Tuesday, August 14, 2012

Mpina sasa kuwasilisha vielelezo vya ufisadi Alhamisi


Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina, (CCM), jana alishindwa kuwasilisha vielelelezo vya taarifa mbalimbali kuthibitisha ufisadi wa Sh. trilioni 11.6 uliotokea kati ya mwaka 1970 hadi mwaka 2008.

Akizungumza na NIPASHE, mjini Dodoma Mpina alisema jana kuwa hakuviwasilisha baada ya kupokea ushauri kutoka kwa ofisi ya Bunge, walimtaka kuviwasilisha Alhamis wiki hii.



“Wamenishauri kuwa ni vema nikaviwasilisha siku ambayo bajeti ya Wizara ya Fedha inasomwa (Alhamis), kwa hiyo sikuviwasilisha leo (jana),” alisema Mpina.

Mpina alikaririwa juzi alisema alimshangaa Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa, alipokuwa akisoma bajeti kuu hakugusia kuhusiana na suala hilo.

Alisema serikali haijafanya uchunguzi wowote na hakuna jitihada zozote za kufilisi na kutaifisha fedha hizo na kuzirejesha nchini badala yake imekaa kimya kana kwamba hakuna kilichotokea.

Alisema serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kitengo cha Financial Intelligence (FIU), Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali (DPP) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) inazo taarifa za sakata hilo.
CHANZO: NIPASHE

No comments: