Advertisements

Wednesday, July 23, 2014

Ridhiwan:Kikwete hana ugomvi na Lowassa

Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhiwan Kikwete

Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhiwan Kikwete, amesema kama Rais Jakaya Kikwete angekuwa na ugomvi na Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa, asingeshindwa kumshughulikia kwa kuwa anayo mamlaka na vyombo vyote vya ulinzi vipo chini yake.

Ridhiwan, ambaye ni mtoto wa Rais Kikwete alisema hayo kupitia kipindi cha wanasiasa kinachorushwa na kituo cha televisheni ya StarTv.
Alisema Rais anayo mamlaka na kwamba, hawezi kuwa na ugomvi mkubwa na kiongozi akamshindwa na kutolea mfano namna viongozi wa nchi nyingine wanavyofanya kwa wapinzani wao wa kisiasa.

Mbunge huyo, ambaye hivi karibuni aliingia mgogoro na vyombo vya habari akiwatuhumu waandishi kuwa ni makanjanja na watu wanaoandika vitu vya ovyo ovyo, alisikika akisema kwamba, wanasiasa hao hawana ugomvi mkubwa badala yake unakuzwa na watu.

Alisema hayo baada ya kutakiwa kuzungumzia makundi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na uhusiano kati ya baba yake, Rais Kikwete na aliyewahi kuwa Waziri Mkuu, Lowassa.

Aliongeza kuwa mambo hayo yanakuzwa na kimsingi hakuna ugomvi mkubwa kama inavyodaiwa na kukuzwa na watu wengi.

Alisema Lowassa na baba yake wamekuwa marafiki kwa miaka mingi na kwamba, watu wanajaribu kuwachonganisha wawili hao.

“Edward (Lowassa) akiwa na shida huwa anafika Ikulu na kufanya mazungumzo na Rais huo mgogoro unaosemwa unakuzwa na watu,” alisema Ridhiwan.

Akizungumza na NIPASHE kuhusu kauli hiyo aliyoitoa katika kipindi cha Star Tv, Ridhiwan alimsikiliza mwandishi swali lake lake na kisha akasema hawezi kujibu kwa kuwa alikuwa kwenye kikao.

“Nipo kwenye kikao, siwezi kujibu kitu. Ndiyo maana ulikuwa unapiga, nakata. Na ndiyo maana nimetoka nje kukusikiliza mara moja,” alisema Ridhiwan.

Ridhiwani alijibu madai hayo kwa kifupi, huku akikataa kutoa ufafanuzi wa kile alichoulizwa na kisha akakata simu.
SOURCE: NIPASHE

1 comment:

Anonymous said...

Siasa si kwakila mtu.zaidi nashindwa kuamini masikio yng kuona a professional lawyer anatoa such incriminatory statements.