Advertisements

Wednesday, June 22, 2016

MKAZI WA JIDA MKOANI MTWARA AFIKISHWA MAHAKAMANI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MTOTO WA MIAKA 8

Kamanda wa Polisi mkoa wa Mtwara Henrry Mwaibambe

Jeshi la polisi mkoani Mtwara limemfikisha mahakamani mtu aliyefahamika kwa jina la Andrea Maiko mkazi wa kata ya Jida wilaya ya Masasi kwa kosa la kumbaka mtoto wa miaka nane mwanafunzi wa darasa la pili katika shule ya msingi Mangumchila na kumuambukiza ugonjwa wa kaswende.

Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa Polisi mkoa wa Mtwara Henrry Mwaibambe amesema mama mzazi wa binti huyo alishitukia nyendo za mtoto wake kwamba hatembei vizuri na ndipo alipomuuliza kilichomsibu.

Amesema hata baada ya mama yake kumuuliza mara kadhaa mtoto huyo aligoma kuzungumza na ndipo aliamua kwenda kituo cha polisi,na baada ya kufika huko alikubali kumtaja kijana huyo na kudai alikuwa akimvizia kila mara wakati akitoka shule na kumpeleka kwenye jumba bovu na kumbaka.

Amebainisha kuwa baada ya kupelekwa hospitali kwa ajili ya vipimo mtoto huyo alibainika ameambukizwa ugonjwa wa kaswende ambapo kwa sasa anaendelea na matibabu.

Amesema upelelezi umekamilika na mtuhumiwa amefikishwa mahakamani na kesi yake inatarajiwa kusikilizwa kesho katika mahakama ya hakimu mkazi wilaya ya Masasi.

Chanzo: ITV

No comments: