Advertisements

Tuesday, March 25, 2014

Mwigulu ala kiapo batili, hata cha uwaziri haramu

Naibu Waziri wa Fedha,Mwigulu Lameck Nchemba Madelu.

Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Lameck Nchemba Madelu, amekula kiapo batili kwa kutamka jina ambalo siyo la kwake.

Jana asubuhi kundi la wabunge ambao walikuwa hawajala kiapo wakifanya hivyo, Mwigulu alikuwa mmoja wao, lakini alijitamka kuwa yeye ni Mwigulu Lameck Nchemba kinyume cha kiapo chake katika gazeti la Serikali la Julai 15, 2011 toleo namba 28.

Katika gazeti hilo taarifa ya kawaida namba 574, Mwigulu alibadilisha jina lake la Mwigulu Lameck Nchemba kwa kiapo kwamba ameliacha na kuanzia Oktoba 12, 2009 amechukua jina jipya la Mwigulu Lameck Nchemba Madelu.

“Ninatangaza kwamba kwa wakati wote kuanzia sasa kumbukumbu na nyaraka zote kwa maandishi na kwa maamuzi yote na mapatano kwa nyakati zote na kwa jambo lolote nitatumia na kusaini jina la Mwigulu Lameck Nchemba Madelu,” imeeleza.

Katika kiapo hicho, pia Mwigulu anasema: “Kwa hali hii naagiza na kuomba watu wote kunitambua na kuniita kwa jina ninalochukua la Mwigulu Lameck Nchemba Madelu na naacha jina langu la zamani la Mwigulu Lameck Nchemba kuanzia Oktoba 12, 2009.

Mwigulu alibadilisha jina na kulisajili kwa mujibu wa sheria ya usajili wa nyaraka.

Alipopigiwa simu na NIPASHE akiwa Dodoma anakohudhuria vikao vya Bunge Maalumu la Katiba, Mwigulu alisema yupo kwenye kikao na kumtaka mwandishi ampigie baadaye au amtumie ujumbe mfupi wa simu (sms) kuuliza swali.

Alipotumiwa ujumbe wa simu, alikiri kula kiapo kama Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba kwa kutumia jina la Mwigulu Lameck Nchemba badala ya Mwigulu Lameck Nchemba Madelu kwa madai kuwa katika hati ya kiapo yalikuwa yameandikwa majina matatu.

“Kwenye hati ya kiapo yalikuwa yameandikwa majina matatu kama utaratibu unavyotaka, hivyo nilitakiwa kuacha jina moja. Hata hivyo, ninatambua hilo na nimeandika memo kwa katibu kutambua majina yangu yote,” alisema Mwigulu ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi.

Baadaye Mwigulu alipiga simu na kueleza kuwa hata katika kiapo cha uteuzi wa kuwa Naibu Waziri wa Fedha, alitumia jina la Mwigulu Lameck Nchemba.

Wengine walioapa ni wabunge Anne Makinda, Mohammed Raza, Zainab Bakari Kihiga, na Godbless Lema.
CHANZO: NIPASHE

No comments: