Advertisements

Wednesday, July 23, 2014

DC avamia mkutano, amtusi mbunge

MKUU wa Wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma, Venance Mwamoto, amevamia jukwaa la mkutano wa NCCR-Mageuzi na kisha kumtolea lugha ya matusi Mbunge wa Muhambwe, Felix Mkosamali.

Mwamoto alijikaribisha kwenye mkutano huo uliokuwa ukihutubiwa na Katibu Mkuu, Mosena Nyambambe kisha akaketi kiti cha mbele walipokuwa viongozi wengine wa chama hicho na kuanza kumchokoza Mkosamali kwa kumtolea lugha chafu kwa sauti ya chini.

Mkuu huyo wa wilaya anadaiwa kufikia hatua hiyo ya kuporomosha matusi kwa kilichoelezwa kuwa alituhumiwa na Mkosamali kwenye mkutano, kwamba amejimilikisha isivyo halali ekari 73 za ardhi katika Kijiji cha Nduta wakati tayari anatumia wanajeshi kuwaondoa wanakijiji hao kwa kile kilichodaiwa ni kutaka kubadili matumizi ya ardhi ili kijiji hicho kiwe hifadhi.

Sokomoko hilo lilimalizwa kwa busara za wabunge, David Kafulila (Kigoma Kusini) na Moses Machali (Kasulu Mjini) baada ya Mwamoto na Mkosamali kukaribia kuzichapa kavu kavu jukwaani.

Mwandishi wa habari hizi, alishuhudia ishara za kutoelewana kati ya viongozi wa NCCR-Mageuzi na mkuu huyo wa wilaya kutokana na kutopendezwa na kitendo chake cha kuvamia mkutano wao.

Mara baada ya Nyambambe kumaliza hotuba yake, Mkosamali wakati akijibu maswali ya wananchi ndipo alitoboa siri ya zogo lililokuwa limetokea, akisema Mwamoto alimvamia jukwaani na kumwambia maneno machafu.

Kwamba Mwamoto alimwambia kuwa wananchi wa Kijiji cha Nduta anaowapigania watahama kwa kutumia nguvu za kijeshi. 

Tanzania Daima

1 comment:

Anonymous said...

Hawa viongozi wetu wa siku hizi bana! Leadership ethics ziko wapi?