Advertisements

Monday, May 4, 2015

Chadema yamng’ang’ania JK kuhusu Uchaguzi Mkuu

Viongozi wa Chadema wakiomba dua kabla ya kuanza kwa kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho kilichofanyika Dar es Salaam jana. Kuanzia kulia ni Makamu Mwenyekiti, Profesa Abdallah Safari, Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu Dk Willibrod Slaa na Naibu Katibu Mkuu (Zanzibar), Salum Mwalimu. Picha na Venance Nestory

Dar es Salaam. Licha ya Rais Jakaya Kikwete kusema hana mpango wa kuongeza muda na kuwa Uchaguzi Mkuu utafanyika Oktoba, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimezidi kuonyesha wasiwasi wake kikieleza kuwa hakuna dalili za uchaguzi huo mwaka huu.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alikieleza kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho kuwa uchaguzi huo unaweza kuahirishwa kama ilivyotokea kwenye Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa.
Kikatiba, uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani unatakiwa kufanyika Jumapili ya mwisho ya Oktoba ambayo itakuwa Oktoba 25, mwaka huu ikiwa ni mwaka wa tano tangu kuchaguliwa kwa Serikali iliyopo madarakani.
Katika kipindi hicho, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilitakiwa kurekebisha mara mbili Daftari la Kudumu la Wapigakura lakini haijafanya hivyo hata mara moja na hii ya sasa inayoendelea katika baadhi ya mikoa bado inasuasua.
Kutokana na kusuasua huko, NEC ililazimika kuahirisha Kura ya Maoni iliyokuwa imepangwa kufanyika Aprili 30, hadi tarehe itakayotangazwa baadaye, licha ya awali kuelezwa mara kwa mara na tume yenyewe au viongozi wa Serikali kuwa kura hiyo ilikuwa palepale.
Ni kutokana na hali hiyo, Chadema na vyama washirika vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vilieleza wasiwasi wa kuwapo uwezekano wa kuahirisha uchaguzi mkuu kwa kisingizio cha kutokamilika uandikishaji wapigakura kama ilivyofanyika kwa kura ya maoni.
Lakini akihutubia siku ya wafanyakazi (Mei Mosi), mjini Mwanza, Rais Kikwete alieleza kuwashangaa wapinzani hao, akisema ni aibu kwao kuzua jambo ambalo halipo, kwa kuwa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba uko palepale na hana mpango wa kuongeza muda.
Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu, Damian Lubuva jana alisisitiza kauli ya Rais akisema uchaguzi huo utafanyika kama Katiba inavyoeleza (wiki ya mwisho ya Oktoba), huku Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu na Bunge, Jenista Mhagama akisema uandikishaji unavyoendelea ni kielelezo kwamba uchaguzi utafanyika kama ulivyopangwa.
Wasiwasi wa Mbowe
Akifungua kikao cha siku mbili cha Kamati Kuu jana, Mbowe alisema: “Wote hatujui kama uchaguzi mkuu upo mwaka huu, waziri mkuu anasema upo, NEC wanasema upo lakini mazingira hayaonyeshi kwamba utakuwapo mwaka huu.”
Alisema bado uandikishaji wapigakura unasuasua na mazingira hayaonyeshi kwamba utakamilika kabla ya siku ya uchaguzi inayoelekezwa na Katiba.
Alisema hata kwenye kura za maoni ya Katiba Inayopendekezwa, mazingira yalionyesha kwamba isingewezekana ifanyike Aprili 30, mwaka huu kama Serikali ilivyotangaza.
“Chadema tulipiga hesabu tukasema haiwezekani kura ya maoni ifanyike siku iliyotangazwa na Serikali, tukapaza sauti lakini viongozi wetu waliendelea na msimamo wao, dakika za mwisho wakatangaza kuahirisha,” alisema Mbowe.
Alisema mazingira ya nchi kuelekea uchaguzi mkuu hayatabiriki na hakuna dalili zinazoonyesha kwamba uchaguzi utafanyika.
Alisema ili nchi iwe na amani na usalama, inatakiwa kutabirika kuwa ni nini kitafanyika katika kipindi fulani.
“Ni lazima tufahamu katika kipindi cha mwaka mmoja au miezi mitatu ijayo kutafanyika nini ni lazima nchi itabirike,” alisema.
Alisema hata miradi ya uwekezaji imesimama na wawekezaji wanahitaji kufahamu nini kinaendelea kwa ajili ya usalama wa miradi yao... “Hatuelewi ni nini kitafanyika baada ya miezi mitatu ijayo, hatujui baada ya mwaka mmoja kama nchi tutafanya nini tunayumba, tunakwenda bila kuwa na uhakika tunakwenda wapi,” alisema Mbowe.
Lubuva
Akifafanua kuhusu sintofahamu hiyo ya Chadema, Jaji Lubuva alisema hadi kufikia mwisho wa mwezi huu, vifaa vyote vya BVR vitakuwa vimewasili nchini.
Alisema jana NEC ilipokea BVR 1,150 na kwamba zitapelekwa wakati wowote kuanzia kesho katika mikoa ya Tabora, Kigoma, Singida na Kagera.
Alisema hivi sasa uandikishaji unaendelea katika mikoa ya Lindi Mtwara, Ruvuma na Iringa kwa kutumia vifaa 2,098 vilivyopo.
“Kwa hiyo nawaomba Chadema waache kuingilia kazi za NEC, ratiba yetu inaonyesha kwamba tunakwenda vizuri na uchaguzi utafanyika kama kawaida,” alisema.
Mhagama
Waziri Mhagama alisema Chadema iache kutafuta umaarufu wa kisiasa kwani uandikishaji unavyoendelea ni wazi kuwa uchaguzi hautaahirishwa.
Alisema uandikishaji unaendelea mikoa mbalimbali na vifaa vinaendelea kuwasili na haelewi wasiwasi wa Chadema unatoka wapi.
Kushuka kwa shilingi
Kuhusu kushuka kwa kushuka kwa shilingi Mbowe alisema: “Athari kubwa ya kushuka kwa shilingi yetu ni kwamba baada ya kipindi kifupi kijacho tutashuhudia mfumuko mkubwa wa bei kwa sababu wafanyabiashara watakuwa wanafidia gharama kubwa ya ununuzi wa bidhaa kutoka nje.”
Mwananchi

No comments: