Advertisements

Thursday, October 20, 2016

SERIKALI KUANZISHA MPANGO WA KITAIFA KUPINGA UKATILI WA JINSIA KWA MAMA NA MTOTO

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bi. Sihaba Nkinga akizungumzia kuhusu serikari inavyounga mkono jituhada za taasisi pamoja na mashirika mbalimbali yakiwemo ya UNICEF na UN Women kujikita katika  utetezi wa ukatili wa kijinsia kwa wanawake. (Picha na Geofrey Adroph)
Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UNWOMEN), Maria Karadenizli akizungumza na waandishi wa habari kuhusu vitendo vya ukatili wa kijinsia pamoja na kuomba ushirikiano wa serikari pamoja na vyombo vya ili kutengeneza mpango mkakati wa manyanyaso ya wanawake na watoto.
Usia Nkhoma Ledama kutoka UNICEF akieleza jambo wakati wa semina kwa waandishi wa habari iliyoandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UNWOMEN) na kuwakutanisha wadau mbalimbali wa serikali na kijamii iliyofanyika katika Hoteli ya Double Tree jijini Dar Es Salaam leo


Na Rabi Hume, MO BLOG
Licha ya kufanya juhudi mbalimbali za kumaliza vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto kuonekana kusindwa kufanikiwa, serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imepanga kuanzisha mpango wa kitaifa wa kuhakikisha vitendo vya ukatili wa kijinsia vikimalizika.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Sihaba Nkinga katika semina ya siku moja ya waandishi wa habari iliyoandandaliwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa ya UNICEF, UNFPA na UN WOMEN na kueleza kuwa tayari wameshafanya maandalizi ya awali ili kuanzisha mpango huo ambao wanataraji utaweza kufanya kazi baada ya iliyopita kuonekana kukwama.

"Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali kwa kutengeneza sera, sheria na hata hata tumekuwa tukisaini mikataba mbalimbali ya kimataifa ili kupinga vitendo hivi, lakini bado takwimu zinaonyesha vitendo vinaendelea, takwimu inaonyesha wanawake wa umri wa miaka 15-30 asimilia 30 wamefanyiwa ukatili,

"Lengo ni kuja na mpango mmoja ambao utatumika kuelezea mikakati  ambayo itatuwezesha kupambana na swala la ukatili kwa watoto, ukimfanyia mtoto ukatili kwa sasa baadae na yeye atakuja kukufanyia ukatili, ni vyema jambo hili lichukulie kwa namna ya kipekee na kwenda kuelimisha jamii ili ifahamu kuhusu ukatili wa kijinsia na athari zake," alisema Nkinga.

Nae mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UN WOMEN), Maria Karadenizli alisema vitendo vya ukatili wa kijinsia vina athari kwa waathirika na wamekuwa wakishirikiana na serikali kuona jinsi gani wanavimaliza lakini pia wameona ni vyema kushirikiana na vyombo vya habari ili kuifikia jamii kwa karibu 

"Tumekuwa tukishirikiana na serikali kupinga vitendo ukatili dhidi ya wanawake na watoto, na hilo linaweza kutekelezwa kupitia sheria za nchi wanawake na kufanikisha kuwepo usawa wa kijinsia kwa wanawake kupatiwa haki zao na watoto kupata haki zao za msingi ikiwepo kusaidiwa ili wapate elimu,

"Tunajua jinsi gani inaweza kusaidia kama mambo haya yakitolewa katika vyombo vya habari, kama kupitia vipindi na picha ambazo zitaonyesha hali ilivyo na hilo itasaidia kuonyesha kwa watanzania jinsi wanawake na watoto wanavyofanyiwa vitendo vya ukatili, tunataka kuona ushirikiano wa wanahabari na kuendelea kutoa elimu kwa jamii," alisema Karadenizli.

Awali akielezea kuhusu semina hiyo, Mtaalumu wa Mawasiliano wa UNICEF, Usia Ledama alisema semina hiyo ina lengo la kuwapa elimu waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali ikiwepo tv, redio, magazeti na blogu ili waweze kuielimissha jamii kuhusu ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto.

"Tunaamini waandishi wa habari na kama wakielewa jambo vizuri wanaweza kusaidia kueleza jamii vyema kwani watakuwa wameshaelewa jinsi ukatili wa mama na mtoto ulivyo na athari kwa jamii," alisema Ledama.
Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Watoto, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Margareth Mussai akizungumzia jinsi mpango mkakati utakaozinduliwa utaweza kupunguza ukatili kwa mama na watoto.
Pedro Guerra kutoka UNICEF akizungumza jambo katika semina iliyowahusisha waandishi wa habari ili kuweza kuripoti habari za kijinsia hasa za manyanyaso ya mama na mtoto.

Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UN WOMEN) Lucy Tesha akizungumza jinsi shirika hilo lilivyoweza kupambana na unyanyasaji wa kijinsia kwa mtoto wa kike
Baadhi ya waandishi wa habari wakichangia mada inayohusu ukatili wa mama na mtoto katika semina iliyofanyika katika hoteli ya Double Tree jijini Dar es Saalaam leo
 Ruth Ayisi kutoka UNICEF  akitoa ufafanuzi kuhusu njia  wanazoweza kuzitumia waandishi wa habari kuripoti habari za unyanyasaji wa kijinsia kwa mama na mtoto.

Baadhi ya waandishi wakijadiliana 

Baadhi ya waandishi wa habari wakiwa kwenye semina

No comments: