Advertisements

Sunday, June 8, 2014

Wabunge waumbuana kupokea rushwa bungeni

Mbunge wa Tunduru, Mtutura Mtutura (CCM).PICHA|MAKTABA

Dodoma. Mbunge wa Viti Maalum, Suzan Kiwanga (Chadema), amewaumbua wabunge wenzake kuwa wanapeana na kuchukua rushwa ndani ya Bunge.
Suzan aliyasema hayo juzi jioni wakati akichangia katika mkutano wa Chama cha Wabunge walio katika Mapambano dhidi ya Rushwa (APNAC). Suzan alisema vitendo hivyo vya rushwa vilionekana wakati wabunge hao walipokuwa wakiwachagua wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki.
“Rushwa ilikuwa ni wazi wazi ukienda chooni unapewa laki mbili (Sh200,000) unaondoka,”alisema Suzan.
Alisema wao kama viongozi ambao wanatunga sheria na wanatakiwa kuisimamia serikali wanapaswa kuwa waadilifu. Hata hivyo, Mbunge wa Njombe Kaskazini, Deo Sanga (CCM), alisema hakuna ukweli kuhusu jambo hilo la baadhi ya wabunge kuchukua rushwa hadi chooni.
Hata hivyo, Mbunge wa Tunduru, Mtutura Mtutura (CCM), alimuunga mkono Suzan na kusema suala hilo ni la kweli na kwamba kama Sanga hakuliona walikuwa wanamkimbia.
“Alichokizungumza Suzan ni cha kweli. Kaka yangu (Sanga) walikuwa wanakukimbia. Ni kweli hilo lilifanyika,” alisema.
Kwa upande wake, Katibu wa APNAC, Vita Kawawa, alisema si vyema wabunge wenye taarifa kuhusiana na masuala ya rushwa wakatoa taarifa katika ofisi za Spika na kamati ya maadili ili liweze kufanyiwa kazi mara moja.
“Ni vyema mkatupa taarifa kitu ambacho kinaashiria rushwa sisi tupo, ofisi ya spika ipo na kamati yetu ya maadili,”alisema.
Alisema rushwa ni mdudu ambao unatakiwa kukataliwa na kila mtu. Alisema rushwa imesababisha maisha ya wananchi kutobadilika ingawa uchumi wa nchi unakuwa.
MWANANCHI

No comments: