Advertisements

Saturday, December 29, 2012

SAKATA LA NAIBU WAZIRI WA ELIMU KUWA NA ELIMU FEKI PAMOJA NA JINA FEKI LACHUKUA SURA MPYA


NAIBU Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Bw. Philipo Mulugo, amesema yupo tayari kumthibitishia Mbunge wa Mbeya Mjini kwa tiketi ya CHADEMA, Bw. Joseph Mbilinyi, maarufu 'Sugu', juu ya elimu aliyonayo kama alivyodai mbunge huyo.

Bw. Mulugo aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na Majira kuhusu madai ya Bw. Mbilinyi ambayo ameyatoa katika vyombo vya habari kuwa, Waziri huyo ana elimu ya kuunga unga na jina lake kamili ni Amim.
Alisema kauli ya Bw. Mbilinyi haina ukweli wowote bali yeye ni msomi na yupo tayari kuthibitisha ukweli huo kwa umma.

“Mimi na Bw. Mbilinyi tuna vilema vingi, akitaka tuumbuane yatabainika mengi hasa katika upande wake, namfahamu muda mrefu kwa sababu nimesoma naye shule moja, nafahamu mambo yake mengi lakini kutokana na hekima zangu sihitaji malumbano na yeye,” alisema Bw. Mulugo.

Alidai kumshangaa Bw. Mbilinyi, kuzungumzia jambo ambalo halifahamu lakini kwa kumsaidia ili asielendelee kuonekana mwanasiasa muongo, aitishe mkutano na waandishi wa habari na yeye atakuwa tayari kuthibitisha elimu yake kwa umma.

Bw. Mulugo aliongeza kuwa, ni kweli wakati anasoma alikuwa akitumia jina la Amim na baada ya kufika elimu ya juu alianza kutumia jina la Philipo ambalo ni la ukoo ambapo Bw. Mbilinyi kama angekuwa makini, angefuatilia kwenye ukoo wake ili kujua jina hilo linamuhusu au la.

Aliongeza kuwa, dhamira yake ni kuhakikisha kuwa Jimbo la Mbeya Mjini ambalo hivi sasa linashikiliwa na Bw. Mbilinyi, mwaka 2015 linarudi CCM na ukweli huo utathibitika katika uchaguzi.

“Mimi ni Waziri kutoka CCM na Mjumbe wa Halmashauri Kuu NEC, hivyo Bw. Mbilinyi, asifikiri kuzua maneno hayo yatanitisha hadi nishindwe kutekeleza sera za chama changu,” alisema.

Alisema ibara ya 5 ya Katiba ya CCM, inamwongoza kuhakikisha chama chake kinashinda uchaguzi wa dola wa ngazi zote pamoja na kulirudisha jimbo la Mbeya Mjini kutoka upinzani.

“Katika Uchaguzi Mkuu ujao, nitatumia nguvu zote kuhakikisha jimbo la Mbeya Mjini linarudi CCM, ninachoweza kumshauri Bw. Mbilinyi, ajifunze kutokana na makosa kwani ameanza kunitafuta siku nyingi lakini mimi sikuwa na muda wa kumjibu bali niliendelea kutekeleza majukumu niliyonayo,” alisema.

Alisema Mbunge huyo na chama chake walijibiwa na wananchi wa Saza katika mkutano wa CHADEMA uliofanyika katika Wilaya ya Chunya na kusahau kilichowapeleka ni kampeni hatimaye wakaanza kunadi elimu ya Mulugo badala yake waliambulia kufukuzwa.

Aliongeza kuwa, Bw. Mbilinyi alipaswa kulisema na hilo kama walifukuzwa na wananchi wa Saza ambao walimwambia wao, wanamfahamu viziri Bw. Mulugo na wamemsomesha wenyewe kwa pesa zao baada ya kuthibitika ni yatima.

Alisema wananchi hao walidai kuchoshwa na matusi ya Bw. Mbilinyi dhidi yake na kumtungia uongo lakini yeye hana muda wa kulumbana naye bali atamjibu kwa ushahidi.

Kauli ya Bw. Mulugo imekuja siku chache baada ya Bw. Mbilinyi kudai kuwa, elimu ya Waziri huyo ni ya kuunga unga kwani alisoma naye Sekondari ya Mbeya Day, wakati huo akiitwa Amim si Philipo Mulugo hivyo kuanzia sasa ataendelea kumuita jina lake halisi na kusisitiza hana uwezo wa kumng'oa jimboni kwake.
UGOMVI ULIANZIA KWENYE HII HOTUBA

No comments: