Advertisements

Thursday, May 31, 2012

Kim: Ivory Coast inafungika


Naibu Waziri wa Wizara ya Habari Michezo na Maendeleo ya Vijana, Amos Makala akimkabidhi Nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania,(Taifa Stars) Juma Kaseja, Bendera ya Taifa baada ya kuiaga timu hiyo inayotarajia kuondoka leo kuelekea nchini Ivory-Coast kwa ajili ya mechi ya kuwania kufuzu fainali za Kombe la Dunia.Picha na Jackson Odoyo.
Sosthenes Nyoni
KOCHA wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Kim Poulsen amesema wanakwenda Abidjan, Ivory Coast na watawaduwaza Ivory Coast kwa mchezo wao wa kwanza kuwania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia, 2014 zitakazofanyika Brazil.

Stars na Ivory Coast zilizopambana Mei 2010 kwenye Uwanja wa Taifa na Ivory Coast kushinda bao 1-0, zitacheza mechi yao Juni 2 ikiwa ni takribani miaka miwili, mchezo utakaofanyika kwenye Uwanja wa Houphouet Boighny ulioko katikati ya jiji la Abidjan.

Timu hiyo imeondoka leo alfajiri ikiwa na msafara wa watu 32 wakiwemo wachezaji 23 na viongozi tisa akiwemo mwandishi wa habari wa magazeti ya Mwananchi Communications Ltd.

Wachezaji hao na viongopzi waliagwa jana na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Amos Makalla na Kim aliwaambia wachezaji wake kwamba njia pekee ya kuweza kuaminiwa na Watanzania ni kuhakikisha wanashinda pambano hilo.

"Jana (juzi) jioni nilikaa na wachezaji nikawauliza mmoja mmoja unafahamu ni kwa nini umeitwa kwenye timu ya taifa, nashukuru kwamba walinijibu kwa usahihi kabisa. 

"Ukweli ni kwamba niliwaambia wajiamini kwanza wenyewe kwa kuhakikisha ushindi unapatikana na  baada ya hapo mashabiki na hata vyombo vya habari vitawaamini,"alisema Kim na kuongeza: "Lakini katika kufanikisha hili nimewasisitizia hakuna mafanikio pasipo nidhamu ya hali ya juu."

Naye Naibu Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo Amos Makalla aliwataka wachezaji wa Taifa Stars kutoweka mawazo kwamba Ivory Coast ni Chelsea kwa kuwa ina wachezaji maarufu kama Didier Drogba na Solomon Kalou ambao wanaichezea klabu hiyo. 

Pia aliwataka waelekeze akili zao katika kupapambana dimbani badala ya kuhofia hujuma za nje ya uwanja za wapinzani wao.

Mkuu wa msafara huo ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, Crescentius Magori na pamoja na Makamu wa Rais wa Chama cha Soka Zanzibar, ZFA, Haji Ameir Haji.
 
Viongozi walioambatana na timu hiyo ni Kim Poulsen na msaidizi wake Sylvester Marsh na kocha wa makipa, Juma Pondamali 'Mensar'.

Wengine ni meneja  wa timu hiyo, Leopord Tasso Mukebezi, daktari wa timu Mwanandi Mwankemwa, mtaalamu wa viungo Frank Mhonda na mtunza vifaa, Alfred Chimela. 

Wachezaji wa Stars ni nahodha: Juma Kaseja, Aggrey Morris, Mwadini Ally, Deogratius Munishi, Nassor Masoud Cholo, Amir Maftah, Erasto Nyoni, Kelvin Yondan, Waziri Salum, Shomari Kapombe na Juma Nyoso.
 
Wengine ni Jonas Mkude, Mwinyi Kazimoto, Salum Aboubakar, Shaaban Nditi, Edward Christopher, Mrisho Ngassa, Frank Domayo, Mbwana Samata, Ramadhan Singano, Simon Msuva, Haruna Moshi 'Boban' na John Boko.


Mwananchi

No comments: