Wednesday, October 30, 2013

Nilishauriwa kumuua, huyu, kisa? mlemavu

Mtoto mwenye ulemavu, Oini Meng’ariki akiwa nyumbani baada ya kutoka shuleni katika Kijiji cha Kivululu wilayani Arumeru Mkoa wa Arusha.Picha na Filbert Rweyemamu 
Na Filbert Rweyemamu, Mwananchi
Hata vidole vyake haviko sawa vilivyo vidole vya miguu vya watu walio wengi. Kwa ujumla ana tofauti ya namna miguu yake ilivyo ukilinganisha na watu walio wengi.
Oini Meng’oriki ni mtoto aliyezaliwa Septemba 11,2009; ni miongoni mwa watoto waliozaliwa akiwa na ulemavu wa viungo,hana mikono na miguu yake ina ulemavu kiasi kwamba hawezi kutembea.
Ni kwamba miguu yake imepinda, kiasi kwamba hata kukanyaga chini ili atembee inakuwa ngumu.
Hata vidole vyake haviko sawa vilivyo vidole vya miguu vya watu walio wengi. Kwa ujumla ana tofauti ya namna miguu yake ilivyo ukilinganisha na watu walio wengi.
Hata hivyo ukionana nae utatamani kuendelea kuwa nae kutokana na kuonekana mwenye tabia njema, sura ya matumaini na kuonyesha furaha muda mwingi wa maisha yake.
Tabia yake ya furaha, imesabisha awe na marafiki wengi, licha ya udogo wake wa umri.
Oini ni mtoto wa kwanza kwa mama yake Eva Meng’oriki (21) akiwa ni mke wa tatu kwa mume wake Meng’oriki Sumeno mkazi wa Kijiji cha Kambala,Wami Dakawa Wilaya ya Mvomero, Morogoro katika jamii ya wafugaji wa Kimasai.
Eva anasema baada ya kujifungua na kuona mtoto aliyempata ana ulemavu alishtuka kwa vile hajawahi kutokewa.
“Kama mwanadamu mwingine yeyote nilishtuka, lakini baada niliona haya ni mambo ya kawaida, naamini ni mpango wa Mungu, hakuna la kufanya zaidi ya kumpenda na kuahidi kumtunza,” anasema.
Anaongeza kuwa “Naamini Mungu ni kila kitu katika maisha yetu yeye akiamua kitu fulani hakuna wa kukipinga,” anasema.
Anaongeza kuwa “Nisingeweza kumkufuru Mungu wala kumlaumu kwa lolote, kwani amenipatia mtoto ambaye ana ulemavu kwa mapenzi yake na anajua kwanini imekuwa hivi.
“Jambo la kushangaza ni kwamba baadhi ya wanawake niliokuwa nao hospitali ya Bwagala,Turiani baada ya kujifungua waliniambia nisimnyonyeshe ili afe kwa njaa.
“Nilisononeka sana kuambiwa kauli ile, nilichojifunza ni kwamba huenda kuna walemavu wengi wanauawa, kwani ni wanawake wengi waliokuwa wakinishauri nimuue, namshukuru Mungu kwamba sikuwahi kukubaliana na ushauri wao hata kidogo, sikutaka mwanangu afe, niliona kama ni mashetani wale waliokuwa wakinishauri huo unyama.

1 comment:

Magai. said...

Kwenye show ya Oprah au you tube angalia pastor Nick Vujicic. Nick hana mikono wala miguu, lakini anafanya Kila kitu, pengine vizuri zaidi kuliko Watu wa kawaida. Anasema kila kitu kinawezekani ukimtegemea Mungu.