Advertisements

Sunday, March 18, 2018

TMA yakanusha taarifa za Tanzania kukumbwa na kimbunga

Mamlaka ya hali ya hewa iliyopo chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano nchini Tanzania imekanusha kutokea kwa hali ya Kimbunga "ELIAKIMU" katika maeneo yanayozunguka nchi na kudai Kimbunga hicho kipo kwenye visiwa vya Madagascar.

Hayo yamebainishwa na taarifa zilizotolewa hivi punde na kurasa rasmi za mamlaka hiyo Machi 17, 2018 na kusema ni ukweli Kimbunga kinachojulikana "ELIAKIMU" kipo eneo la Kaskazini Mashariki mwa kisiwa cha Madagascar na kinaelekea Kusini mwa kisiwa hicho.

Aidha, Mamlaka ya hali ya hewa imesema imefuatilia mwenendo wa Kimbunga hicho tangu kilipojitokeza mapema mnamo Machi 15, 2018 majira ya saa 11 asubuhi na kutoa utabiri wa hali ya hewa nchini kwa kuzingatia mifumo yote ya hali ya hewa inayojitokeza.

Kwa upande mwingine, mamlaka hiyo imesema itajitahidi kutoa taarifa  na tahadhari za utabiri kadri inapobidi kufanya hivyo.

No comments: