Tuesday, September 3, 2024

WAZIRI KOMBO AWASILI NCHINI CHINA KUSHIRIKI FOCAC


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) akiwa katika mazungumzo na Balozi wa China nchini Tanzania Mhe. Chen Mingjian na Balozi wa Tanzania nchini China Mhe. Khamis Mussa Omar muda mfupi baada ya kumpokea katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Beijing, China.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) akiwa katika mazungumzo na Balozi wa China nchini Tanzania Mhe. Chen Mingjian muda mfupi baada ya kuwasili jijini Beijing, China.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) amewasili katika Jamhuri ya Watu wa China leo tarehe 2 Septemba 2024 kushiriki katika Mkutano wa Kilele wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (Forum on China-Africa Cooperation-FOCAC) utakaofanyika jijini Beijing kuanzia tarehe 4 hadi 6 Septemba 2024.

Mkutano huo unaolenga kukuza ushirikiano na maendeleo ya pamoja kati ya China na Afrika utatanguliwa na mkutano wa ngazi ya Makatibu Wakuu uliofanyika leo tarehe 2 Septemba 2024, ambapo Tanzania imekilishwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samuel Shelukindo na ngazi ya Mawaziri tarehe 3 Septemba 2024.

Katika mkutano huo wa ngazi ya Mawaziri miongoni mwa masuala mengine, kipaumbele ni kujadili na kupitisha rasimu ya agenda ya Mkutano wa Kilele wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa FOCAC.

Agenda zingine ni pamoja na kufanya tathimini ya utekelezaji wa masuala yaliyofikiwa katika mkutano wa 8 wa FOCAC uliofanyika jijini Dakar, Senegal, na kujadili na kupitisha rasimu ya tamko na mpango wa utekelezaji.

Mbali na kushiriki mkutano wa FOCAC, Waziri Kombo anatarajiwa kufanya mikutano ya pembezoni na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchini Algeria, Egypt na Libya ambapo watajadili masuala mbalimbali yanayolenga kudumisha na kukuza zaidi ushirikiano wa kiuchumi na kidiplomasia.

Mkutano huu unaofanyika kwa mara ya 9 tokea kuanzishwa kwake mwaka 2000, unaongozwa na kaulimbiu isemayo “Kushirikiana ili Kuendeleza Usasa na Kujenga Jamii Bora ya China na Afrika kwa Mustakabali wa Pamoja”. Kauli mbiu hii inalenga kuwahamasisha Viongozi Wakuu wa Nchi na Serikali wa Afrika na China kujadili kuhusu masuala muhimu katika kuimarisha ushirikiano kati ya nchi za Afrika na China ili kuchagiza kasi ya maendeleo kwa manufaa ya pande zote mbili.

Akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Beijing Waziri Mhe. Mahmoud Thabit Kombo amepokelewa na Balozi wa Tanzania nchini China Mhe. Khamis Mussa Omar na Balozi wa China nchini Tanzania Mhe. Chen Mingjian.


No comments: