Sunday, August 19, 2012

Meneja Bonite Bottlers nusura auawe


Meneja wa Kampuni ya Bonite Bottlers tawi la Tanga Ramadhan Mbwana (32), mkazi wa Sahare jijini hapa amenusurika kuuawa na watu wasiojulikana waliojitambulisha kama askari polisi ambapo walimpiga risasi katika mkono wake wa kushoto.

Akizungumzia tukio hilo muda mfupi tu baada ya Mbwana kuingizwa katika chumba cha upasuaji, babu wa majeruhi huyo, Hashim Twalib, alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 18, mwaka huu majira ya saa 1.30 asubuhi huko katika eneo la Gofu jijjini hapa.



Kwa mujibu wa maelezo ya majeruhi huyo, alisikia sauti ya watu wakizungumza na mlinzi huku wakidai kuwa wao ni askari polisi na wamefika katika eneo hilo kumkamata mtuhumiwa aliyefanya tukio la uhalifu katika eneo la Barabara ya 14 jijini hapa.

Twalib alisema kuwa mara tu Mbwana alipotoka ndani ya ofisi yake alikutana na watu wawili wakiwa wameshika mitutu ya bunduki huku wawili wengine wakiwa nje ya geti na ndipo bila mazungumzo walianza kumshambulia kwa risasi.

“Majambazi hao walifika na usafiri wa pikipiki hadi hapo depot na wawili walibaki nje wawili wakaingia ndani na ndipo baada ya mbwana kutoka nje wakaanza kumshambulia kwa risasi nyingine alizikwepa ila nyingine ndiyo ilimpata mkononi na kama hivyo sasa ameingizwa kwenye chumba cha upasuaji,” alisema.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Constantine Massawe, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa majambazi hao walifanikiwa kupora fedha taslimu Sh. milioni 7 zilizokuwa zikitarajiwa kupelekwa benki zilizotokana na makusanyo ya mauzo ya Agosti 17, mwaka huu.




 
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments: