ANGALIA LIVE NEWS

Wednesday, December 29, 2010

Muhimu kwa walio kwenye ndoa na wanaotarajia -2

HII ni mada ya mwisho kwa mwaka huu wa 2010 katika ukurasa huu wa Uwanja wa Huba. Naamini umejifunza mengi sana katika kipindi chote hicho. Rafiki zangu, zimesalia siku mbili kabla ya kumaliza mwaka huu na kuingia mwaka mpya wa 2011. Tuombe Mungu pamoja tufike!


Yes...sasa nirudi kwenye mada yetu ya msingi, ambayo leo nafikia tamati. Rafiki zangu, lazima mjue mbinu za kuboresha uhusiano, uchumba au ndoa. Lazima ujitambue mwenyewe kwanza, kabla mtu mwingine hajakuambia chochote.

Kabla sijaanza kuchambua vipengele muhimu vya kuzingatia kwa walio kwenye ndoa na wanaotarajia, nataka kuzungumza na rafiki zangu ambao wanaamini eti wao hawavutii...eti wabaya...eti hawawezi kupata wenzi!

Acha kujidanganya rafiki yangu! Utashinda kutwa nzima kwenye kioo ukijiangalia kama wewe ni mzuri, utanunua kila aina ya manukato na sabuni za kujichubua ili uwe mrembo lakini bado utaendelea kubaki vile vile!
Kuna mwingine utakuta anamwambia mpenzi wake; “Mwanamke gani wewe? Kwanza nimekuoa kwa bahati mbaya tu. Huna mvuto, sura mbaya, uso umekomaa utadhani unapuliza moto!” Huu ni ujinga. Si kauli nzuri kwa mpenzi wako.

Kwa mtu ambaye anakufulia, anakupikia na kukunyooshea nguo zako. Mtu ambaye anakutunzia familia yako. Ni maneno machafu sana.
Hata hivyo, fanya uchunguzi taratibu;  utagundua wengi wanaoambiwa kwamba wao eti si ‘wazuri’, hawavutii, wao wenyewe HAWAJIAMINI! Utakuta hana amani, anadhani yeye ni mbaya, anajipa presha isiyo na maana. Acha mawazo hayo.

Ishi katika kujiamini
Lazima ujivunie jinsi ulivyo, rafiki yangu wewe ni mzuri kama ulivyo. Usikubali kukatishwa tamaa, lakini nataka kukupa moyo kwamba, ukianza kujiamini na kujiona kuwa ni mzuri na unavutia, utaendelea kuwa hivyo.
Sifia uumbaji wa Mungu wako, jitazame kwa furaha, tabasamu, sema: “Nimeumbika,” utaona unavyozidi kung’aa.

Ukiwa na mawazo sana, ukidhani jamii inakucheka jinsi ulivyo, hata sura yako itakunjamana na kukufanya uwe ‘mbaya’ kweli mbele za watu. Siri kubwa nakupa, JIAMINI kuwa unavutia na unaweza kuwa na mwenzi bora.

Hakuna mtu ‘mbaya’, jamani wala hakuna ‘mzuri’, ndiyo maana waswahili wanasema: “Ukimuona wa  nini wenzio wanawaza watampata lini?” Upo hapo rafiki yangu. Huu ni utangulizi kwako wakati tukielekea katika vipengele vingine.

KWA WANAOTARAJIA KUINGIA KWENYE NDOA
Muhimu kwenu ni kuchunguzana, kuwa na subira na kuacha papara. Usikurupuke, fanya uchunguzi wako taratibu. Ni kweli anafaa kuwa wako? Ana sifa unazozihitaji? Umeichunguza vema familia, ndugu zake?
Maana kuna wengine wanakutana usiku kwenye kumbi za starehe, wanalala pamoja na wiki moja baadaye wanaitana wachumba.

Baada ya miezi mitatu wanatambulishana na taratibu za ndoa zinaanza? Wewe!... mmependana saa ngapi? Mmechunguzana saa ngapi? Lazima ujue nyumba unayokwenda kuingia ni ya namna gani, usikimbilie kuoa au kuolewa kama ‘fasheni’ kwako. Lazima ufanye maamuzi sahihi ambayo hautayajutia baadaye. Tupo jamani?

Utamjuaje mlaghai?
Hana alama usoni, wala kamba mguuni. Mara nyingi matapeli ndiyo wanaongoza kwa maneno matamu ya kutia moyo na kukufanya ujihisi unaingia kwenye ndoa kesho. Matapeli wanajua udhaifu wa wanawake wengi ni kutaka kuolewa.

Wanajua kwamba wengi wanataka kuolewa  kwa kuamini kuwa hayo ndiyo maisha yenye heshima, kwahiyo akikutokea mtu kati ya maneno ya kwanza ni kukutamkia kukuoa. Hata kwenu anaweza kuja na pete ya uchumba akakuvalisha, lakini ndani ya siku chache atakukimbia!

Kuwa makini, pima ahadi zake, angalia kauli zake, tumia muda mwingi kumchunguza. Kama ana nia na wewe ni rahisi kumtambua mapema.
Unajihami vipi?
Huna haja ya kuwa na haraka kwa chochote. Kuwa msikilizaji zaidi kuliko muongeaji, hiyo itakusaidia zaidi kumjua kwa undani kwa kumpima maneno yake na ahadi zake.

Usiruhusu mambo ya ngono, kuwa mjanja, kukwepa  kukaa naye sehemu zenye vificho ambavyo kwa namna moja ama nyingine vinaweza kukutumbukiza kwenye anguko la dhambi ya uzinzi. Kama anakupenda kweli, hawezi kuwa na haraka.
Pete aliyokuvisha, ambayo wakati mwingine inaweza kuwa ‘urembo’ tu kidoleni mwako, isiwe chanzo cha yeye kukufanya chombo cha starehe. Najua wanaume wengi watakuwa wamechukia sana kusoma mada hii, lakini ndiyo ukweli.

KWA WANANDOA
Hapa ndipo kwenye shida zaidi, maana hawa wakishaingia (kwa baadhi ya imani) si rahisi kutoka. Wengine waliongia humu kwa mtindo nilioandika hapo juu, hujuta wakitamani sana kutoka, lakini tayari kuna vizingiti, hawezi tena kutoka, kwahiyo kinachofuata ni kulia maisha yao yote!
Ndoa haijaribiwi rafiki zangu, lazima ujipange kwanza. Na si kujipanga ukiwa na marungu na mapanga, ni wewe kuwa tayari kwa kila hali ndani ya ndoa yako. Uwe umemkubali mwenzako kikamilifu. Kwa haraka haraka, ngoja nikupe dondoo chache zitakazokusaidia zaidi kwenye ndoa yako.

(i) Jenga tabia ya usikivu na heshima kwa mwenzako; Tanguliza thamani yake kwanza kabla ya kitu kingine chochote. Mpende kama yeye, kutaweza kukusaidia kuongeza nguvu ya penzi lenu.

(ii) Kuwa msaada kwa mwenzako, hata kama kuna kitu hajui, usimtukane, mueleweshe kwa upendo na sauti inayoonesha kuumizwa na kutokujua kwake, si kwa matusi na kumdhihaki.

(iii) Ndoa si furaha siku zote, tena nataka kukuambia kwamba ndoa nusu ni furaha na nusu ni karaha. Kuna kugombana na kutofautiana kwa kila hali. Ikitokea, kuwa wa kwanza kuanzisha mjadala wa namna ya kutatua tatizo hilo. Usiliache hadi liwe kubwa, kiasi cha kuwashirikisha watu wengine.

(iv) Washauri wa kweli wa ndoa yenu ni wewe na mwenzako tu. Tafuta amani kadri uwezavyo, wewe mwenyewe na mwenzako. Acha kupeleka mambo yako kwa rafiki zako, wengine wanaweza kukushauri vibaya na kujikuta ukitamani kuachana na mwenzako.

(v) Vumilianeni na tafuteni njia za kuboresha penzi lenu. Wataalamu wa Saikolojia ya Mapenzi wanasema kutoana ‘out’ japo mara chache kunaweza kutia nakshi na mwenzako katika penzi  lenu na kumuona mwenzako mpya kila siku.

Kwa hayo machache, naomba niweke kituo kikubwa hapa. Ahsanteni na nawatakieni maandalizi mema ya kuupokea mwaka mpya.
Nawapenda sana!

Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Mambo ya Mapenzi ambaye anaandikia magazeti ya Global Publishers, ameandika vitabu vya True Love na Secret Love vilivyopo mitaani.

No comments: