Advertisements

Thursday, May 28, 2015

Afrika Kusini yakanusha ilitoa hongo

Afrika Kusini yakanusha ilitoa hongo
Inadaiwa kuwa Afrika kusini ilitoa hongo ya dola milioni 10

Shirikisho la soka la Afrika Kusini SAFA, limekanusha madai yote ya kuhusishwa na hongo.

Afisa wa mawasiliano wa Safa Dominic Chimhavi amewataka wote wenye ushahidi dhidi ya shirikisho hilo kuuweka wazi ilikuondoa shaka iliyoibuka kufuatia kukamatwa kwa maafisa wakuu wa FIFA.

Tuhuma hizo ziliibuka baada ya polisi wa Uswisi kuwakamata maafisa wakuu wanaotuhumiwa kwa kushiriki ufisadi na kula kiinua mgongo cha takriban dola million 150 ndani ya kipindi cha miaka 20.

Tuhuma hizo zilifuatia uchunguzi wa idara ya ujasusi ya Marekani.

Kwa Upande wake, waziri wa michezo wa Afrika Kusini amekanusha kuwa shirikisho la soka nchini humo lilitoa hongo ya dola milioni 10 ili taifa hilo lipewe uwenyeji wa kombe la dunia la mwaka wa 2010.

Waziri Fikile Mbalula alisema kuwa ni uongo mtupu na kuwa serikali haikumlipa yeyote.

Uchunguzi wa vitendo vya rushwa ndani ya Fifa umebainisha kuwa viongozi 3 walipokea hongo ya dola milioni kumi iliwanachama watatu waipigie kura Afrika Kusini kuandaa kombe la dunia la 2010.
Hata madai hayo yanafuatia mawasiliano baina ya SAFA na wanakamati wengine wa FIFA ambapo serikali iliahidi kutoa dola milioni 10 iwapo makamu wa rais wakati huo Jack Warner angewashawishi wanawkamati wenza kuipigia kura Afrika kusini badala ya Morocco.

Kulingana na taarifa ya upande wa mashtaka Afrika kusini ilishindwa kulipa pesa hizo moja kwa moja na hivyo ikapanga FIFA iwalipe moja kwa moja Ripoti hiyo ya FBI ilisema.

Awali waziri wa ofisi ya rais Jeff Radebe alikanusha madai ya kutolewa kwa hongo yeyote akisema kuwa kamati andalazi iliwajibikia kila senti iliyopata kwaajili ya maandalizi ya kombe la dunia lililofanyika mwaka wa 2010 kwa mara ya kwanza ndani ya bara la Afrika.

Serikali ya Uswiss imesema itaidhinisha haraka kusafirishwa kwa maafisa hao waliokamatwa kwenda Marekani .

Mwanzoni mwa mwezi huu, Blatter alisema anafahamu baadhi ya wafanyakazi wenzake wa zamani walikuwa wakichunguzwa lakini amekanusha kuwa uchunguzi huo ulimhusu pia.-BBC

No comments: