Advertisements

Wednesday, August 27, 2014

Walioondolewa kupisha mgodi wa Geita walia kukosa tendo la ndoa

Baadhi ya wananchi waliohamishwa kupisha shughuli za Mgodi wa Geita, wamelalamikia kukosa huduma ya tendo la ndoa kutoka kwa wake zao kwa kipindi cha miaka minane.

Serikali iliwaondoa wananchi hao kwenye makazi yao ya awali bila kuwalipa fidia na kuwatelekeza kwenye ofisi za kata ya Kalangalala.

Kufuatia hali hiyo, Umoja wa Makanisa ya Kikristo nchini, ulilazimika kuwasaidia chakula na mahema ya kulalia kupitia Kanisa la AICT Geita ili kupunguza adha kubwa ya kaya 86 kulala kwenye chumba kimoja cha jengo la ofisi ya kata.

Serikali kupitia Jeshi la Polisi wilayani Geita, iliwaondoa kwa nguvu wananchi waliokuwa wakiishi kwenye eneo la Main Mpya na eneo hilo likakabidhiwa kwa wawekezaji wa mgodi wa GGM kwa ajili ya shughuli za uchimbaji madini.

Kwa mujibu wa mmoja wa waathirika hao, Abdallah Abeid, hivi sasa wameathirika kisaikolojia kutokana na baadhi yao kukosa haki ya kufanya tendo la ndoa kwa kipindi kirefu.

Abeid alisema sababu kubwa ni kwamba baadhi yao wanaishi kwenye hema lenye chumba kimoja huku wakiwa na watoto kati ya wawili hadi wanne pamoja na wakwe zao ambao walikuwa wakiwalea tangu awali, hivyo kukosa sehemu iliyofichika kwa ajili ya kukidhi tamaa ya mwili.

"Hapa ndugu zangu mnavyoniona nina miaka minane sijawahi kufanya tendo la ndoa na mke wangu...hii yote imesababishwa na aliyekuwa Mkuu wetu wa Wilaya ya Geita, Philemon Sherulete na OCD wake ambao waliamuru tuondolewe kwenye maeneo yetu pasipo hata kulipwa fidia ya nyumba na mazao yetu kumpisha mwekezaji wa GGM," alisema.

Meneja Uhusiano na Habari wa GGM, Tenga Tenga, akizungumzia madai ya wananchi hao ya kutolipwa fidia za maeneo yao kabla ya mgodi huo kutwaa ardhi hiyo, alisema GGM haidaiwi hata senti moja kwa ajili ya malipo ya wananchi hao kwani walikwisha kutekeleza mapema wajibu wao kwa serikali.

"Naomba ifahamike kuwa GGM haidaiwi hata chembe ya fidia ya wananchi hao. Sisi tuliiomba serikali kufanya tathmini ya maeneo tuliyoyahitaji kwa shughuli za uchimbaji madini na baadaye serikali ikatueleza kiasi kinachohitajika kisha GGM tukalipa kwa serikali ili ifikishe malipo hayo kwa walengwa," alisema Tenga.

Aliongeza: " Mgodi haukuhusika kulipa moja kwa moja walengwa bali serikali yenyewe ambayo tuliipatia malipo hayo (hakuyataja) kwa kuwa ndiyo iliyokuwa ikifahamu thamani ya kila eneo la mtu. Kwa hiyo kusema GGM inadaiwa ni kutoitendea haki kampuni yetu".

Hata hivyo, GGM inatekeleza mradi wa ujenzi wa nyumba 18 zenye thamani ya Sh. bilioni 1.1 kwa ajili ya waathirika hao ikiwa ni hatua ya kusogeza uhusiano mwema kwa jamii na kwamba hiyo imetolewa kama fadhila ya GGM katika kuchangia maendeleo ya jamii baada ya serikali kuomba msaada wa nyumba hizo.

NIPASHE lilipotaka kujua sababu za kujenga nyumba 18 wakati waathirika wa tukio hilo 86, Tenga alisema kuwa hatua hiyo ilitokana na ombi maalum la serikali na kwamba hawezi kujua ni watu gani kati ya waathirika hao watakaokabidhiwa nyumba hizo.

Alisema hilo ni jukumu la serikali na kwamba wao jukumu lao lilikuwa kutekeleza ujenzi huo. Kwa upande wake, mmoja wa waathirika hao, Elizabeth Paulo, aliiambia NIPASHE kuwa hatachukua nyumba hizo zinazojengwa eneo la Kasamwa kwa madai kwamba anachohitaji ni fidia halali ya nyumba na mazao yake yaliyoharibiwa vibaya wakati wa kuondolewa kwa nguvu kwenye makazi yake ya awali.

Mkuu wa wilaya ya Geita, Manzie Mangochie, alipotafutwa kuzungumzia sakata hilo, alidai hana muda wa kukutana na waandishi wa habari kwa kuwa ratiba yake imebanana na kwamba wamtafute siku nyingine ili wazungumze vizuri.

Mwaka 2007, serikali iliwaondoa wakazi 86 kwenye eneo la Main Mpya baada ya mgodi wa GGM kuhitaji eneo hilo kwa za shughuli za uchimbaji madini.
CHANZO: NIPASHE

No comments: