Advertisements

Thursday, September 8, 2011

Urafiki Usiharibu Nchi

Na  Augustino Malinda
Lilipotokea janga la kashfa kwa bwana David Jairo, kitu cha kwanza kilinijia akilini “hawezi kufanywa lolote”,lakini baada ya kauli ya waziri mkuu bwana Mizengo Pinda kuwa alisikitishwa sana na kitendo hicho lakini yeye siye aliyemweka hapo ila ni rais Jakaya Mrisho Kikwete ambaye wakati alikuwa ziarani Afrika ya kusini, kwa mujibu wa bwana Pinda angeongea na rais, Kwa kauli hiyo nilipata tumaini la huyu bwana kuondoka.

Kwanini nilifikili kuwa bwana Jairo haiwezi kuondolewa, nilikuwa na sababu muhimu tatu, moja hii sio mara kwanza kupatwa na mauzauza ya tuhuma, pili kufanya kazi kwa muda mrefu, urafiki binafsi na wakikazi alionao na mtoa maamuzi na tatu rais kikwete mwenyewe amekuwa akiachia uzembe na kashfa kubwa kuliko hiyo bila kuwafanya kitu wahusika au kwa kifupi utawala wa bora liende.


Katibu mkuu ofisi ya rais ambaye ndio mkuu wa watumishi wote wa serikalini, bwana Luhanjo alipokuja taarifa ya kumrudisha kazini na vitisho vya kuwachukulia wenye uchungu na nchi kwa kuibua kashfa ya Jairo, nilihisi hakuwa yeye bali yalikuwa ni maagizo ya mkuu ya fanya unavyofanya lakini Jairo abaki kazini.Sasa hapa ndipo ninapokuja swali kwa mheshimiwa rais Kikwete, bora urafiki au nchi?

Ninampenda na ninamheshimu sana mheshimiwa Kikwete lakini kwa kutofanyia maamuizi eti kwasababu zinazoelezwa kuwa ni urafiki uliopita kiasi kati yake na bwana Jairo kwa kweli hapo “ameteleza”.

Kwa muda mrefu nimekuwa nikimjua bwana David Jairo na nilishawahi kupambana naye akiwa msaidizi wa waziri wa nishati,maji na madini wakati huo Kikwete akiwa ndio waziri, kipindi hicho mimi nikiwa ripota mtoto ndivyo walivyokuwa wakiniita kipindi hicho nilikuwa nikifuatilia kashfa ya Shirika la maji wakati huo likiiitwa NUWA la kununua madawa ya kusafishia maji yaliyokwisha muda wake, wakati nikiwa nimeshamaliza uchunguzi wangu huku nikiwa na uthibitisho na nyaraka nilikwenda kumuona mheshimiwa waziri kikwete kwaajili ya kujibu hizo tuhuma na ikiwezekana yeye kama waziri achukue hatua.

Kama mwandishi wa habari za uchunguzi nilikuwa nimeshakwenda kumuhoji mkurugenzi wa NUWA bwana Mutalemwa,kumbuka haya ni madawa yaliyokwisha muda wake yaani ni sumu,mkurugenzi ameyanunua hivyohivyo na amekuwa akilazimisha yawekwe kwenye maji ambayo yatatumiwa na watanzania wanaoishi mjini Dar es salaam.
Baada ya Mutalemwa kuona kuwa ninauthibitisho na nyaraka, aliniomba nisiandike hiyo habari kwani NUWA ilishalipa pesa kwa msambazaji, madawa hayo yalikuwa ni tani 200, huku akionyesha dalili zote za kunipa mshiko (rushwa) ili niachane na hiyo kashfa, kipindi hicho nilikuwa siangalii makunyanzi ndugu.
Acha nifanye stori iwe fupi, baada ya mazungumzo yangu na waziri KIkwete, Jairo aliingia na kusikia mazunguzo yetu na nakumbuka waziri alimuuliza kama ana habari yeyote kuhusu hayo madawa, alijibu kuwa hajui.

Lakini nilipofika ofisi kwangu Jairo alikuja na kuniambia kuwa anajua habari yote hiyo ila anaomba niachane nayo kwani Mutalemwa ni class mate wake na tayali ameshaonyesha kuwa yuko tayali kutoa ushirikiano yaani mshiko, kweli nilipandwa na jazba kuona msaidizi wa waziri tunayeheshimiana anakuja kuongea maswala ya rushwa, nilisikitika sana. Unajua nini nilifanya niliandika ile habari na pia nikaongeza na kile kitendo cha Jairo kuniongelea mambo ya rushwa,piga picha ya hasira aliyokuwa nayo bwana Jairo ( niko kwaajili ya nchi na sio urafiki).

Baadaye waziri alimuondoa na kumuweka Bwana Mtawa kuwa msaidizi wake,hasira yake kwangu haikwisha lakini kwamimi kama mwandishi nilishatimiza wajibu wangu, lakini nilikuwa nikijua urafiki wao uliendelea licha ya kutokuwa msaidizi wake pale Nishati. baada ya miaka kadhaa akaibukia kuwa msaidizi wa Kikwete tena, lakini safari hii wa rais wa nchi “Ikulu jamani”.Kuna mengine mengi tu nayajua kuhusu huyu jamaa alipokuwa pale nishati,nilitetemeka.
Kwa utaratibu wa kawaida tu mtu kama huyu na katika kipindi hiki cha kujivua magamba rais Kikwete hakupaswa kumuachia kwani watu kama hawa ambao wanaeleweka kuwa ni marafiki zake na maswahiba lakini rekodi zao si nzuri hawapaswi kuachiwa kuharibu jina ambalo amekuwa akijitahidi kulisafisha.

Tayali CCM imeshatangaza kujivua gamba,Rostam kesha ng’oka na Lowassa yuko njiani, bwana Luhanjo anakuja na sababu zisizojaa kikombe kuwa hiyo ni kawaida hivyo bwana Jairo anarudishwa madarakani,na kama hiyo haitoshi anawatishia waliotoa hiyo kashfa kuwa waache mara moja umbea wa kutoa siri na kuwa atatumia njia zote hadi wawajue halafu wawachukulie hatua. hata siamini masikio na macho yangu, rais atamwambia nini waziri mkuu wake ambaye tayali alishatoa kauli ya kusikitishwa na kitendo hicho?, ila hakuwa na uwezo wa kumchukulia hatua bwana Jairo?.

Hivi atawaeleza nini wakina Lowassa na Rostam ambao wanadai kuwa msukumo wa kutakiwa kuondoka unatokana na siasa za urais 2015 na sio ufisadi au kujivua gamba kama CCM inavyodai?,Kikwete atawaeleza nini wabunge ambao wanajua kabisa kuwa lile fungu la pesa lilikuwa kwaajili ya kuwashikisha ili bajeti ya Jairo na Ngereja ipite kirahisi?,atawaeleza nini wananchi alipodai ccm inajivua gamba ilihali haihusishi serikali katika kuyaondoa magamba?, labda namshauri atangaze ujivuaji gamba hauhusishi serikali ni wa chama tu, na kuwa wakati muafaka ukifika atatangaza azimio lingine la serikali kujivua gamba kwa lakini kwasasa ni CCM tu.
Atawaeleza nini watanzania kuwa ndio utaratibu wa serikali kuchangisha mashirika yaliyochini yake na kuweka pesa zao katika akaunti zisizo za serikali kwaajili ya kuweka mambo sawa bungeni?.Hata kama utaratibu huo umekuwa ukitumika lakini ni mbovu na unapaswa kuachwa mara moja.

Nakumbuka miaka hiyo hata waandishi walikuwa wakipata mishiko ili kutokandia bajeti za wizara husika, mimi nikiwa mmoja waandishi wa habari kipindi hiko nilikuwa nikikataa huo mchezo kwani ilikuwa ni rushwa full stop, kuna mawaziri wengine wengi tu wenye dhamira safi walikuwa wakipinga mchezo huo mchafu.

Mheshimiwa rais anapaswa kuelezwa kuwa watanzania wa miaka ile sio wasasa, kizazi kilishabadilika yeye mwenyewe anajua alivyoponea tundu ya sindano kinyang’anyilo kilichopita, na tayali CCM kimeshapakwa matope ya ufisadi na nasikia kinaitwa chama cha mafisadi (CCM),aangalie maslahi ya nchi zaidi badala ya urafiki wake na Jairo.
Nategemea mheshimiwa rais ataangalia tena suala hili na kulitolea uamuzi sio tu kwa rafiki yake Jairo hata kwa waziri Ngereja na Malima nao waondoke badala bwana Luhanjo kuja kutoa vitisho visivyo na msingi.NCHI KWANZA URAFIKI BAADAYE.
Kama una swali na maoni unaweza kuniandikia email amalinda3@hotmail.com

1 comment:

Anonymous said...

A professional journalist would get the other side of story before any publication. I'm not trying to repudiate the fact that Jairo, Ngeleja, Malima and even the president himself are not clean. I'd respefully expect you to interview them first before airing your brutal attack based on your past experience and probably personal hatreate. Those are ethics of fareness in journalism. How would you feel if a journalist treated you the same way, bearing in mind that you are not clean either.