ANGALIA LIVE NEWS

Friday, September 4, 2026

SHANGWE CHEM CHEM SAFARI LODGE WAKISHINDA TENA TUZO HOTEL BORA YA KIFAHARI AFRICA



Na. Mussa Juma, Babati

mussasiwa@gmail.com 


KWA mwaka wa pili mfululizo, hoteli ya kitalii ya Chem Chem Lodge imeshinda tuzo ya hotel Bora ya kifahari barani Afrika katika tuzo ambazo ziliandaliwa na shirika la kimataifa la Utalii, World Travel Awards (WTA).

Chem Chem Safari Lodge iliyopo eneo la hifadhi ya Jamii ya Wanyamapori (WMA) la Burunge, wilaya ya Babati,Mkoa wa Manyara imeshinda tuzo hiyo mfululizo mwaka 2025 na mwaka 2026.

Ushindi huu ni sehemu ya malengo ya muda mrefu ya waanzilishi wa hotel hiyo, Nicholas Negri na Fabia Bausch kuifanya Burunge WMA kuwa hifadhi ya Jamii Bora zaidi barani Afrika ,kwa kutoa huduma bora za Utalii,kuongezeka Wanyamapori na kuwa na mazingira bora zaidi ya kufanya Utalii wa kifahari.

Wakizungumzia baada ya kukabidhiwa tuzo hizo mbili, Lodge bora ya kifahari Tanzania na Afrika, wafanyakazi wa Chem Chem na viongozi wa Serikali Mkoa Manyara walisema mafanikio hayo ni mkakati wao wa Muda mrefu.

Meneja Mkuu wa Chem Chem Safari Lodge,Jorg Weytjens anasema ushindi huo unathibitisha huduma bora wanazotoa na kuvutia watalii.

"Tunashukuru Sana watalii kutoka sehemu mbalimbali Duniani kuendelea kutupigia kura na kutupa ushindi kutokana na huduma bora tunazotoa"anasema

Mkurugenzi wa halmashauri ya Babati vijijini,Anna Mbogo anasema ushindi wa Chemmchem unadhihirisha ushirikiano baina ya Serikali,wananchi wa vijiji 10 vinavyounda hifadhi hiyo na wafanyakazi wa Chemmchem.

"Sisi kama Serikali tunapongeza ushindi huu kwani utaendelea kutangaza wilaya yetu ya Babati lakini pia kuongeza mapato na kutimiza dhamira ya Rais Samia Suluhu kuvutia watalii Tanzania"amesema

Meneja Rasilimali watu wa Chem Chem Jennifer Giray anasema ushindi waliopata unatokana na kuendelea kutoa huduma bora ambazo zinavutia watalii.

"Jambo kubwa tunashukuru Sana wakurugenzi wetu Nicolas na Fabia Kwa usimamizi mzuri, malengo makubwa waliotuwekea na sasa tunafanya vizuri Afrika"anasema 

Anasema wafanyakazi wa hotel hiyo wanafanyakazi Kwa ushirikiano mkubwa na katika mazingira Mazuri ambayo yanawavutia kutoa huduma bora 

Muongoza watalii wa Chem Chem Isack Joseph anasema wanajivunia tuzo hiyo na kuahidi wataendelea kutoa huduma bora zaidi Kwa watalii.

Joseph anasema wataendelea kutoa huduma Bora na kuvutia mamilion ya watalii na hivyo kuongeza mapato ya hotel na Kwa Serikali.

Meneja wa huduma katika hotel hiyo, George Andrew anasema lengo Lao wakati wote ni kutoa huduma bora Kwa watalii.

Hata hivyo alipongeza ushirikiano ambao wanapewa na Serikali kuanzia ngazi ya Taifa hadi vijijini na hivyo kuwafanya watalii kuwa Salama na wenye furaha wanapowatembelea Muda wote 

Ushindi wa Chemmchem ulitangazwa katika hafla ya kutoa tuzo hizo zilizofanyika wiki 

iliopita Zanzibar.










Wednesday, September 2, 2026

TAWA YATINGA MOROGORO KWA KISHINDO NA TUZO ZA WORLD TRAVEL AWARDS 2026

 


📍Kamishna Kabange ampongeza Rais Samia, asema ushindi huo umefungua milango mipya ya utalii na uwekezaji


✍️ Na Beatus Maganja, Morogoro


MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imewasili rasmi mkoani Morogoro leo, Septemba 2, 2026 ikiwa na tuzo mbili za World Travel Awards 2026 zilizotwaliwa na Hifadhi zake za Selous na Mpanga-Kipengere, siku chache baada ya kutangazwa washindi katika hafla ya tuzo hizo iliyofanyika Agosti 28, 2026, Zanzibar. 


 Akizungumza katika hafla ya mapokezi ya tuzo hizo, iliyofanyika katika Ofisi za Makao Makuu ya taasisi hiyo Morogoro, Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA Mlage Y. Kabange amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi za kuitangaza Tanzania na vivutio vyake katika soko la kimataifa, akisema jitihada hizo zimechangia nchi kufahamika zaidi duniani. Ametaja filamu za Tanzania The Royal Tour na Amazing Tanzania kuwa miongoni mwa juhudi zilizoongeza mwonekano wa Tanzania, huku akiwapongeza pia watumishi wa TAWA, wananchi na wadau wa utalii ndani na nje ya nchi waliohamasisha na kupiga kura na kuziwezesha Hifadhi zake kushinda katika mashindano hayo.

Amesema mafanikio hayo yana uzito wa kipekee kwa kuwa yamepatikana katika mwaka wa kwanza kwa TAWA kushiriki mashindano hayo.

Kabange amesema ukubwa wa ushindi huo unaonekana zaidi kwa kuzingatia ushindani wa vivutio mbalimbali barani Afrika, akifananisha mafanikio hayo na timu inayotwaa ubingwa wa Afrika katika mchezo wa soka. “Tunaongelea mashindano ya Afrika. Kama kwenye mpira, haya ni mashindano ya CAF. Sisi tumekwenda kwenye fainali ya Afrika kwa mara ya kwanza na tumetoka na ushindi. Kwa hiyo siyo kitu kidogo,” amesema Kabange.

Amesema matokeo ya ushindi huo yameanza kujionesha baada ya wadau wa utalii kuanza kutafuta taarifa za namna ya kufika Mpanga-Kipengere mara tu baada ya tuzo kutangazwa Zanzibar. Kwa mujibu wa Kabange, kampuni moja ya ndege ya Zanzibar imeonesha utayari wa kuanzisha safari za moja kwa moja kwenda hifadhini humo mara miundombinu husika itakapokuwa tayari. Amesema kuwa mwitikio huo unaashiria fursa ya kuongeza watalii, mapato, uwekezaji na manufaa kwa jamii zinazozunguka maeneo hayo.

Kutokana na fursa hizo, Kabange amewakaribisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika miundombinu, malazi na huduma nyingine za utalii katika maeneo ya TAWA. Amesema uzoefu wa mafanikio ya Selous na Mpanga-Kipengere umeipa Mamlaka ujasiri wa kuyapeleka maeneo mengine katika ushindani wa kimataifa, huku Makuyuni Wildlife Park na Hifadhi ya Pande yakiwa miongoni mwa yaliyotajwa. 

Kwa upande wake, Naibu Kamishna wa Uhifadhi Emmanuel B. Musamba, *ndc* amesema tuzo hizo zina maana kubwa kwa kuwa ni uthibitisho wa kimataifa wa ubora wa rasilimali za utalii za Tanzania na juhudi zinazofanywa katika kuzihifadhi. “Hii ni kura ya imani kwa Tanzania, ni kura ya imani ya kimataifa kwa utajiri wa rasilimali tulizonazo Tanzania, lakini pia kwa juhudi za uhifadhi na uwezo wa maeneo yetu ya wanyamapori kutoa uzoefu wa kipekee,” amesema Musamba.

Musamba amesema ushindi huo pia ni heshima kwa watumishi wa TAWA na wale waliotangulia katika jukumu la kulinda rasilimali za wanyamapori, wakiwemo waliopoteza maisha katika utekelezaji wa jukumu hilo. Amesema mafanikio hayo yanaongeza wajibu wa Mamlaka kuhakikisha usalama wa wanyamapori, ubora wa maeneo na uendelevu wake vinaimarishwa kadri Tanzania inavyopanua nafasi yake katika soko la utalii la kimataifa.

“Tuzo hizi mbili siyo mwisho, ni mwanzo wa safari,” amesema Musamba, akisisitiza kuwa heshima iliyopatikana lazima iambatane na wajibu wa kuhakikisha ukuaji wa utalii hauathiri rasilimali zinazoubeba, bali unaimarisha uhifadhi endelevu, uchumi wa jamii na mchango wa sekta hiyo kwa Taifa.

Tuzo hizo ziliwasili Morogoro zikisindikizwa na shamrashamra zilizorindima kuanzia Kituo cha Treni ya Mwendokasi (SGR) cha Jakaya Mrisho Kikwete hadi Makao Makuu ya TAWA ambako viongozi, maafisa, Askari wa TAWA , watumishi wa taasisi mbalimbali pamoja na baadhi ya wananchi walikusanyika kuzipokea. 

Selous imetwaa Africa’s Leading TouristAttraction 2026, huku Mpanga-Kipengere ikitwaa Africa’s Leading Honeymoon Destination 2026 mafanikio yaliyoiwezesha TAWA kuibuka na tuzo mbili katika ushiriki wake wa kwanza.









TAMASHA LA 44 LA KIMATAIFA LA SANAA NA UTAMADUNI BAGAMOYO KUFANYIKA OKTOBA 28-31 MWAKA HUU, VIKUNDI 104 KUSHIRIKI

 


Mji wa Bagamoyo unatarajiwa kulipuka kwa burudani wakati Tamasha la 44 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo litakalofanyika Oktoba 28 hadi 31 2026, likiwakutanisha wasanii na vikundi 146 kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Septemba 2, 2026, Kaimu Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) Bw. Gabriel B. Kiiza, amesema kati ya vikundi hivyo, 104 vinatoka ndani ya Tanzania huku 42 vikiwa vya kimataifa.

Amesema shughuli za Tamasha zitaanza rasmi kwa mkesha utakaofanyika Oktoba 27, kabla ya kuendelea na matukio mbalimbali ya sanaa na utamaduni katika siku nne ambazo Tamasha hilo litatimua vumbi.

Katika kipindi hicho, wananchi na wageni watapata fursa ya kushuhudia burudani na maonesho mbalimbali yatakayohusisha muziki, ngoma, maigizo, sarakasi, ushairi, vichekesho, mazingaombwe na filamu.

Mbali na burudani, tamasha hilo pia litakuwa jukwaa la kukuza na kuonesha kazi za sanaa za ufundi pamoja na shughuli za biashara zinazohusiana na sanaa na utamaduni.

Kwa upande mwingine, washiriki wa tamasha watapata fursa ya kuifahamu zaidi historia na utamaduni wa Mji wa Bagamoyo kupitia ziara katika baadhi ya vivutio muhimu vya kihistoria na kiutamaduni, ikiwemo Mji Mkongwe wa Bagamoyo, Magofu ya Kaole (Kaole Ruins) na Boma la Wajerumani.

Tamasha la 44 la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo ni sehemu muhimu ya kuendeleza, kuhifadhi na kutangaza sanaa na utamaduni wa Tanzania, huku likitoa nafasi kwa wasanii wa ndani na nje ya nchi kukutana, kubadilishana uzoefu na kuonesha vipaji vyao.





Sunday, August 23, 2026

WATALII WAFURAHIA UTALII WA BOTI HIFADHI YA NYERERE

 



Hifadhi ya Taifa ya Nyerere imeendelea kuwavutia watalii kutoka ndani na nje ya Tanzania, huku utalii wa boti katika Mto Rufiji ukiwa miongoni mwa shughuli zinazotoa uzoefu wa kipekee kwa wageni.

Wakiwa ndani ya boti, watalii hupata fursa ya kuvuka kwenye mandhari ya kuvutia ya Mto Rufiji na kushuhudia kwa karibu wanyamapori mbalimbali wanaoishi pembezoni mwa mto, wakiwemo viboko, mamba, tembo na ndege wa aina mbalimbali. 

Tabasamu na furaha za watalii zinadhihirisha namna safari hii ya maji inavyobadilisha ziara ya Hifadhi ya Nyerere kuwa kumbukumbu isiyosahaulika.

Nyerere si safari ya kutazama wanyamapori pekee—ni uzoefu wa kuishi na kufurahia uzuri wa asili ya Tanzania kwa njia ya kipekee. 

Karibu Hifadhi ya Nyerere, panda boti, tembelea Mto Rufiji na ujionee Tanzania yenye sura ya kipekee.










Saturday, August 22, 2026

NAIBU SPIKA SILLO APONGEZA VIONGOZI KWA UBUNIFU WA MANYARA TANZANITE MARATHON

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Daniel Sillo


Mbio za Hisani za Manyara Tanzanite Marathon zimefanyika leo mkoani Manyara, zikihudhuriwa na watu mbalimbali kutoka maeneo tofauti ya nchi pamoja na viongozi mbalimbali, huku lengo kuu likiwa ni kuchangisha fedha kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Daniel Sillo, aliyemwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alitarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mbio hizo, amepongeza uongozi wa Mkoa wa Manyara kwa ubunifu wa kuanzisha mbio hizo zinazolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya kuimarisha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Sillo amesema hatua hiyo ni mfano wa ubunifu unaopaswa kuigwa na maeneo mengine nchini, akisisitiza umuhimu wa kushirikisha jamii na wadau katika kusaidia kuboresha huduma za afya.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa TAMISEMI, Jafari Rajabu, amesema mbio hizo zimeleta tija kubwa katika juhudi za kuokoa maisha ya watoto, akiwataka wananchi na wadau kuendelea kuunga mkono jitihada zinazolenga kuboresha afya ya watoto.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewashukuru wadau wote walioshiriki na kuunga mkono maandalizi ya mbio hizo, akisema ushiriki wao umewezesha kufanikisha azma ya kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto wanaohitaji huduma maalumu za afya.

Baadhi ya washiriki wa mbio hizo wamesema, pamoja na kushiriki kwa ajili ya mazoezi na kuimarisha afya zao, wameona umuhimu wa kuwa sehemu ya harakati za kuchangia maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Wamesema ushiriki wao katika Manyara Tanzanite Marathon umewapa fursa ya kufanya mazoezi huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kusaidia kuokoa maisha ya watoto, hivyo kuwataka wananchi wengine kuendelea kushiriki katika matukio yenye malengo ya kijamii na kiafya.



















Monday, August 17, 2026

MASHINDANO YA NGALAWA YANOGESHA MSIMU WA PILI WA FuToPiA ZANZIBAR 2026



ZANZIBAR - Ngalawa ya "Baba Karudi" iliyoongozwa na Hassan Thajo imeibuka mshindi wa kwanza katika mashindano ya mbio za ngalawa yaliyofanyika Bahari ya Fumba.

Mashindano hayo yalishuhudia ushindani mkubwa kutoka kwa ngalawa 12 na ni sehemu ya program ya michezo ya asili katika msimu wa pili wa tamasha la FuToPiA Zanzibar lililofanyika tarehe 8-9 Agosti, 2026.

Katika mbio hizo, Ngalawa ya "Wape Kazi" iliyoongozwa na Nahodha Aboubakari Kondo ilishika nafasi ya pili, huku nafasi ya tatu ikinyakuliwa na Ngalawa ya "Utoto Raha" iliyoongozwa na Nahodha Hussein Thajo.

Akizungumza baada ya mashindano, Mratibu wa Michezo ya Asili wa FuToPiA Zanzibar, Joseph Klanda amesema mashindano hayo yanalenga kuwakaribisha wananchi wa maeneo ya Nyamanzi, Dimani na Fumba Town kujumuika na kufurahia tamasha hilo pamoja.

"Chombo cha 'Baba Karudi' washindi wa kwanza kilipewa nguvu na kampuni ya Fortitude Security. Chombo cha 'Wape Kazi' mshindi wa pili kilipeperusha bendera ya FuToPiA Zanzibar, na chombo cha mshindi wa tatu kilipeperusha bendera ya Clouds Media," amesema Klanda.

Aidha, amesema washindi wote kuanzia nafasi ya kwanza hadi ya 12 walipata zawadi ya fedha taslimu pamoja na shukrani za ushiriki.