Advertisements

Friday, June 9, 2023

SERIKALI KUJENGA KITUO CHA UTALII KIHESA - KILOLO


Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii inatarajia kujenga Kituo cha Utalii cha Kihesa – Kilolo kwa lengo la kutoa huduma za utalii ikiwa ni pamoja na vibali vya kuendesha utalii, kutoa taarifa zinazohusiana na maeneo ya uwekezaji wa utalii.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) ameyasema hayo leo Bungeni jijini Dodoma kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Iringa Mjini, Mhe. Jesca Msambatavangu aliyetaka kujua lini Serikali itajenga kituo cha utalii Kihesa – Kilolo.

Aidha, Mhe.Masanja amesema kujengwa kwa Kituo hicho cha Utalii kutatoa fursa kwa sekta binafsi kwa kuweka jukwaa la kukaa pamoja na kujadiliana fursa na changamoto mbalimbali zinazoikabili Sekta hiyo.

Amefafanua kuwa Serikali imekamilisha taratibu za usanifu na makadirio ya ujenzi hivyo kinasubiriwa kibali cha Benki ya Dunia (no objection) ili taratibu za manunuzi zianze.

Kufuatia hatua hiyo, Mhe.Masanja amesema ifikapo mwezi Julai mwaka huu wanatarajia kupata Mkandarasi tayari kwa ajili ya kuanza kazi ya ujenzi wa kituo hicho.

Mhe. Masanja ameweka bayana kuwa ujenzi wa kituo hicho ni mwendelezo wa jitihada za Serikali za kuhakikisha zinatanua wigo wa masuala ya utalii ikiwemo kuunganisha vifurushi vya utalii (packages) vya Kusini mwa Tanzania kwa kuunganisha utalii wa utamaduni, kihistoria na utalii wa wanyamapori.

No comments: