Advertisements

Sunday, October 16, 2016

TABATA KIMANGA JIJINI DAR ES SALAAM WAIOMBA MANISPAA YA ILALA KUWAJENGEA DARAJA LITAKALO WAUNGANISHA NA TABATA CHANG'OMBE

 Mtoto Juma Ramadhan mwanafunzi wa darasa la pili katika Shule ya Msingi ya Tabata Kimanga, akiwa amembeba mdogo wake Sara Sadiki wakati wakipita katika daraja la miti linalounganisha wakazi wa Tabata Kimanga na Tabata Chang'ombe Dar es Salaam , ambapo wakazi wa eneo hilo wanaiomba Manispaa ya Ilala iwajengee daraja la kudumu.

Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Amani, Jonathan Mlay akimuonesha mwandishi wa mtandao huu, daraja la miti wanalolitumia lililojengwa kwa nguvu za wananchi kwa ajili ya kukabiliana na changamoto hiyo.

Na Dotto Mwaibale

WANANCHI wanaoishi mpakani mwa Tabata Kimanga na Chang'ombe katika Manispaa ya Ilala jijini Dar es Salaam wameomba kujengewa daraja ili waweze kutumia muda mfupi wa kufika katika maeneo hayo badala ya kupitia Tataba Mawenzi.

Ombi hilo wamelitowa Dar es Salaam jana wakati wakizungumza na mtandao wa www.habari za jamii.com kuhusu changamoto mbalimbali zilizopo katika eneo hilo ikiwemo ya kujengewa daraja hilo lililopo Mtaa wa Amani.

Akizungumzia changamoto ya daraja hilo, mkazi wa eneo hilo Tusekelege Ambonisye alisema wamekuwa wakitumia muda mwingi wa kuzunguka na gari kupitia Tabata Bima na kwenda Tabata Chang'ombe lakini kama daraja hilo linalounganisha maeneo hayo lingejengwa lingewarahisishia" alisema Ambonisye.

Aliongeza kuwa adha kubwa waliyonayo ni pale ikinyesha mvua kwani maji yanajaa na barabara hiyo kushindwa kupitika ikiwa ni pamoja na kuhatarisha maisha ya watu wanaojaribu kupita kaika eneo hilo.

Alisema kutokana na adha waliyokuwa wakiipata wananchi wa eneo hilo walikusanya nguvu na kujenga daraja la miti la muda ambalo linatumika lakini sio salama kwa watumiaji.

Mjumbe wa Serikali ya Mtaa huo wa Amani, Jonathan Mlay alisema changamoto ya daraja hilo ni ya muda mrefu kwani waliwahi kuiwasilisha kwa wabunge wa jimbo hilo waliopita na wa sasa Bonah Kaluwa lakini bado halijapatiwa ufumbuzi wowote.

"Kupitia vikao vyetu vya kamati ya maendeleo ya mtaa changamoto hii tuliipeleka kwa wabunge waliopita pamoja na huyu wa sasa tupo tunasubiri matokea yake" alisema Mlay.

No comments: