Saturday, May 25, 2013

KURIDHIKA NI TIBA YA USALITI KATIKA MAPENZI

KWA mara nyingine tunakutana tena kwenye kona yetu ya Mapenzi na Uhusiano katika siku ya leo kwa uwezo wa Mungu.
Leo nataka kuelezea jinsi ya kudhibiti hisia zako. Mada ya hii inatokana na kujibu swali la dada yangu mmoja ambaye jina lake hakupenda litajwe gazetini.

Yeye aliomba kusaidiwa kuzuia hisia zake kwa rafiki wa mumewe ambaye kila akimuona huwa katika hali mbaya na kuomba msaada wa kujizuia au airidhishe nafsi yake?

Kwanza kabla ya kumjibu ningependa kumsifu kwa ujasiri aliouonyesha kwa kuliweka wazi liusumbualo moyo wake. Ningependa jibu hili liwe kwa wote wenye tatizo hili, kwa kuanza kuangalia nini maana ya hisia?
Hisia ni hali ya kutengeneza kitu akilini au moyoni kwa kuona au kusikia kikiwa katika hali furaha au majonzi. Kwa mfano mtu baada ya kuvutiwa na mtu hutengeneza hisia za kuwa naye kwa kuamini kile anachokifikiria kina ukweli.
Siku zote wanadamu tumekuwa tukiongozwa na nafsi zetu, ambazo hupenda vitu vizuri tu, hakuna nafsi ya mtu inayopenda kitu kibaya kama yupo atakuwa na tatizo.
Hii imesababisha watu wengi wasio na uwezo wa kuzidhibiti nafsi zao ambazo huongozwa na hisia kujikuta wanafanya jambo ambao hulijutia baada ya tendo.

Macho au masikio yanapopokea kitu hukipeleka kwenye ubongo na kutafsiri kisha hupelekwa kwenye moyo, kama zuri hujikuta akicheka kama baya hujikuta analia au amehuzunika.
Si kila kitu kizuri lazima ukipate, vipo vinavyowezekana kupatikana na vingine havipatikani, hivyo inatakiwa kula kwa macho.

Tuzungumzie katika mapenzi hasa ndani ya uhusiano, unapojiona ukielemewa na hisia zako ambazo mwelekeo wake ni mbaya. Lazima ujitahidi kuzishinda.

Utazishindaje?
Kuridhika na kile ulichonacho na kukiona ni bora kuliko kitu chochote mbele yako. Kama ni mkeo au mumeo mheshimu na kuwa tayari kuwa muaminifu kwake kwa kuyashinda matamanio ya moyo wako pale yanapompenda mtu asiye kuwa wake.

Kama nilivyoelezea katika mada ya ‘usiwe mtumwa wa mapenzi’, vilevile haina tofauti na kusema usiwe mtumwa na nafsi na kushindwa kuzizuia hisia zako. Kama hujaoa au hujaolewa ni vizuri kuziweka wazi hisia zako kwa yule umpendaye akae akielewa kuwa yeye ndiye chanzo cha maradhi yako ya mapenzi.
Lakini kama umeolewa au kuoa ni kudhibiti hisia zako kwa kuheshimu ndoa yako kuuheshimu utu wako na kuuthamini mwili wako ambao ni mahususi kwa mtu mmoja.

Kudhizibiti hisia zako ni kuridhika na kile ulichonacho na kukiona kina thamani kubwa.

Kwa hayo machache tukutane wiki ijayo.

No comments: