Advertisements

Monday, June 29, 2015

Kinana aitolea uvivu Serikali ya CCM

Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana akizungumza katika mkutano wa hadhara kwenye viwanja vya furahisha jijini Mwanza jana.Picha na Michael Jamson.

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana ameikosoa Serikali ya chama chake kwamba imekuwa siyo sikivu kwa matatizo ya wananchi na kuwa wabunge wa chama hicho wanapitisha sheria ambazo zinakuwa mzigo kwa wananchi.
Akihutubia katika mkutano wa kuhitimisha ziara yake, jijini Mwanza jana, Kinana alisema atafanya kikao cha kwanza na wabunge wa CCM baada ya uchaguzi ili kuwaeleza majukumu yao ya msingi ikiwamo kuiwajibisha Serikali.
Alisema wabunge wa CCM wamekuwa wakiunga mkono kila jambo linaloletwa bungeni bila kutathmini matokeo ya sheria hizo kwa wananchi wanaowawakilisha.
Alisema lazima ifike wakati wabunge wa CCM wabadilike na kuwatumikia wananchi wao.
“Nitakutana na wabunge wa CCM na kuwaambia kwamba sheria walizozipitisha haziwasaidii wananchi… lazima chama kiwe na nguvu ya kuielekeza au kuiwajibisha Serikali yake,” alisema Kinana huku akishangiliwa na wananchi waliohudhuria mkutano huo.
Katibu Mkuu huyo alisema kuna haja ya kubadilisha mfumo wa utendaji kazi wa chama na mojawapo ni kuchagua mtu mwingine wa kuongoza wabunge wa CCM bungeni badala ya Waziri Mkuu kama ilivyo sasa.
Alisema Waziri Mkuu ataachwa atekeleze jukumu lake la kuiongoza Serikali bungeni, lakini kuwe pia na kiongozi wa wabunge wa CCM bungeni. Alisema mfumo huo utakipa chama nguvu zaidi ya kuisimamia Serikali yake.
“Wamekaa wabunge tena na kupitisha sheria ya kila gari kuwa na kizimamoto, nani alisema gari langu lina mpango wa kuungua?” alihoji kiongozi huku na kusema sheria nyingine zinatakiwa kufutwa kwa sababu hazimsaidii mwananchi.
Aliishangaa Serikali ya CCM kwa kushindwa kufuta baadhi ya sheria ambazo zimebainika kuleta usumbufu kwa wananchi na kusisitiza kuwa lazima ifike wakati Serikali ifanye tathmini ya sheria zake na kuzifuta ambazo hazifai kwa sasa.
“Nimekuwa waziri na kiongozi serikalini kwa muda mrefu, lakini sijawahi kuona Serikali ikifuta sheria. Wamekuwa wakiongeza sheria mpya kila siku. Hivi karibuni Serikali imepeleka miswada mingine 11 na yote imepitishwa. Kwa namna hiyo tunambebesha mwananchi mzigo mkubwa,” alisema.
Kinana aliitaka Serikali kuwashirikisha wananchi wakati wa kutunga sheria ili kuondoa changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza mara kwa mara.
Kuhusu ahadi za Rais
Kinana alisema Serikali imefanya mambo mengi katika kuliletea Taifa maendeleo kwa kutekeleza kikamilifu Ilani ya CCM ya mwaka 2010 na ahadi nyingine zilizotolewa na Rais Jakaya Kikwete wakati wa kampeni za urais.
Alisema wakati Serikali ikiingia madarakani mwaka 2005, kulikuwa na wanafunzi wa elimu ya juu 48,000 tu, lakini sasa wanafikia 200,000. Aliongeza kuwa zaidi ya vijiji 1,000 vimeunganishwa na umeme.
“Katika kipindi cha miezi 26 ambayo tulikuwa tunatekeleza maazimio ya mkutano mkuu wa mwaka 2012, nimejifunza mambo mengi. Nimeyajua matatizo ya wananchi kwa karibu zaidi, lazima Serikali iwe sikivu,” alisema Kinana.
Akimkaribisha Kinana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye aliwataka Watanzania wasimame imara kukataa senti tanotano kutoka kwa wanaotaka kununua uongozi ambao baadaye wanataka kurudisha fedha zao.
“Ndiyo maana tunakumbana na ‘skendo’ kibao, kesho Escrow, keshokutwa Richmond, vyote hivi dawa yake moja, lazima tuzuie wanaotaka kununua uongozi… na kama hiki ndicho wanachokitaka, safari hii tutazuia wanaotaka kununua uongozi.
“Hatuwezi kuzunguka nchi nzima kusafisha chama halafu, wachache wanakaa chini wanasema nitanunua hawa, halafu sita nitakuachia… watashika adabu mwaka huu na hii itakuwa fundisho.
“Niko tayari kuliongoza jeshi la vijana kukataa biashara ya kununua uongozi na matumizi mabaya ya fedha kwenye uchaguzi… haya ndiyo yanayoharibu maadili ya nchi hii kwamba mtu anaamua yake na mwaka huu Mungu atawalaani,” alisema Nape.
Nape aliwatahadharisha wananchi kuepuka siasa za ushabiki kwani wakati wao (wananchi) wakiathirika, watu wachache ndiyo wanaonufaika. Alisema CCM imejipanga kuja kivingine katika jitihada za kuwatumikia wananchi.
“Chama cha Mapinduzi hakiuzi uongozi. Natoa wito kwa wale wote wanaofikiri kuwa wanaweza kufanya hivyo watambue mapema kwamba haiwezekani,” alisema.
Akimpongeza Kinana kwa juhudi zake za kukiimarisha chama kwa kutoka ofisini na kwenda kwa wananchi, Nape alisema ziara za katibu mkuu huyo zimetumia miezi 26 na siku 18 katika mikoa 31 nchini.
alisema katika ziara hizo, ametembea umbali wa kilomita 193,574 huku akizindua miradi 2,671 na kuingiza wanachama wapya 208,432 na kati yao, 38,934 walitoka Chadema.
Katika mkutano huo, Nape alimtambulisha mwimbaji mpya ambaye atarithi mikoba ya marehemu John Komba kuongoza bendi ya TOT katika uhamasishaji wa chama.
Alimtaja mrithi huyo kuwa ni Twalib Neka na kusema kuwa ameshakamilisha albamu yake ya kwanza akiwa na bendi hiyo.
Mwananchi

3 comments:

Anonymous said...

Mh. Kinana ni bora useme ukweli unaotuumiza sana wana CCM kwa kuwa Serikali na viongozi wake wametufikisha hapa tulipo, wamaekuwa wanajifikiria wao wenyewe tu na kutekeleza ilani na kuwatumikia wananchi imekuwa ni hadhithi kila mwaka!! Hii ni aibu na tumewachoka saana hawa viongozi wetu kwa kulindana kila siku na kuweka dhima mifukoni mwao. Wakati umefika wa kusema ukweli na kiongozi yeyote yule wa CCM anayetaka kuingia kwenye awamu hii ijayo atueleze ukweli nini alichokifanya sio atakachofanya muda huo hatuna sasa hivi umepitwa na wakati.

Unknown said...

Mmh

Anonymous said...

FUTUHI IN ACTION ....