Advertisements

Tuesday, July 31, 2012

Lissu awalipua wabunge saba *Adai ndio wanahusika na kashfa ya rushwa *Yumo Ole Sendeka, Vicky Kamata, Nassir

Na Benedict Kaguo, Dodoma

MNADHIMU wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Bw. Tundu Lissu, jana amewataja kwa majina wabunge saba wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), anodai kuhusika na kashfa za rushwa ambayo inalihusu Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Bw. Lissu aliwataja wabunge hao nje ya ukumbi wa Bunge mjini Dodoma katika mkutano wake na waandishi wa habari.

Hatua hiyo imekuja wakati ambao wabunge, wanasiasa, wananchi na  wanaharakati wakiwa na shauku ya kutaka kuwajua wabunge ambao wanatuhumiwa kwa kashfa hiyo.

Katika kikao hicho, Bw. Lissu ambaye ni Mbunge wa Singida Mashiriki (CHADEMA), bila ya kuuma maneno, alisema wabunge wanaotuhumiwa kwa kashfa ya rushwa ni wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini (iliyovunjwa na Spika Bi. Anne Makinda).

Aliwataja wajumbe hao kuwa ni Bw.  Christopher Ole Sendeka (Simanjiro), Bi. Sara Msafiri (Viti Maalum), Bi. Mariam Kisangi (Viti Maalum), Bw. Yusuph Nassir (Korogwe Mjini), Bw. Charles Mwijage (Muleba Kaskazini) Bi. Vicky Kamata (Viti Maalum) na Bi. Munde Tambwe (Viti Maalum).


Alisema hadi sasa, kambi ya upinzani ina ushahidi juu ya ushiriki wa wabunge hao katika kashfa hiyo na kutaka wachukuliwe hatua.

Aliongeza kuwa, wajumbe wengine wa kamati hiyo kutoka CHADEMA, Bw. John Mnyika (Ubungo), Bw. David Silinde (Mbozi Magharibi) na Mwanamrisho Taratibu Abama (Viti Maalum), hawahusiki kabisa katika kashfa hiyo.

Alisema Bi. Msafiri na Bi. Tambwe, wamekuwa wakipewa tenda ya kuiuzia matairi TANESCO huku wakijua wao ni wajumbe wa kamati hiyo ambapo Bw. Mwijage, amekuwa akifanya kazi ya Mtaalamu Mwelekezi wa Kampuni ya Puma Energy.

Bw. Lissu alisema, kampuni hiyo nayo imeingia katika mgongano wa kimasilahi na kampuni nyingine ambapo Bw. Nassir na Bi. Kisangi, wanamiliki vituo vya mafuta hivyo wana mgongano wa kimasilahi ndani ya Wizara hiyo.

Akimzungumzia Bw. Ole Sendeka, alisema mbunge huyo hana kituo cha mafuta wala mgongano wa kimasilahi bali amekuwa mtetezi mkubwa wa Kampuni ya Orxy na Camel.

Alisema kampuni hizo zimekosa tenda ya kuizuia mafuta IPTL, huku akimtaja Bi. Kamata na kudai kuwa, mbunge huyo hana mgongano wa kimasilahi ila ana masilahi binafsi.

Hata hivyo, Bw. Lissu alisema wabunge hao wamejihusisha na vitendo ambavyo ni kinyume na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya mwaka 1995, inayokataza kuwepo migongano ya kimasilahi.


“Wabunge wote waliotuhumiwa na rushwa wachukuliwe hatua, namuomba Spika wa Bunge, azivunje kamati nyingine hasa ya Mashirika ya Umma ambayo inaongozwa na Bw. Zitto Kabwe.

“Kamati nyingine ni ile ya Hesabu za Serikali za Mitaa ambayo inaongozwa na Bw. Augustino Mrema, kwa sababu zimetajwa kuhusika na vitendo vya rushwa,” alisema.

Zitto ahusishwa na rushwa

Bw. Lissu alisema, tuhuma za Bw. Zitto kuhusishwa na rushwa amezisikia ila CHADEMA hawajapata nafasi ya kukaa nae kupata maelezo yake na kudai kuwa, kama itabainika amehusika na vitendo hivyo chama hicho kitachukua hatua.

Kuhusu ujumbe mfupi wa maandishi ambao inadaiwa Bw. Zitto alimtumia Katibu Mkuu wa Nishati na Madini, Bw. Eliakim Maswi,  alisema ujumbe huo uchunguzwe na ukweli uwekwe hadharani.

Hata hivyo, ujumbe huo ambao inadaiwa Bw. Maswi alitumiwa na Bw. Zitto, unasomeka hivi; “Maswi, sijawahi gombana na wewe kwa kuwa nakuheshimu sana, tuhuma ambazo wewe na Waziri wako mnatoa dhidi yangu ni uwongo, uzushi na za kupikwa.

“Mwambie Waziri wako na wewe binafsi, sijawahi kushindwa vita ya kulinda credibility yangu, sipendi ujinga hata kidogo, mimi nina uhuru wa kusema ninachoamini, sina bei tupambane tu tuone nani ataumia,” ujumbe huo unasomeka hivyo.

Bw. Lissu alisema, uchunguzi utakapokamilika hawatasita kuchukua hatua na kutaka ufanyike haraka ili kuondoa sintofahamu ambayo imeligubika sakata hilo.

Wabunge waliojatwa wajibu mapigo

Wakizungumza na Majira ili kujibu tuhuma hizo, wabunge ambao waliotajwa na Bw. Lissu kuhusika na kashfa ya rushwa, walishangaa mbunge huyo kuwahusisha na tuhuma hizo na uchunguzi ufanyike badala ya kutoa kauli za upotoshaji ili kupoteza ukweli.

Charles Mwijage (Muleba Kaskazini)

Akizuingumzia tuhuma hizi, Bw. Mwijage alisema hajawahi kufanya kazi ya Utaalamu Mwelekezi wa katika Kampuni ya Puma Energy na kudai alichokifanya Bw. Lissu, ametumiwa ili kuivuruga Kamati ya Maadili isiweze kuwabaini watuhumiwa husika.

“Lissu ametumiwa ili kuivuruga kamati ya Maadili isiweze kubaini watuhumiwa husika kwani Mheshimiwa Selasini alishasema bungeni suala la rushwa liko upande wa CCM na CHADEMA hivyo anahofia watu wake wasije wakajulikana,” alisema.

Mariam Kisangi (Viti Maalumu)

Bi. Kisangi alisema hahusiki na tuhuma hizo na hana tatizo kwani anapigania haki za wananchi.

“Sikubaliani na Bw. Lissu, kamati zinapangwa kwa uwezo ndio maana yeye akapangiwa Kamati ya Sheria...sihusiki niko tayari nasubili, nafanya biashara kwa zaidi ya miaka 20 kabla sijawa mbunge na sijawahi kuiuzia TANESCO hivyo hoja yake haina msingi imelenga kunichafua tu,” alisema Bi. Kisangi.

Ole Sendeka (Simanjiro)

Akizungumzia sakata hilo, Bw. Ole Sendeka alisema haamini kama Bw. Lissu amemtaja kuhusika na ufisadi lakini kama ni kweli, atakuwa na tatizo la akili.

“Mimi sidhani kama kweli atakuwa amenitaja kuwa ni fisadi, kama ni kweli, Mheshimiwa Lissu atakuwa na tatizo la akili ni vizuri aweze kuthibisha hilo vinginevyo atakuwa mgonjwa.

“Nitaeleza vizuri kwanini nilisema taratibu za manunuzi zimekiukwa na Katibu Mkuu, mimi sikutetea kampuni hata moja ya mafuta nilitaka uchunguzi ufanyike TANESCO.

“Katibu Mkuu alivunja taratibu za manunuzi ila kwa sasa niko jimboni nikifika Dodoma nitalieza vizuri suala hili ila msimamo wangu ni ule ule, kuwa kanuni zimekiukwa,” alisema.

Sara Msafiri (Viti Maalumu)

Alisema taarifa za kutajwa na Bw. Lissu amezipata na tayari Spika alishatoa maelekezo, kuvunja Kamati ya Nishati na Madini na kulipeleka suala hilo kwenye Kamati ya Maadili ukweli ufahimike

“Tuviachie vyombo husika vifanye kazi yake na ukweli utajulikana, yeyote mwenye ushahidi apeleke kwenye kamati husika ili kusaidia uchunguzi kuliko kutaja majina,” alisema Bi. Msafiri.

Yusuph Nassir (Korogwe Mjini)

Alisema hausiki kuiuzia mafuta TANESCO kwani yeye ni mfanyabiashara mdogo wa mafuta ambaye biashara yake ni kuuza mafuta kwa watu wa kawaida si shirika hilo.

Vicky Kamata (Viti Maalumu)

Akizungumzia madai ya Bw. Lissu, alisema kuna uadui umezuka baada ya kuweka msimamo wa kukataa vitendo vya rushwa katika  Wizara hiyo ndio maana anazushiwa.

“Hiyo ni vita, wanataka kunichafua...hawashindi vita hiyo wanatafuta kujinasua lakini hawanipunguzi kasi ya kuendelea kutetea ukweli, naamini uongo una mwisho na ukweli utajulikana, mimi najiamini kwa zaidi ya asilimia 100,” alisema.

Hata hivyo juhudi za kumpata Bi. Tambwe kuzungumzia tuhuma hizo hazikuzaa matunda.


Majira

No comments: