Thursday, January 14, 2016

Lukuvi atoa siku 18 ghorofa livunjwe D’salaam

By Raymond Kaminyoge, Mwananchi
Dar es Salaam. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi ametoa siku 18 kwa uongozi wa Manispaa ya Ilala kuvunja jengo la ghorofa 16 lililopo katika Mtaa wa Indira Gandhi kabla halijaleta maafa.

Akizungumza jana katika jengo hilo, Lukuvi alisema anashangaa hadi sasa kazi ya kuvunja jengo hilo haijaanza licha ya manispaa kuelekezwa kulivunja.

Uamuzi wa Serikali kulivunja ulikuja baada kuporomoka kwa jengo katika mtaa huo lililosababisha vifo vya watu 37 na wengine 18 kujeruhiwa mwaka 2013.

“Ni aibu, manispaa mnataka jengo hilo liporomoke na kuua watu tena! Tutachekwa kwa uzembe kama ikitokea tena ajali,” alisema.

Lukuvi alisema kuanzia Februari Mosi uvunjaji wa jengo hilo unatakiwa kuanza vinginevyo wahusika wajiandae kuchukuliwa hatua.

“Nataka nikipita hapa siku yoyote kuanzia mwezi ujao nikute mkandarasi anabomoa jengo hili vinginevyo hatutaelewana,” alisema.

“Hili ni eneo hatarishi hata tuliosimama hapa hatari yoyote inaweza kutukuta lakini Manispaa ya Ilala haioni kwamba hapa kuna tatizo,” alisema.

Waziri alisema uvunjaji wa jengo hilo utakapoanza, wananchi wanaoishi jirani watatakiwa kuhama kwa muda kwa tahadhari.

“Mkuu wa Wilaya ya Ilala, wakianza kuvunja jengo hilo tafadhali waondoeni wakazi wote kwa sababu eneo hili litakuwa hatarishi,” alisema.

Jengo hilo linamilikiwa kwa pamoja kati ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) na Ali Raza Investment.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Isaya Mngulumi alisema kilichochelewesha ni makandarasi walioshinda zabuni hiyo kujitoa katika hatua za mwisho wakitoa sababu mbalimbali.

Alisema hivi sasa amepatikana mkandarasi Patty Interplan ambaye yuko katika hatua za mwisho za kupewa kazi hiyo.

“Tutaanza kazi kama ulivyoelekeza,” alisema Mngulumi.

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Raymond Mushi, alisema atatoa ushirikiano kwa manispaa hiyo ili kuhakikisha jengo hilo linabomolewa.

3 comments:

Anonymous said...

Na lile jengo liliojengwa lina chungulia ikulu , Vipi au umelisahau ? Kaazikweli kweli hizi siasa za zimamoto hizi , mpaka kiongozi aseme ndio lina tekelezwa jambo ! wekeni katiba iliyo pendekezwa na watanzania wote ili muachane na mchezo wa kiongozi kasema ndio lifanyike jambo !

Anonymous said...

Fyuuuuu ccm
Imenitoka

Tazama said...

Kweli hapo juu! Katiba ya wananchi ndio mambo yote! Itaondoa kuchagua nani abomolewe na nani aachwe...Mmmh!