Advertisements

Sunday, October 9, 2016

MWANAFUNZI ALIYESHAMBULIWA ALIWEKWA 'RUMANDE' SAA 5

Mwanafunzi Sebastian Chinguku.

By Elizabeth Edward na Brandy Nelson, Mwananchi mwananchipapers@mwananchi.co.tz


Dar/Mbeya. Mwanafunzi aliyeshambuliwa na walimu watano wa Shule ya Sekondari ya Kutwa ya Mbeya, Sebastian Chinguku, aliwekwa ofisini kwa takribani saa tano baada ya kupata kipigo hicho kilichoibua mjadala nchi nzima.

Tukio hilo liliibua mjadala baada ya picha za video kusambaa kwenye mitandao ya kijamii katikati ya wiki na kusababisha Serikali kuwatimua walimu hao waliokuwa wameenda shuleni hapo kwa mafunzo ya vitendo.

Picha hizo zinawaonyesha walimu hao wakimkamata mwanafunzi huyo mikono yote, baadaye kumpiga ngwala na kuanza kumpiga kwa makofi, ngumi, mateke na fimbo, huku mmoja wao akionekana kushughulika kumpiga kichwani mithili ya mtu anayeua nyoka.

Kumekuwa na maelezo tofauti kuhusu tukio hilo, baadhi wakisema mwanafunzi huyo alionyesha kiburi alipotakiwa apige magoti kama adhabu ya kutofanya zoezi la Kiingereza alilopewa na mwalimu wake, Frank Msigwa.

Lakini habari ambazo Mwananchi imezipata zinasema kuwa baada ya kufikishwa ofisini, mwanafunzi huyo alionyesha utovu wa nidhamu uliosababisha walimu hao kufanya vitendo vya kikatili vya kumchangia kumpiga na baadaye kumuweka ofisini kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 8 mchana wakati kengele ya kutoka ilipopigwa.

Walimu hao, ambao walikuwa shuleni hapo kwa ajili ya mafunzo ya vitendo waliingia ofisini wakiwa wamemshika mwanafunzi huyo na baadaye kumtaka apige magoti, lakini akakataa kufanya hivyo.

“Sikujua walikoanzia ila niliona wazi hakukuwa na amani. Mwanafunzi aliambiwa piga magoti, akakataa, wakambadilishia adhabu na kumwambia akae chini, lakini pia akagoma sisi bado tukawa tumepigwa na bumbuwazi,” alisema shuhuda aliyezungumza na Mwananchi.

“Kitendo hicho kilisababisha walimu hao kutumia bakora kumchapa, lakini yule Sebastian akawa anashika fimbo na hapo ndipo walimu hao vijana walipoamua kushirikiana kwa pamoja kutumia nguvu kumlaza chini na kumpiga.”

Baada ya Sebastian kuadhibiwa kwa kipigo hicho kisicho cha kawaida shuleni, walimu hao walimchukua kwa ajili ya kumrudisha darasani, lakini wakiwa njiani alitaka kukimbia.

“Kitendo hicho kiliwafanya wamrudishe ofisini na kumuita mwalimu wa nidhamu ambaye alielezewa hali ilivyokuwa, naye akamuita makamu mkuu wa shule ambaye alimtaka mwanafunzi aandike barua ya kuomba msamaha,” alisema shuhuda huyo.

Alisema baada ya hapo walimu hao walimtaka Sebastian akae ofisini hadi watakapomuhitaji. Mwanafunzi huyo alilazimika kukaa ofisini hadi kengele ya kutoka ilipogongwa saa 8:00 mchana.

Uchunguzi wa Mwananchi unaonyesha kuwa hiyo haikuwa mara ya kwanza kutokea tukio kama hilo.

“Ilishawahi kutokea mwanafunzi alichelewa shule na kuamua kuruka ukuta, lakini walimu walimuona wakamwita na kutaka kumuadhibu, akakataa huku akitaka kurusha ngumi. Ilibidi walimu wengine wajongee eneo la tukio ili kumdhibiti,” alisena shuhuda huyo.

“Wakati huohuo simu ikapigwa polisi ambao walikuja na gari wakamchukua kilichoendelea sikufuatilia.”

Katika tukio la wiki hii, Sebastian ametoa maelezo tofauti katika mazungumzo na Mwananchi jana. Amedai kuwa baada ya tukio hilo, mwalimu mkuu msaidizi alimtaka aandike barua ya kujieleza kwa madai ya utovu wa nidhamu aliouonyesha.

Alisema wakati anapigwa na walimu hao wa chuo, walimu wengine walikuwa kwenye kikao ofisi ya taaluma na baada ya kupigwa, walimgeuzia kibao wakidai kuwa yeye ndiye aliyewashambulia.

“Waliwaeleza walimu waliokuwa kwenye kikao kuwa mimi ndiyo nimewapiga na ndipo makamu mkuu wa shule akaniamuru niandike barua ya kujieleza kwa utovu wa nidhamu,” alisema Sebastian.

Alisema kabla ya kuanza kuandika barua hiyo, alikuja mwalimu wa zamu na akamweleza hali halisi na alimtaka aandike barua ya kuelezea tukio zima lilivyokuwa, wakati mwalimu akipeleleza kwa wanafunzi wengine ili kujua ukweli.

“Baada ya kuandika barua nikaitwa ofisi ya taaluma na wakanieleza kuwa wamebaini ukweli kuwa walimu ndiyo walionipiga na ndipo walimu wengine wakaanza kunipa pole na kunishauri nirudi nyumbani kutibiwa,” alisema.

Alisema tukio hilo lilimfanya ahofie kuwa angefukuzwa shule baada ya kugeuziwa kibao, hadi akaona awaambie kuwa amesamehe ili aweze kuendelea na shule.

“Ninachojua ukiambiwa uandike barua ya kujieleza ni lazima ufukuzwe shule au usimamishwe na hilo ndilo ilikuwa hofu yangu kubwa na ndiyo maana niliwaambia walimu kuwa nimesamehe,” alisema.

Kuhusu suala la kushiriki makundi ya wavuta bangi, mwanafunzi huyo alisema anashangazwa na tuhuma hizo ambazo alishawahi kupewa hadi kutakiwa aandike maelezo na alipofanya hivyo, shauri hilo likaisha.

Baba mzazi wa mwanafunzi huyo, John Chinguku alisema amesikitishwa na ujumbe unaosambaa katika mitandao ya simu kuwa Sebastian aliwahi kumjibu vibaya mbele ya walimu alipokuwa amekwenda kumtetea asifukuzwe shule.

Pia tuhuma kuwa aliwahi kuvunja televisheni na kwamba baba yake hamtaki nyumbani.

“Maelezo hayo si ya kweli ni upotoshaji...kwangu sina hata umeme. Bado naendelea na ujenzi wa nyumba yangu. Na huo ujumbe wa kuwa simtaki Sebastian si kweli kwa kuwa ni kijana ninayemtegemea kwa kazi za nyumbani, hasa kusimamia ujenzi wa nyumba,” alisema.

Pia aliukana ujumbe mwingine ambao alisema umesambaa mitandaoni kuwa anaomba msada wa matibabu na kutaja namba ya simu na akaunti ya benki.

“Sihusiki na ujumbe huo wala hakuna mahali popote nilipoomba msaada kwa kuwa mimi ni mtumishi wa benki ya NMB. Kama masuala ya matibabu kwa mtoto wangu, yamefanywa na mwajiri wangu,” alisema.

Kamanda wa polisi mkoani hapa, Dhahiri Kidavashari alisema jeshi hilo linashikilia watu wanane kwa mahojiano, wakiwamo walimu hao na kwamba uchunguzi unaendelea.

1 comment:

Anonymous said...

Hata kama alikataa adhabu hiyo sio sababu ya kumshambulia mwanafunzi au binadamu yoyote kama walivyomfanyia,ni kuliuka sheria za binadamu na wachukuliwe sheria iwe fundisho kwa walimu wengine,wanafunzi wanapigwa sana wengine hata kuzimia na walimu,enough is enough