Advertisements

Wednesday, September 14, 2016

WATUMISHI HEWA WAFIKIA 17,201

SERIKALI imewaondoa watumishi hewa 17,201 katika utumishi wa umma, ambapo licha ya kupokea mishahara pia mikopo mingi ilitolewa visivyo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki alisema hayo jana mjini Dodoma wakati wa kuapishwa kwa wakurugenzi watendaji wapya 13 walioteuliwa Septemba 10, mwaka huu na Rais John Magufuli.
Kairuki alisema kuanzia Machi mwaka huu hadi sasa wameondoa watumishi hewa 17,201 kwenye utumishi wa umma na zoezi hilo bado linaendelea.
“Tumegundua mikopo mingi imetolewa visivyo,” alisema Kairuki na kuongeza kuwa asilimia 80 hadi 90 ya watumishi hewa ni watoro.
“Kwenye sekta ya elimu kuna Mratibu wa elimu kata, maofisa elimu lakini wamekuwa hawafuatilii walimu wengi wamekuwa hawapo kwenye vituo vya kazi lakini wanapokea mishahara,” aliongeza waziri huyo na kubainisha kwamba kumekuwa na tabia ya walimu ambao hawako kazini kwa kipindi kirefu, lakini walimu wenzao wamekuwa wakiwaandikia kwenye kitabu cha mahudhurio na kuwasainia ili kuonesha kuwa wapo kazini, jambo ambalo ni kinyume cha utaratibu.

“Mwarobaini wa walimu wanaowajazia vitabu vya mahudhurio walimu ambao hawafiki kazini dawa yao iko jikoni, tutafuatilia kituo kimoja hadi kingine kuwabaini na tutachukua hatua,” alieleza na kuongeza kuwa maofisa utumishi wengi wamekuwa wakijifanya ndio wakurugenzi jambo ambalo limekuwa likisababisha tatizo la watumishi hewa kuendelea.
Alisema michakato ya maombi ya watumishi inaanza Novemba, hivyo wakurugenzi wahakikishe wanaletewa ikama wajiridhishe ili wapate watumishi kulingana na mahitaji. Akizungumzia suala la watumishi hewa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene alisema “Hatuwezi kuajiri wakati tuna hewa lazima tuchambue na kujiridhisha.”
Pia alisema mitandao ya kijamii ni janga kubwa kwani kuna watu wanatoa taarifa mitandaoni kuwa ni taarifa ya waziri kumbe uongo. “Utakuta mtu kakataa kaandika speech ya Waziri, kila mtu anayeweza anachapisha, wapi nilisema walimu wa sanaa hawataajiriwa?” Alihoji.
Alisema hivi karibuni kwenye mitandao ya kijamii watu waliweka taarifa kuwa Tamisemi inaajiri na watu watume maombi jambo ambalo lilileta usumbufu mkubwa.
Aidha, alisema watu wanahoji uteuzi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Hudson Kamoga aliyekuwa mtangazaji wa Clouds Tv, lakini ukweli ni kuwa aliteuliwa kulingana na sifa na uwezo.
Rais ana mamlaka ya kuteua mtu yeyote ambaye anaamini anaweza kufanya kazi, Wizara hii iko chini ya Rais,” alisema na kuwashangaa watu wanaobeza uteuzi huo na kutaka wakurugenzi hao wakachape kazi.

CHANZO: HABARI LEO

No comments: