Advertisements

Friday, March 27, 2020

Marekani sasa yaongoza kwa wagonjwa wa corona

Washington. Nchi ya Marekani sasa ndio inayoongoza kwa kuwa na wagonjwa wengi wenye maambukizi ya virusi vya corona kuliko nchi zote duniani ambapo imeripotiwa kuwa na maambukizi 85,594 na vifo 1,300.

Takwimu mpya zilizotolewa Alhamisi Machi 26, 2020 zinaonyesha kuwa Marekani imeipita China na Italia kwa idadi ya visa vya corona vilivyothibitishwa.
Bado nchi ya Italia inaendelea kuwa nchi inayoongoza kwa vifo ambapo hadi sasa watu 8,000 wamefariki kwa virusi hivyo huku China ambapo ndipo ugonjwa huo ulianzia ikiripoti vifo 3,000 hadi sasa.

Idadi ya maambukizo ya virusi vya corona inazidi kuongezeka siku hadi siku duniani hali ambayo inazidi kufanya nchi mbalimbali kuchukua hatua za dharura kujilinda na ugonjwa huo.
Taarifa hizo za kuongezeka kwa wagonjwa nchini Marekani zinakuja baada ya Shirika la Afya Ulimwenguni wiki hii kutabiri kuwa itakuwa na idadi kubwa ya wagonjwa kutokana na kasi iliyokuwa inaonekana ya maambukizi ya ugonjwa huo nchini humo.
Jiji la New York pekee Alhamisi Machi 26, 2020 lilirekodi vifo vya watu 100 kwa masaa 24 tu hali inayozua hofu kuwa hali ya vifo inaweza kuongezeka zaidi nchini humo.
CHANZI-DAILY MAIL

No comments: