ANGALIA LIVE NEWS

Tuesday, July 14, 2026

REKODI MPYA MLIMA KILIMANJARO MZEE WA MIAKA 90 AKWEA KILELE CHA UHURU

 



Raia kutoka nchini Marekani daktari mstaafu  Art Ulene, ameandika historia mpya baada ya kufanikiwa kufika katika Kilele cha Uhuru, Mlima Kilimanjaro, na kuvunja rekodi ya kuwa miongoni mwa watu wenye umri mkubwa zaidi kufikia kilele hicho jana Julai 13, 2026. Mafanikio hayo yameambatana na sherehe ya kipekee ya kukata keki juu ya kilele ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku yake ya kuzaliwa.

Katika tukio hilo Dkt. Ulene alikata keki akiwa amezungukwa na waongoza watalii, wapagazi, na wapandaji wenzake huku wakimpongeza kwa ujasiri, wakimtakia afya njema na pamoja na kumpongeza kwa adhma yake ya kutimiza ndoto hiyo katika umri wa miaka 90.

Mafanikio hayo yameendelea kuitangaza Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro na Tanzania kwa ujumla kama kitovu cha utalii wa milima duniani, yakionyesha uwezo wa Mlima Kilimanjaro kuwavutia wageni wa rika mbalimbali wanaotafuta changamoto, mafanikio binafsi na mandhari ya kipekee.




THE PRIDE RETURNS HOME




KLABU ya Simba SC wameingia mashirikiano na Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) kuelekea  Simba Day katika kusherekea miaka 90 ya tokea kuanzishwa kwake hapa nchini, "The Pride Returns Home".

Awali wakizungumza kwenye tukio hilo maalum Jijini Arusha, Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Abdul-Razaq Badru amesema:

 "Leo Julai 13,2026 ni siku ya fahari kwetu Ngorongoro na Klabu ya Simba ya kuunganisha utalii na michezo kama sekta mbili ambazo zinafanya kazi pamoja kwa namna tofauti. 

Tunafahamu kwamba mpira wa miguu unaunganisha watu wengi kwahiyo tunaamini kwamba tunapoamini ni fursa ya kuunganisha watu wa aina mbalimbali kupitia utalii."



"Tunapokutana leo tunafahamu kwamba katika sekta ya mpira wa miguu, Simba SC ni chapa kubwa. Tunasherekea namna chapa ambazo zitafanya kazi pamoja. Chapa mbili zitapaishana kutokana na ukubwa wake. Chapa ya Ngorongoro ni kubwa sababu ya historia, chapa hii inahusisha wanyama wa aina zote wale maarufu na kwa wingi katika eneo moja dogo."

"Sisi tunaamini wenzetu wa Klabu ya Simba wamerudi nyumbani lakini pia sababu Hifadhi ya Ngorongoro inajulikana duniani. Kutakuwa na kampeni ya Simba Visit Ngorongoro, The Pride Reurns Home na hii itakuwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 90 ya Klabu ya Simba."

"Wale wote ambao wanatembelea hifadhi na watakaokuja wajue kwamba wanachangia wafahamu kwamba wanachangia katika uhifadhi na ukuaji wa nchini yetu. Mwakani tutakuwa wenyeji wa AFCON na dunia nzima itaelekea huku hivyo tunaamini hii ni shamrashamra na tumeamua kuanza na hili. Fursa hii tuliyoipata itatupaisha zaidi."- Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Abdul-Razaq Badru.



Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Simba SC, Zubeda Sakuru amesema:

: "Tangu kuanzishwa kwa Klabu ya Simba mwaka 1936 tumekuwa tukitumia mnyama Simba. Lakini tukizungumzia hifadhi ambayo imetambuliwa  hadi na UNESCO tunazungumzia Hifadhi ya Ngorongoro. Na sisi tumeona kusherekea miaka 90 kwa kurudi nyumbani ambako ni Ngorongoro. Tunaamini miaka hii 90 ya Simba ambayo tumepita mambo mengi lakini tumeweza kusimama sababu asili ya Simba ni kushinda."

"Klabu ya Simba ndio klabu inayofatiliwa zaidi Afrika Mashariki na Kati, hili sio nguvu ndogo. Hii tunaiona kama fursa pekee ya kuweza kuunganisha nguvu yetu pamoja na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro. Tunapokelekea katika miaka 90 tutafanya shughuli za tangu kuanzishwa kwetu katika Hifadhi ya Ngorongoro ambako tutafanya uzinduzi wa matawi na programu nyingi."

"Niwatake Wanasimba wote dunia nzima kuungana nasi katika kuadhimisha miaka 90 tangu kuanzishwa kwa Simba kwa kufatilia Wiki ya Simba na shughuli ambazo tutazifanya. Lakini kwa kipekee kabisa tunapokwenda kuzindua jezi mpya lakini jezi mpya itaonekana katika Wiki ya Simba. Natoa wito wa kipekee kuungana nasi."- CEO wa Simba SC, Zubeda Sakuru.



Nae Mwenyekiti wa Bodi wa Simba SC, Crescentius Magori amesema: "Hii maana yake tumeanza count down kuelekea kwenye Simba Day. Kama kuna mkoa Simba tukija huwa tunasikia raha ni Arusha kuna wakati mwingine huwa nafatilia kwa mkuu wa mkoa kuuliza ule uwanja unaisha lini. Nadhani mkoa ambao utakuwa wa kwanza kupata shughuli ya Simba Day kwa miaka ijayo ni Arusha sababu ya ule uwanja."

"Simba ilikuwa ya kwanza kusupport utalii kwa Visit Tanzania, lakini kama mnakumbuka mwaka juzi tulizindua jezi kwa kibegi na kikaenda Mlima Kilimanjaro. Mwaka huu tumeamua kusherekea miaka 90 na kusherekea Wiki ya Simba kupitia Hifadhi ya Ngorongoro. Niwahakikishie kwa kushirikiana na Simba itakuwa na faida kwa taasisi zote mbili."

"Niwahakikishie mmefanya maamuzi sahihi kushirikiana na Simba. Simba inawafuasi kwenye mitandao zaidi ya milioni 20, kwahiyo ushirikiano huu ambao tutafanya na countdown hadi tunakwenda kuzindua tutapata wateja wengi sana wa ndani na nje. Tutumie wakati huu kutangaza product nyingi kwelikweli. Sisi tunakuhakikishia tutakusupport, tupo tayari kusupport hifadhi, utalii na uchumi wa nchi hii uzidi kupaa."- Mwenyekiti wa Bodi, Crescentius Magori.



Kwa upande wa Makamu mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro, Dkt. Harrieth Mtae nae amebainisha kuwa: 

"Nishukuru Klabu ya Simba kwa kukubali kuwa mshirika wetu hasa katika safari hii muhimu ya kuitangaza Tanzania kupitia michezo mbalimbali pamoja na utalii. 

Leo ni mwanzo mpya ya jinsi ya sekta ya umma na taasisi za michezo zinavyoweza kushirikiana  katika kuleta thamani kwa taifa letu. Tunaziunganisha chapa mbili kubwa za Afrika katika kuitangaza Tanzania."

"Bodi ya Wakurugenzi inaunga kikamilifu kwakuwa unaendana na kabisa na maono ya kuifanya Ngorongoro kuwa destination ya kiwango cha kimataifa lakini pia ikitoa mchango wa utekelezaji wa vipaumbele vya taifa vya kukuza utalii, kukuza uchumi na diplomasia ya kimkakati."

"Tunaamini kupitia kampeni ya Simba na Ngorongoro ya The Pride Returns Home, mamilioni ya Watanzania na mashabiki wa mpira wa miguu watapata sababu mpya ya kutembelea Ngorongoro na kujivunia urithi wa nchi yao. 

Tunapoelekea kwenye AFCON 2027 ushirikiano huu unaonyesha kwamba michezo inaweza kuwa chombo cha kutangaza utalii, kuhamasisha uhifadhi na kuijenga Tanzania kama destination bora ya Afrika. 

Kwa mara nyingine nawashukuru viongozi wa Simba Sports Club kwa maono haya ya pamoja. Tunatarajia ushirikiano  wa muda mrefu utakaoleta manufaa kwa taasisi zote mbili na kwa taifa kwa ujumla. Karibuni Nyumbani, Karibuni Ngorongoro."- Makamu mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro, Dkt. Harrieth Mtae.








Sunday, July 12, 2026

FIFA WORLD CUP EARNINGS FOR AFRICA TEAMS 2026



🇲🇦 Morocco — $31.5M

🇪🇬 Egypt — $17.5M

🇸🇳 Senegal — $13.5M

🇩🇿 Algeria — $13.5M

🇨🇩 DR Congo — $13.5M

🇨🇻 Cape Verde — $13.5M

🇨🇮 Ivory Coast — $13.5M

🇿🇦 South Africa — $13.5M

🇬🇭 Ghana — $13.5M

🇹🇳 Tunisia — $10.5M 

#WorldCupwithMicky

#FIFAWorldCup

ZINGATIA HAYA UKIWA MAHAKAMANI

 


1. Fika muda na siku uliyoambiwa usichelewe hata dakika 5

Kesi yako inaweza kufutwa au kuondolewa dhamana. 


2. Toa sauti kubwa unapozungumza

Inakera sana Hakimu/Jaji anapokusikia kwa chini na hutaki kuongeza sauti, kumbuka yeye ndie mtoa maamuzi. 


3. Ongea kwa taratibu au kwa kituo.

Ili Hakimu au Jaji apate nafasi ya kuandika, kuwa speed itapelekea ushahidi wako muhimu kwa bahati mbaya unaweza usirekodiwe na kushindwa kesi.


4. Usiikasirikie Mahakama na kuzira.

Tumia maneno yenye hekima na ushawishi kujenga hoja zako.


5. Hakikisha unaushahidi kwa kila hoja unayojenga.

Maamuzi yanatokana na ushahidi zaidi kuliko maneno matupu.


6. Usiongee uongo.

Ukijulikana unadanganya hutoaminika tena


7. Epuka mapozi hasa wanawake.

Mahakamani ni sehemu serious sio sehemu ya kujishebedua na kuonyesha urembo


8. Usitoe Rushwa au kumpa Zawadi Hakimu au jaji.

Hasa kwenye dhamana au ili kushinda, ni kosa kisheria na unaweza kukamatwa on spot.


9. Usikatae kutoa ushahidi na kukaa kimya kwa kiburi unaweza pia kuchukuliwa hatua.


10. Mwisho Uhakimu na Ujaji ni kazi ya MUNGU aliyowapa watu wachache wenye MAADILI kufanya kwa niaba yake katika HAKI

WASHIRIKI ZAIDI YA 500 KUCHAGIZA UTALII WA NDANI, ARUSHA TOURISM MARATHON IKIRINDIMA HIFADHI YA TAIFA ARUSHA




Na. Calvin Katera - Arusha.


Zaidi ya washiriki 500 kutoka ndani na nje ya mipaka ya Tanzania ikiwemo Kenya, Uganda, Uingereza na Ujerumani wachagiza utalii wa ndani kwa kushiriki mbio za Arusha Tourism Marathon zilizorindima ndani ya Hifadhi ya Taifa Arusha ikihusisha mbio ndefu na mbio fupi za kilometa 2.5, kilometa 5, kilometa 10 na kilometa 21, leo Julai 12, 2026, jijini Arusha.


Washiriki hao walitumia tukio hilo kama fursa ya kujionea vivutio vya kipekee vinavyopatikana ndani ya Hifadhi ya Taifa Arusha, ikiwemo Serengeti ndogo, wanyamapori na ndege mbalimbali, misitu na mandhari ya mlima Meru, jambo lililowapa uzoefu unaounganisha michezo, utalii na uhifadhi.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi na Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Arusha Witness Shoo, alisema mbio hizo zimeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo hifadhini, kuhamasisha utalii wa ndani na mchango wa michezo na burudani katika kuzitangaza Hifadhi za Taifa, kitaifa na kimataifa.

Kwa upande wake, Bw. Cornell Magoti, Mkurugenzi na Mwanzilishi ya mbio hizo za Arusha Tourism Marathon alisema lengo la mbio hizo ni kuunganisha sekta ya michezo na utalii kwa kuhamasisha watu kutembelea vivutio vya Tanzania, huku zikichochea uchumi wa eneo kupitia ongezeko la wageni wanaotumia huduma mbalimbali za utalii, malazi na usafiri.

Aidha, washiriki walieleza kufurahishwa na mazingira salama na yenye kuvutia ya hifadhi hiyo, wakisema mbio hizo zimewapa fursa ya kipekee ya kufanya mazoezi huku wakifurahia mandhari ya kipekee ndani ya hifadhi, hali iliyowafanya wengi kuahidi kurejea tena pamoja na familia na marafiki zao kutalii na kujiunga na matukio mengine ya kimichezo na burudani yatakaoendelewa kubuniwa na kuibuliwa.

Arusha Tourism Marathon imejenga msingi na kuwa moja ya matukio muhimu ya utalii wa michezo nchini, ikiiunga mkono jitihada za Serikali kupitia TANAPA na wadau wa sekta ya utalii na uhifadhi, kuongeza idadi ya watalii wa ndani na kimataifa, pamoja na kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii barani Afrika.












KAIMU MKURUGENZI WA IDARA YA MISITU NA NYUKI AVUTIWA NA TAFITI ZA TAFORI KUHUSU UBORA WA ASALI YA TANZANIA

 


📍 Viwanja vya Sabasaba, Dar es Salaam


Matokeo ya tafiti za Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) yanayoonesha kuwa asali ya Tanzania inakidhi viwango vya soko la kikanda na kimataifa kwa kuzingatia ubora wake, yamekua kivutio kwa Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Daniel Pancras, alipotembelea taasisi hiyo katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Bw. Pancras alitembelea  TAFORI leo Julai 12, 2026, wakati wa ziara yake ya kukagua na kutembelea taasisi na idara zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii zinazoshiriki maonesho hayo yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba jijini Dar es Salaam.

Akiwa katika banda hilo, alipata maelezo kuhusu tafiti mbalimbali zinazotekelezwa na TAFORI, ikiwemo utafiti uliochambua ubora wa asali inayozalishwa katika maeneo mbalimbali nchini kwa kuzingatia mikoa, hali ya hewa, aina ya udongo na vyanzo vya maua.

Matokeo ya utafiti huo yanaonesha kuwa sifa za asali ya Tanzania, zikiwemo utamu, riha na viambata vyake, zinakidhi viwango vya soko la kikanda na kimataifa.

Bw. Pancras pia ameipongeza TAFORI kwa kuendelea kusogeza huduma za kitafiti karibu na wananchi na wadau kupitia ushiriki wake katika maonesho hayo.

TAFORI inaendelea kuwakaribisha wananchi na wadau kutembelea banda lake ndani ya Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii ili kupata elimu, ushauri wa kitaalamu na kufahamu matokeo ya tafiti zinazochochea maendeleo ya sekta ya misitu na nyuki.




WANANCHI WAZIDI KUFURIKA BANDA LA MUHIMBILI KATIKA MAONESHO YA SABASABA 2026



Mamia ya wananchi wameendelea kufurika katika Banda la Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba ili kupata huduma mbalimbali za afya, elimu na ushauri wa kitaalamu kutoka kwa wataalamu wa hospitali hiyo.

Wananchi wanaotembelea banda hilo wanapata fursa ya kujionea huduma za kisasa za kibingwa na kibingwa bobezi zinazotolewa na Muhimbili, ikiwemo elimu ya huduma za dharura, uchunguzi wa awali wa afya, ushauri wa kitaalamu pamoja na maonesho ya teknolojia zinazotumika katika utoaji wa huduma za upasuaji.

Baadhi ya wananchi waliofika katika banda hilo wamesema wamevutiwa na namna Muhimbili ilivyowasogezea huduma karibu, hatua iliyowawezesha kupata elimu sahihi ya afya na kuelewa kwa undani zaidi huduma mbalimbali zinazopatikana katika hospitali hiyo ya taifa.

Kutokana na mwitikio huo mkubwa, Hospitali ya Taifa Muhimbili imeendelea kuwakaribisha wananchi kutumia siku zilizobakia za maonesho kutembelea banda hilo ili kupata elimu ya afya, ushauri wa kitaalamu na kujionea ubingwa na ubobezi unaotolewa na hospitali hiyo katika kuimarisha afya na kuokoa maisha ya Watanzania.





Thursday, July 9, 2026

TFS KUIMARISHA UREJESHAJI WA MISITU ILIYOHARIBIWA



Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeanza kutekeleza ahadi ya kurejesha ardhi ya misitu iliyoharibiwa kwa kiwango kikubwa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha ardhi inaendelea kuwa hai na yenye uwezo wa kuhimili mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Akizungumza katika kikao kazi cha kujadili Mradi wa Urejeshaji endelevu wa Mazingira na Uhifadhi wa Bayonuai, Naibu Katibu Mkuu Muungano kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdallah Mitawa, amesisitiza umuhimu wa kutunza mazingira, akieleza kuwa ardhi ndiyo msingi wa maisha na nguzo muhimu ya maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Vyanzo vya Mbegu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Dkt. Fortunata Senya, amesema ushirikishwaji wa wadau, taasisi na mashirika mbalimbali ni nguzo muhimu katika kuhakikisha lengo la kurejesha ardhi iliyoharibiwa linafikiwa kwa ufanisi na kwa matokeo endelevu.

Naye Mkurugenzi wa Uzalishaji wa Mbegu za Miti wa TFS, Dkt. Hamza Katety, amesema kikao kazi hicho kinatarajiwa kutoa majawabu na mapendekezo yatakayosaidia kuimarisha utekelezaji wa mpango wa urejeshaji wa ardhi ya misitu na kuhifadhi bayonuai nchini.











RAIS DKT. MWINYI: TAMKO LA PAMOJA CCM NA ACT-WAZALENDO LAFUNGUA NJIA YA UTEKELEZAJI WA SERIKALI YA UMOJA WA KITAIFA



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Tamko la Pamoja kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo linafungua njia ya utekelezaji wa uundaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa na kuimarisha amani, umoja, mshikamano na maendeleo ya Zanzibar.

Rais Dkt.Mwinyi ameyasema hayo baada ya kushuhudia utiaji wa saini wa ajenda zilizokubaliwa kwa pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi kufuatia Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa Zanzibar baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo katika Viwanja vya Ikulu Zanzibar leo tarehe 09 Julai, 2026.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema maridhiano hayo yanaonesha dhamira ya viongozi kuweka mbele maslahi ya taifa, huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote kuhakikisha mchakato huo unadumisha utulivu, utawala bora na maendeleo endelevu.


Halikadhalika, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongeza hatua hiyo akieleza kuwa maridhiano hayo yanafungua ukurasa mpya wa kuimarisha umoja, utulivu na mshikamano miongoni mwa Wazanzibari, na ni ishara ya ukomavu wa kisiasa na dhamira ya kujenga mazingira ya amani na maendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Taifa, Mhe. Othman Masoud Othman, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa kuendeleza mchakato wa maridhiano, akisema umefungua njia ya kupatikana kwa ufumbuzi wa kudumu wa changamoto za kisiasa Zanzibar.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi; Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume na Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein; Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla; Viongozi wa vyama vya siasa, Viongozi wa dini, Viongozi wa Serikali za SMT na SMZ, Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Mabalozi, Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa pamoja na wananchi mbalimbali.