za kisasa kwa wananchi.

Akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Wafamasia yanayoadhimishwa kila mwaka kuanzia Juni 10 hadi 16, Dkt. Kimambo alisema ni muhimu kwa wataalamu hao kuelewa mwelekeo wa maboresho yanayotekelezwa hospitalini, kutambua mahitaji ya Muhimbili mpya na kutoa ushauri wa kitaalamu utakaosaidia kufanikisha mabadiliko hayo. Alisisitiza kuwa mafanikio ya mageuzi hayo yanategemea ushirikiano, ubunifu na utayari wa watumishi kuyapokea na kuyasimamia kwa pamoja.

Aidha, Dkt. Kimambo alihimiza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya wafamasia na kada nyingine za afya ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na kuhakikisha wagonjwa wanapata matibabu salama na yenye ubora unaokusudiwa.

Kwa upande wao, wafamasia wameishukuru Serikali pamoja na uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya famasi kupitia uwekezaji unaofanyika katika upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na miundombinu ya kisasa inayorahisisha utoaji wa huduma. Wamesema hatua hizo zimekuwa chachu ya kuimarika kwa huduma na kuongeza uwezo wa hospitali kuhudumia wananchi kwa ufanisi zaidi.

Maadhimisho ya Wiki ya Wafamasia mwaka huu yanaongozwa na kauli mbiu isemayo, Famasi: Ufunguo wa Maono ya 2050 katika Sekta ya Afya, ikisisitiza nafasi muhimu ya taaluma ya famasi katika kufanikisha maendeleo ya huduma za afya nchini.






Monday, June 15, 2026

PATUTA YATOA WITO WA UMOJA, AMANI NA MARIDHIANO KWA MUSTAKABALI BORA WA TANZANIA



Kilele cha Tamasha la Bulabo Kanda ya Ziwa 2026 kilichofanyika katika Viwanja vya Ngomeni, Kisesa – Mwanza, kimeacha funzo kubwa kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuhifadhi utamaduni, kuimarisha umoja na kujenga maridhiano kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

Miongoni mwa taasisi zilizoshiriki kwa mafanikio makubwa ni Taasisi ya Pamoja Tutashinda Tanzania (PATUTA ORGANIZATION), ambayo imeendelea kuonyesha dhamira yake ya kuunganisha Watanzania kupitia misingi ya uzalendo, mshikamano na amani.

Mgeni rasmi wa tamasha hilo, Said Mtanda, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza aliyemwakilisha Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Chifu Hangaya, aliwapongeza machifu wa jadi kwa kuendelea kuhifadhi na kurithisha mila, desturi na maadili mema ya Kitanzania.

Alisisitiza kuwa utamaduni wetu unatufundisha kuheshimiana, kusikilizana na kutafuta suluhu za tofauti zetu kwa njia ya mazungumzo. Huo ndio msingi wa kudumisha amani, mshikamano na maendeleo endelevu katika Taifa letu.

Kaulimbiu ya Tamasha la Bulabo 2026 iliyosema:-

"MARIDHIANO KWA NJIA YA AMANI NDIYO JADI YETU, LINDA MAADILI YA MTANZANIA"

imebeba ujumbe mzito unaohitaji kuendelea kuishi mioyoni mwa Watanzania wote. Leo zaidi kuliko wakati mwingine wowote, Taifa linahitaji watu wanaojenga madaraja ya upendo badala ya kuta za migawanyiko; watu wanaotanguliza maridhiano badala ya migogoro; na watu wanaolinda maadili ya Kitanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Ushiriki wa PATUTA ORGANIZATION katika tamasha hili ni ishara kwamba taasisi na wananchi wana nafasi kubwa ya kuendeleza utamaduni wa amani, umoja na uzalendo. Kutoka maeneo mbalimbali ndani na nje ya Mkoa wa Mwanza, wanachama wa PATUTA waliungana kuonesha kuwa nguvu ya Taifa lolote ipo katika mshikamano wa watu wake.

Tamasha la Bulabo 2026 limetukumbusha jambo moja muhimu: Tofauti za mawazo si sababu ya chuki, bali ni fursa ya kujenga maelewano. Tukidumisha amani, tukalinda maadili yetu na kuendeleza utamaduni wa kusikilizana, Tanzania itaendelea kuwa mfano wa umoja na utulivu barani Afrika.

Hongereni PATUTA ORGANIZATION kwa kuwa sehemu ya ujumbe huu mkubwa wa kitaifa.

PAMOJA TUTASHINDA TANZANIA

"Umoja hutujenga, amani hutudumisha, na maridhiano hutuvusha kwenda kwenye maendeleo ya kweli."

Imetolewa na:-

Cde JAMAL ALLY

Katibu Mkuu PATUTA ORGANIZATION





MSAMAHA WA VAT KWA MAFUTA YA KULA, KUCHOCHEA UZALISHAJI WA MAZAO YA MAFUTA NCHINI


 

Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar akisoma hotuba ya bajeti bungeni.

Msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwa mafuta ya kula yanayozalishwa kwa kutumia mbegu zinazozalishwa ndani ya nchi unatarajiwa kuongeza uwekezaji, ushindani wa viwanda vya ndani na kuchochea uzalishaji wa mazao ya mafuta nchini.

Hayo yamesemwa na mchambuzi wa uchumi, Marandu Marwa, akizungumzia hatua mpya za Serikali zilizotangazwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27.

Amesema hatua hiyo itawapa motisha wawekezaji kutumia malighafi zinazozalishwa ndani ya nchi kwa kuwa zitawasaidia kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza faida.

“Kila mwekezaji ataona kutumia mbegu zinazozalishwa ndani ya nchi kama njia rahisi ya kuongeza faida na kupunguza gharama za kodi. Hii itaongeza ushindani na kuwanufaisha wazalishaji wa ndani,” amesema.

Marwa amesema kwa muda mrefu tofauti ndogo ya ushuru kati ya bidhaa zinazoagizwa kutoka nje na zinazozalishwa nchini imekuwa ikidhoofisha ushindani wa viwanda vya ndani na kupunguza hamasa ya uwekezaji mkubwa katika sekta hiyo.

Kauli hiyo inakuja baada ya Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar, kutangaza kuwa Serikali imependekeza kusamehe VAT kwenye mafuta ya kula yanayozalishwa kwa kutumia mbegu zinazozalishwa ndani ya nchi.

Akiwasilisha bajeti ya Serikali ya Sh62.3 trilioni kwa mwaka wa fedha 2026/27, Waziri huyo amesema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza uzalishaji wa ndani na kuimarisha sekta ya viwanda.

Mbali na msamaha huo, Serikali imeendelea kutoza ushuru wa forodha wa asilimia 35 au dola za Marekani 300 kwa tani moja ya mafuta safi ya kula (refined edible oil), kutegemea kiwango kitakachokuwa kikubwa zaidi.

Pia, Serikali imeandaa kanuni za uagizaji wa mafuta ya kula kwa lengo la kudhibiti uingizaji wa mafuta hayo kutoka nje ya nchi na kuhamasisha ukuaji wa tasnia ya mafuta yanayozalishwa kwa kutumia mbegu za ndani.

Aidha, imependekeza kuanza kutoza ushuru wa forodha wa asilimia 10 kwa mwaka mmoja kwenye mafuta ghafi ya soya, karanga, nazi, mnyonyo na haradali, kutoka kiwango cha sasa cha asilimia sifuri.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, hatua hiyo inalenga kuoanisha viwango vya ushuru wa mafuta hayo ghafi na vile vya mafuta ghafi ya alizeti, pamba na mahindi ambayo tayari yanatozwa ushuru wa asilimia 10.

Serikali inaeleza kuwa hatua hizo zitasaidia kulinda na kukuza uzalishaji wa mbegu za mafuta ya kula nchini, kuongeza ajira na kupunguza matumizi ya fedha za kigeni zinazotumika kuagiza mafuta kutoka nje ya nchi.




Serikali Yaweka Mkakati Kuhifadhi Aina 57 za Miti Hatarini Kutoweka



Na Mwandishi Wetu, Dodoma


Serikali imeanza utekelezaji wa mradi maalumu wa kuimarisha uhifadhi wa aina 57 za miti iliyo katika hatari kubwa ya kutoweka nchini, hatua inayolenga kulinda bioanuwai ya Taifa na kuendeleza matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.


Mradi huo wa miaka mitatu unaojulikana kama Enhanced Conservation of 57 Highly Threatened Tanzanian Tree Species ulizinduliwa jijini Dodoma na mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. John Elia.


Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Elia alisema Tanzania imejaliwa kuwa na utajiri mkubwa wa bioanuwai, lakini baadhi ya spishi za miti zinaendelea kukabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa makazi ya viumbe hai na matumizi yasiyo endelevu ya rasilimali za misitu.


Alisema Serikali imeamua kuchukua hatua madhubuti za uhifadhi baada ya zaidi ya aina 376 za miti nchini kuorodheshwa katika Orodha Nyekundu ya Umoja wa Kimataifa wa Uhifadhi wa Mazingira (IUCN) kuwa katika viwango tofauti vya hatari ya kutoweka.


“Mradi huu ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha spishi hizi zinaendelea kuhifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” alisema Elia.


Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi na Kamishna Msaidizi Muandamizi pamoja na Meneja wa Biolojia ya Mbegu za Miti wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Bw. Fandey Mashimba, alisema mradi huo unafadhiliwa na Franklinia Foundation na Missouri Botanical Garden kwa gharama ya dola za Marekani 390,000.


Alisema mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano kati ya TFS na Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) na utahusisha ukusanyaji wa mbegu, uzalishaji wa miche, utafiti wa kisayansi, urejeshaji wa makazi ya asili ya spishi husika pamoja na ujenzi wa uwezo wa wataalamu wa uhifadhi.


Mashimba alisema utekelezaji wa mradi huo utaimarisha juhudi za taifa za kuhifadhi bioanuwai na kuweka msingi wa kuokoa spishi nyingine za miti zinazokabiliwa na changamoto za kutoweka.


Uzinduzi huo ulihudhuriwa na viongozi wa Serikali, wataalamu wa misitu, watafiti na wadau wa uhifadhi kutoka ndani na nje ya nchi.












Friday, June 12, 2026

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA AFYA NA MASUALA YA UKIMWI YAKOSHWA NA TMDA



Na. Mwandishi Wetu,

Dodoma.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya  UKIMWI  yatembelea ofisi za TMDA Makao Makuu Dodoma Juni 10, 2026 kwa lengo la kujionea utendaji wa taasisi na inavyotekeleza majukumu yake. 

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe.  Johannes Lukumayi (Mb) amesema lengo la kamati ni kujionea kwa macho namna taasisi hii muhimu katika kulinda afya ya jamii imejipanga katika kuwahakikishia wananchi wanalindwa afya yao kupitia  bidhaa za dawa na vifaa tiba.

"Tunafahamu umuhimu wa taasisi hii ndani ya nchi katika kulinda afya zetu na nje ya nchi pia katika kuongoza taasisi nyingine" alisema   Mhe.  Lukumay.

Akichangia wakati wa kuhitimisha ziara hiyo, Mhe. Adonis Bitegeko (Mb), aliipongeza Mamlaka kwa mapinduzi makubwa katika kuwekeza katika mifumo ya TEHAMA na aliitaka Mamlaka kuendelea kutatua changamoto ya mifumo ya uingizaji mizigo kwa kushirikiana na wadau wengine kufuatia mabadiliko yaliyopo katika mfumo huo. Aidha alitoa wito kwa Mamlaka  kujipanga ili kuendana na ukuaji wa sayansi na Tecknolojia katika masuala ya udhibiti.

Ziara hiyo pia ilihusisha viongozi wa Wizara ya Afya akiwemo Katibu Mkuu Dkt. Seif Shekalage ambao kila mmoja aliipongeza Mamlaka kwa utendaji na namna inatekeleza majukumu yake.